Wednesday 23 November 2011

Waziri- Z'bar ijadili Katiba kwa maslahi ya taifa

WAZIRI wa Katiba na Sheria Zanzibar, Abubakar Khamis Bakar amewasihi Wazanzibari kujadili Muswada wa Sheria ya Katiba kwa lengo la kupata Katiba mpya yenye maslahi ya Wazanzibari na Watanzania kwa ujumla.

Waziri huyo aliyasema hayo jana katika Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani Kikwajuni mjini Unguja, alipozungumza na wananchi, wanasiasa pamoja na waandishi wa habari juu ya muswada huo na utaratibu wa kupatikana kwa Katiba mpya.

Alisema upatikanaji wa Katiba mpya yenye maslahi kwa Wazanzibari inatokana na kuwepo kwa umoja na uzalendo ambao unatanguliza maslahi ya Zanzibar mbele na siyo kujali maslahi ya vyama.

Aliwataka pia wananchi wa Zanzibar kujikusanya na kuipitia Katiba iliyopo na kuyajadili mapungufu yaliyomo katika Katiba hiyo ili muda utakapofika wa kutoa maoni juu ya Katiba mpya, wafanye hivyo.

Aidha, alisema muswada huo uliopitishwa karibuni na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao pia unasubiri kutiwa saini na Rais Jakaya Kikwete ni mzuri na wenye kujali maslahi ya Zanzibar.

Waziri huyo wa Katiba na Sheria Zanzibar aliwatahadharisha wananchi kuwa makini na watu ambao wanaweza kuwapotosha wananchi katika kipindi hiki cha kujadili mchakato wa kupata Katiba mpya.

Kwa upande wa wananchi waliochangia katika mkutano huo wamewaomba viongozi na wanasiasa kupita katika majimbo yao ili kuendelea kuwaelimisha wananchi juu ya upatikanaji wa Katiba mpya.

Aidha, wameviomba vyombo vya habari Zanzibar kuandaa vipindi mbalimbali na kushiriki kikamilifu katika makongamano na warsha mbalimbali juu ya upatikanaji wa Katiba hiyo.

No comments:

Post a Comment