WAZIRI wa Katiba na Sheria Zanzibar, Abubakar Khamis Bakar amewasihi
Wazanzibari kujadili Muswada wa Sheria ya Katiba kwa lengo la kupata
Katiba mpya yenye maslahi ya Wazanzibari na Watanzania kwa ujumla.
Waziri huyo aliyasema hayo jana katika Ukumbi wa Baraza la
Wawakilishi la zamani Kikwajuni mjini Unguja, alipozungumza na wananchi,
wanasiasa pamoja na waandishi wa habari juu ya muswada huo na utaratibu
wa kupatikana kwa Katiba mpya.
Alisema upatikanaji wa Katiba mpya yenye maslahi kwa Wazanzibari
inatokana na kuwepo kwa umoja na uzalendo ambao unatanguliza maslahi ya
Zanzibar mbele na siyo kujali maslahi ya vyama.
Aliwataka pia wananchi wa Zanzibar kujikusanya na kuipitia Katiba
iliyopo na kuyajadili mapungufu yaliyomo katika Katiba hiyo ili muda
utakapofika wa kutoa maoni juu ya Katiba mpya, wafanye hivyo.
Aidha, alisema muswada huo uliopitishwa karibuni na Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania ambao pia unasubiri kutiwa saini na Rais Jakaya
Kikwete ni mzuri na wenye kujali maslahi ya Zanzibar.
Waziri huyo wa Katiba na Sheria Zanzibar aliwatahadharisha wananchi
kuwa makini na watu ambao wanaweza kuwapotosha wananchi katika kipindi
hiki cha kujadili mchakato wa kupata Katiba mpya.
Kwa upande wa wananchi waliochangia katika mkutano huo wamewaomba
viongozi na wanasiasa kupita katika majimbo yao ili kuendelea
kuwaelimisha wananchi juu ya upatikanaji wa Katiba mpya.
Aidha, wameviomba vyombo vya habari Zanzibar kuandaa vipindi
mbalimbali na kushiriki kikamilifu katika makongamano na warsha
mbalimbali juu ya upatikanaji wa Katiba hiyo.
No comments:
Post a Comment