Tuesday 15 November 2011

CCM- Serikali ya Umoja Z’bar imedumisha amani

15/11/2011
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema uamuzi wake wa kuafiki kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar, ulikuwa sahihi ili kuipa nafasi demokrasia ichukue mkondo wake.

Katibu wa Kamati Maalumu ya Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) Zanzibar, Itikadi na Uenezi, Issa Haji Ussi alisema hayo jana katika mkutano wake na wajumbe wa Kamati ya Siasa Jimbo la Muyuni katika Mkoa wa Kusini Unguja.

Ussi alisema hatua iliyofikiwa ya kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa kimsingi ililenga kuendeleza misingi ya amani, utulivu na umoja miongoni mwa Wazanzibari wote.

“Tumechukua uamuzi thabiti usioweza kusahaulika kwa maslahi ya usalama wa visiwa vyetu lakini kuipa nafasi demokrasia kuchukua mkondo wake hatua ambayo leo hii sote tunashuhudia ustawi wa demokrasia pamoja na amani na utulivu,” alisisitiza.

Alisema CCM ni chama chenye uwezo wa kutathmini na kupambanua mambo na kwamba utulivu uliopo hivi sasa Zanzibar unatokana na umahiri wa viongozi na wanachama wake.

Katibu huyo alisema CCM imesoma alama za nyakati na kufanikiwa kukwepa wimbi la pupa la mabadiliko ya pepo za mageuzi ya kidemokrasia.

Alisema kimsingi CCM imetumia jasho jingi katika meza ya mazungumzo ili kukataa kumwaga damu nyingi wakati wa vita.

Ussi aliwaeleza wanachama hao wa CCM kuwa uamuzi wa kuelekea kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa ulipitishwa na vikao vya NEC na kwamba chimbuko lake lilianza tangu mwaka 1995.

“Ni dhamira na nia ya CCM ya siku nyingi iliyofanya hadi kufikiwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa, kimsingi tumechonga mwiko ili kunusuru mikono isiunguzwe,” alisema.

Hata hivyo aliwahimiza wana CCM kujipanga na kutambua kuwa ujio wa Serikali hiyo unatokana na utashi wa chama hicho bila ya kuwa na lengo la kuifuta Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Alisema kuwa Serikali iliyopo ni ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya mfumo wa Umoja wa Kitaifa na kwamba Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein amekula kiapo cha kuongoza Serikali hiyo.

“Thamani ya utu wetu imetokana na Mapinduzi ya Januari 12 1964, ni upuuzi wa mwisho kuyapuuza Mapinduzi kwakuwa ni sehemu ya maisha na uhai wa kila Mzanzibari,” alisema

Chanzo: Habari leo

No comments:

Post a Comment