Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania,
(UWT) Asha Bakari Makame, amesema hajafurahishwa na Rais wa Zanzibar
kula kiapo kuwa Waziri asiyekuwa na Wizara maalum katika Baraza la
Mawaziri la Muungano.
Aliyasema hayo wakati akichangia muswada
wa mabadiliko ya Katiba ya Muungano uliowasilishwa katika semina ya
wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Waziri wa Katiba na Sheria Zanzibar
Abubakari Khamis Bakari
“Mheshimiwa Mwenyekiti sijafurahishwa
Rais wetu kuapishwa kuwa Waziri asiyekuwa na wizara maalum na lazima
hilo liangaliwe upya katika Katiba mpya,” alisema Asha ambaye ni
mwanasiasa mkongwe Zanzibar.
Alisema wajumbe wa Baraza la Wawakilishi
wana dhamana kubwa ya kutetea maslahi ya nchi na kuwataka wajiamini hasa
katika kutetea maslahi ya Zanzibar katika kuelekea mchakato wa kupata
Katiba mpya ya muungano
Hata hivyo Waziri wa Kilimo na Maliasili
Zanzibar, Mansoor Yussuf Himid, alisema kuwa, Rais wa Zanzibar, Dk. Ali
Mohammed Shein, hastahili kulaumiwa kwa sababu ametekeleza matakwa ya
Katiba na jambo hilo limeanza kabla ya uongozi wake.
“Rais tusimlaumu kwa jambo alilolikuta, kama hatutaki tuliondoshe na wakati wake ndio huu” alisema Mansoor.
Hata hivyo, alisema kwamba muswada wa
kuweka utaratibu wa mabadiliko ya Katiba baada ya kupitishwa na bunge,
lazima pia upitishwe na Baraza la Wawakilishi kabla ya kuanza
kutekelezwa kwa sheria hiyo.
“Tusije kukubali muswada kupitishwa
bungeni iwe mwisho, lazima uletwe Baraza la Wawakilishi kabla ya kuanza
utekelezaji wake” alisema Mansoor ambaye pia mweka Hazina CCM Zanzibar.
Nafasi ya Rais wa Zanzibar kuwa Makamu wa
Rais wa Muungano ilifutwa baada ya mabadilko ya 11 ya Katiba Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania kufuatia kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka
1992 na kuanzishwa nafasi ya mgombea mweza kuwa makamu wa rais wa
mungano
Kwa mujibu wa Ibara ya 54 (1) ya Katiba
ya muungano, Rais wa Zanzibar anakuwa mjumbe wa Baraza la Mawaziri
katika serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment