Tuesday 15 November 2011

Mwakilishi ahoji Rais wa Zanzibar kuapa Baraza la Mawaziri

15th November 2011

Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania, (UWT) Asha Bakari Makame, amesema hajafurahishwa na Rais wa Zanzibar kula kiapo kuwa Waziri asiyekuwa na Wizara maalum katika Baraza la Mawaziri la Muungano.
Aliyasema hayo wakati akichangia muswada wa mabadiliko ya Katiba ya Muungano uliowasilishwa katika semina ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Waziri wa Katiba na Sheria Zanzibar Abubakari Khamis Bakari
“Mheshimiwa Mwenyekiti sijafurahishwa Rais wetu kuapishwa kuwa Waziri asiyekuwa na wizara maalum na lazima hilo liangaliwe upya katika Katiba mpya,” alisema Asha ambaye ni mwanasiasa mkongwe Zanzibar.
Alisema wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wana dhamana kubwa ya kutetea maslahi ya nchi na kuwataka wajiamini hasa katika kutetea maslahi ya Zanzibar katika kuelekea mchakato wa kupata Katiba mpya ya muungano
Hata hivyo Waziri wa Kilimo na Maliasili Zanzibar, Mansoor Yussuf Himid, alisema kuwa, Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, hastahili kulaumiwa kwa sababu ametekeleza matakwa ya Katiba na jambo hilo limeanza kabla ya uongozi wake.
“Rais tusimlaumu kwa jambo alilolikuta, kama hatutaki tuliondoshe na wakati wake ndio huu” alisema Mansoor.
Hata hivyo, alisema kwamba muswada wa kuweka utaratibu wa mabadiliko ya Katiba baada ya kupitishwa na bunge, lazima pia upitishwe na Baraza la Wawakilishi kabla ya kuanza kutekelezwa kwa sheria hiyo.
“Tusije kukubali muswada kupitishwa bungeni iwe mwisho, lazima uletwe Baraza la Wawakilishi kabla ya kuanza utekelezaji wake” alisema Mansoor ambaye pia mweka Hazina CCM Zanzibar.
Nafasi ya Rais wa Zanzibar kuwa Makamu wa Rais wa Muungano ilifutwa baada ya mabadilko ya 11 ya Katiba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufuatia kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992 na kuanzishwa nafasi ya mgombea mweza kuwa makamu wa rais wa mungano
Kwa mujibu wa Ibara ya 54 (1) ya Katiba ya muungano, Rais wa Zanzibar anakuwa mjumbe wa Baraza la Mawaziri katika serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment