Saturday 26 November 2011

Utozaji ushuru mara mbili Bara, Z`bar waondolewa

26th November 2011
 
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), imewataka wafanyabaisha kutoka pande mbili za Muungano kuchangamkia biashara mbalimbali kwa kuwa kikwazo cha kulipa ushuru mara mbili kimeondolewa.
Awali, wafanyabiashara walikuwa wakilalamikia hatua ya TRA kuwatoza ushuru wanaponunua bidhaa Zanzibar na pia zinapofika Tanzania Bara zinatozwa tena.
Hayo yalisemwa jana jijini Dar es Salaam, na Ofisa Mkuu wa Elimu kwa Walipa Kodi Kanda ya Mashariki, Hamisi Lupenja, alipozungumza na waandishi wa habari.
Lupenja alisema ushuru huo uliondolewa kufuatia mapendekezo ya kamati maalum iliyoundwa na Rais Jakaya Kikwete, kwa ajili ya kushughulikia kero za Muungano.
Alisema hivi sasa ushuru unalipwa kwa upande mmoja tu wa Muungano kwa bidhaa mbalimbali tofauti na ilivyokuwa siku za nyuma, ambapo mfanyabiashara alikuwa akilipa Zanzibar na akifika Tanzania Bara analipa tena.
Lupenja alisema mpango huo umekwisha kuanza ingawa hakusema ulianza lini, lakini alikiri kuwa kwa sasa kuna unafuu kwa wafanyabiashara wa pande mbili za Muungano.
Wakati huo huo, TRA imeanzisha mpango wa kutoa elimu kwa wafanyabiashara wenye ulemavu wa kuona (vipofu), kwa lengo la kuongeza wigo wa ulipaji kodi kwa hiari.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment