Waziri
wa Katiba na Sheria wa Zanzibar, Abubakar Khamis Bakary, amesema
Zanzibar haitachagia gharama za kufanikisha mchakato wa kupata Katiba
Mpya ya Tanzania.
Abubakary alisema hayo wakati anafunga
mjadala kuhusu katiba mpya katika kongamano lililofanyika katika ukumbi
wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo mjini hapa jana.
Alisema gharama zote za kufanikisha
upatikanaji wa katiba mpya zitabebwa na Serikali ya Muungano ikiwemo
vifaa, malipo ya makamishina wa Tume, Wajumbe wa Bunge la Katiba na
watendaji wa tume.
“Mfuko wa Fedha wa Muungano ndiyo utatumika kufanikisha kazi zote na sie Zanzibar ndio tumenufaika zaidi katika hilo,” alisema.
Hata hivyo, hakutaja kiasi cha fedha
ambacho kinatarajiwa kutumika kama gharama za kufanikisha upatikanaji wa
katiba mpya ambayo inatakiwa kuwa imekamilika kabla ya Uchaguzi Mkuu wa
mwaka 2015.
Waziri Abubakary alisema wabunge na
wajumbe wa Baraza la Wawakilishi watakuwa sehemu ya Bunge la Katiba
pamoja wajumbe 116 ambao watatoka katika asasi za kiraia Tanzania Bara
na Zanzibar.
Kuhusu kero za Muungano, Waziri huyo
alisema wananchi watumie fursa hiyo kutoa maoni yao juu ya mambo ya
msingi ya kuzingatiwa katika mabadiliko ya Muungano.
Alisema zipo kero za Muungano na kutoa mfano kwamba wapo mabalozi wa Tanzania nje ya nchi 30, lakini Wazanzibari ni watatu tu.
Waziri huyo alisema katiba ni mali ya
wananchi na itajengwa na wananchi wenyewe na ndiyo maana serikali
imeamua kuwapa nafasi wananchi ya kutoa maoni kabla ya kuandikwa upya
kwa katiba hiyo.
Kuhusu urasimu wa upatikanaji wa
Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi, alisema wapo watendaji wa SMZ
wamekuwa wakifanya vitendo hivyo kwa makusudi kwa malengo ya kutaka
kuchafua hali ya kisiasa ya Zanzibar
Hata hivyo alisema Serikali ya Umoja wa
kitaifa ipo macho na haitokubali kuona Wazanzibari wananyimwa haki ya
kupinga kura ya maoni kwa kukosa Vitambulisho hivyo.
Viongozi wengine waliyoshiriki katika
mjadala huo ni Waziri wa Afya, Juma Duni Haji; Waziri Asiye na Wizara
Maalum, Haji Faki Shaari; Naibu Waziri wa Afya, Dk. Sira Ubwa Mamboya;
Mrajisi Mkuu wa Serikali, Abdallah Waziri na viongozi wa vyama vya siasa
Zanzibar.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment