Tuesday 19 November 2013

CUF YAKIRI DK SHEIN NDIYE MSEMAJI WA SMZ

Mwinyi Sadallah – Zanzibar
CHAMA cha Wananchi (CUF), kimesema kinaunga mkono kauli ya Rais wa Zanzibar Dk Ali Mohamed Shein kuwa yeye ndiye msemaji wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, na yaliyosemwa na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad ni mtazamo wake binafsi, kama kiongozi wa kisiasa. Msimamo huo umewekwa wazi na Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar, Hamad Masoud Hamad katika mahojiano maalumu na Gazeti la Mwananchi, Mtendeni mjini Unguja jana. Hatua hiyo ya Hamad imekuja siku chache baada ya Rais wa Zanzibar, Dk Shein kuwaambia waandishi wa habari kuwa hakuna mwenye mamlaka ya kuizungumzia Zanzibar, isipokuwa yeye. Hamad alisema Makamu wa Kwanza wa Rais anapozungumza na kutoa msimamo wake juu ya mambo ya Muungano na siasa, hufanya hivyo kama kiongozi wa CUF ndiyo maana hutumia jukwaa la kisiasa kuzungumza na wafuasi pamoja na wanachama wa chama hicho:
“Rais wa Zanzibar ndiye msemaji wa Serikali na kiongozi mkuu, lakini Makamu wa Kwanza anapozungumza katika jukwaa na wafuasi wake, hutoa msimamo wa chama chake kama kiongozi wa juu,” alisema Hamad. Maelezo hayo ya Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar, yamekuja kufuatia tofauti ya kimtazamo na kimsimamo iliyojitokeza kuhusu ni nani mwenye mamlaka ya kuizungumzia Zanzibar. Akizungumzia tathmini yake ya miaka mitatu ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar (SUK), Hamad alisema kimsingi imefanikiwa kudumisha amani na kuondoa mivutano ya kisiasa na malumbano yaliyochangia kurudisha nyuma maendeleo ya Zanzibar. Hata hivyo, alisema muundo wa SUK unahitaji kuangaliwa upya kwa ngazi ya watendaji na viongozi wa kisiasa ili kuleta taswira ya umoja wa kitaifa. Mawaziri na Naibu Mawaziri, wanafanya kazi kwa ushirikiano, lakini watendaji wakuu wa SUK bado wameshindwa kutekeleza majukumu yao na kuendeleza baadhi ya vitendo vinavyowanyima haki wananchi. Alisema haikuwa mwafaka muundo wa SUK kuhusisha mawaziri na naibu wao, bila ya kuangalia nafasi nyingine za watendaji wakuu wa Serikali wakati wa marekebisho ya 10 ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984. 
Alisema pamoja na rais kuzungumzia mwelekeo wa kuimarika na kukua kwa uchumi wa Zanzibar, bado hali ya vipato kwa wananchi wa kawaida ni duni kutokana na kuanguka kwa sekta ya viwanda na kuzorota kwa uzalishaji wa ndani.Hamad alisema sekta za uwekezaji, viwanda, mifugo na uvuvi lazima zipewe kipaumbele ili lengo la kuwapatia maisha bora wananchi, liweze kufikiwa.
Chanzo: Mwananchi

Saturday 17 August 2013

MWANASHERIA MKUU SMZ ” SERIKALI 2 NI KUVUNJA MUUNGANO

Na Salim Salim
Mwanaseria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi wa Zanzibar leo amesema lengo la kuandikwa kwa Katiba Mpya si kuyafanyia Marekebisho katiba iliyokuwepo sasa bali ni kandika Katiba Mpya katiba ambayo itakuwa Muarubaini kwa kero za Muungano na Muungano wenyewe. Mwanaseheria Mkuu liyasema hayo leo asubuhi alipokwa akifunguwa Baraza la Katiba la Vyuo Vikuu liliondaliwa na ZAHILFE Shirikisho la Wanafunzi wa Vyuo Vikuu Zanzibar liliofanyika katika Ukumbi wa Salama Hal Bwawani.
Alilisifu Baraza hilo na kusema kuwa ni Baraza la Vijana wasome na kuwasifu Vijana kwa ile sifa yao kubwa ya kuleta mapinduzi katika jamii yeyote.Alimtaja kijana Sir King ndie waliosababisha Zanzibar iiteme Tanganyika mwaka 1895 Ogast na Tanganyika kuangukia katika mikono wa Wajerumani. Na kumtaja Gerald Pota alietumwa na Waingereza kuja kuunda Serikali na kumpangia Mfalme mshahara ambako alikuwa akilipwa paund 250 kwa mwaka. Msingi wa Muungano wa Tanzania ni kuungana kwa Nchi mbili huru Tanganyika na Zanzibar lengo la kuungana kwa nchi mbili hizi ni kufanya mambo yao pamoja na kupata faida zaidi na sio Nchi moja kuitawala Nchi nyengine alisema, hukua akiendela kusema:
Zanzibar si mkowa wala wilaya, Zanzibar ni Nchi, katika Muungano tulikubaliana baadhi ya mambo kufanya pamoja na sio Zanzibar kuwa Jimbo la Tnganyika. Alisema duniani kuna miungano mingi mizuri akiutolea mfano Muungano wa Uswis ambao una Serikali 24 na ule wa Muungano wa Maerkali wenye Serikali 52 na kusema kuwa ni uongo kuwa Serikali Tatu zitavunja Muungano na kusema Serikali Mbili ndizo zitakazovunja Muungano, na hata Muungano wa Serikali Tatu ukivunjika si kioja. Serikali Tatu hazitovunja Muungano Serikali Mbili ndizo zitakazo vunja Muungano. Alisema Uruhani wa Serikali ya Tanganyika ndio kero kubwa ya Muungano na Serikali tatu itairudisha Serikali ya Tanganyika ambako kero kubwa itakuwa ishatatuliwa.
Aliitaja Sheria ya Kuanzishwa na Bank Kuu ya Tanzania kuwa aliisaini Karume mwenyewe lakini Karume alipoona mapungufu ya Seria hiyo ndio maana akaanzisha PBZ. Aidha alisema kama Zanzibar inataka kuishtaki TFF itashinda na TFF haitokuwemo FIFA kwani TFF haiwakilishi Tanzania kama ilivyokuwa ZFA ilivyokuwa haiwakilishi Tanzania. Hivi hatuoni haya kubakia hivi hivi kuwa Manispaa wakati Zanzibar ilikuwa Empire alihoji Mwanasheria Mkuu na kuendelea kusema hivi tutamuamini vipi mtu ambae leo anasema Zanzibar si Nchi atakapokuwa Rais wa Tanzania ambao Zanzibar haitokuwa na Mamlaka atasema Zanzibar ni jimbo la Tanganyika na kumalizia kusema wengi wa Watanganyika wanachuki na Zanzibar. Aliwataka wanafunzi hao kuzungumzia mambo ya Muungano na kutaka kuwe na usawa “Bila ya kuwa na usawa katika Mungano huu huo si Muungano bali ni ukoloni” alisema, na kutaka kuwe na mfumo wa usawa katika Baraza la Mawaziri na Bunge na kuwe na makubaliano ya thuluthi mbili kila upande katika kupitisha sheria na kuengezwa au kupunguzwa mambo ya Muungano.
Alisema katika Muungano wa Serikali Tatu ni lazima Rasilimali zitumike kwa Usawa na sio kama hivi sasa Tanganyika inavyotumia Rasilimali za Muungano wao peke yao katika kusoma na kuinyima Zanzibar. Tume ya Pamoja ya Fedha haijaanza kazi mpaka leo, na katika Muungano kuna mapato ya Muungano na Matumizi ya Muungano na Mapato ya Muungano siku zote huwa mengi ambako Tnganyika hawataki tugawane. Alisema si kweli kama Muungano wa Serikali tatu una harama bali Muungano wa Serikali Mbili ndio wenye gharama na Zanzibar ndio inaharamika zaidi, aliwataka viongozi wawe wakweli na waache kuwapotosha wananchi. Aliwaonya Wazanzibar kuwacha kulumbana na badala yake kukaa pamoja kuidai nchi yao. Alisema Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliundwa ili kuondowa tofauti kwa Wazanibar na kusema kuwa kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa ni kuala gumu kuliko mabadiliko ya Muungano. Alisema Wanaotaka Seriakali Mbili hoja zao hazina msingi na hakuna haja ya kubakia kwenye Serikali mbili na wengi wanaotaka Serikali Mbili wanalinda maslahi yao ya kidunia.
Hoja yangu nawataka wanaotaka Serikali Mbili na Wanaotaka Mkataba wakae pamoja wajadiliano Mfumo wa Muungano wa Serikali Tatu mfumo ambao utakuwa na Mslahi na Zanzibar. Awali Mwenyekiti wa ZAHILFE alikanusha taasisi yake kuandaa kungamano la tarehe 6 mwezi wa 7 lililofanyika Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kingeni na badala yake kongamano hilo liliandaliwa na Mkowa wa Wanafunzi wa Vyuo Vikuu vywa CCM na kusema Taasisi yake haina mafungamano na chama chochote cha siasa. Kongamano hilo lilianza na Wimbo wa Taifa wa Zanzibar na lilihudhuriwa na baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi. Marais 10 wa Serikali za Wanafunzi waliochangia katika Kongamano hilo walitaka Zanzibar yenye Mamlaka Kamili na Usawa Katika Muungano.
Chanzo: habari leo

Friday 26 July 2013

Muungano wa Tanzania au Tanganyika na Zanzibar?

KWA mujibu wa Mkataba wa Muungano, uliotiwa sahihi Aprili 22, 1964, kati ya Mwalimu Julius Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume, na kwa mujibu pia wa Sheria ya Muungano, Namba 22 ya 1964, iliiyoridhia Mkataba huo na kuupa nguvu ya Kisheria na kutumika nchini, jina sahihi la Muungano limetajwa kama:
Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, kuanzia siku ya Muungano na baada ya hapo, zitaungana kuwa Jamhuri moja kwa jina la Jamhuri ya Tanganyika na Zanzibar.
Kufikia hapo, wengi wanaweza kujiuliza; kama hapajawa na Muungano mwingine, jina hili la ‘Muungano wa Tanzania’ linatoka wapi? Na kama jina Tanzania limebuniwa baada ya Muungano, ina maana kwamba katika kipindi cha Muungano tangu ulipotiwa sahihi hadi kubuniwa kwa ‘Tanzania,’ hapakuwa na Muungano? Marekebisho yapi yalifanyika kufikia ‘Tanzania’ badala ya ‘Tanganyika na Zanzibar’? Na kwa nini?
Haya ni maswali mepesi, lakini yenye utata kwa Mtanzania yeyote yule. Yana utata kwa sababu historia ya Muungano, haijaandikwa itakiwavyo na kuwekwa wazi. 
Watanzania wamekuwa wakipewa tafsiri za kisiasa, nyepesi na za majukwaani. Na kwa kuwa ilikuwa ni dhambi kuu kuhoji juu ya Muungano wala kutoa maoni juu ya muundo na aina gani ya Muungano uliokusudiwa, Watanzania wameishi kwa kuuchukulia Muungano huo kama ‘fumbo la imani’ tu, huku kero za Muungano zikichipuka kama uyoga kwenye shamba lenye rutuba lililotelekezwa.
Jina la Muungano huu limetajwa kwenye Sheria ya Muungano Namba 22 ya mwaka 1964, kifungu cha 4, kuwa ni “Jamhuri ya Tanganyika na Zanzibar” (URTZ), kuanzia siku ya Muungano na baada ya hapo.
Wakati nchi mbili hizi zikiungana hapakuwa na Katiba iliyoandaliwa kusimamia Muungano. Kwa hiyo, ilikubaliwa kwamba katika kipindi cha mpito (wakati Muungano huo ukiandaliwa Katiba yake), Katiba ya Jamhuri ya Tanganyika itumike (na ilitumika) pia kama Katiba ya Muungano kwa kufanyiwa marekebisho kuingiza yale mambo 11 yaliyopitishwa kushughulikiwa na Serikali ya Muungano na kuwapo kwa Serikali ya Zanzibar (Sheria ya Muungano-Kifungu cha 5).
Mambo hayo ni Katiba na Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Mambo ya Nje, Ulinzi, Polisi, Mamlaka juu ya hali ya hatari na Uraia. Mengine ni Uhamiaji, Biashara ya Nje na Mikopo, Utumishi wa Jamhuri ya Muungano, Kodi na Ushuru wa Forodha, na mwisho, Bandari, ndege za kiraia, Posta na simu za maandishi (telegraph).
Itakumbukwa kwamba Zanzibar haikuwa na Katiba yake wakati Muungano unafanyika, hadi mwaka 1984. Lakini Zanzibar ilikuwa na Sheria zake zitokanazo na maagizo ya Rais (Decrees).
Kwa hiyo, kwa kutambua kwamba Serikali za Tanganyika na Zanzibar hazikufa baada ya Muungano, iliwekwa bayana kuwa Sheria za Tanganyika na zile za Zanzibar, zitaendelea kutumika katika nchi hizo (Kifungu 8 cha Sheria ya Muungano na Ibara ya 5 ya Mkataba wa Muungano), bila kuingilia au kuingiliwa na shughuli za Serikali ya Muungano.
Ndiyo kusema kwamba Muungano wa Tanganyika na Zanzibar (URTZ), uliundwa kwa ajili ya, na ili kushughulikia mambo 11 tu ya kila nchi, wakati ule, ambapo Serikali za Tanganyika na Zanzibar zilibakia hai kuendelea kushughulikia mambo mengine yote yasiyo ya Muungano katika maeneo yake, huku Katiba ya Tanganyika ikiendelea kutumika kama Katiba ya Muungano pia.
Jamhuri ya Muungano ilitakiwa kuwa na Katiba yake katika muda wa miezi 12 iliyofuata kuanzia Aprili 26, 1964, yaani kufikia Machi 26, 1965, kwa mujibu wa Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano; lakini haikuwa hivyo.
Ilipofika Machi 24, 1965, Bunge lilipitisha Sheria Namba 18 ya mwaka 1965 kuongeza muda wa kuitisha Bunge la Katiba “hadi hapo itakapoonekana vyema kufanya hivyo.”
Kuongezwa kwa muda wa kuitisha Bunge la Katiba, kulimaanisha kuchelewa kupatikana kwa Katiba halali ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kama ilivyotakiwa chini ya Mkataba na Sheria ya Muungano ya 1964.
Ili kuokoa Muungano huo usiendelee kuchangia Katiba na Serikali ya Tanganyika, Julai 10, 1965, Bunge lilipitisha Katiba ya Muda (Sheria No. 43 ya 1965) ya Tanzania, iliyotambua kuwa “Tanzania ni Jamhuri ya Muungano” (Ibara ya 1) inayoundwa na Tanganyika na Zanzibar (Ibara ya 2), na kwamba kutakuwa na Chama kimoja cha siasa Tanzania (Ibara ya 3); lakini hadi hapo TANU na ASP vitakapoungana, Chama cha siasa kwa Tanganyika kitakuwa “The Tanganyika African National Union (TANU), na kwa Zanzibar, kitakuwa “Afro-Shirazi Party” (ASP).
Hapa, Katiba ilijikanganya. Kulikuwa na Chama kimoja vipi Tanzania wakati kulikuwa na TANU na ASP?
Hapo ndipo jina la “Tanzania” lilipoanza kuonekana katika ‘Katiba ya Muungano’ na kuleta mgongano kati yake na jina asilia la Muungano huo linalotambulika katika Mkataba wa Muungano, na katika Sheria ya Muungano ya 1964.
Ifahamike kwamba vyama vya siasa havikuwa na havijawa jambo la Muungano. Kwa hiyo, kwa kuingiza vyama vya siasa katika suala la Muungano, Katiba ya Muda ya 1965, ilikuwa imekiuka Mkataba/Sheria ya Muungano.
Utata huu unazua maswali pia juu ya uhalali wa Tume ya Vyama vya TANU na ASP, iliyoteuliwa kuandaa mapendekezo ya Katiba ya kudumu ya mwaka 1977. Ni kuingizwa kwa vyama vya siasa katika muundo wa Muungano kulikozua, na kunaendelea kuzua, mitafaruku na kero ndani ya Muungano hadi sasa.
Lakini kwanini haya yaliruhusiwa kuingia katika Katiba wakati kulikuwa na Wanasheria wenye elimu nzuri na uelewa wa juu katika kuutahadharisha Uongozi? Au ni kwa sababu ya wanasiasa wasioambilika?
Ni vyema nikumbushe pia kwamba Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano, ndivyo msingi mkuu wa Katiba ya Muungano, vinginevyo hakuna Katiba ya Muungano wala ya Zanzibar, na hivyo, hakuna Muungano.
Wala Bunge la kawaida la Muungano halina mamlaka ya kurekebisha Mkataba/Sheria ya Muungano, au kuongeza ambacho hakikukusudiwa au kutajwa katika Mkataba wa Muungano. Hadi sasa, Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano vinasomeka kama vilivyopitishwa mwaka 1964, lakini Katiba imeendelea kugeuzwa na kurekebishwa kwa matashi ya wanasiasa.
Hapa maswali yafuatayo yanajitokeza. Jina ‘Tanzania’ lilitoka wapi, na liliingiaje katika msamiati wa Katiba ya Muungano? Je; kutumika kwa jina hilo kunabatilisha jina asilia la ‘Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar?’ Kama halibatilishi, nini suluhisho la mgongano huu?
Ilikuwa hivi: Miezi mitatu baada ya Tanganyika na Zanzibar kuungana, lilitangazwa shindano la kubuni jina litakalowakilisha hadhi na kuwapo kwa Muungano wa nchi hizi mbili. Mshindi aliahidiwa zawadi ya pauni 10 za Uingereza, sawa na Shilingi 20/= za wakati ule za Tanzania.
Kamati ndogo ya Baraza la Mawaziri iliteuliwa kupokea na kuchambua maoni ya washindani 1,534 yaliyopokelewa na kuwasilisha machache (idadi haifahamiki) kwenye Baraza la Mawaziri kwa uamuzi wa mwisho. Maoni yalipokelewa kutoka ndani na nje ya nchi, zikiwamo Urusi, Uingereza, Sweden, Uchina, Ufaransa, Poland, Italia na Australia.
Katika mkutano na Waandishi wa Habari, Ikulu, Oktoba 29, mwaka 1964, Rais Julius Nyerere alitangaza kwamba Baraza la Mawaziri limechagua jina ‘Tanzania’ kuwakilisha Jamhuri ya Muungano, lakini hakutaja jina la mshindi ambaye hajajulikana hadi leo. 
Aliwafundisha pia namna ya kulitamka jina jipya, kwamba ni ‘Tan-Zan-ia,’ na si ‘Tanzania’ kama inavyotamkwa sasa. Tan-zan-ia ni kifupisho chenye kumaanisha Tan – Tanganyika na Zan – Zanzibar, ambapo herufi– ‘ia’ kukamilisha Tan-zan-ia, zimetoka Zanzibar (i) na Tanganyika (a). Kati ya majina manne yaliyochuana hadi mwisho na ‘Tan-Zan-ia,’ ni pamoja na ‘Tanzan,’  ‘Tangibar’ na ‘Zantan.’
Hapa ifahamike kwamba, jina hili ‘Tan-Zan-ia,’  mbali na kuzua mgongano na jina la Muungano (URTZ) kwa mujibu wa Mkataba na Sheria ya Muungano, lilikusudia kuwakilisha jina la ‘Muungano’ na mambo ya Muungano tu, lakini halikufuta, na hatudhani kwamba lilikusudia kufanya hivyo, muundo wa Muungano uliokusudiwa, wala kufuta Serikali ya Tanganyika na Zanzibar na mamlaka zake, kama tulivyoelezea hapo mwanzo.
Kuonyesha kwamba Tanganyika ilikuwa na hadi sasa ni hai, Katiba ya mwaka 1965 kwa mfano, Ibara ya 12, ilitambua Rais wa Jamhuri ya Muungano kuwa pia ndiye Rais wa Tanganyika, chini ya Katiba ya Muda.
Nayo Ibara ya 13 (1) ilitambua kuwa na Makamu wawili wa Rais, mmoja (wa pili) akiwa Msaidizi wa Rais kwa mambo ya Muungano nchini Tanganyika.
Ibara ya 20 ilimpa Rais mamlaka ya kuteua Mkuu wa Mkoa kwa kila Mkoa nchini Tanganyika, ambapo Ibara ya 25 ilizungumzia kuhusu Tanganyika kuwa na majimbo ya uchaguzi; na mifano mingine mingi.
Wataalamu wa mambo ya Sheria na Katiba bado wanahoji, kama Bunge la kawaida lililobadili jina la Muungano lilikuwa na mamlaka au uwezo wa kufanya hivyo kisheria.
Katiba ya Muda ya 1965 ilibainisha wazi kuwa Muungano wa ‘Tanzania’ unaundwa na Tanganyika na Zanzibar kwa maana ya kutambua kuwako kwa nchi hizi mbili.
Lakini Katiba ya 1977 inataja kuwa Muungano huo unaundwa na ‘Tanzania Bara’ na ‘Tanzania Zanzibar,’ kwa maana ya majina hayo kuchukua nafasi ya majina ya Tanganyika na Zanzibar.”
Kama lilivyo jina la ‘Tanzania,’ majina ya ‘Tanzania Bara’ na ‘Tanzania Zanzibar’ hayajulikani katika Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano ambayo haijabadilika hadi leo.
Nini athari ya mgongano huu na uhalali wa mabadiliko haya kwa Mkataba/Sheria ya Muungano? Je; Bunge la Katiba lililopitisha Katiba hiyo, ndilo lile la aina ya lililotakiwa chini ya Mkataba na Sheria ya Muungano? Je; Serikali ya Muungano ina mamlaka na uwezo wa kubadili (majina) yaliyomo katika Mkataba uliyoiunda? Je; yai laweza kumbadili kuku?
Kupata majibu ya maswali haya, hatuna budi kufanya rejea kwa ufupi tu, mchakato mzima wa Katiba tatu za Muungano zilizopita ili kuona utata ulipo.
Hakuna ubishi kwamba Mkataba wa Muungano (Articles of Union) wa 1964, na Katiba ya muda (Interim Constitution) ya 1964 na ile ya 1965, zilitambua kuwapo kwa Serikali ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Serikali ya Tanganyika na Serikali ya Zanzibar zikiwa na mamlaka kamili kuhusu mambo ya nchi yasiyo ya Muungano.
Ilikubaliwa pia kwamba iandaliwe Katiba ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa utaratibu uliowekwa, na ipatikane ndani ya mwaka mmoja tangu siku ya Muungano; na kwamba wakati hilo likifanyika, Katiba ya Tanganyika itumike pia kama Katiba ya Tanganyika, na hapo hapo kama Katiba ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa kufanyiwa marekebisho kutambua kuwapo kwa Serikali ya Zanzibar, kama ilivyokuwa kwa Serikali ya Tanganyika.
Tatizo lilianza na Katiba ya Muda ya mwaka 1965, ambayo, chini ya Ibara ya 12 (1), ilibainisha kwamba “Mamlaka ya Utendaji (the Executive) kuhusu mambo yote ya Muungano, katika, na kwa ajili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, na (pia) kwa (Serikali ya) Tanganyika, yatakuwa kwa Rais wa Serikali ya Muungano.”
Kwa maana hii, Rais wa Kwanza wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Mwalimu Julius Nyerere alikuwa wakati huo huo Rais wa Tanganyika pia.  Ingekuwa vivyo hivyo, kama Rais Abeid Karume wa Zanzibar angeteuliwa kuwa Rais wa Kwanza wa Muungano, kwamba angesimamia Serikali ya Muungano na Serikali ya Tanganyika, kwanza kama Rais wa Muungano, na pia angesimamia Serikali ya Zanzibar kama Rais wa Zanzibar. 
Huu ulikuwa ni mpangilio wa muda kusubiri kuandikwa kwa Katiba ya Muungano ambapo madaraka na mamlaka hayo yangetenganishwa kwa kuzingatia Mkataba wa Muungano.
Utata huu ulizidishwa na Ibara ya 49 ya Katiba hiyo iliyoweka wazi kwamba mamlaka ya kutunga Sheria kuhusu mambo yote ya Muungano katika na kwa ajili ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, na kwa mambo yote katika na kwa ajili ya Serikali ya Tanganyika, ni ya Bunge la Muungano.
Hii ilimaanisha sasa kwamba Rais wa Muungano ndiye aliyekuwa Rais wa Tanganyika, na Bunge la Muungano ndilo lililokuwa Bunge la Tanganyika pia.
Kama tunaweza kuufananisha Muungano huu na taasisi mbili zilizokubaliana kuunda ubia (Jamhuri) kwa njia ya hisa zilizo sawa (tuseme hisa 11 kila moja, kama yalivyokuwa mambo ya Muungano), basi Tanganyika imetoa kila ilicho nacho juu na zaidi ya hisa ilizopaswa kuchangia katika Muungano, tofauti na matakwa ya Mkataba.
Na kwa kuwa mchango huo wa ziada hautambuliki katika hati zote za kuanzisha Ubia huo, basi, inakuwa imetoa kwa hiari na haiwezi kuongezewa gawio wala kuwa na sauti na kauli katika Ubia huo kwa hicho cha ziada.  Kufanya hivyo ni kuhodhi mamlaka ya Muungano ambako Wazanzibari wanaita ‘kumezwa kwa Zanzibar.’
Lakini kwa upande wa Zanzibar, mamlaka ya utendaji kwa Serikali ya Zanzibar, kwa mambo yasiyo ya Muungano, yalibakia kwa Rais wa Zanzibar.  Vivyo hivyo, mamlaka ya kutunga Sheria kwa mambo yasiyo ya Muungano, yalibaki kwa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.
Hapo ndipo Bunge na jina la Tanganyika lilianza kupotea kimiujiza, wakati jina la mdau wa pili, Zanzibar, likaendelea kudumu, na wakati huo huo Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano, ziliendelea, na zinaendelea kuutambua Muungano kwa jina la Tanganyika na Zanzibar.
Nyundo ya chuma ilipigiliwa kichwani mwa Tanganyika, pale Sheria Na. 24 ya mwaka 1967 ilipotungwa kumpa Rais uwezo wa kuweka neno ‘Tanzania’ badala ya neno ‘Tanganyika’ katika maandishi na nyaraka zote za kisheria, lakini haikubadili majina hayo katika Hati ya Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano.
Mabadiliko yote haya, kwa kuanzia na Katiba ya Muda ya mwaka 1965, ndiyo yaliyorithiwa bila utafiti makini na kuingizwa katika Katiba ya Kudumu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977.
Ni kutokana na mabadiliko hayo, yanayofanya watu wafikirie na kuamini kwamba Tanzania ndiyo Tanganyika, na Tanganyika ndiyo Tanzania; wakati si kweli.   Na hii ndiyo dhana potofu ya Serikali mbili – Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar.
Chanzo: Raia Mwema

Thursday 25 July 2013

Wanasiasa Z’bar na propaganda dhaifu

Leo nalazimika kuandika makala haya kwa mshangao mkubwa wa baadhi ya wanasiasa hapa Zanzibar kutengeneza taswira ambayo haikubaliki wala kuendana na wakati tulionao.
Kuna baadhi ya wanasiasa wanatumia propaganda dhaifu kwamba wanaodai mabadiliko katika muundo wa Muungano wanataka kumrejesha Sultan!
Hii ni ajabu ya mwisho, pia ni aibu kusikia kauli kama hizo baada ya takriban miaka hamsini ya kujitawala.
Inafahamika vizuri kwamba Zanzibar ni nchi kamili na watu wake waliamua kujitawala wenyewe kupitia mapinduzi yaliyoung’oa utawala kisultan Januari 1964 na Aprili mwaka huu Jamhuri ya watu wa Zanzibar ikaungana  na Jamhuri ya Tanganyika kuunda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 Sultan wa mwisho kutawala Zanzibar ni Jamshid bin Abdullah Al Said ambaye kwa sasa anaishi Portsmouth, Uingereza akiwa na umri wa miaka 83.
Hakuna anayemtambua katika medani za kisiasa kwa Zanzibar ya leo zaidi ya kubaki katika vitabu vya kihistoria tu, lakini kizazi hiki kinachojali ni nchi yao iliyo huru ambayo ilikombolewa kutoka kwa wakoloni.
Umezuka mtindo kwa wasiokuwa na nguvu ya hoja kudai eti kuna watu vibaraka wa Sultan, ndiyo maana wanadai mabadiliko katika Muungano!
Huu ni uzushi na uongo usiokuwa na hata chembe ya ukweli, wananchi wa Zanzibari chini ya Afro Shiraz Party ndio waliompindua Sultan na kuirejesha nchi yao mikononi mwa wazalendo ambao ni wakwezi na wakulima; iweje leo miaka 49 tukijiandaa kuadhimisha jubilee ya miaka 50 ya Mapinduzi watamani kutawaliwa tena?
Kama leo itapigwa kura, kuulizwa nani kati ya Abeid Amani Karume na Sultan Jamshid anayefahamika, jawabu lisilokuwa na hata chembe ya shaka ni Karume. Sultan hana mlango wa kuingilia Zanzibar.
Kabla ya Mapinduzi, Zanzibar haikuwa Jamhuri, ilikuwa chini ya Sultan, lakini Mapinduzi ya umma ndio yaliyoifanya Zanzibar kuwa Jamhuri.
Umoja wa Mataifa uliyatambua Mapinduzi hayo kuwa ni halali na uliokuwa Umoja wa nchi huru za Afrika (OAU) uliyatambua pia.
Sheria na mikataba ya kimataifa haitoi nafasi kwa Sultan kujipenyeza Zanzibar na wala hicho kiti chake huko UN hakipo, kilibiruka mwaka 1964. Kwa hiyo msipoteze muda kwa propaganda mfu na zisizokuwa na mashiko.
Vuguvugu la mabadiliko lililoanzia na Mapinduzi ya kule Ufaransa yaliamsha ari na kuwatia shime wazalendo wa Zanzibar kufanya Mapinduzi yaliyosimamiwa na kuratibiwa na ASP.
Athari za Mapinduzi ya Ufaransa zilienea kote duniani na ilipofika Januari 12, 1964, Wazalendo wa Zanzibar chini ya Afro Shiraz Party walirejesha heshima na utu kwa wakulima na wakwezi.
Wazanzibari sasa wanataka mabadiliko, hawatafanya kama wale wa Ufaransa isipokuwa watatumia haki ya kutoa mawazo yao, iwe wanataka Serikali tatu au mbili ni haki yao.
Saa ya mabadiliko imefika, vijana wasiokuwa na ajira, uhakika wa chakula wala kulala wamefikia pahala wanataka kuona mabadiliko ya kweli yanatokea siyo tu katika siasa bali hata katika uchumi na ndiyo maana wengi wanaunga mkono pendekezo la tume ya Jaji Warioba la kuwa na shirikisho.
Ni lazima wanasiasa wetu wafahamu kuwa ulimwengu wa leo, vijana haukubali tena kuburuzwa na mara nyingi vijana wa kileo waliozaliwa katika Teknohama wanaunga mkono siasa yenye uchumi na wanazuoni wanaipima hoja hiyo katika  mizania miwili; mosi, msukumo binafsi wa kijana wa Zanzibar wa uhitaji wa mabadiliko na pili, ni mhemko wa majira.
Mhemko huu ni kama kilevi ambapo kama ukweli ulivyo idadi kubwa ya vijana ndio wanywaji ambao hawatapenda kunywa kilevi kama togwa kisichokuwa na ‘stim’ yoyote kwao.
Demokrasia ya kisasa inalazimisha kuheshimu mawazo ya wengine hata kama huyataki, ndiyo maana watu makini wanaamini kuwa uvumilivu mzuri ni ule unaojiepusha na chuki zisizo na msingi (prejudice).
Hata kama anayetoa maoni au kueleza ni yule msiyeafikiana, au kimaumbile si mzungumzaji mzuri jaribu kuuweka sawa ujumbe wake kwa misingi ya nguvu ya hoja huku ukizingatia alichokizungumza siyo namna alivyozungumza. Mara zote chuki isiyo na msingi huviza mabadiliko.
Ikiwa dhana ya ujana ndio nguvu ya mabadiliko katika jamii, wanaobeza msimamo wa wale wanaotaka Serikali tatu, tumeona namna watu wa Zanzibar na Tanganyika walivyotoa mawazo yao kutaka mabadiliko ya msingi katika muundo wa Muungano.
 Watu wasijadili suala la muundo wa Muungano kwa jazba wala chuki kama ilivyoanza kujitokeza hivi karibuni kwa upande wa Tanganyika ambao wanawachukulia Wazanzibari kama wakorofi.
Hawa wanaokejeli wenzao tunawafahamu ndio masalia ya wanasiasa waliochoka kimawazo, wengine wana joto lao la kushindwa maisha na kukosa vyeo walipokuwa Serikalini, ndio leo wanamalizia hasira zao kwa wale wanaotoa hoja za kudai Muungano wenye usawa baina ya nchi ya Zanzibar na Tanganyika .
Haitawezekana kwa hali yoyote ile wananchi wa Zanzibar walio huru waliokataa kutawaliwa eti baada ya miaka 49 ya Mapinduzi watamani kutawaliwa tena na ukoloni wa Sultan!
Hili ni jambo la kushangaza kuona kwamba katika Afrika hii kuna watu wanamuota Sultan, napenda kuwaeleza kwamba Sultan na watu wake hawana hata chembe ya nafasi katika Zanzibar mpya, wala ya zamani.
Itakumbukwa pia kuwa mara tu baada ya Mapinduzi mwaka 1964, Rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume kama ilivyo kwa Mwalimu Nyerere naye alichukia sana ubaguzi na ndio maana aliongoza kampeni ya ndoa za mchanganyiko wa rangi na makabila mbalimbali hapa Zanzibar.
Mzee Karume hakulazimisha watu kuoana bali aliwataka wazazi wawape watoto wao uhuru wa kuoa na kuolewa na wawapendao. Waarabu hawakutaka mabinti wao waolewe na Waafrika ilhali, na kinyume chake baadhi ya Waafrika walikataa watoto wao kuoa Waarabu.
Chanzo: Mwananchi

Thursday 30 May 2013

MAPENDEKEZO YA KAMATI YA MARIDHIANO ZANZIBAR KUHUSU UPI UWE MWELEKEO WA WAZANZIBARI

MAPENDEKEZO YA KAMATI YA MARIDHIANO ZANZIBAR KUHUSU UPI UWE MWELEKEO WA WAZANZIBARI KATIKA KUIJADILI RASIMU YA KATIBA YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA ITAKAYOTOLEWA NA TUME YA MABADILIKO YA KATIBA
UTANGULIZI:
… Baada ya wananchi wa Zanzibar kutoa maoni yao juu ya vipi Muungano wa Zanzibar na Tanganyika unapaswa kuwa, hatimaye Tume ya Mabadiliko ya Katiba inatarajiwa kutoa rasimu ya awali ya Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kati ya mwishoni mwa mwezi Mei na mwanzoni mwa mwezi Juni 2013.
Wakati tunaisubiri kwa hamu rasimu hiyo itolewe na kujua kilichomo, sisi wajumbe wa Kamati ya Maridhiano Zanzibar tumekaa na kutafakari juu ya upi unapaswa kuwa mwelekeo wa Wazanzibari katika kuijadili rasimu hiyo pale itakapotoka.
Baada ya mashauriano ya kina kati ya wajumbe wa Kamati ya Maridhiano na pia kwa kuwahusisha watu wengine mashuhuri hapa Zanzibar, tumekuja na mapendekezo yafuatayo ambayo leo hii tunayawasilisha kwa wananchi wa Zanzibar kupitia Kongamano hili. Haya si maagizo bali ni mashauri yenu na pindi mkiyakubali basi tutakuombeni tuyafanyie kazi kwa pamoja kwa kuyatumia katika kuipokea na kujadili rasimu pale itakapotolewa.
Mapendekezo yetu ni kama ifuatavyo:
1. Jina la Muungano:
Muungano huu umetokana na Jamhuri mbili kuungana kwa hiyari. Jamhuri hizo ni Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na Jamhuri ya Tanganyika. Jina la awali lililotajwa katika Mkataba wa Muungano la muungano wa jamhuri hizi mbili lilikuwa ni Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Jina hili baadaye mwezi Oktoba 1964 lilibadilishwa na kuitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Ukiangalia mifano ya nchi nyingine zilizoungana, jina la muungano huweka bayana kwamba zilizoungana ni zaidi ya nchi moja, zaidi ya falme moja au zaidi ya jamhuri moja. Kwa mfano, muungano wa nchi (states) za Marekani unaitwa kwa kiingereza United States of America (USA), ule uliokuwa muungano wa jamhuri za kisovieti ukiitwa Union of Soviet Socialist Republics (USSR) na ule muungano wa falme za kiarabu unaitwa United Arab Emirates (UAE).
Ili kuondosha dhana iliyojengeka kwamba muungano wa jamhuri zetu mbili umeunda nchi moja na kuzifuta nchi zetu, Katiba Mpya inapaswa kuweka jina linalotambua msingi huo na historia hiyo. Hivyo basi, jina jipya liwe ni Muungano wa Jamhuri za Tanzania na kwa kiingereza United Republics of Tanzania.
Jina hili litasaidia utambulisho wa nchi wanachama katika uwanja wa kimataifa pale litapoambatanishwa katika nyaraka zote rasmi pamoja na jina la nchi husika. Kwa maana hiyo katika uwanja wa kimataifa na katika pasi za kusafiria utaweka wazi na kuwa na “UNITED REPUBLICS OF TANZANIA – REPUBLIC OF ZANZIBAR” na “UNITED REPUBLICS OF TANZANIA – REPUBLIC OF TANGANYIKA”.
2. Mipaka ya Zanzibar na Tanganyika:
Wakati zinaungana, Zanzibar na Tanganyika zilikuwa tayari ni nchi zenye mamlaka kamili zikiwa ni wanachama wa Umoja wa Mataifa na hivyo kila moja ilikuwa na mipaka yake inayoeleweka. Katiba na sheria za nchi mbili hizi ziliweka bayana mipaka hiyo na mipaka hiyo ilitambuliwa chini ya sheria za kimataifa.
Rasimu ya Katiba Mpya ni lazima itamke kwa uwazi kabisa na kutambua na kuheshimu mipaka ya nchi mbili hizi kama ilivyokuwa kabla ya siku ya Muungano tarehe 26 Aprili, 1964.
Baada ya hapo, Katiba ya Zanzibar na Katiba ya Tanganyika (itakayotungwa baada ya kupata Katiba mpya ya Muungano) kila moja iweke wazi mipaka yake.
3. Uraia:
Uraia ndiyo msingi wa ujananchi. Kwa vyovyote vile Katiba Mpya isijumuishe suala la Uraia kuwa la pamoja kupitia Muungano. Kila nchi mwanachama katika muungano ibakie na uraia wake na iratibu masuala yote yanayohusu uraia wake na raia zake. Kwa kufuata mfano kama wa Muungano wa Ulaya (European Union), unaweza kuwa na haki inayotambulika kikatiba ya uhuru wa raia wa nchi moja mwanachama kwenda katika nchi nyengine mwanachama kupitia utaratibu maalum utakaowekwa (free movement of people). Hata hivyo, kila nchi mwanachama iwe na haki ya kuweka utaratibu wa vipi raia hao watafaidi haki na fursa za nchi mwanachama nyingine.
Hili ni la muhimu hasa kwa nchi ndogo kama Zanzibar ambayo ina rasilimali ndogo ya ardhi na hasa ikizingatiwa kuwa ardhi ilikuwa mojawapo ya sababu kuu za kufanyika Mapinduzi. Katika hali kama hiyo, Zanzibar ina sababu nzito za kuona inadhibiti na kusimamia wenyewe Uraia wake na utambulisho wa raia hao.
Hivyo basi, suala la Uraia lisiwemo katika mambo ya Muungano na badala yake kila nchi isimamie yenyewe masuala ya Uraia.
Hata hivyo, kunaweza kukawepo chombo cha pamoja kinachojumuisha nchi mbili hizi cha kuratibu masuala ya Uraia na haki na fursa ambazo raia wanaweza kuwa nazo kwa kila upande.
4. Uhamiaji:
Kutokana na sababu tulizozitaja hapo juu kuhusiana na suala la Uraia inapelekea wazi kuwa kila nchi mwanachama idhibiti na kusimamia wenyewe mambo ya Uhamiaji. Hivyo basi, rasimu ya Katiba Mpya isijumuishe suala la Uhamiaji kuwa ni suala la Muungano.
Kila nchi mwanachama kati ya Zanzibar na Tanganyika iwe na paspoti yake yenyewe yenye kubeba jina la nchi yake na nembo yake ya Taifa na yenye kudhamini usalama wa raia wake nje ya nchi kupitia uhakikisho unaotolewa na Serikali ya nchi husika.
Ili kuonesha sura ya kuwepo muungano wa kisiasa, paspoti za nchi mbili hizo zinaweza kuwa na jina la Muungano juu na kufuatiwa na jina la nchi mwanachama likiambatana na nembo ya Taifa ya nchi hiyo. Kwa mfano, “UNITED REPUBLICS OF TANZANIA – ZANZIBAR PASSPORT” na “UNITED REPUBLICS OF TANZANIA – TANGANYIKA PASSPORT”.
Kwa upande mwengine kunaweza kukawa na mamlaka ya kuratibu masuala ya uhamiaji wa nchi hizi mbili (Union immigration regulatory authority) kwa lengo la kuweka na kuratibu mfumo mzuri wa mawasiliano kati ya mamlaka za uhamiaji za nchi mbili hizi.
5. Mambo ya Nje:
Mamlaka juu ya mambo ya nje na uwezo wa nchi kuingia mikataba na nchi nyingine na mashirika ya kimataifa ndiyo roho ya nchi yoyote duniani kutambulika kimataifa na kuweza kusimamia mamlaka yake ya ndani yanapohitaji mashirikiano na nchi nyengine.
Ili nchi iweze kutambulika kimataifa inapaswa kuwa na mambo manne yafuatayo:
(a) eneo la ardhi lenye mipaka inayotambulika;
(b) watu wanaoishi kwenye eneo hilo wanaojitambulisha na eneo hilo;
(c) serikali inayotekeleza majukumu yake; na
(d) uwezo wa kuingia katika mahusiano ya kimataifa na nchi nyengine.
Kwa msingi huo, Wazanzibari wanahitaji kuona kuwa Mambo ya Nje haijumuishwi katika orodha ya mambo ya Muungano na badala yake kila nchi isimamie yenyewe mamlaka yake juu ya mambo ya nje.
Hata hivyo, uratibu wa sera ya mambo ya nje (foreign policy coordination) inaweza kuwa ni suala la muungano lakini utekelezaji wake kila nchi ikausimamia kupitia Wizara yake ya Mambo ya Nje. Uratibu wa sera ya mambo ya nje unaweza kufanywa kupitia chombo cha pamoja kitakachoundwa na Wizara za Mambo ya Nje za nchi mbili hizi kwa mfano kuwa na Council on Foreign Policy.
Kutokana na hoja hizo hapo juu inabaki kuwa kila nchi iwe na uanachama na kiti chake katika Umoja wa Mataifa na jumuiya nyengine za kimataifa. Hayo si ajabu katika miungano. Umoja wa Jamhuri za Kisoshalisti za Kisovieti (USSR) ulikuwa na uanachama na kiti chake Umoja wa Mataifa lakini miongoni mwa nchi wanachama, Jamhuri tatu za Ukraine, Belarus na Georgia ziliamua kuwa na uanachama na viti vyao katika Umoja wa Mataifa na hilo liliwezekana.
Kwa msingi huo huo, Zanzibar iwe na uanchama wake katika Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika, Jumuiya ya Madola, Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya SADC na jumuiya nyengine za kikanda na za kimataifa.
6. Sarafu, Benki Kuu, Mikopo na Biashara ya Nchi za Nje, Ushuru wa Forodha, Kodi ya Mapato na Kodi ya Mashirika:
Uchumi si suala la Muungano hata katika Katiba inayotumika sasa. Hata hivyo, nyenzo za kuendeshea na kusimamia uchumi wa nchi kwa maana ya sera za fedha na uchumi (fiscal and monetary policies) zimeendelea kudhibitiwa kupitia Serikali ya Muungano.
Vyombo vikuu vinavyosimamia sera hizo ambavyo ni Benki Kuu (BOT), Mamlaka ya Kodi Tanzania (TRA) na Wizara ya Fedha ya Serikali ya Muungano vimekuwa vikifanya maamuzi na kuyatekeleza bila ya kuzingatia kuwa kwa maumbile uchumi wa Zanzibar ambao ni uchumi unaotegemea utoaji wa huduma (service oriented economy) hauwezi kuwa sawa na uchumi wa Tanganyika ambao unategemea rasilimali (resource based economy). Sera za fedha na uchumi zikiwemo zile zinazohusu udhibiti wa sarafu na viwango vya kodi, ushuru na riba katika mabenki zimekuwa zikitungwa bila ya kuzingatia msingi huo wa chumi mbili zilizo tofauti na badala yake mara zote zimeegemezwa kwenye kulinda maslahi ya uchumi wa Tanganyika.
Sarafu ya pamoja imekuwa ikishuka thamani kwa kasi kila uchao kutokana na sababu nyingi lakini miongoni mwake zaidi zinatokana na uendeshaji mbaya wa uchumi wa Tanganyika. Serikali inapochapisha sarafu zaidi ili kudhibiti mfumko wa bei athari zake zinaikumba pia Zanzibar.
Zanzibar inahitaji kujikomboa kiuchumi ili iweze kutekeleza malengo ya Mapinduzi kwa wananchi wake na hivyo inahitaji kuwa na mamlaka yake kamili katika kusimamia masuala ya sera za fedha na uchumi yakiwemo masuala yote yanayohusu sarafu, viwango vya kodi na ushuru pamoja na riba katika mabenki, mikopo na biashara ya nchi za nje.
Kutokana na hali hiyo, masuala ya sarafu, benki kuu, mikopo na biashara ya nchi za nje, ushuru wa forodha, kodi ya mapato na kodi ya mashirika kila nchi inapaswa iyasimamie yenyewe.
7. Polisi:
Pamoja na kuwemo katika mambo ya awali ya Muungano lakini uendeshaji wa Polisi umekuwa na matatizo yake katika muungano. Miaka yote Polisi Zanzibar imekuwa ikilalamika kuwa inachukuliwa kama vile ni Mkoa tu na hata bajeti na mahitaji yake mengine yanachukuliwa hivyo hivyo na makao makuu ya Polisi yaliyopo Dar es Salaam.
Katika nchi nyingi duniani Polisi ambayo inashughulika na usalama wa raia na mali zao imekuwa ikiendeshwa chini ya Serikali za Manispaa na hata Majimbo seuze kwa nchi kama ilivyo Zanzibar.
Ukiondoa mishahara na bajeti ndogo ya uendeshaji inayotolewa na makao makuu ya Polisi, gharama nyengine za uendeshaji wa polisi kwa Zanzibar zimekuwa zikichangiwa na mamlaka za Zanzibar ikiwemo Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB).
Hivyo basi, wakati umefika kuona mamlaka kuhusu Polisi yanaondolewa katika orodha ya mambo ya Muungano na kila nchi ishughulikie yenyewe Polisi yake.
8. Mafuta na Gesi Asilia (pamoja na maliasili nyengine zote):
Baraza la Wawakilishi la Zanzibar kwa niaba ya Wazanzibari lilishafanya maamuzi mwezi Aprili 2009 kuyaondoa masuala ya mafuta na gesi asilia kutoka kwenye orodha ya mambo ya Muungano. Mbali na maazimio ya Baraza la Wawakilishi, masuala ya mafuta na gesi asilia yanahusu uchumi ambalo si suala la Muungano.
Katiba Mpya haipaswi kuyajumuisha masuala hayo mawili (pamoja na maliasili nyengine kwa ujumla) kuwa mambo ya Muungano.
Hivyo basi, rasimu yoyote itakayoyajumuisha masuala hayo ya Mafuta na Gesi Asilia (pamoja na maliasili nyengine zote kwa ujumla) kuwa masuala ya Muungano haitakubalika kwa Wazanzibari.
9. Vyama vya Siasa:
Muungano uliundwa na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na Jamhuri ya Tanganyika kupitia serikali zao. Mazungumzo yaliyopelekea muungano huo na hata utekelezaji wa hatua za kuunganisha nchi mbili hizi katika muungano hayakuhusisha vyama vya siasa vya wakati huo, ASP kwa upande wa Zanzibar na TANU kwa upande wa Tanganyika. Ndiyo maana kwa miaka 13 ya Muungano (kuanzia 1964 hadi 1977) kila nchi kati ya nchi mbili hizi iliendelea kuongozwa na chama chake cha siasa.
Moja kati ya dhoruba kubwa dhidi ya makubaliano ya asili ya muungano huu ambayo ni Mkataba wa Muungano ilikuwa ni kuunganisha vyama vya siasa vya ASP na TANU na kuunda CCM ambacho kilijitangazia kushika hatamu na kuwa juu ya vyombo vyengine vyote vya nchi zikiwemo Serikali. Utaratibu huo uliingizwa ndani ya Katiba za nchi na hivyo kuuhalalisha kisheria. Tokea wakati huo, Zanzibar imekosa mamlaka ya kisiasa ya kufanya maamuzi yake kwa mambo yanayoihusu. Na pale ilipofanya hivyo ilifanya kwa kutegemea na kujiamini kwa uongozi uliopo Zanzibar ingawa majaribio ya kutumia nguvu ya vyama kuzuia maamuzi kama hayo yamekuwa yakifanyika na baadhi ya wakati kufuzu.
Maongozi ya nchi yoyote yanategemea historia, mila na utamaduni wa watu wa nchi husika.
Kwa msingi huo basi, na ili Zanzibar iweze kurejesha mamlaka yake ya kisiasa katika kufanya na kusimamia maamuzi kwa mambo yake, rasimu ya Katiba haipaswi kujumuisha suala la vyama vya siasa kuwa ni jambo la Muungano. Zanzibar na Tanganyika kila moja iweze kuandikisha vyama vyake vya siasa.
10. Utaratibu wa uendeshaji wa Mambo ya Muungano:
Kwa yale mambo yatakayokubaliwa kubaki katika Muungano kama vile:
- Katiba ya Muungano wa Jamhuri za Tanzania;
- Serikali ya Muungano wa Jamhuri za Tanzania;
- Uratibu wa Sera ya Mambo ya Nje;
- Ulinzi;
- Usalama;
- Mamlaka juu ya mambo yanayohusika na hali ya hatari;
- Utumishi katika Serikali ya Muungano wa Jamhuri za Tanzania; na
- Mahkama ya Rufani ya Muungano wa Jamhuri za Tanzania.
Utaratibu wa uendeshaji wake uwekwe wazi katika Katiba kwamba maamuzi yote yatafanywa kwa mashauriano na makubaliano kati ya nchi mbili zinazounda Muungano huu na yatakuwa halali tu iwapo yatafuata msingi huu.
HITIMISHO:
Haya kimsingi ndiyo mapendekezo yetu Kamati ya Maridhiano. Tunayaleta kwenu muyapokee, muyajadili na kuwaomba muyaridhie ili yawe ndiyo msingi wa mwelekeo wa wananchi wa Zanzibar ambao wengi wao waliojitokeza mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba walitaka nchi yao iwe na mamlaka kamili.
Kwa mapendekezo haya, tunadhani Zanzibar na Tanganyika zitaendelea kuwa na mashirikiano ya kidugu kupitia mfumo mpya wa Muungano na wakati huo huo kila nchi mwanachama wa muungano ikibaki na mamlaka yake kamili katika yake maeneo ya msingi ambayo kila nchi hupenda kuwa nayo.
Imetolewa:
Zanzibar
25 Mei, 2013
Source: Jussa’s Wall on facebook

Thursday 14 March 2013

WATANZANIA WAASWA KUNYWA MAJI KWA WINGI

WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amewahimiza Watanzania kuwa na tabia ya kunywa maji mengi kila siku ili kujikinga na matatizo ya figo ambayo yanazidi kuongezeka kila siku. Ametoa wito huo leo mchana (Alhamisi, Machi 14, 2013) wakati akizungumza na mamia ya wananchi wa mji wa Arusha waliohudhuria kilele cha maadhimisho ya Siku ya Afya ya Figo Duniani yaliyofanyika kwenye viwanja vya hospitali ya AICC jijini humo. Kaulimbiu ya Siku ya Afya ya Figo Duniani mwaka huu ni “Figo Salama kwa Maisha yako: Epusha Madhara Makubwa kwa Figo” au “Kidneys for Life: Stop Acute Kidney Injury”. Waziri Mkuu
alisema mtoto wa miaka 10 hadi mtu mzima wanatakiwa wanywe maji kiasi kisichopungua lita moja na nusu kwa siku wakati mtoto mwenye mwaka mmoja anatakiwa anywe maji yasiyopungua nusu kikombe (sawa na mililita 100) na kwamba kiasi hicho huongezeka kadri umri wa mtoto unavyoengezeka. “Hii itasaidia kuhakikisha hawaishiwi maji mwilini,” aliongeza.
Kwa mujibu wa takwimu zilizopo, imekadiriwa kuwa watu milioni mbili hupoteza maisha kila mwaka kutokana na maradhi ya ghafla ya figo wakati asilimia 20 ya vifo vya wagonjwa waliolazwa hospitalini husababishwa na maradhi hayo.
“Wataalam wanasema maambukizi ya magonjwa hayo husababisha madhara makubwa ya figo (Acute Kidney Injuries) ambayo huchangia kwa kiasi kikubwa kuharibika kwa utendaji kazi wa figo. Hali hiyo husababisha watu kupata ugonjwa wa ghafla wa figo (mshtuko wa figo) na pia kusababisha athari kubwa kwenye figo na kuzifanya zishindwe kufanya kazi ipasavyo,” alisema.
Alisema maradhi yanayoweza kujitokeza ghafla na kuharibu figo hayajatiliwa mkazo ipasavyo, hasa katika nyanja za utoaji mafunzo ya tiba, utafiti na elimu ya afya ya figo kwa umma. “Hali hii husababisha kutotumika kikamilifu kwa fursa za kubaini maradhi yanayojitokeza ghafla na kuharibu figo; pia inaathiri utoaji huduma za afya ya figo usiokidhi, na hivyo wagonjwa kulazwa kwa muda mrefu hospitalini,” alisititiza.
Chanzo: MjengwaBlog

Saturday 9 March 2013

Sympathy ya wakenya yamnyanyuwa Kenyatta

Rais Kenyatta akipiga kura
Inavyoonekana katika uchaguzi wa Kenya ni jinsi gani wananchi wa Africa wasivokuwa na imani na mahakama ya kimataifa, duru nyingi zilimpa nafasi Odinga kuwa angeshinda kirahisi hasa ukitizamia kuwa Kenyata anakabiliwa na mashitaka kwnye mahakama ya ICC. Lakini wananchi wa Kenya wamemchaguwa mtuhumiwa kama vile ni kuionesha mahakama hiyo kuwa huyu munaemshitaki kwetu sisi ni lulu. Na tunasubiri tuone jee nchi za kiafrica zitamuunga mkno Kenyata au Marekani na mataifa mengine ya ulaya ambayo yalionesha wazi kumuunga mkono Raila Odinga? Nawapongeza wakenya kwa uzalendo halisi wa kujali utu wao na kutokuburuzwa na mataifa yasiyowapendelea mema. Tungojee tuone.Mungu ibariki Africa

Sunday 3 March 2013

Tukiri Muungano Unazidi Kudhoofika

KWA muda mrefu sasa watu wengi wa Zanzibar wamekuwa wakilalamika kimya kimya kwamba pamekuwa pakifanyika kile wanachokiona kama mizengwe ya kuwalazimisha kukubali kuongozwa na watu ambao ndugu zao wa Tanzania Bara wanawaona wanaofaa kushika hatamu za uongozi visiwani.
Tafsiri iliyokuwa inapatikana miongoni mwa watu hawa ni kuwa watu wa visiwani hawajui kutenganisha kizuri na kibaya, kile chenye manufaa na maslahi na wao na kile ambacho hakina faida kwao na nchi.
Kwa kiwango kikubwa unaweza kusema watu hawa wamekuwa wanahisi wanaonekana kuwa hawajui tofauti iliyopo ya mbichi na mbivu.
Kwahivyo, njia nzuri ya kuwasaidia ni kuwafanyia uamuzi badala ya wao wenyewe kujiamulia wanataka nini.
Kwa bahati mbaya sana, wale ambao wamekuwa wakilalamikia mwenendo huu, wamekuwa wakipachikwa kila aina ya majina ambayo ni ya kejeli na kumfanya mtu aonekane si mzalendo na hata kupachikwa majina kama vile; “Huyo sio mwenzetu’, ‘Ametumwa’, ‘Hana nia njema’, ‘Anakwenda kinyume na utaratibu tuliojiwekea’ na kadhalika.
Lakini hivi sasa hali inaonekana kubadika, kwani hata baadhi ya wale walioweka chama chao cha siasa mbele kuliko nchi na kudharau uamuzi wa wengi, wameanza kuamka kutoka katika usingizi mzito waliokuwa nao.
Usingizi huu ulijengwa na utamaduni wa kuitikia ‘hewalla bwana’ au ‘hewalla bibi’ na kupiga makofi, hata pakiwa hapana sababu ya kufanya hivyo.
Yote haya yametokana na kutokuwa na ubavu wa kutamka “hapana” au kutoa maoni ya kupinga baadhi ya mwenendo unaotumika katika chama chao kwa kisingizio cha kile walichokuwa wanakiita “jeuri ya chama”. Sijui jeuri hii ni ya maana au vinginevyo.
Lakini sasa wingu la kiza linaonekana kutoweka na mwanga umeanza kuonekana.
Hivi karibuni pameanza kusikika sauti za baadhi ya hao wanaotaka mambo ya chama chao yasiingiliwe, wakielezea hadharani kutaka mabadiliko ili watu wa Zanzibar waachiwe kuchagua wale wanaowaona wao ndio wanaofaa kuwaongoza.
Miongoni mwa sauti zilizosikika zikitaka mabadiliko ya kutaka Zanzibar kuachiwa mamlaka ya kumchagua mgombea urais wa CCM wa visiwa vya Unguja na Pemba, badala ya utaratibu wa sasa unaoshirikisha wenzao wa Tanzania Bara ni ya Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Zanzibar, Vuai Ali Vuai.
Katika mahojiano yake ya hivi karibuni, Vuai anasema suala hilo linajadiliwa, na kwamba ana matumaini kuwa litapatiwa ufumbuzi muafaka.
Anasema ndani ya CCM upo utaratibu ambao chama hicho umejiwekea wa kupata viongozi, lakini suala la kuchaguliwa mgombea urais wa Zanzibar kutoka kwenye vikao vya Dodoma linawagusa, na sasa wapo kwenye mchakato wa kulijadili ili upatikane ufumbuzi.
Hakuelezea mchakato huo umefikia wapi. Hata hivyo, Vuai alikwenda mbali zaidi kwa kueleza kuwa hata suala la kupokezana urais kati ya pande mbili za Jamhuri ya Muungano na jinsi ya kupata viongozi wengine kama wabunge na wawakilishi, linajadiliwa ndani ya CCM (hakueleza wapi) kwa kina.
Ama kweli zama zimebadilika kwa sababu kwa muda mrefu yeyote yule aliyeweza kujitokeza hadharani kutoa kauli kama hiyo, angelisakamwa na viongozi wenzake wa CCM na angelielezwa kuwa “sio mwenzetu” na “amekwenda kinyume na utaratibu tuliojiwekea”.
Hapa tunachojifunza ni kwamba, kero (au malalamiko) juu ya Muungano hayapo tu katika mfumo na uendeshaji wa shughuli za Serikali ya Muungano, bali hata ndani ya chama tawala cha CCM.
Kutokana na hali hii, tunajifunza kwamba upo umuhimu mkubwa kwa mfumo wa Muungano ukaangaliwa upya na kwa upana na urefu kwa sababu kila kukicha malalamiko yanazidi na kuyafumbia macho sio suluhu.
Ukweli ni kwamba kuyafumbia macho kunaudhoofisha Muungano ijapokuwa tunajaribu kujidanganya kwamba kila siku zikienda mbele unazidi kuimarika, badala ya kukiri kwamba unadhoofika.
Hivi sasa mchakato wa kupata katiba mpya umepamba moto nchini kwetu, na kwa upande wa Zanzibar
suala lililochukua nafasi kubwa ya mjadala na watu wengi hata kuonekana kutojali mengine yote yanayohusu katiba ni hili la Muungano.
Mmoja wa wajumbe wa tume anakiri kwamba Wazanzibari wanatofautiana kwa mengi kisiasa, lakini linapokuja suala la Muungano sauti yao ni moja na unakuwa hujui ni nani CCM , CUF au chama kingine.
Kwa bahati mbaya wapo watu waliotaka Watanzania wanapojadili na kutoa maoni juu ya katiba mpya wasiuguse Muungano kama vile suala hilo limejaa utukufu kama maneno yaliyokuwemo kwenye Kuran au Biblia, na kwahivyo halipaswi kuguswa kwa lengo la kufanya mabadiliko yoyote.
Huu sio mwendo sahihi, na kulipuuza suala la Muungano katika kutenegeneza katiba mpya hakutawasaidia Watanzania waliopo Bara wala Visiwani.
Tunawajibika kuwa wakweli na kuukubali ukweli kwa maslahi yetu binafsi na nchi yetu, hata huo ukweli ukiwa na ladha ya uchungu au maumivu.
Suala la Muungano kwa watu wengi wa Zanzibar, sasa linaonesha kuwa hata ndani ya nyoyo za makada na viongozi wa juu wa CCM, lina matatizo yanayohitaji kushughulikiwa kitaifa na sio kichama.
Kama CCM wanahisi chama chao kinayo haki ya kuendelea kuwachagulia wagombea wa uchaguzi Dodoma, hilo ni suala la wanachama wenyewe kuamua, na wanaweza kuendelea kufanya hivyo kama katiba yao inawaruhusu.
Lakini ni vema ieleweke wazi kwamba hao wanaochaguliwa na baadaye kuitumikia Zanzibar, huwa watumishi wa umma sio wa CCM peke yake.
Suala la kuwepo zamu ya urais kati ya Bara na Visiwani (hizi ni nchi mbili zilizoungana kuunda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania) nalo lisipuuzwe kwa kisingizio cha kwamba Zanzibar ni ndogo kama baadhi ya watu Bara, wakiwemo wabunge walivyojaribu kueleza katika kutaka malalamiko ya watu wa Visiwani yasitiliwe maanani.
Hili ni suala nyeti, na ni lazima hekima na busara itumike na ukweli wa kwamba Zanzibar na Tanganyika ni washirika sawa katika Muungano ionekane kwa vitendo.
Sio vibaya, kama kiongozi wa awamu mbili au tatu akatoka upande mmoja wa Muungano, lakini hii ifanyike kwa ridhaa, na pande zote mbili za Muungano kuwa hazina kinyongo.
Katika miaka ya nyuma mwenendo huu wa uamuzi wa watu wa Zanzibar kuwekwa pembeni na yale ya Dodoma kutawala umezusha hisia mbaya Visiwani.
Wapo watu ambao hadi leo wanahisi wenzao wa Bara hawawatendei haki na kwamba Muungano wa vyama vya ASP na TANU na kuunda CCM na wa serikali mbili (Zanzibar na Tanganyika) umekuwa ukisababisha watu wa Visiwani kuburuzwa na kulazimishwa mbichi kuiita mbivu.
Kwa upande mwingine wapo wanaofanya jeuri ya kuwaambia wenzao wa Visiwani kama hawatamchagua yeye hashituki kwa sababu atapigwa jeki na kura za watu kutoka Bara wanapokutana Dodoma.
Katika mchakato wa katiba mpya, sauti za Wazanzibari juu ya mfumo wa Muungano zimesikika na itakuwa vizuri kama Tume ya Jaji Warioba itaziheshimu na kutozibana katika majumuisho yake kabla ya kuandikwa katiba mpya.
Kinachotakiwa hapa ni nini wananchi wanataka na sio wanasiasa.
Vinginevyo malalamiko juu ya Muungano yataendelea kusikika kila upande na kuwalaumu hao wanaopiga kelele bila ya hoja za msingi.
Hatimaye kitachotokea ni kuzidi kuudhoofisha Muungano ambao Watanzania wengi wanautaka na kuuthamini, lakini wanaonekana kutofautiana juu ya mfumo wake na namna ambavyo baadhi ya shughuli za Serikali ya Muungano zinavyoendeshwa.
Si ajabu watu hao watakaotoa maoni tofauti wakaitwa “Uamsho” kwani huu ndiyo mwenendo wa siasa za hapa nchini.
Hali hii ya kupuuza sauti za wananchi ndiyo iliyosababisha kuonekana baadhi ya watu kuona Bara inaionea na kuisakama Zanzibar, hasa kiuchumi, na wapo wanaohisi na kuamini kuwa Zanzibar inadekezwa ndani ya Muungano, na kwa kweli inafaidika zaidi kuliko upande wa pili wa Muungano.
Yote haya yatakwisha kama dosari za Muungano zilizopo zitashughulikiwa vyema kwa manufaa ya watu wa pande mbili za Jamhuri ya Muungano.
Chanzo: Tanzania Daima

Friday 1 March 2013

Kama Muungano wetu ni Zimbabwe na Pemba, tutarajie nini kidato cha nne?

MIONGONI mwa habari ambazo zinatawala kwenye vyombo mbalimbali vya habari nchini mwetu, ni matokeo ya kutisha ya mitihani ya kuhitimu kidato cha nne, ambapo zaidi ya asilimia 60 ya watahiniwa wamefeli.
Ingawa matokeo hayo yamewashitua wengi, lakini kimsingi halikuwa jambo lisilotarajiwa. Kwa muda mrefu, sekta ya elimu imekuwa ikipewa kipaumbele kwa kauli zaidi kuliko vitendo vya dhati. Wakati chama tawala, CCM, ambacho kwa vyovyote vile hakiwezi kukwepa lawama kuhusu matokeo hayo mabovu, kimekuwa mahiri kuonyesha kuwa kinathamini sana umuhimu wa elimu, na hivyo kuipigia mstari katika kila manifesto zake za chaguzi kuu zilizopita, ukweli unabaki kuwa sekta ya elimu imekuwa ikipuuzwa.
Pengine, huwezi kuelewa mazingira mabovu yanayozikabili shule mbalimbaliza msingi na sekondari mpaka utoke nje ya miji. Kimsingi, wanafunzi wengi katika maeneo ya vijijini wanasoma katika mazingira magumu sana, na kitu pekee kinachowasukuma wazazi kupeleka watoto wao shuleni ni ukweli kuwa bado wanaamini kuwa elimu ni ufunguo wa maisha, hata kama ufunguo huo umepotea au haupo kabisa!
Binafsi, nadhani moja ya sababu kubwa za matokeo hayo mabaya ni mgogoro wa muda mrefu kati ya Serikali na walimu. Kilio kikubwa cha walimu kimekuwa ni kuitaka Serikali iboreshe mazingira ya utoaji na upatikanaji wa elimu, hususan kwenye maeneo ya mishahara na makazi ya walimu, pamoja na vitendea kazi vyao, sambamba na nyenzo muhimu kwa wanafunzi kama vile madarasa na madawati.
Hata hivyo, kama ilivyozoeleka kila inapojitokeza migogoro kati ya Serikali na watumishi wake, ubabe ulitawala kuliko busara. Pasi kujali busara kuwa ‘unaweza kumpeleka punda mtoni lakini huwezi kumlazimisha kunywa maji,’ walimu walipoonyesha dalili ya kuchoshwa na ‘kupuuzwa kwao’ na kufanya migomo ya hapa na pale, walishurutishwa kurejea mashuleni kufundisha.
Pengine walimu wanaweza kulaumiwa kwa matokeo hayo mabaya, na tayari kuna taarifa kuwa watachunguzwa na Serikali, lakini ni muhimu kabla ya kuwalaumu tukaelewa kwa undani mazingira ya kazi ya walimu wetu.
Binafsi, ni mhanga wa kumomonyoka kwa mfumo wetu wa elimu, ingawa si kwa kiasi kikubwa. Nilikuwa miongoni mwa wanafunzi wa kwanza wa shule ya sekondari ya Kilombero, kule Ifakara, mkoani Morogoro, ilipoanzishwa mwaka 1986.
Pamoja na kufanikiwa kuwa mmoja wa wanafunzi wanne waliopata daraja la kwanza miaka minne baadaye, lakini ukiachilia mbali masomo ya sanaa (arts), tulisoma masomo ya sayansi kama vile Kemia, Fizikia na Baiolojia kwa nadharia tu kwani maabara yetu ilikuwa ya kufikirika zaidi kuliko uhalisia.
Nilipokwenda kidato cha tano katika shule ya sekondari ya Wavulana Tabora (Tabora Boys’), nikakumbana na tatizo la ukosefu wa mwalimu wa somo la Jiografia, ambapo ilitulazimu kwenda shule ya jirani ya Sekondari ya Wasichana Tabora (Tabora Girls’) kumfuata mwalimu wa somo hilo. Na japo nilifanya vizuri kwenye mitihani ya kuhitimu kidato cha sita, uzoefu niliopata unanikumbusha mengi kuhusu sekta ya elimu huko nyumbani.
Lakini angalau wakati huo nilipokuwa mwanafunzi kulikuwa hakuna vitu vinavyoweza ‘kumpa faraja feki mwanafunzi.’ Hapa ninazungumzia maendeleo ya teknolojia ya mawasiliano ambapo tunakutana na vitu kama Facebook,YoutTube, BBM na kadhalika.
Ingawa kwa maeneo ya vijijini upatikanaji wa teknolojia hiyo bado ni wa kubahatisha, ni rahisi kwa wanafunzi wa mijini ‘kumalizia hasira zao za shuleni’ kwa ku-chat kwenye Facebook, kutumiana meseji kupitia BBM au kuangalia video huko YouTube!
Na ni wazi kuwa mwanafunzi anayetumia muda mwingi kwenye vitu kama hivyo, anajinyima nafasi ya kujisomea na hivyo kujitengenezea mazingira mazuri ya kufeli. Lakini wakati ni rahisi kukilaumu ‘kizazi cha Facebook’ ni vema tukatambua pia ili mwanafunzi aweze kujisomea, sharti awe na kitu cha kusoma.
Ukichanganya ufundishaji wa walimu ‘wanaofunika kombe ili mwanaharamu apite’ (wanatimiza tu wajibu wao) na uhaba wa vitabu vya kiada, hata mwanafunzi mwenye kiu ya kujisomea binafsi anakuwa na wakati mgumu kufanya hivyo.
Tukiweka kando lawama, ni vigumu japo kufikiria jinsi taifa letu linavyoweza kuirejesha elimu kwenye viwango kama vile vya zama za Ujamaa. Ninasema ni vigumu kwa vile kinachohitajika zaidi si kauli za porojo, bali uwekezaji wa kutosha katika sekta ya elimu.
Na ili uwekezaji huo uwezekano, inalazimu kuwapo na fedha. Sasa wakati Tanzania yetu inakabiliwa na deni la ndani na nje lenye thamani ya matrilioni ya Shilingi, na huku watawala wakigoma kuelewa kuwa sisi ni masikini na tunapaswa kupunguza matumizi ya anasa zisizo za lazima, tutakuwa tunajidanganya tukidhani kuwa uwekezaji huo katika sekta ya elimu utawezekana.
Vipaumbele vya watawala wetu vipo katika kuboresha maslahi ya wabunge badala ya kuboresha walau mazingira tu ya shule zetu, achilia mbali maslahi ya walimu. Ni busara gani iliyotumika kuongeza posho na mishahara ya wabunge wetu hadi kufikia zaidi ya Shilingi milioni 10 kwa kila mmoja ilhali shule kadhaa hazina madawati na majengo yake ni ya ‘mbavu za mbwa?’
Kuwaruhusu wanafunzi waliofeli warudie mitihani ilhali watajiandaa na mitihani hiyo katika mazingira yaleyale yaliyowafelisha mwanzoni, ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu. Kuwachunguza walimu ilhali sababu zilizopelekea matokeo mabaya zinajulikana, ni kutafuta mchawi asiyekuwapo.
Lakini tunaweza kwenda mbali zaidi na kuihoji Serikali kama kweli inathamini sekta ya elimu. Hivi kama Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo, anaamini kuwa Muungano wa Tanzania ni matokeo ya Muungano wa visiwa vya Zimbabwe na Pemba, tutarajie nini kwa mwanafunzi wa kawaida?
Na Waziri Mulugo anataka Serikali isilaumiwe, bali wadau wote wa elimu waangalie uwajibikaji katika nafasi zao. Kwanini asionyeshe mfano kwa kuwajibika yeye kwanza, kisha adai wengine waige mfano wake? Kimsingi, huyu mtu hakustahili kuendelea kushika wadhifa huo baada ya ‘mchemsho’ wake wa Muungano. ‘He is a pretty bad influence.’
Nimalizie makala haya kwa kuikumbusha Serikali kuwa mpango wake kabambe wa maendeleo ambao unaojumuisha hatua kama kuwawajibisha mawaziri walioshindwa kazi, hauwezi kufanikiwa kwa stahili hii inayoonekana katika picha hii. Badala ya kusubiri mawaziri waboronge, ingekuwa vema mpango huo ukaanza kwa mifano hai na kumwajibisha Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa, ambaye ameshatamka kuwa hatojiuzulu, na Naibu wake Mulugo, ambaye ameshaliaibisha taifa vya kutosha.

Chanzo: Raia Mwema

Tusikipuuze kitisho cha ugaidi, tusikikuze pia

SITI binti Saad, malkia wa waimbaji wa kike Wakizanzibari, aliwahi kuimba nyimbo iliyokuwa na maneno: “Unguja ni njema, atakaye naje.”
Siti aliyaghani maneno hayo kwa madaha na maringo zaidi ya miaka 60 iliyopita lakini majisifu yake ya kuiringia nchi yake bado yanasibu.
Unguja na Pemba yake zote ni njema. Atakaye naje. Lakini aje kwa udhu na heshima. Aje akitambua kwamba Zanzibar ina maadili yake.
Visiwa hivyo vinaendelea kuwa visiwa vya amani na utulivu. Utulivu huo ndio moja ya sababu zinazowavutia watalii kutoka sehemu mbalimbali za dunia kuizuru Zanzibar licha ya shida ilizo nazo za miundombinu.
Jengine lenye kuwavutia wageni ni ukarimu wa watu wake na upendo wao wa kuishi kwa amani. Kadhalika wenyeji wake wana moyo mkunjufu kwa wageni na ndio maana Wazanzibari wakawa hivi walivyo na michanganyiko yao ya damu.
Tena ni watu wavumilivu. Nchi yao iliyo ya Kiislamu ndiyo chimbuko la Ukristo katika Afrika ya Mashariki. Kutoka huko Ukristo ulivuka bahari na kuenea katika eneo zima la Maziwa Makuu na bara ya Afrika ya Mashariki.
Hatusemi kwamba kwa kuwa na taswira hiyo Zanzibar ya leo ni pepo. Wala hatusemi kama hakuna vitendo vya uhalifu vinavyotokea.
Uhalifu upo. Mfano mmoja ni tukio la Februari 17 la kuuawa Padri Evaristus Mushi wa Kanisa Katoliki. Hicho kilikuwa ni kitendo cha uhalifu wa kinyama.
Binadamu yeyote yule anayedhulumiwa maisha yake akiwa padri asiwe padri anastahiki kuliliwa. Na aliyemuua anastahili kulaaniwa na kuapizwa kwa maapizo yote tuyajuayo. Tena asakwe mpaka apatikane ili atiwe adabu kama inavyostahiki.
Hadi sasa hakuna aliyejitokeza kudai kwamba alihusika na mauaji hayo na sababu gani zilizoyasababisha.
Serikali ya Zanzibar nayo hadi sasa haijatwambia mauaji hayo yalitekelezwa na akina nani. Haijatwambia kwa sababu ingali inaendelea na upelelezi na bado haijui wahusika ni nani na sababu gani zilizowafanya wamuue Padri Mushi.
Inasikitishakuona kwamba badala ya kusubiri matokeo ya upelelezi unaofanywa baadhi ya mawaziri wa Serikali ya Muungano pamoja na baadhi ya viongozi wa Kikristo na vyombo vya habari wameyarukia mauaji hayo na wanayatumia kama fimbo ya kuwapigia Wazanzibari.
Mmoja wa viongozi walioshangaza ni Waziri wa Mambo ya ndani wa Jamhuri ya Muungano, Dk. Emmanuel Nchimbi ambaye mara baada ya Padri Mushi kuuawa aliruka na kuanza kutoa matamshi yasio na ithibati yoyote kwamba walioua ni ‘magaidi’.
Hivi karibuni aliuawa mchungaji Mathayo Kachila wa Kanisa la Pentekoste la Assemblies of God huko Geita lakini hatukumsikia Nchimbi akishutumu kwamba Kachila aliuliwa na magaidi. Wala hatukumsikia akitoa shutuma kama hizo Katibu wa Mufti wa Zanzibar Sheikh Fadhil Soraga alipomwagiwa tindikali au alipopigwa mapanga imamu wa msikiti Sheikh Ali Khamis Ali na kuuawa.
Kwa vile Nchimbi hana ushahidi matamshi yake yanakua matamshi ya uchochezi wenye kutia fitina. Dhamira yake ni kuipaka tope Zanzibar na kuufanya ulimwengu uamini kwamba kuna mtandao wa kigaidi Visiwani wenye lengo la kuwaua Wakristo.
Nchimbi akijua vilivyo kwamba vyombo vya dola vinavyohusika vilikua vikiendeleana upelelezi na kwamba serikali yake imeiomba Idara ya Upelelezi ya Marekani (FBI) iisaidie.
Inavyosemekana ni kuwa mashirika kadhaa ya kigeni ya upelelezi na ya kijasusi yameombwa yaisaidie serikali katika upelelezi huo. Nimedokezwa na chanzo kimoja nje ya Tanzania kwamba Shirika la Ujasusi la Israel, Mossad, ni mojawapo ya mashirika hayo.
Mwaka juzi Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu aliizuru Kenya. Baada ya ziara yake ofisi ya waziri mkuu wa Kenya Raila Odinga ilisema kwamba Netanyahu aliahidi kusaidia kuunda ‘muungano dhidi ya itikadi kali ya kidini (ya Kiislamu)’ utaoziunganisha nchi za Kenya, Ethiopia, Sudan ya Kusini na Tanzania.
Mwaka jana nilitahadharisha kwenye gazeti hili kwamba kuna watu nchini wasioridhika na Maridhiano yaliopatikana Zanzibar. Niliandika kwamba wakitakacho watu hao ni kuzusha fujo Zanzibar zitazoweza kuisambaratisha Serikali ya Umoja wa Kitaifa na hata kuzusha hali zitazosababisha mchakato wa Katiba usimamishwe.
Mkakati wao ni kuwatumia vijana wachochee fujo kwa kuwatomeza wenye jazba wachome moto makanisa ili ulimwengu uamini kuwa kwa Wakristo na Wabara Zanzibar hapakaliki.
Watasema kwamba wenye kuleta fujo hizo ni wafuasi wa Jumuiya ya Uamsho. Halafu watawahusisha viongozi wa Jumuiya hiyo na mtandao wa kigaidi wa al-Qa’eda na kwa mpigo mmoja watawahusisha viongozi wa CUF na Uamsho na harakati zao.
Tangu nitoe indhari hiyo shutuma zote hizo zimetolewa hata kabla ya kuuliwa Padri Mushi. Na sasa zinazidi kushadidiwa.
Wenye kutoa shutuma hizo wanatumai kwamba wataweza kuwafanya wakubwa wa dunia hii waiangalie Zanzibar kwa jicho jingine. Wanachotaka hasa ni kuzizima harakati za kuujadili Muungano na kuudhoofisha mshikamano wa Wazanzibari.
Wengine wenye kushtusha ni waandishi wa habari walioamua bila ya kufanya utafiti wowote kwamba magaidi wenye funganisho za kimataifa ndio waliomuua Padri Mushi, kwamba magaidi hao wanahusika na Uamsho. Na kuna waliosihi jumuiya hiyo ipigwe marufuku.
Ukweli ni kwamba kwa muda unaokaribia miezi sita viongozi wote wa Uamsho wameshikwa na wako jela wakisubiri kesi walizoshitakiwa. Muda wote huo wafuasi wao hawakufanya fujo. Wameusikiza (wametii) wito wa viongozi wa kisiasa Visiwani wakiwataka wawe watulivu.
Waandishi wengine wakafika hata kudai kwamba hao ‘magaidi’ wana wenzao ndani ya Serikali ya Zanzibar.
Huo ni uzushi na uzandiki usiofaa kuandikwa na mwandishi yoyote wa maana. Ukweli tuujuavyo ni kwamba hakuna ushahidi wowote wenye kuonyesha kwamba kuna mtandao wa kigaidi Zanzibar wenye kuwalenga Wakristo.
Kitisho cha ugaidi kipo Tanzania nzima na kinatokana na magaidi wa Al-Shabaab wenye kutishia amani ya kanda ya Afrika ya Mashariki.Lazima taifa liwe macho kukikabili lakini tusikikuze kuliko kilivyo.
Ukweli mwingine ni kwamba Waislamu wa Zanzibar, ambao takriban ni asilimia 98 ya wakaazi wa visiwa hivyo, wataendelea kuishi kwa amani na ndugu zao wachache Wakikristo na Wakihindu.
Ikiwa nia ya maadui wa Zanzibar ilikuwa kuyatumia mauaji ya Padri Mushi kwa kuliharibu jina la Zanzibar na kuyadanganya mataifa ya nje kuhusu ugaidi basi hawakufanikiwa.
Madola ya Magharibi hayakushtushwa na matamshi ya Nchimbi na ndio maana hayakutoa taarifa za kuwazuia au hata kuwatahadharisha wananchi wao wasiizuru Zanzibar.
Chanzo: Tanzania Daima

Monday 25 February 2013

TAMKO LA JUMUIYA NA TAASISI ZA KIISLAMU ZANZIBAR KULAANI MASHAMBULIZI NA MAUAJI YA VIONGOZI WA DINI PAMOJA NA KUPINGA KAULI ZA UCHOCHEZI DHIDI YA ZANZIBAR

Masheikh wa Jumuia na Taasisi za kiislamu Zanzibar, kutoka kushoto ni Sheikh farid, Sheikh Mselem na sheikh Azzan

TAMKO LA JUMUIYA NA TAASISI ZA KIISLAMU ZANZIBAR KULAANI MASHAMBULIZI NA MAUAJI YA VIONGOZI WA DINI PAMOJA NA KUPINGA KAULI ZA UCHOCHEZI DHIDI YA ZANZIBAR
Kila sifa njema anastahiki Mwenyezi Mungu Mtukufu Mlezi wa Viumbe. Sala na salamu zimfikie Mtume wetu Mtukufu Muhammad (S.A.W), jamaa zake, maswahaba zake waongofu na wote wanaowafuata kwa wema hadi Siku ya Malipo.
Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar lililokaa Jumapili tarehe 23/2/2013 katika kikao cha kutathmini matukio ya kushambuliwa na kuuliwa viongozi wa Dini yakiwemo ya karibuni ya kupigwa risasi na kuuliwa Padri Mushi pamoja na kupigwa mapanga na kuuliwa Sheikh Ali Khamis Bin Ali Khatibu wa Mwakaje na kuendelea kutolewa kwa kauli za uchochezi dhidi ya Zanzibar linatamka ifuatavyo:
1. Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar linalaani vikali na kwa nguvu zote matukio ya kushambuliwa na kuuliwa viongozi wa Dini likiwemo tukio la karibuni la kupigwa risasi na kuuwawa Padri Mushi kulikofanywa na wahalifu wasioitakia mema Zanzibar.
2. Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar linapenda kuweka wazi kuwa uhai ni tunu kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu aliyotunukiwa binaadamu hivyo hakuna mwenye mamlaka ya kuiondoa haki hiyo isipokuwa yeye mweyewe Mwenyezi Mungu. Kutokana na ukweli huu ndio maana Sheria za Kiislamu zimeweka wazi mtu mwenye kumuuwa mwenziwe naye auliwe kama inavyoelezwa katika Kitabu kitufu cha Quran kama ifuatavyo:
“Na humo (katika Taurati) tuliwaandikia ya kwamba mtu (huuwawa kwa sababu ya kuuwa mtu) kwa mtu, ……….” (5:44)
Hivyo, vitendo vya kiharamia vya kushambuliwa viongozi wa Dini kulikoanzia kwa kumwagiwa tindi kali Sheikh Soraga, kupigwa risasi Padri Ambrose Mkenda, kuuliwa Padri huko Musoma, kupigwa risasi na kuuwawa Padri Mushi na kushambuliwa kwa mapanga na kuuliwa Sheikh Ali Khamis Bin Ali Khatibu wa Mwakaje kwa dhulma kulikofanywa na wahalifu ni jambo lisilokubalika na Uislamu na Waislamu wenyewe. Aidha wahusika wa matendo haya wawe wafuasi wa Dini yoyote ile bado watahesabika ni wahalifu kwani vitendo vya kihalifu na kiharamia kamwe haviwezi kunasibishwa na Dini fulani.
3. Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar linaviomba vyombo husika kufanya upelelezi wa kina kuhusu matukio haya kwa kuzingatia uadilifu na misingi ya kazi zao ili kuwabaini wahalifu na kufikishwa katika vyombo vya kisheria. Aidha Baraza linavitahadharisha vyombo hivyo kuepuka kufanya kazi yao kwa kusukumwa na matashi binafsi, jazba, chuki, matashi ya baadhi ya wanasiasa na viongozi wa Dini pamoja na shindikizo la baadhi ya vyombo vya habari.
4. Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar linalaani na kupinga kwa nguvu zake zote kauli aliyoitoa Waziri wa Mambo ya Ndani wa Tanzania na baadhi ya vyombo vya habari kuihusisha Zanzibar na ugaidi kutokana na tukio la kuuliwa Padri Mushi. Kauli hii inaonesha kuwa Mheshimiwa Waziri anaibagua Zanzibar katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwasababu tunavyoelewa sisi suala la usalama wa nchi ni suala la Muungano hivyo huwezi kuihusisha Zanzibar pekee na suala la ugaidi. Hivyo, Baraza linaona kuwa kauli hizi zinazotolewa ni mbinu za makusudi za kuichafua Zanzibar katika Jumuiya ya Kimataifa kutokana na chuki binafsi dhidi ya Zanzibar na watu wake.
5. Aidha Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar linamtaka Mheshimiwa Waziri kwa kulinda heshima yake kuwajibika kwa Watanzania kwa kujiuzulu kutokana na kushindwa kulinda usalama wa wananchi wakiwemo viongozi wa Dini ambao ndio walezi wa jamii.
6. Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar linalaani kauli za uchochezi zinazoendelea kutolewa na baadhi ya vyombo vya habari zinazochochea chuki, uadui, hasama na mtafaruku kati ya Waislamu na Wakristo na kusahau kuwa Waislamu wameishi na Wakristo kwa amani, mapenzi na mashirikiano hapa Zanzibar karne na karne. Baraza linaona kuwa vyombo hivyo vya habari vinatekeleza ajenda ya kuivuruga Zanzibar kwa kuchochea vita vya kidini ili kufikia malengo yao wanayoyajua wenyewe. Hivyo, Baraza linaiomba Serikali kuvidhibiti kwa kuvichukulia hatua vyombo vyote vinavyotumia matukio haya kuchochea uadui na chuki kati ya Waislamu na Wakristo.
7. Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar linaviomba vyombo vya habari vya Zanzibar kuwajibika kwa Wazanzibari wanaolipa kodi kwa kuwapasha taarifa sahihi juu ya matukio muhimu yanayotokea katika jamii yao badala ya wananchi kutegemea kupokea taarifa za upotoshaji na uchochezi kutoka katika vyombo vya habari visivyotutakia mema.
8. Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar linaziomba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Umoja wa Kitaifa ya Zanzibar kuwasilisha kwa Watanzania taarifa ya wazi ya matokeo ya uchunguzi wa matukio haya kwa kuanzia na lile la kumwagiwa tindi kali Sheikh Soraga, kupigwa risasi Padri Ambrose Mkenda, kuuliwa Padri huko Musoma, kupigwa risasi na kuuwawa Padri Mushi na kushambuliwa kwa mapanga na kuuliwa Sheikh Ali Khamis Bin Ali Khatibu wa Mwakaje.
9. Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar linawaomba Wazanzibari wote kuwa watulivu katika kipindi hichi ambapo upelelezi wa matukio haya ukiendelea. Aidha Baraza linawasihi Wazanzibari wote bila ya kujali tofauti zao za kidini kulinda umoja wao na kudumisha amani pamoja na kukataa kugawanywa ili kuwatoa katika ajenda yao ya msingi ya kudai Mamlaka Kamili ya Zanzibar katika Muungano.
MOLA WETU MTUKUFU TUNAKUOMBA UINUSURU ZANZIBAR NA WATU WAKE DHIDI YA MAADUI WA NDANI NA NJE WASIOITAKIA MEMA NCHI YETU
Imesainiwa na:
Sheikh Ali Abdalla Shamte
Amir wa Baraza la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar

Saturday 23 February 2013

TUSIPOTUMIA AKILI ZETU VIZURI, WAZANZIBAR TUTAPIGANISHWA KAMA MAKUCHI

Matukio ya kusikitisha, kufedhehesha na yakushangza yamekuwa yakitokea Zanzibar tangu mwaka jana baada ya wazinzabar kuanzisha harakati za kurudisha Zanzibar yenye mamlaka kamili (Zanzibar huru), harakati zilizoanzia kwenye baraza la wawakilishi mwaka 2010, kwa kubadili katiba ya Zanzibar na kuitaja Zanzibar kuwa ni nchi kamili! Vugu vugu lililochagizwa zaidi na jumuia ya mihadhara na ya kiislam ( al maarufu kama UAMSHO)!
Vugu vugu hilo lilipelekea mvutano kati ya jeshi la polisi na wafuasi wa masheikh wanaoongoza jumuia ya UAMSHO. Chakushangaza mvutano au mapambano yalikuwa ni kati ya polisi na wafuasi wa UAMSHO, lakini tukaamka asubuhi nakusikia MAKANISA kadhaa yamechomwa moto! Eti waZanzibar hao (UAMSHO) ambao wamekuwa wakiishi kwa amani na upendo na wakristo kwa karne tele zilizopita, leo hii wameacha nyumba zote za askari wanaopigana nao, wanaCCM, viongozi wa SMZ, na masheha badala yake wameenda kuchoma moto makanisa! Hapa tukaambiwa uchunguzi utafanyika na wahusika watafikishwa kwenye vyombo vya sheria….watu wakakamatwa kwa nzo, wakatafutwa kila mwenye ndevu akanyolewa, wakahilikishwa, na kwa kutumia technologia (kama alivyosema Kamishna Mussa), wakaangalia kanda za video kubaini walokuwepo kwenye vurugu zile na kuwakamata! Tukasubri majibu , tuambiwe ni nani hasa alochoma makanisa? Ikabaki kuwa “watu wasiojulikana” Jibu mpaka leo hakuna!
Tutakaa tena kidogo, tukasikia Sheikh Farid katekwa, jeshi la polisi likasema hajui alipo, itakuwa kajiteka! Vurugu zikazuka tena, makanisa yakachomwa tena, lakini mara hii wakaongeza na kuchoma maskani za CCM, na polisi mmoja akauliwa kwa kukatwa katwa kwa mapanga! Mkuu wa jeshi la polisi nchini Said Mwema, akasema ametuma makachero wenye ujuzi wa hali ya juu (walobobea) kutoka makao makuu Dar es salaam, kuja Zanzibar kuwatafuta wahusika wote walouwa na kuchoma makanisa ili wafikishwe kwenye vyombo vya sheria…tukasubiri na tunaendelea kusubiri, bila kupata majibu mpaka leo!
Hatujakaa vizuri, tukasikia Sheikh Soraga, kamwagiwa tindi kali usoni, na “mtu asiejulikana”! Kama kawaida tukaambiwa tena, jeshi la polisi linafanya uchunguzi kuwatia nguvuni wahusika….mpaka naandika habari hii hakuna jibu la nani alommwagia Sheikh Soraga tindi kali! Jeshi la polisi bado lafanya uchunguzi tu!
Tukiwa bado tunatafakari hayo, tunasikia tena Padri Ambrose kashambuliwa kwa risasi, na “watu wasiojulikana”! Lengo ilikuwa ni kumuuwa, lakini bahati nzuri yupo hai! Hili likaendelea kutushangaza wengi, eti mara hii wazanzibar wamekuwa wanamiliki silaha za moto, na ni wajuzi wakuzitumia?!! Hapa sasa tukasikia kauli kali zaidi, tena kutoka kwa viongozi wajuu zaidi kisiasa katika nchi yetu, akiwemo Rais wa Tanzania, Kanali, Dr. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa serkali ya Zanzibar Biochemist, Dr. Ali Shein, wakilaani nakuvitaka vyombo vyote vya jeshi la polisi, wakiwemo usalama wa taifa kufanya uchunguzi kwa weledi wajuu kabisa ili kubaini na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria wahusika! Tukasubiri na tunaendelea kusubiri kuwajuwa wahusika, lakini mpaka sasa hakuna jibu!
Eeeh juzi tena tunasikia Pandri Mushi, ameuliwa kwa risasi na “watu wasojulikana”! Mauaji hayo yanatokea tena ndani ya Zanzibar hiyo hiyo! Mara hii Tanzania zima ikatikisika, kauli nzito nzito, kutoka kila kiongozi wanchi hii, kuanzia rais wa Tanzania, rais wa SMZ, waziri wa mambo ya ndani, n.k…karibu kila mwenye mdomo (access ya vyombo vya habari) alisema na kulaani. Tukaambiwa FBI, CIA, Mossad wote hao wakishirikiana na TISS watakuja kuchunguza na kuwatia nguvuni walomuuwa na walo ratibu mauwaji hayo….tukasubiri nab ado twasubiri!
Tukiwa bado tumehamanika na matukio hayo, tukiwa bado tunanyoosheana vidole, na kutupiana lawama, tukiwa tunazidi kuandamwa na wingo zito…leo tunasikia imamu sheikh Ali Khamis huko kitope (kaskazini Unguja), ameuliwa kwa kukatwa katwa mapanga na “ watu wasiojulikana”! Nategemea kauli zitakuwa hizo hizo “Uchunguzi utafanyika…” Na sisi ni kama vifaranga vya kuku…tutanyonya kesho, nabado twasubiri kunyonya!
Kwa kweli ukiangalia ukubwa wa visiwa vyetu (Zanzibar) na population yake na ukilinganisha na matukio haya, utaona kwamba ni matukio mengi sana na yametokea katika kipindi kifupi sana, matukio yakusikitisha na kulaaniwa na kila muungwana! Matukio yasiyopaswa kutokea katika jamii ya watu walostaarabika kama Zanzibar.
Chakusikitisha na kutisha ambacho ndicho kilichonisukuma kuandika haya, ni kuwa matukio yote haya, yamekuwa yakiishia kuhukumiwa na jamii kwa hisia tu, huku serkali ikiishia na jibu la “watu wasojulikana upelelezi unaendelea”, lakini jamii, na hata viongozi wa serkali na dini wamekuwa wakitumia hisia zao, utashi na mihemko yao kushutumu na hata kuhukumu baadhi ya kikundi au kundi katika jamii.
Mwanzaoni wapo walojaribu kuhusisha matukio hayo na CUF, lakini walipoona wazanzibar wa hivi sasa hawatopigana wala kuuwana kwa sababu ya vyama vya siasa, wakakosa nguvu! Lakini mara zote kundi la UAMSHO, likawa ndio kitambaa chao (leso) cha kufutia mafua, jasho, mate, n.k., kila tukio likitokea, basi utaskia UAMSHO hao, kauliwa padre “UAMSHO” , Kamwagiwa tindi kali sheikh -“UAMSHO”, limechomwa kanisa-“UAMSHO”! Khaa, mengine enhe, lakini mengine nkinehe!
Serkali imeacha kufanya kazi yake (Jeshi la polisi) kama walivyoafanya kule mwanza alipouliwa RCO , badala yake imeachia jamii ihukumu kwa hisia, ni hatari! Maana sasa viongozi wa UAMSHO wako ndani, UAMSHO hajulikani ni nani, lakini mauwaji yanaendelea! Sasa akiuliwa padri au kuchomwa kanisa utaskia ni waislam hao, naam hisia hisia, waislam hao wa Zanzibar sasa washakuwa magaidi! Si ndo alivyosema Nchimbi! Na sasa akiuliwa sheikh au ikichomwa misikiti, kwa hisia tu watasema “ WAKRISTO hao” na wakristo nao washakuwa magaidi! Tunako kwenda siko!
Siamini na kamwe sitoamini kwamba eti matukio haya yanafanywa na mzanzibar wakawaida, awe mkiristo au muislam, kamwe siamini kama mzanzibar wakawaida anamiliki silaha ya moto, na amekuwa mjuzi wakuitumia kiasi kwamba anaweza kulenga shabaha kwa ustadi mkubwa huku akiwa kwenye vespa na kumuuwa padri! Siamini kabisa, kama kweli mzanzibar anaweza kumvamia sheikh na kumkata kata mapanga! Nani basi anae fanya haya? Na anafanya haya kwa nini? Na Kwanini mapaka leo Kamishna Mussa hajatoa majibu ya walofanya matukio haya?
Inasikitisha na kushangaza sana, waziri mwenye dhamana na ulinzi wa taifa hili, anaibuka akiwa na maruwe ruwe (hangover) ya mapombe yake alokunywa “Rose garden” anasema eti wanaofanya matukio hayo ni MAGAIDI, huyu ni msomi wa PhD, eti daktari wa falsafa! Kwa falsafa ya aliepata Div 0 matokeo ya mwaka huu ya form 4, basi inatosha kumwambia waziri wakati unatanganza hayo, hukupaswa kuendelea kuwa waziri wa wazara hiyo tena! Ikiwa umeshindwa kudhibiti magaidi mpaka wameweza kuingia ndani ya nchi yako, lakini kama haitoshi, wakaweza kumiliki silaha, wakaweza kupanga na kutekeleza mauwaji na uharibifu wa nyumba za ibada wakati wewe ndie mwenye dhamana ya kulinda hayo yasitokee, sijui alikuwa au bado anangoja nini kwenye ofisi yake? Lakini pia angetwambia hawa magaidi wana demand (madai) nini?
Maana ya neno gaidi (terrorist), ni mtu anaeletea madhara katika jamii au anaefanya mashambulizi au utekaji kwa lengo la kugofya mamlaka au mtu husika ili atekelezewe madai yake! Kwa misingi hiyo gaidi huwa akishatenda huwa hutokeza wazi wazi na kusmema, mimi ndio niliofanya jambo kadhaa, ili unipe, au utekeleze masharti kadhaa, usipotekeleza ntafanya tena jambo kadhaaa…! Sasa matukio yote haya hakuna kikundi, wala mtu alojitokeza kukiri kufanya na kusema amefanya ili apewe nini au anadai nini. Sasa Dr. Nchimbi atwambie magaidi wake hawa wana mdai nini? Atwambie, wanauwa mapadri ili wapewe nini na kanisa katoliki? Wanauwa masheikh ili wapewe nini na waislam?
Nakumbuka, nilipokuwa na miaka 12, ilikuwa tukifunga skuli (nilikuwa skuli ya Jadida, Wete), nikienda kwa bibi yangu Pandani kwa mwewe, kuna mengi niliyapenda huko pandani ikiwemo kuchota maji kwenye kisima cha ndoo kwa kutumia “roda”, lakini jambo jengine ilikuwa lilonifanya niamke mapema sana ni “mchezo wa kupiganisha kuku” ! Niliupenda sana mchezo huu! Walipiganishwa majongoo wakila aina kuanzia makuchi, majogoo upanga n.k. Lakini ugomvi wa makuchi ulikuwa mtamu sana, hawachoki haraka, wajuzi wakupigana, hawakubali kushindwa, si woga na wepesi wakupiganishwa!
Walipiganishwa makuchi wale bila wenyewe kuwa na sababu ya msingi yakupigana! Walipiganishwa bila kujuwa kwanini wanapigana? Walipigana sababu tu wametumwa kupigana! Kupigana kwao makuchi hawa ndo furaha ya wapiganishaji, pengine wapiganaishaji hucheza kamari, na mwenye kuchi alieshinda akapata malipo!
Historia ni mwalimu nzuri, tunasoma kwamba kule India wakati wa harakati za kudai Uhuru zilizokuwa zikiongozwa na Mahtma Gandhi, wakati huo India ikiwa koloni la British, wakoloni hawa walikuwa wakiwapiganisha waislam na wahindu, ili kujenga hoja ya kutowapa uhuru! Walikuwa wakichinja nguruwe kasha wakiwatupa kwenye misikiti ya waislam…kwa hisia waislam wakiwashutumu wahindu kwa kuwatupia nyama haramu, najisi kenye nyumba zao tukufu za ibada, kisha wakoloni hawa wakichnja ng’ombe na kuwatupa kwenye mahekalu ya wahindu, wahindu nao kwa hisia tu, wakawashutumu waislam, kwamba ndio wanaowauwa miungu yao (wahindu wanaabudu ng’ombe kama mungu wao), kisha wanawatupa kwenye nyumba zao za ibada! Kwa hisia wakaishia kupigana na kuuwana….mkoloni akazidi kutawala!
Hali hii ndio nnayo iona Zanzibar, matukio ya kumwagia mavi visima vya maji, kuchomwa moto nyumba za masheha, kulipuliwa mabomu ofisi za CCM, tuliyaona mageni yalipoanza miaka 90 kule kisiwani Pemba, tukawa twaambiwa ni wapinzani, wafukuwa hadi barabara na kuvunja mabomba ya maji! Lakini kisha tukayazoea, na jamiii ikamjuwa hasa anaefanya hayo ni nani! Sasa kuna kumezuka jipya, lakini safari hii si Pemba, ni kwa dada yake, Unguja, kumezuka fasheni ya sampuli yake ya kuwauwa viongozi wa dini, wanauliwa mapadri leo, na kesho wanauliwa masheikh, kwa zamu!
Ni lazima tutumie akili zetu vizuri katika kutafakari mambo haya! Tuweke hisia zetu na misukumo ya kiimani pembeni! Tumuombe Mungu wetu atupe hekima ya kuangalia matukio haya kwa jicho la 3, atupe hekma ya kuwa waadilifu katika kuchambuwa matukio haya! La sivyo, basi, leo atauliwa Padri John, kwa hisia upande mmoja utasema –“WAISLAM hao”, kesho atauliwa Sheikh Abdalllah, kwa hisia upande mwengine utasema – “WAKRISTO hao”, kitakachofuata sihitaji kukieleza hapa, maana wote tunajuwa! Mungu atunusuru!
Wapiganishaji watakuwa wamekaa pembeni wakitutazama tunavyouwana kwa ujinga wetu! Watakuwa wanasubiri kuleta misaada ya kibinaadam” (kama wanavyoita wenyewe), watasubiri kuleta majeshi yao kusimamia amani, watapa habari za kutanganza kwenye vyombo vyao vya habari kama vile CNN, BBC, Al jazeera n.k Zanzibar itakuwa maarufu kama ilivyo afghanstan, Iraq, Syria, n.k! Watapata sababu za kutosha za kuifanya Zanzibar kuwa mkoa wa Tanzania! Utamaduni na asili ya Zanzibar sasa ndo itapotea kabisa!
Tusikubali kufanywa makuchi tukapiganishwa sie kwa sie….!
Chanzo: Mzalendo