Na Ahmed Rajab
HATUNA budi tushukuru kwamba mwaka jana visiwa vya Zanzibar viliweza
kukwepa machafuko, migawanyiko na migogoro ya kisiasa iliyozikumba nchi
kadhaa barani Afrika na ulimwenguni kwa jumla.
Kinyume na kawaida, mwaka ulipita bila ya kuzuka vituko vyovyote au
mapambano yoyote ya kisiasa baina ya wafuasi wa vyama vikuu viwili vya
CCM na CUF Visiwani humo au kama ilivyokuwa zamani baina ya vyama vya
ZNP na ASP.
Hilo ni jambo kubwa hasa kwa vile mwaka huo ulizaliwa miezi isiyotimu
hata mitatu baada ya Uchaguzi Mkuu uliokuwa na matokeo ambayo wengi wa
wafuasi wa chama cha CUF waliyapinga. Na hapa hekima iliyotumiwa na
uongozi wa CUF inastahili pongezi.
Kulikuwa na hatari kwamba matokeo hayo yangesababisha vurugu nyingine
za kisiasa visiwani humo. Vurugu aina hizo ndizo zilizokuwa zamani
zikizusha mifarakano miongoni mwa Wazanzibari na kuleta mpasuko katika
jamii, mpasuko ambao wengi wakidhani hauna dawa.
Ukweli ni kwamba mpasuko huo ulikuwa na dawa. Waliokuwa na dawa hiyo
walikuwa wenyewe Wazanzibari. Watu wa nje na taasisi zao walipojaribu
kuleta suluhu hawakufanikiwa. Lakini wenyeji walipong’amua kuwa kila
wakiuendekeza uhasama wao ndipo wanapozidi kuathirika, wakajizatiti
kuukomesha kwa maslahi yao wenyewe.
Rais mstaafu, Amani Abeid Karume na Katibu Mkuu wa CUF, Seif Sharif
Hamadi walionyesha ustadi mkubwa wa kisiasa kwa kufikia Maridhiano. Kuna
Wazanzibari wenzao kadhaa ambao waliwatia moyo na kuwasaidia kuyafikia
hayo Maridhiano. Ninaamini kwamba iko siku wanahistoria watapokuwa
wanakipitia na kukitalii kipindi hiki watawatambua kuwa ni mashujaa wa
amani.
Miongoni mwao ni Hassan Nassor Moyo aliyekuwa mshenga mkuu katika
ndoa hii ya kisiasa. Mzee Moyo ni mmoja wa waasisi wa Mapinduzi ya
mwaka 1964, aliyewahi kuwa waziri katika serikali za Zanzibar na
Tanzania na ambaye sasa ameziweka upande siasa za kichama na kuwahimiza
Wazanzibari na viongozi wao wa kisiasa waungane kwa maslahi ya taifa
lao.
Msimamo wake huo na wa wengine kama yeye wenye itikadi tofauti
unaashiria kuwa yale mapambano ya kisiasa ya baina ya mwaka 1957 na
mwaka 2010 hayatoendelezwa tena. Badala yake yatakuwa ni mambo ya
kukumbukwa.
Kwa hakika, kwa muda mrefu Wazanzibari wamekuwa wakitambua kwamba
siasa za vyama na historia ndefu ya siasa hizo, ndizo zilizokuwa
zikiwagawa na kuzusha ukinzani miongoni mwao. Wakati ule utiifu kwa
vyama na sera za vyama ulionekana kuwa ni muhimu zaidi kushinda maslahi
ya nchi.
Hizo tofauti za kisiasa zilikuwa na athari mbaya kwa maendeleo ya
Zanzibar kwa upande wa kiuchumi na hata wa kijamii. Maridhiano
yaliyopatikana na yaliyoleta umoja katika nchi yameleta vile vile hali
ya matumaini makubwa kwa mustakbali wa Zanzibar.
Matokeo ya yote hayo ni kwamba hivi sasa kuna uwezekano wa Zanzibar
kuweza kunusurika isiporomoke kabisa kisiasa, kiuchumi na kijamii. Hali
kadhalika kuna tumaini kubwa kwamba visiwa hivyo murua vinaweza
kuokolewa na kupatiwa maendeleo kwa manufaa ya vizazi vyake vya sasa na
vijavyo.
Wazanzibari walifanya busara kubwa walipoamua kuyasahau yaliyopita na
kuganga yajayo, hususan kuhusu mustakbali wa nchi yao na wapi
wanakotaka ielekee baada ya miaka 47 ya Muungano.
Mwaka 2011 ulishuhudia kuimarishwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa
ambayo nayo iliustawisha umoja wa Wazanzibari bila ya kujali utiifu wao
wa kichama. Serikali hiyo pia ilionekana ikichukuwa hatua kwa
kuzingatia manufaa ya nchi badala ya maslahi ya chama chochote cha
kisiasa.
Huu ni mwanzo mwema. Hatukutaraji kwamba katika kipindi cha mwaka
mmoja serikali hiyo itaweza kuyatatua matatizo yote ya visiwa hivyo.
Matatizo yanayoikabili ni makubwa mno. Kila sekta unayoiangalia na
kuitathmini unaona ina mashakil yasiyosemeka.
Jitihada zinafanywa lakini kila uchao jitihada hizo zinapambana na
uzembe, ubadhirifu wa fedha za umma, urasimu usiohitajika, ulaji rushwa
na ufisadi kwa jumla. Huo ndio uzoefu wa muda mrefu wa watumishi wa
serikali.
Pia ingawa viongozi wamenuia kuujenga umoja wa Wazanzibari bado kuna
kubaguana-baguana katika uteuzi wa watendaji wa ngazi za juu
serikalini. Hiyo ndiyo hali halisi.
Pamoja na hayo serikali haikufanikiwa kuwapatia wananchi huduma za
umeme na maji bila ya kuwakatiakatia. Hizo ni miongoni mwa kasoro
zilizopo. Katika sekta hii ya huduma hizo pia Zanzibar inaweza
kujifunza kutoka visiwa vingine vya Bahari ya Hindi, hasa Mauritius na
Ushelisheli, visiwa vyenye mengi yanayofanana na Zanzibar.
Kwa upande wa uchumi, serikali imejaribu kupandisha bei za karafuu na
inaonyesha ina nia ya kupunguza bei za baadhi ya bidhaa za maisha ya
kila siku. Safari lakini ni ndefu na kuna mengi ya kufanywa na
kusawazishwa, ikiwa ni pamoja na marekebisho ya mishahara ya
wafanyakazi wa serikali ili angalau waweze kukidhi mahitaji yao muhimu
ya kila siku.
La kutia moyo, hata hivyo, ni kuona kwamba serikali imeazimia kwamba
inahakikisha itakuwa na mamlaka au madaraka ya kusimamia shughuli zote
zinazohusu uchumi wa Zanzibar.
La awali katika orodha ya masuala ya kiuchumi ambayo Zanzibar inataka
iwe na madaraka kamili juu yake ni suala la mafuta na gesi asilia ya
Zanzibar. Kwa muda wa zaidi ya miaka 10, suala hili lilizifanya
serikali za Zanzibar na Muungano zisuguane ‘roho’ na mpaka sasa
hapajapatikana ufumbuzi ulio wazi.
Wengi Visiwani wanaendelea kujiuliza iweje mali za asili za Tanzania
Bara kama gesi asilia na maadini zisiwe za Muungano bali za Bara tu na
mafuta na gesi asilia ya Zanzibar yawe ya Muungano?
Kuhusu suala hili msimamo wa serikali ya Zanzibar ni wazi na si wa
kutetereka: inataka iwe na mamlaka kamili ya kusimamia shughuli zote
zinazohusu mafuta yake na gesi asilia kuanzia uchimbaji hadi mauzo na
kwamba, mapato yatayopatikana yataingia katika hazina ya Zanzibar.
Jingine la kutia moyo ni kuona kwamba kwa mara ya kwanza tangu mwaka
1964 hivi sasa Zanzibar ina ajenda yake ambayo ni tofauti na ile ya
mwenzake ndani ya Muungano.
Ajenda hii, kama tulivyoieleza katika makala zilizopita,imepiga hatua
kubwa tangu ianze kupigiwa debe na inavyoonyesha Wazanzibari wengi
hawana wasiwasi nayo. Msingi wake ni kutaka usawa baina ya Zanzibar na
Tanganyika.
Wanaamini kwamba ni sera hii tu itakayoweza kuwakomboa wao na wale
wanaopigania usawa huo kwa upande wa Tanganyika pia. Wanaamini vilevile
kwamba watapata hasara kubwa pindi watapoiacha hiyo Ajenda yao au
watapojiachia wagawike tena kivyama.
Bila ya shaka kusema haya hakumaanishi kwamba Wazanzibari hawautaki
mfumo wa vyama vingi vya kisiasa au kwamba wameuzika upinzani wa
kisiasa, la hasha.
Katika kila jamii lazima kuna watu au mtu mwenye mitizamo na misimamo
tofauti ya kisiasa. Lakini katika jamii za kidemokrasia watu wenye
misimamo tofauti huvumiliana na kuridhiana panapohusika maslahi ya
kitaifa.
Zaidi panapokuja masuala nyeti yenye kuhusu uhuru au uhai wa taifa
lao basi pande zenye kukinzana huzika tofauti zao na huwa na msimamo
mmoja. Huzitupilia mbali ilani za vyama vyao zisije ilani hizo
zikageuka na kuwa laana kwa taifa.
Huo ndio wenye kuitwa umoja wa kitaifa. Ilani za vyama huwa
haziruhusiwi kuwa chachu ya watu kukimbilia mapanga kila wanapozozana
kisiasa.
Ni matumaini ya wengi wa Wazanzibari kwamba mwaka huu wa 2012,
mshikamano huu uliopo sasa utafungua ukurasa mwingine wa malengo
yaliyokusudiwa ya kuijenga Zanzibar mpya na kunyanyua hali za maisha za
watu wake.
Kazi hiyo ni ngumu. Lakini katika karata hizi za kisiasa turufu haimo
mikononi mwa Rais Ali Mohamed Shein na serikali yake tu, bali pia imo
mikononi mwa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, chombo kikuu cha
utungaji wa sheria visiwani.
Wazanzibari ndio waliowapa turufu hiyo tokea walipopiga ile kura ya
kihistoria ya maoni kuunga mkono Maridhiano katikati mwa mwaka 2010.
Mzee Moyo na wenzake wamekwishatoa mchango wao. Ni mchango wa
kihistoria na wenye kuonyesha uzalendo wa hali ya juu.
Sasa taasisi hizo tatu — Rais, serikali na Baraza — zina changamoto
ya kuicheza vizuri turufu hiyo kwani taasisi hizo ndizo zenye dhima ya
kuisarifu hiyo turufu. Wazanzibari wanaukaribisha 2012 huku wakiwa na
matumaini makubwa kwamba hawatovunjwa moyo.
Chanzo: Raia Mwema
Sheikh Ahmed maneno yako mazima kabisa, kinachohitajika ni kwa Wazanzibari kuungana kuikombowa nchi yao badala ya kuhubiri siasa za vyama hii itakuwa ni njia muafaka ya kumuenzi mzee moyo
ReplyDelete