Thursday 26 January 2012

Kwa hili, Jussa Hana haja ya kuomba radhi

Ally Saleh
Nimesoma makala ambayo inaelekea kua imechapishwa katika gazeti kuhusu matamshi ya Waziri wa Muungano wa Ardhi na Makazi, Professa Anna Tibaijuka na kufadhaishwa na udhaifu wa ufahamu wake katika suala linalohusu Hoja Binafsi ya Mheshimiwa Ismail Jussa.

Kama Profesa Ana Tibaijuka angefahamu Hoja Binafsi ya Jussa basi asingetamka kabisa kuwa Jussa aombe radhi, wala asingetamka kabisa kuwa Serikali ya Zanzibar ilirishirikishwa.

Alichosema Jussa na anachokisema Professa Tibaijuka ni vitu viwili tofauti, na kama Professa Tibaijuka alipita baina ya mstari kwa mstari wa Tamko la Jussa basi kwa hakika yeye alipaswa kuilaumu Serikali ya Zanzibar na sio Jussa.

Lakini hata hilo la kuilamumu Serikali ya Zanzibar halipo, kama ambavyo nitaeleza.

Anavyodai Profesa Tibaijuka ni kuwa mchakato si wa leo na jana na kwamba ulianza tokea mwaka 2007 na wakati wote kulikuwa na ushiriki kamili wa maafisa wa Serikali ya Zanzibar na hata kushiriki katika safari ya kwenda New York kukabidhi andiko hilo.

Tukubali hilo la ushiriki wa SMZ, lakini ndio linalifanya jambo hilo kwa ukubwa na upana wake liwe halali? La.

Kwanza ni haramu kwa kuwa mwaka 2009 Baraza la Wawakilihsi lilipitisha Azimio la Baraza kwamba mambo yote kuhusu mafuta na suala la bahari na mipaka yake litoke au litolewe na kusimamiwa na Zanzibar wenyewe.

Kwa hivyo kuanzia 2009 mtu yoyote aliyefanya chochote kinyume na Azimio la Baraza alikuwa anakwenda kinyume na sheria na kinyume na Katiba.

Pili, kuanzia mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka jana kuwa Zanzibar inarudisha mipaka yake yote ilikuwa yake kabla ya kuja kwa Jamhuri ya Muungano, inakifanya kila kitu kinachohusu mipaka kikifanywa na Serikali ya Muungano bila ya ridhaa ya Zanzibar ni haramu na batili.

Najua hapa kunaweza kuwa hoja kwamba Katiba ya Muungano ni Katiba mama na kwa hivyo mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar hayawezi kukiuka matakwa ya Katiba ya Muungano, lakini hilo ni kosa kuamini hivyo kwa sababu katiba hizo mbili ni sawa katika ukubwa wake.

Tatu, Profesa Tibaijuka ajue kuwa Hoja ya Jussa haijakataa uwepo wa mipaka ya Tanzania, lakini ilichokuwa ikitaka ni pande mbili hizi kufahamiana ndani ya mipaka ya Tanzania haki za Zanzibar ni zipi kwa sababu katika bahari kuna suala la uchumi, uvuvi na uwekezaji mambo ambayo yote si ya Muungano,

Bila ya kwanza kumalizana ndani kujua haki za Zanzibar itakuwa kama vile suala la Jumuia ya Afrika Mashariki ambapo katika Mambo 14 ya Afrika Mashariki ni 3 tu ambayo ni ya Muungano na kwa hivyo Tanzania inaisemea na kuichukulia maamuzi Zanzibar katika mambo 11 ambayo si ya Muungano.

Profesa Tibaijuka ni Waziri wa Ardhi, Makazi na Nyumba mambo ambayo yote si ya Muungano, anapataje haki na uwezo wa kwenda kuiwakilisha Tanzania na kuisemea Zanzibar wakati katika wizara yake suala la bahari halimo.

Na hata kama lingekuwemo basi bahari si suala la Muungano na kwa hivyo pande hizi mbili zingebidi zikae upya kuamua kufikiria iwapo ipo au hakuna haja ya kulitia suala hilo katika Mambo ya Muungano.

Au kwa wakati huu kwa kuwa si la Muungano pande hizi mbili lingelikabili vipi suala hilo kama ajenda ya Muungano. Kwamba mawaziri wameshiriki na Serikali kutoa wajumbe hakulifanyi jambo hilo liwe halali kama ambavyo hakulifanyi jambo hilo liwe la Muungano.

Pia Professa Tibaijuka kama angemfahamu Jussa na kwa hivyo mawazo ya Wazanzibari ni kuwa hawaamini jambo lolote linalofanywa na Serikali ya Muungano kuhusiana na Zanzibar na kwa hivyo chochote kile kinapaswa kufikiwa maamuzi na hata kukatibiana na mapema.

Sijui kama Professa Tibaijuka anajua kuwa shaka hii ni kubwa na imeonekana katika mambo kadhaa wa kadhaa na kama anataka afaidi mtizamo wa Wazanzibari juu ya wanavyouona Muungano na pingamizi zake asome makala ya Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar Othman Masoud “ Masuala ya Muungano Yasiokuwa na Majibu.”

Hadaa, mbinu na hila mbali na udhaifu katika utekelezaji na maamuzi umeonekana katika mambo mengi kiasi ambacho inatisha na Muungao huu umekuwa ukenda msege mnege na kupindana mkono kuliko ridhaa ya upande mmoja.

Maamuzi kadhaa yanayofanywa kwa kuwa hayana mashiko ya kikatiba na sheria katika zile zinaozoitwa kero za Muungano, yamebaki kama yalivyo na kwa kweli asilimia 95 ya kero za Muungano ni zile zenye kuibana na kuikandamiza Zanzibar.

Waziri Professa Tibaijuka ambaye ni mgeni sana katika kilinge cha Muungano alipaswa afahamu taswira yote hii na asione malalamiko ya Jussa ni ya kuzuka tu na yasiokuwa na mashiko.

Kwa kumalizia hata kama Serikali ya Zanzibar ilishiriki basi wananchi wanasema wamefanyiwa khiyana na Serikali yao na kwa kupitia kwa Baraza la Wawakilishi wanataka Serikali yao ijue kuwa ilifanya makosa kushiriki katika mchakato huo bila ya kwanza kujua nafasi ya Zanzibar.

Profesa Tibaijuka fikiri jambo moja tu juu ya Serikali ambayo unasema ilishiriki katika mchakato huo. Wewe ni Waziri lakini uliyepewa kufuatana naye kwenda New York alikuwa ni Mkurugenzi Ayoub Muhammed Mahmoud wakati Wizara hiyo ina Naibu Waziri mzima…wewe ulijisikiaje kufananishwa na Mkurugenzi kuwa ndio colleague wako?

Kwa hili Ismail Jussa hana haja ya kuomba radhi. Ni kama alivyosema Muhammed Ghassany mwandishi wa habari wa Zanzibar. Mwizi anakamatwa amemebeba vitu vya watu anasepa navyo na alipokabiliwa akasema, “Mwizi mie…niombeni radhi.”

No comments:

Post a Comment