Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete (kulia), akiendesha Kikao cha
Kamati Kuu ya CCM Taifa kilichokaa jana Mjini Zanzibar kwa ajili ya
kujadili na kuchagua mgombea atakayekiwakilisha Chama cha Mapinduzi CCM
katika uchaguzi mdogo wa Uwakilishi katika Jimbo la Uzini,
Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imemteua mwanachama wake,
Mohammed Raza Daramshi kuwa mgombea wa Uwakilishi jimbo la Uzini mkoa wa
kusini Unguja. Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Itikadi na
Uenezi, Nape Nnauye alisema kwamba kikao hicho kilichofanyika chini ya
Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete kimempitisha Raza baada ya
kuridhika na sifa zake.
Nape alisema, Kamati Kuu pia imemteua Makamu Mwenyekiti wa CCM
(Zanzibar), Dk. Aman Karume kufungua kampeni za CCM za kuwania jimbo
hilo ambazo zitafanyika Januari 28, mwaka huu katika Uwanja wa mpira wa
Ghana.
Alisema wakati kampeni zitafunguliwa na Dk. Karume, ufungaji kampeni
hizo utafanywa na Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi kwenye Uwanja wa mpira
wa Tunduni.
Uchaguzi mdogo wa uwakilishi jimbo la Uzini unafanyika kufuatia
kufariki dunia aliyekuwa mwakilishi wake kwa tiketi ya CCM, Mussa Khamis
Silima aliyefariki kwa ajali ya gari, Septemba 23, mwaka jana.
Kuhusu minong’ono kwamba Raza ana utata katika uraia wake, Nape
alisema Kamati Kuu imelitaza jambo hilo kwa makini lakini haikuweza
kulipa uzito wa kumyima Raza nafasi ya kugombea kwa kuwa hakuna ushahidi
wowote uliowasilishwa kuthibitisha hilo.
“Bado tunao muda wa kutosha, kama yupo mwenye ushahidi wa kutosha
kuhusu hili anaweza kuleta ushahidi, ukiwa na uzito hatutaupuuza”,
alisema Nape.
No comments:
Post a Comment