na Haji Nasor, Pemba
MKUU wa Mkoa wa Kaskazini Pemba, Dadi
Faki Dadi amewataka wananchi kisiwani humo kujadili kwa kina nafasi ya
Zanzibar kwenye Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakati utakapofika wa
kutoa maoni juu ya kuandikwa kwa katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania utakapofika.
Alisema ili kulifanikisha hilo
wakati huo tume itakapopita kukusanya maoni, waache woga, jazba, na
wasiwasi na badala yake wajitarishe vyema kwa kuzungumzia kwa kina
nafasi ya Zanzibar ndani ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Mkuu huyo wa mkoa, alitoa kauli hiyo
ukumbi wa mikutano wa ZSSF, Chake Chake alipofungua mdahalo wa
kuwajengea uwezo wananchi juu ya kutoa maoni ya kuandikwa kwa katiba
mpya ya Tanzania wakati tume itakayoteuliwa itakapopita.
Dadi alieleza kuwa jazba, woga
na fujo hazitosaidia kutoa maoni yao kwenye mchakato huo na badala yake
wawe makini kuyaelezea kwa kina mambo wayatakayo kwenye katiba hiyo, ili
kuona Zanzibar inafaidika mara dufu kwenye Muungano huo.
Aliendela kueleza kuwa, Katiba
katika taifa lolote lile ulimwenguni ndio nguzo kuu na dira kwa
maendeleo ya wananchi husika, hivyo katika uandikaji wa Katiba hiyo ni
vyema kwa wananchi hao kujipanga ili kupata katiba waitakayo.
“Wananchi hamnabudi kuhakikisha
wakati ukifika wa kutoa maoni yenu muwe makini na msisahau kuwa katiba
ndio dira na msingi mkuu wa kufikia maendeleo katika taifa
hili’’,alifafanua Dadi.
Katika hataua nyengine Mkuu huyo
wa Mkoa wa Kaskazini Pemba amewataka wananchi kuifahamu vyema katiba ya
sasa na mambo yaliyomo, hilo litasababisha kuwa na mchango mzuri kwenye
mchakato wa kukusanya maoni kuelekea kuandika Katiba mpya.
Mapema akitoa maoni yake juu ya
mambo yanayopaswa kuingizwa kwenye katiba mpya mwanasiasa, Said Soud
alisema kuwa ni vyema katiba hiyo mpya kubanisha juu ya kuwepo kwa
serikali tatu ili katika mgawanyo wa rasilimali za muungano kuwepo kwa
uswa katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na ya Muungano.
Soud alieleza kuwa Tanzania
ilipaswa iwe na katiba tatu moja ikiwa ya Zanzibar, Tanganyika, na ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo itakuwa ikijumuisha pande mbili
za Muungano huo.
Naye Nassor Harith alisema
katiba ijayo ni vyema ikaweka mgawanyo sawa wa misaada na rasilimali za
Muungano ili nayo Zanzibar ineemeke na matunnda ya Muungano huo na sio
kama ilivyo sasa.
Aidha wananchi wengine
waliochangia kwenye mdahalo walisema, ni vyema kabla ya kupita kwa tume
maalum wananchi wakaendelea kuelimishwa juu ya njia bora na sahihi ya
kutoa michango yao wakati tume hiyo itakayoteuliwa itkapoanza kazi
rasmi.
Nae Mwenyekiti wa mwemvuli wa
Jumuia zisizo za Serikali Kisiwani Pemba, Abubakary Mohamed, ambao ndio
walioandaa mdahalo huo alisema kuwa, wanajipanga ili kuhakikisha
wanagawa kopi za katiba kwa wananchi wa Pemba ili kuzisoma na
kuzifahamu.
Aliongeza kuwa pamoja na ahadi
hiyo ni vyema kwa wale walio na uwezo kuzitafuta katiba zote mbili
kuzisoma na kuzifahamu ili wakati utakapofika waweze kuchangia mambo
wanayoyafahamu.
Mdahalo huo ambao
uliwashirikisha wananchi wa makundi mbali mbali ikiwa ni pamoja na
wasomi, wananchi wa kawaida, wenye ulemavu na viongozi wa jumuia za
kiraia ulikuwa na lengo la kuwajengea uwezo wananchi ili kuwaweka tayari
wakati utakapofika wa kutoa maoni wawe na uhakika.
No comments:
Post a Comment