Friday 20 January 2012

SMZ yatakiwa kutoa maelezo juu ya nyongeza ya masafa ya bahari

Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Pandu Ameir Kificho akiendesha kikao cha baraza hilo kinachoendelea katika ukumbi wa Mbweni nje kidogo ya Mji wa Zanzibar

Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Pandu Ameir Kificho ameitaka Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati kutoa taarifa katika baraza la mawaziri suala la Tanzania kuwasilisha ombi la nyongeza masafa ya bahari kuu kwenye Umoja wa Mataifa. Kificho alisema hivyo baada ya Waziri wa Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati, Ali Juma Shamuhuna kusema kwamba yeye kama wizara taarifa anayo hiyo lakini katika baraza la mawaziri hakuna taarifa ya jambo hilo iliyowasilishwa.

“Nakuomba waziri mheshimiwa Ali Juma Shamuhuna kuleta taarifa hiyo baraza la mawaziri kwa ajili ya kuifanyia kazi pamoja na wajumbe wa baraza la wawakilishi” alisema Spika Kificho.

Kificho, aliwaambiwa wajumbe wa baraza hilo wasubiri na kuiagiza Serikali kulifuatilia suala hilo kikamilifu ili wananchi wa Zanzibar wajue lengo la hatua hiyo kwa serikali ya Tanzania.

Alitoa agizo kwa serikali kutoa maelezo juu ya upande mmoja wa Muungano kupeleka maombi hayo kwa Umoja wa Mataifa bila kuushirikisha upande wa pili.

Aliitaka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kufuatilia jambo hilo kabla ya maamuzi ya Umoja wa Mataifa hayajatolewa kuhusiana na suala hilo kwani suala hilo linahusu pande mbili na wananchi wa Zanzibar wana haki ya kujua mwenendo wa mambo katika nchi yao.

Awali Mwakilishi wa jimbo la Mji Mkongwe (CUF) Ismail Jussa Ladhu alitoa taarifa mbele ya wajumbe wa baraza la wawakilishi kwamba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imewasilisha ombi katika umoja wa mataifa kuomba kuongezewa masafa zaidi ya maili mia mbili katika bahari kuu.

Jussa alitoa hoja ndani ya baraza la wawakilishi akiwataka wajumbe wa baraza hilo lijadili suala hilo kwa uwazi hasa kwa kuzingatia suala hilo lina athari kubwa kwa wazanzibari iwapo litafanikiwa.

Alisema hatua hiyo ya Serikali ya Muungano ni nzito na inayogusa wananchi kwa hiyo, ilitakiwa kuangaliwa vizuri kwani waathirika wakuu huenda wakawa zaidi ni wazanzibari.

Jussa alifahamisha kuwa kwa mujibu wa taarifa iliyotoka ndani ya vyombo vya habari ombi hilo linawasilishwa jana katika ofisi za Umoja wa Mataifa huko New York, Marekani.
“Waheshimiwa wawakilishi hoja hiyo imetugusa sana wananchi wanzanzibari tunaomba muichangamkie, hatutaki mambo ya hewala bwana, hoja ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kusema kuwa Zanzibar imeshirikishwa kwa vile mjumbe mmoja kutoka Zanzibar anaonekana katika picha ya pamoja na mama tibaijuka katika kuwasilisha ombi hilo la umoja wa mataifa hatuitaki wala haitoshelezi” alisema Jussa katika kikao hicho cha baraza la wawakilishi kinachoendelea huko Mbweni Zanzibar.
Kwa upande wake Mwakilishi wa Kuteuliwa na Rasi, Ali Mzee Ali, alisema kuwa ingekuwa jambo la maana suala kama hilo likapigiwa kura kutokana na umuhimu wake kitaifa na sio kuamuliwa na upande mmoja.

Suala la masafa ya bahari kuu limekuwa na mgogoro kati ya Zanzibar pamoja na serikali ya jamhuri ya muungano wa Tanzania kiasi ya baraza la wawakilishi kupitisha azimio kuhusu jambo hilo, ambalo limeingizwa katika orodha ya kero za muungano.

Akitoa ufafanuzi zaidi, Shamuhuna alisema kwamba wizara yake inayo taarifa kamili ya suala hilo ambapo alitakiwa yeye kufunga safari kwenda umoja wa mataifa kuwasilisha ombi hilo pamoja na waziri wa ardhi, nyumba na maendeleo ya makaazi wa jamhuri ya muungano Bi Anna Tibaijuka.

Hata hivyo Shamuhuna alisema kwamba kutokana na kutingwa na kazi nyingi alimtuma afisa wake kufuatana na ujumbe huo kwenda katika safari hiyo.

“Ujumbe huo kwa sasa upo katika umoja wa mataifa na tayari unatarajiwa kuwasilisha ombi hilo ambapo Tanzania baadaye itapangiwa tarehe kwenda kusikiliza shauri lao”.

Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar baadhi yao wamehoji hatua ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania kupeleka maombi Umoja wa Mataifa (UN) kuomba kuongezewa ukubwa wa eneo la bahari na kutaka ufafanuzi wa suala hilo kuwasilishwa ndnai ya kikao hicho, hatua ambayo kimsingi Spika Kificho alikubaliana nao wajumbe hao na kuiagiza serikali kuwaislisha suala hilo barazani hapo.

Tanzania inawasilisha ombi la kuongezwa zaidi masafa ya eneo la bahari kuu kutoka mia mbili na sasa kufikiya mia nne, kama shauri hilo litakubaliwa.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, anaelezwa kuwasilisha hoja hiyo na kuiwasilisha Umoja wa Mataifa (UN) huko New York Marekani.

1 comment:

  1. Shamhuna anauza nchi yetu kwa thamani ndogo ya kutegemea urais 2020, ila wazanzibari mujuwe hivi ni vita anavoviandaa baada ya wao kuondoka katika dunia hii, kwani wanatakiwa wajuwe wao hawatokaa hapa milele, Allah atakwenda kuaadhibu kwa kuigawa nchi tukufu ya kiislamu kwa watanganyika na pia umwagaji damu utakaofuata pia wao watakuwa questionable kwani watoto wetu nna uhakika hawatokubali

    ReplyDelete