Sunday 8 January 2012

Abood Apinga Urais wa Kupokezana

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili Mohammed Aboud Mohammed amesema ni hatari Rais wa Muungano kupatikana kwa zamu katika mfumo wa Muungano wa Tanganyika Zanzibar.

Tamko hilo amelitoa alipokuwa akizungumza katika mahojiano maalum kuhusu maadhimisho ya miaka 48 ya Mapinduzi ya Zanzibar huko Ofisini kwake Vuga mjini Zanzibar jana.

Alisema kuwa na mfumo wa kutoa urais kwa zamu ni mwanzo wa kuligawa taifa na kuvuruga umoja wa kitaifa wa Tanzania.

“Ni hatari kuwa na mfumo wa kutoa urais wa muungano kwa zamu kwa sababu ni mwanzo wa kuligawa taifa vipande,” alisema Waziri Aboud.

Alisema utaratibu unaotumika sasa wa kupata mgombea wa nafasi ya urais kwa kuzingatia sifa na uwezo bila ya kuangalia anatoka upande gani wa muungano ndiyo unafaa kuendelea kutumika kwa sababu umesaidia kuimarisha muungano.

Aidha, alisema kwamba mawazo kama hayo hayafai kupewa nafasi kwa sababu ni mwanzo wa kuanza kujenga ubaguzi jambo ambalo kinyume na misingi ya umoja wa kitaifa.

“Kama leo tukisema kuwepo na zamu ya urais wa Muungano baina ya Tanzania bara na Zanzibar badaye wataibuka watu wakitaka kuwe na zamu urais wa Zanzibar baina ya visiwa vya Unguja na Pemba". alisema.

Alisema kutokana na Tanzania kuwa na mikoa mingi kutaibuka watu wakitaka zamu ya kutoa urais katika mikoa yao kama Mwanza, Tabora, Rufiji, Kigoma na kuwa mwanzo wa kuzorotesha umoja wa Watanzania.

Waziri Aboud alisema utaratibu unaotumika sasa ni mzuri kwa sababu umesaidia kupata viongozi wanaofanyakazi bila ya kuzingatia wanatoka upande gani wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Waziri Aboud alisema katika kipindi cha miaka 48 ya Mapinduzi, Muungano umeleta faida kubwa katika kuimarisha amani na umoja wa kitaifa kwa wananchi wake.

Alisema Muungano umesaidia kujenga misingi ya kiuchumi kutokana na wananchi wa Zanzibar wapatao milioni 1.2 kupata nafasi ya kulitumia soko la biashara la Tanzania bara la watu milioni 40.

Hata hivyo alisema wakati huu wa kuelekea mchakato wa mabadiliko ya katiba ya muungano ni vizuri wananchi wakapata nafasi ya kujadili na kuamua wanataka katiba ya aina gani kwa maslahi ya maendeleo ya nchi na vizazi vijavyo.

“Upande wangu mie binafsi napendelea mfumo wa serikali mbili ndiyo umesaidia kuimarisha Muungano wetu,” alisema.
Chanzi: Nipashe

1 comment:

  1. Duh!!! Huu mtihani wetu wazanzibari, yaani tunaambiwa tuwe kitu kimoja katika kipindi hichi cha kuelekea kwenye katiba mpya lakini kinyume chake hao ambao ni viongozi wa kutuunganisha kwenye kuelekea kwenye kutetea maslahi ya Zanzibar ndio hao kila mmoja ana misimamo yake, huu ni mtihani kwa wazanzibari,
    Labda niwaulize huyu maalim haya mawazo kayatowa kichwani kwake bila ya kushauriana na hawa akina Mohammed Abood au hawa akina Abood wanaendeleza zile siasa za kutegana kwa ajili ya kujijengea maslahi binafsi bila ya kuzingatia maslahi ya ZAnzibar?

    Allah aibariki Zanzibar na awabariki na watu wake na atuepishe na viongozi ambao wanaweka maslahi yao mbele bila ya kuzingatia maslahi ya Zanzibar na Uislamu kwa ujumla

    ReplyDelete