Thursday 19 January 2012

Wapalestina wajifunze kwetu, nasi tujifunze kutoka kwao

Ahmed Rajab
“JITAYARISHE kunyanyaswa na kudhalilishwa,” ndivyo alivyoniambia sahibu yangu mmoja mwenye asili ya Kipalestina kama miaka miwili iliyopita. Alikuwa akiniaga baada ya kunikirimu kwa chakula cha usiku nyumbani kwake mjini Amman, Jordan. Alihisi lazima anionywe hivyo kwa vile siku ya pili alfajiri nilikuwa ninaelekea Israeli kwa mara yangu ya mwanzo.

Nilipanga kuingia Israeli kwa kuivuka Daraja ya Allenby au kama inavyoitwa siku hizi Daraja ya Mfalme Hussein, niweke maskani mjini Jerusalem kwa wiki nzima ili niweza kuizuru miji mingine ya Israeli na halafu nivuke mpaka wa Eratz na kuingia Ukanda wa Gaza kwa ziara ya siku mbili.

Sikutaka kukaa sana Gaza kwa sababu kulikuwa moto. Wiki sita kabla, mabomu ya Israeli yaliitwanga Gaza, yakazifanya shule na majumba yawe vifusi na kuwaua Wapalestina chungu nzima. Na rafiki yangu wa Amman aliponiambia nijitayarishe kunyanyaswa alikusudia kunyanyaswa na ‘vijijanajeshi’ vya Kiyahudi kwenye kivuko cha mpakani cha Eratz cha kuingilia Gaza. Hayo yalinikuta.

La kuudhi zaidi ni kwamba wanyanyasaji ni vitoto vidogo unaweza ukafikiri kama vina umri wa miaka 16. Lakini wana silaha nzito na ufedhuli umewajaa kwenye ndimi zao. Kwa hivyo wao wanakuwa mabwana — ingawa wengine ni wasichana — na wewe unakuwa mtoto.

Kwa hakika, niliyaona mengi Israeli. Nilizifuata nyayo za Yesu Kristo, nikatembea kwenye Mji Mkongwe wa Quds, yaani Jerusalem, nikaswali Ijumaa mbili kwenye msikiti wake wa Al Aqsa. Kiguu na njia nikaizuru miji ya Tel Aviv, Jaffa, Sderot na Be’er Sheva ambao ni mji mkubwa katika Jangwa la Negev.

Niliiona Israeli kuwa ni nchi ya kuta, vizuizi, vikwazo, vipingamizi na vikaratasi vya ruhusa na vibali vya kila aina wanavyotakiwa Wapalestina wawe navyo.  Daima wanadhalilishwa kwa kila namna ya idhilali. Nyumba zao zinabomolewa, wanafukuzwa makwao na lengo la Wazayoni mjini Jerusalem ni kuufanya mji mzima uwe na sura ya Kiyahudi. 

Wapalestina hawaruhusiwi kujenga Jerusalem ya Magharibi kwa Wayahudi lakini Wayahudi wanaruhusiwa kujenga Jerusalem ya Mashariki kwa Wapalestina. Ajabu ni kwamba juu ya yote hayo Wapalestina wanaendelea kucheka, kutabasamu na wanaweza kufanya dhihaka.

Siku moja nilialikwa kwenye Bunge la Israel, Knesset, na Dakta Dov Khenin, Mbunge wa chama cha Hadash, chama pekee cha Wayahudi na Waarabu na ambacho ni cha mrengo wa kushoto na chenye wabunge wanne. Khenin hali kadhalika ni mjumbe wa Kamati Kuu ya chama cha Kikomunisti cha Israel, Maki.

Ofisini mwake bungeni Khenin ametundika picha ya Che Guevara. Nilipomwambia kwamba tathmini yake ya mustakbali wa mzozo wa Israel na Wapalestina inakosa rajua, ikiyaona mambo yote kuwa hayana mbele wala nyuma, yamejaa misiba na mashakil alinijibu kwa kumnukuu mwanafalsafa wa Kitaliana, Antonio Gramsci.

Alinikumbusha kwamba Gramsci akitaka pawepo na ‘pessimism of the intellect, optimism of the will’ yaani pawepo na ukosefu wa rajua ya akili, (lakini) pawepo na msimamo wa kutegemea mazuri katika dhamira.’ Gramsci akitaka hivyo ili ukosefu wa rajua uwe ni kichocheo cha kuchukuwa hatua, na msimamo wa kutegemea mazuri uwe ni ukakamavu wa kuamini kwamba hatua hiyo italeta mageuzi ya maana hata pakiwa na nakama. 

Mbunge huyo alinisikitikia kwamba ubovu wa Israeli ni kuwa hakuna mlingano wa aina yoyote kati ya Waarabu na Wayahudi. Jamii hizo mbili zimegawika vibaya. Hajakusudia Wapalestina na Wayahudi lakini Waarabu wa Israel na Wayahudi wao.

Si tu kwamba Waarabu na Wayahudi wanazungumza lugha tofauti lakini hata misamiati wanayoitumia ni tofauti, dhana (concepts) zao pia ni tofauti katika siasa hata katika utamaduni na katika maingiliano yao ya kijamii ambayo ni madogo mno na pia kwa namna wanavyoangaliana.

Kwa ufupi, pande zote mbili zina hofu. Wayahudi wanatishwa na Waarabu; Waarabu nao wanawaogopa Wayahudi. Lakini aliniambia alitaka nitambuwe kwamba 'Israeli sio tu pahala pa kukutania matatizo lakini pia ni pahala penye uwezekano mwingi,’ yaani kuna mengi yanayoweza kutendeka.

‘Je, Israeli ni dola la ubaguzi wa kikabila?’ Swali hilo nilimuuliza mwandishi habari maarufu Gideon Spiro kwenye mgahawa wa Bookworm Café mjini Tel Aviv. Bookworm, kwa hakika, ni duka la vitabu lakini lina mgahawa na ni mahali ambapo Waisraeli wa mrengo wa kushoto hupenda kukutana.

Sijui nini kiliniandisi nimuulize Gideon swali hilo kwa vile jibu nilikuwa nalo. Labda nikitaka kushangazwa, kumsikia Mwisraeli mwenye siasa za mrengo wa kushoto akiutetea msimamo wa Serikali yake kuhusu suala hilo kwa kukana kwamba dola lao si la kibaguzi.

Siku chache kabla nilimuuliza mwandishi mwingine Wakiisraeli mwenye mawazo ya wastani na jibu alilonipa halikuwa na shaka yoyote. Alisema kwamba Israel ni dola la kibaguzi.

Lakini Gideon, mzee wa miaka 77, akiwa na tabasamu iliyokunjika ikichezacheza kwenye ndimi zake na macho yake yakimetameta, alilipima jibu lake: ‘Ni mfumo wa utawala wa kimbari (ethnocracy)’. Akasita, akapiga fundo la kahawa aipendayo aina ya Cappuccino iliyojaa povu la maziwa na akaendelea kunieleza hivi:

‘Kwa Wayahudi ni utawala wa demokrasia yenye mipaka, kwa Wapalestina walio kwenye maeneo yanayokaliwa na Israeli ni utawala wa udikteta wa kijeshi na kwa Waarabu wa Israeli ni utawala wa demokrasia yenye ubaguzi. Lakini kwa Wayahudi na Waarabu pamoja utawala huo si wa demokrasia,’ alisema.

Gideon Spiro aliongeza kunena kwamba hata miongoni mwa wenyewe kwa wenyewe Wayahudi wanabaguana. Wayahudi wenye asili za kizungu ndio walio tabaka la juu lenye kutawala na Wayahudi waliosalia, hasa walio weusi, wako chini, wa mwisho, fungu la Mungu.

Nilipoingia Ukanda wa Gaza sikuona kitu ila maangamizi na maafa na mji uliovunjwavunjwa na kuangushwa kwa mabomu ya Waisraeli. Ijapokuwa umasikini umezagaa na watu wengi wanaishi chini ya ule uitwao mstari wa ufukara, hata hivyo niliwasikia wakiangua vicheko na niliziona nyuso zao zikiwa na bashasha.

Nilipata wasaa wa kwenda Ramallah, kwenye Ufukwe wa Magharibi, kwa siku moja. Nililizuru kaburi la Yasser Arafat na niliona ushahidi wa jinsi Wapalestina walio ughaibuni wanavyomimina fedha kwao na kukujenga. Hilo ni funzo moja kwetu sisi.

Jingine lililonivutia Ramallah ni namna watu wenye dhamana katika utawala wa huko walivyobobea katika fani zao mbalimbali. Nina hakika kwamba watapopata uhuru wao na kuondoshewa bughdha za 'kukaliwa' na Waisraeli basi watapiga hatua kubwa mbele kuishinda Israeli katika muda wa miaka 20 tu ijayo, juu ya rushwa iliyosambaa.

Katika kutafakari kwangu baada ya kuyazuru maeneo ya Wapalestina yanayokaliwa na Israeli niliona kwamba kuna mingine tunayoweza kujifunza kutoka kwa Wapalestina na yapo ambayo Wapalestina wanayoweza kujifunza kutoka kwetu.

Kwa upande wetu ni kuwa umma unaposema kwa sauti moja kuwa umechoshwa watawala huwa hawana budi ila kuridhia. Hivyo, umma unapovinjari unakuwa na nguvu ya kuleta mabadiliko.

Pili, ni kwamba mabavu au ubabe hauwezi kudumu milele. Huu ni ukweli wa kihistoria. Utawala wa Arafat uliandamwa na kashfa za rushwa na ubadhirifu. Hata mkewe Arafat, Suha, aliingizwa kundini kuwa miongoni mwa waliokuwa wakiramba asali.

Hatimaye umma ulivinjari na wakuu wa Mamlaka ya Palestina akiwemo Waziri Mkuu, Ahmed Qurei walijiuzulu. Lilipoingia wimbi la kujivua gamba waliingia walokuwemo na wasiokuwemo, kila mmojawao akibeba dhamana ya kuwa ndani ya Serikali iliyoshindwa kutekeleza matarajio ya wananchi. Huko ndiko kuwajibika.

Tatu, tunaweza kujifunza kutokana na maendeleo ya kijamii, hasa Ukanda wa Gaza ambako pamoja na vikwazo na hali ngumu inayotokana na ukandamizaji unaoendelea wa dola ya Kiyahudi, utawala wa chama cha Hamas bado unaungwa mkono kwa vile unawajali na kuwafaraji walalahoi.

Lile ambalo Wapalestina wanaweza kujifunza kutoka kwetu ni haja ya kuwa na Serikali ya Umoja wa Kitaifa kama iliyoko Zanzibar. Serikali kama hiyo haikupatikana Palestina tangu chama cha Hamas kilipokishinda chama cha Fatah katika uchaguzi wa mwaka 2006 huko Gaza na kukilazimisha chama cha Fatah kuhodhi mamlaka ya utawala katika Ufukwe wa Magharibi pekee.

Licha ya makubaliano yaliyofikiwa mwishoni mwa mwaka jana jijini Cairo kati ya pande hizo mbili serikali aina hiyo bado haijapatikana. Hivyo panakosekana msimamo mmoja wa Wapalestina dhidi ya Israeli.

Kufanikiwa kwa Palestina mwaka jana kujiunga na Shirika la  Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (Unesco) 2011, kunaibua swali la kwa nini  iwe ni vigumu kwa Zanzibar, licha ya kuhudhuria vikao mbalimbali  vya  shirika hilo mjini Paris?

Zanzibar kwa muda mrefu imekuwa ikipigania kuwa na uwakilishi katika jumuiya kadhaa za kimataifa kama Jumuiya ya Nchi Za Kiislamu  na hata  Shirikisho la Soka Afrika (CAF) na lile la dunia FIFA. Juhudi hizo zimekwama hadi sasa. Pengine serikali imeshindwa kulivalia njuga vya kutosha suala hilo.

Kuna usemi kwamba katika siasa kila kitu kinawezekana. Ikiwa Misri imefikia amani na Israeli, kwa nini pasiwe na uwezekano wa Hamas kukaa pamoja na Israeli kuendeleza mchakato wa kupatikana amani?

Na kwa Tanzania, kwa nini tusiweze siku moja kushuhudia Tanganyika na Zanzibar zikiingia katika enzi mpya na kuwa na uhusiano mpya uliojengeka juu ya msingi wa haki na usawa kati ya nchi mbili zilizo huru? Yote hayo yanawezekana kwani uamuzi wa haki na wenye nguvu ni ule wa umma na sio wa viongozi.
Raia Mwema

No comments:

Post a Comment