Sunday 18 December 2011

Zanzibar sasa wataka zamu urais Tanzania

MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amesema Zanzibar inataka kuwepo kwa muundo ambao utagawa zamu ya nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika katiba.

Maalim alisema Zanzibar haifurahishwi na mfumo wa sasa ambapo Rais anatoka sehemu moja tu ya muungano ambayo ni Tanzania Bara.

“Kipaumbele chetu katika marekebisho ya katiba tunataka kuwepo kwa muundo utakaoonesha na kutamka wazi wazi muda wa zamu ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania...Zanzibar ni sehemu inayounda muungano huo,” alisema.

Seif alisema hayo katika mahojiano na waandishi wa habari hapo katika ukumbi wa baraza la wawakilishi la zamani ambapo alizungumzia mafanikio ya serikali ya umoja wa kitaifa tangu kuundwa mwaka jana.

Alisema kuwepo kwa utaratibu unaotambuliwa kisheria kwa kiasi kikubwa utasaidia kujua kipindi hichi rais anatoka kutoka katika upande upi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Maalim alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa sasa haifurahishwi na utaratibu uliopo sasa ambapo rais wa Jamhuri ya Muungano anatoka Tanzania Bara tu na Zanzibar kubaki na nafasi ya Makamu wa Rais.

Kwa mara ya mwisho, Zanzibar ilitoa Rais wa serikali ya Muungano, Mzee Ali Hassan Mwinyi mwaka 1985 aliyekaa madarakani hadi mwaka 1995 alipompisha Benjamin Mkapa.

Hata hivyo, Maalim aliwataka wananchi wa Zanzibar kujitokeza kwa wingi wakati muda utakapofika wa kutoa maoni ya marekebisho ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kwa ujumla alisema Zanzibar imejizatiti katika marekebisho hayo kuona kwamba maslahi ya Zanzibar katika mchakato huo yanazingatiwa kwa umakini mkubwa.

Alitoa mfano wa visiwa vya Comoro ambapo katika katiba yake vimeweka bayana kwamba mwaka huu raia anatoka kisiwa kimoja na katika uchaguzi unaofuata, raia anatoka kisiwa kingine.

“Utaratibu kama huo ndiyo unaokubalika ambao unataja wazi wazi mwaka huu rais anatoka wapi hatua ambayo ni nzuri kwani inasaidia kuondosha malalamiko ya muungano,” alisema Maalim.
Chanzo: Habari leo

1 comment:

  1. Mara hii ni zamu yetu jamani urais, hao akina lowasa na wenzake wanaojikomba kwa makanisa waache mtindo huo

    ReplyDelete