Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi CUF
Maalim Seif Sharif Hamad amezungumzia tena baadhi ya mambo muhimu
yanayopaswa kuzingatiwa wakati wa kutoa maoni ya katiba mpya ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania na kuwataka viongozi na wananchi kuungana katika
kutetea maslahi ya Zanzibar ndani ya Muungano.
Amesema iwapo Wazanzibari
wataungana na kuwa na sauti moja juu ya jambo hilo, kauli yao itakuwa na
nguvu na upande wa pili wa Muungano utalazimika kuheshimu maamuzi hayo
ya wazanzibari.
“Viongozi na wananchi wote tushikamane
na tuweni na kauli moja juu ya jambo hili, na kamwe tusikubali
kugawanywa kwa maslahi ya nchi yetu”, alisema Maalim Seif.
Maalim Seif ambaye pia ni Makamu
wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar ameeleza hayo katika viwanja vya
demokrasia Kibandamaiti mjini Zanzibar wakati akiwahutubia maelfu ya
wanachama na wananchi waliohudhuria mkutano wa hadhara uliotishwa na
CUF.
Amebainisha baadhi ya mambo
yanayopaswa kuzingatiwa na kuingizwa katika katiba mpya kuwa ni haja ya
Zanzibar kuwa na benki kuu yake ikiwa ni nia moja wapo ya kudhibiti
uchumi wake.
Mambo mengine ni pamoja na
Zanzibar kuweza kuwa na sauti huru juu ya sera zake za fedha na uchumi
ikizingatiwa kuwa suala la uchumi si katika mambo ya Muungano,sambamba
na serikali kuendelea kushikilia msimamo wake wa kutaka suala la mafuta
liondolewe katika orodha ya mambo ya Muungano.
Maalim Seif amefahamisha kuwa
Zanzibar inastahiki pia kuwa na uwezo wa kuweka viwango vyake vya kodi,
pamoja na kuwa na mitaala yake ya elimu inayoendana na mazingira ya
Zanzibar kwa maslahi ya Wazanzibari.
Wiki iliyopita Maalim Seif
alielezea umuhimu wa kuwepo utaratibu maalum wa kikatiba utakaoruhusu
nafasi ya Urais wa Muungano kutumikiwa kwa awamu kati ya Tanzania bara
na Zanzibar, tofauti na utaratibu uliopo sasa ambao hautoi fursa kwa
Wazanzibari kuitumikia nafasi hiyo kubwa kabisa ya uongozi nchini.
Aidha Makamu wa Kwanza wa Rais
alitumia fursa hiyo kutoa mkono wa pole kwa Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania kutokana na baadhi ya wananchi hasa wa mkoa wa Dar
es Salaam kupoteza maisha yao, hali iliyosababishwa na mafuriko
yaliyotokana na mvua kubwa.
Amesema mwisho mwa mwezi huu
chama chake kimepanga kuzitembelea kambi wanazoishi watu walioathirika
na kupoteza makaazi kutokana na mafuriko hayo kwa lengo la kutoa pole na
mchango wake kwa waathirika hao.
Wakati huo huo Naibu Katibu mkuu
wa CUF Zanzibar Mheshimiwa Ismail Jussa Ladhu amewataka wanachama wa
chama hicho kupuuza uvumi juu ya mgogoro ndani ya Chama hicho, na kwamba
chama hakina mgogoro na kiko imara wala hakitumbi.
Amesema uvumi huo unaosambazwa
kupitia vyombo vya habari umekuwa ukitolewa kwa malengo maalum ya
kukivuruga chama, malengo ambayo amesema hayatofanikiwa.
Nae mkurugenzi wa haki za
binadamu, habari na mawasiliano ya umma wa chama hicho Bwana Salim
Bimani amesema bado serikali ya Muungano haijatoa fursa zinazostahiki
kwa Zanzibar katika masuala ya kimataifa ikiwa ni pamoja na kuinyima
nafasi za kibalozi nchi za nje.
No comments:
Post a Comment