TAREHE 06/12/2011
Mheshimiwa, Mgeni rasmi, Waziri wa Nchi Afisi Ya Rais Fedha Uchumi, na Mipango Ya Maendeleo.
Naibu Kamishna TRA,
Waheshimiwa, Wafanyabiashara wa Zanzibar,
Wageni Waalikwa,
Mabibi na Mabwana.
Assalaamu Alaykum.
1)Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu Mwingi wa Rehema kwa viumbe vyake vyote, kwa kutujaliia kuwa na afya njema katika siku hii adhimu ya Mlipa Kodi katika mwaka huu wa 2011.
2)Napenda vile vile kueleza
shukurani zetu za dhati kwa Mamlaka ya Mapato (TRA) Zanzibar kwa
kutupatia nafasi ya kueleza mawazo ya wafanyabiashara katika hafla hii.
Tutajaribu kueleza yale ambayo tunaamini yanaweza kuletea ufanisi
katika kutekeleza jukumu kubwa walilopewa wenzetu wa Mamlaka ya Mapato
(TRA) Zanzibar. Jukumu hilo ni lile la kukusanya kodi kwa lengo la
kukuza uchumi wa Zanzibar na kuendeleza huduma za kijamii kwa wananchi
wake. Kwa ujumla maudhui yangu ni kuwa kodi inayokusanywa Zanzibar ni
kwa maendeleo ya huduma za kijamii na za kiuchumi za Zanzibar.
3)Kwa ujumla kodi ni makusanyo ya
sehemu ya mapato yanayofanywa na utawala wa nchi kutoka wenye kipato
kulingana na sheria ili mapato hayo yaweze kutumika kutoa huduma za
jumla ambazo ni za lazima na haziwezi kutolewa na mtu mmoja mmoja,
katika jamii nzima. Mfano wa hayo ni usalama wa raia, barabara, elimu na
hata ulinzi wa nchi. Orodha wa yale ambayo yanaweza kuhudumiwa kwa
kutumia kodi ni mrefu wala sina madhumuni ya kuelezea zaidi upande huo,
isipokuwa tu kuongeza kuwa kwa ujumla madhumuni yake ni kuleta maendeleo
ya nchi.
Zaidi ya yote hamasa na hiari ya
ulipaji kodi usio wa kushurutishwa unachangiwa sana pale mlipa kodi
anapoona kuwa kodi yake inatumika ipasavyo na kwa uangalifu na kwamba
mwisho ya yote inamrudia mwenyewe kwa kupata huduma stahiki kama vile
matibabu bora, elimu , huduma za maji nk. Hivyo ni jambo la msingi
serikali iwe na uangalizi mkubwa katika suala la matumizi ili ipige vita
aina zote za ubadhirifu ili mlipa kodi aone matunda ya kodi yake.
4)Kwa hapa Zanzibar vyombo
vinavyokusanya kodi mbali na TRA, ni pamoja na Zanzibar Revenue Board,
Mabaraza ya Manispaa, Halmashauri, na Vitengo vyengine vya Idara za
serikali, ambavyo hukusanya “kodi” kwa majina mbalimbali.
5)Kwa upande wetu
wafanyabiashara, tunahisi ingekuwa vyema kama shughuli hii ya leo
ingelijumuisha pia na Bodi ya Mapato Zanzibar, na vyombo vyote vya
ukusanyaji “mapato” kwani kwa mtazamo wetu Bodi hii, pamoja na vitengo
vyengine vya serikali, vinawajibika moja kwa moja kwa Serkali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, na muhimu zaidi vinakusanya kodi kutoka mlipa
kodi mmoja huyo huyo. Mkusanyiko wa vyombo vya ukusanyaji hapa leo
ungeipa serikali picha halisi ya mzigo wa kodi na mzigo wa kuwajibika
kulipa kodi (cost of compliance) kwa mlipa kodi. Katika mipango yake ya
kutaka kodi kutoka kwa wafanyabiashara tunaiomba serikali isisahau
kwamba kuna gharama za kuwajibika na kulipa kodi, mbali na kodi yenyewe.
Serikali ina wajibu wa kupunguza gharama hizo na ikiwezekana
kuziondosha kabisa.
6)Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
kitendo cha kuiweka siku maalum ya mlipa kodi ni kitendo cha
kimaendeleo. Si mara nyingi watu, hata viongozi wanaoelewa yakua walipa
kodi ndio “engine’ ya shughuli zote za Serikali. Mara nyingi watu huhisi
yakua Serikali inazo tu fedha lakini hawajui zinatoka wapi. Kwa hivyo
kitendo
cha kuelimisha jamii juu
ya umuhimu wa kulipa kodi ni kitendo muwafaka kabisa. Ni katika
kuiendeleza dhana hii ndio serikali inapata fursa ya kuanzisha
ushirikiano na walipa kodi katika mfumo wa PPP wenye lengo la kuleta
maendeleo ya wote kwa jumla.
7) Kitendo cha kuwapa tunzo
walipaji kodi wazuri ni kitendo cha kiungwana na chenye kuleta faraja,
kwani wahenga wanasema “mcheza kwao hutunzwa”, hata kama kitakuwa kidogo
lakini hufarijika na kuwashajiisha wengine kuiga mfano mwema na
hatimaye kujenga utamaduni wa kulipa kodi kwa hiari. (Voluntary Tax
Compliance). Haitakuwa vibaya kama katika hafla kama hii siku za mbele
serikali au TRA ikavitambulisha vigezo vilivvyotumiwa kupata walipa kodi
wazuri. Jambo hilo yumkin huenda likawashajiisha na wengine kujaribu
kuvifikia. Kwani wafanyabiashara wakijaribu, hata kama hawakuvifikia
watakua wamechangia katika makusanyo ya kodi.
8) Mheshimiwa Mgeni Rasmi, Labda
tuulizane hii mbinu ya kuwazawadia walipa kodi wazuri inatosha kuongeza
kodi kwa serikali? Sisi tunadhani mbinu hii inachangia sana lakini
haitoshi pekee, na kwa hivyo mbinu nyengine kutoka upande wa sera
itabidi ziangaliwe. Itabidi tuliangalie suala hili katika daraja ya sera
na si ile daraja ya ukusanyaji pekee. Katika daraja ya sera kama
tunataka kuongeza makusanyo hapana budi mbinu nyengine za ziada
zitumiwe ili wigo utanuke, au biashara na uzalishaji utanuke zaidi.
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
9) Katika uwanja wa biashara ni
vipi tutaweza kuongeza makusanyo wakati soko la Zanzibar la watu milioni
moja ni lile lile? Sisi wafanyabiashara tunadhani biashara inaweza
kutanuka kama Zanzibar itajipatia soko kubwa zaidi ya lile la visiwa
hivi viwili. Uanzishwaji wa Jumuia ya Africa Mashariki, pamoja na
Zanzibar kuwa ni sehemu ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania ni nafasi
ambazo zinaweza kutumiwa kisera kuipatia Zanzibar soko kubwa la bidhaa
ambalo litaweza kutoa kodi ya kutosha kwa maendeleo ya Zanzibar. Kwa
mantiki hii mbinu za kulifikia soko la Jumuia ya Africa Mashariki ndio
kazi kubwa ya kuangaliwa watunga sera wetu.
10) Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Naomba kutoa mfano mdogo kihesabu na uzoefu kuhusu namna ya kuitumia
kodi kama nyenzo ya kuongeza mapato. Mfano Zanzibar inatoza wastani wa
kodi ya 30% kwa bidhaa fulani bandarini, na mizigo 1,000 ya bidhaa hizo
ikaingizwa nchini kwa kipindi fulani. Zanzibar itapata kodi sawa na
mizigo 300. Lakini ikiwa itapunguza kodi hadi 5% tu (badala ya 30%) na
mizigo ikapungua bei na ikaingizwa 50,000 (badala ya 1,000) basi
Zanzibar itapata kodi ya wastani wa mizigo (5%x50,000 = 2,500). Ongezeko
la hapa ni kutoka Zanzibar kupata wastani wa kodi wa mizigo 300 hadi
kufikia mizigo 2,500. Papo hapo ieleweke hakuna namna ya mizigo
kuongezeka kutoka 1,000 hadi kufikia 50,000 bila ya kazi hiyo kuongeza
ajira nchini. Na vile vile tujiulize, Jee ni lazima mizigo iongezeke
hadi kufikia 50,000 kutoka 1,000. La, hasha. Hata kama mizigo
ingeongezeka kufikia 7,000 (kutoka 3,000) tu basi tayari wastani wa
mizigo 300 umeshapitwa. Ninalojaribu kusema ni kuwa uko uwezekano
kuongeza mapato ya kodi na ajira hata katika kupunguza viwango.
Tunavyoiona TRA sisi wafanyabiashara wa Zanzibar ni kuwa ina sera maalum
ya kuidhibiti Zanzibar isitumie fursa zilizomo ndani ya Muungano huu,
na mbaya zaidi inaonekana ina mamlaka makubwa ya kutojali maamuzi ya
viongozi wa Jamhuri Ya Muungano. TRA inaonekana ina sera ya kuitumia
kodi kama kidhibiti Zanzibar!
11) Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Wafanya Biashara sote hatuwezi kuwa walipa kodi bora, lakini sote
tunaweza kuwa walipa kodi wazuri na kukaribiana katika ulipaji kodi kwa
mujibu wa biashara zetu zilivyo. Aidha mchango wa kodi katika makusanyo
unaweza kuongezeka kutokana na sera tunazoziomba kuwapa mwanya zaidi
wafanyabiashara wetu kupata uhuru wa kufanya biashara wakiwa hapa
Zanzibar, na kulipa kodi zao hapa Zanzibar bila ya kushurutishwa
kuhamishia biashara zao Tanzania Bara au sehemu nyengine za Africa
Mahariki. Katika mkakati wa kuendeleza Tanzania TRA nao waelimishwe
yakua Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri hii na maendeleo au mafanikio ya
Zanzibar ni maendeleo ya Tanzania na wao wawe watekekezaji wa sera za
kuendeleza Tanzania yote.
12) Mheshimiwa Mgeni Rasmi, hivi
sasa tunaona wafanyabiashara wetu wengi wakihamisha sehemu kubwa ya
biashara zao na kuzipeleka Tanzania Bara na huku wakituambia yakua
vikwazo vya kodi hasa ya bandarini vimewaondokea katika biashara zao za
huko bara. Jee kuna sera mbili za kuendeleza Tanzania. Jee kuna manufaa
yeyote kwa Tanzania kama upande wake mmoja utadumaa. Sisi
wafanyabiashara wa Zanzibar na ambao tunalipa kodi hapa Zanzibar,
tunadhani kuna upotofu katika muelekeo huu wa TRA kuhusu biashara za
Zanzibar; na kwa vile kijiografia Dar-es-salaam ndio njia ya bidhaa za
Zanzibar kuingia katika soko la Africa Mashariki kwenda Uganda, Rwanda
Burundi na Kenya suala hili lina umuhimu wake na tunaomba
lisidharauliwe.
13) Mheshimiwa Mgeni Rasmi, Hapa
naomba kutoa mfano hai wa yanayofanywa na TRA kuhusu biashara za
Zanzibar ziendazo bara na zipitiazo bara kwenda nchi za nje. Super Shine
ni kiwanda kipo eneo la Viwando Vidovidogo Amani kwa sheria za ZIPA
EPZ kama mwekezaji tokea 1996. Kinazalisha audio cassettes, video
cassttes, CDs, DVDs na bidhaa za plastic kwa kuuza 20% ndani ya nchi na
80% nje ya nchi.
Kinyume na
makubaliano ya nyuma na sheria za EPZ kuanzia Aug 2011 wameanza
kulazimishwa kulipa VAT na Import Duty kwa bidhaa zinazoingizwa Tanzania
bara. Kwa maana hii bidhaa zinazozalishwa Zanzibar ni bidhaa za kigeni
zinapoingizwa Bara. Wakati huo huo bidhaa zote za viwanda vya bara km
saruji hailipishwi kodi hizi zinapoingizwa Zanzibar.
14)
Jengine ni kuwa kuanzia Aug 2011 wamelazimishwa kulipa VAT na Import
Duty kwa zile bidhaa wanazosafirisha nje ya nchi. Haya ni maajabu,
bidhaa zinapita tu Tanzania bara na zinatozwa VAT ambayo ni kodi ya
mlaji (wa Zambia) na Import duty wakati bidha hizi ni Exports zinapita
njia tu. (maelezo kamili yapo kwenye pamphlet ambayo tutaomba tukupe
Mheshimiwa Mgeni Rasmi.), pamoja na hotuba yetu hii.
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
15) Sisi wafanyabiashara
tunashukuru kuwa mwaka 2009 tulipatiwa fursa ya kutoa maoni yetu
ingawa ufumbuzi bado umekuwa hafifu, hata hivyo tunathamini umuhimu wa
siku hii ya mlipa kodi, kwa matumaini yakua maoni yetu yatasikilizwa na
kupatiwa ufumbuzi na mengine kuendelea kufanyiwa kazi kwa manufaa ya
Zanzibar. Wakati huo huo kuna masuala mengine yamejitokeza na tunahisi
kuwa ni muhimu kuangaliwa ili kumfanya mlipa kodi wa Zanzibar awe na
shauku ya kulipa kodi na vile vile kuwashawishi wafanyabiashara wetu
waendeleze biashara zao Tanzania nzima pamoja na Africa Mashariki huku
wakiishi na kulipa kodi Zanzibar. Hii ni kwa dhamira ya kuona yakua si
lazima kwa wafanyabiashara wahamie bara ili waendeleze biashara zao
huko. Sasa naomba nieleze, kwa muhtasari yale ambayo tuliyasema mwaka
2009 na ambayo hayakuchukuliwa hatua pamoja na mepya ambayo ni muhimu
kushughulikiwa.
16) Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
ingawa ni vyema kwa walipa kodi kulipa kodi, ni vyema vilivile wapewe
uhuru wa kupata mapato ili walipe kodi.
17) Mheshimiwa Mgeni Rasmi, leo
hii tunazungumzia walipa kodi na mchango wao katika maendeleo. Si vibaya
tukazungumzia wakusanyaji kodi nao mchango wao katika kuhakikisha yakua
kodi inakuwa nyingi hapa Zanzibar ili ikusanywe na kuwasilishwa
serikalini.
18) Mheshimiwa Mgeni Rasmi, hapo
juu nilitoa mfano wa kimahesabu kuhusiana na kodi na mienendo yake.
Mfano ulikuwa wa kuongeza makusanyo ya kodi kwa kupunguza viwango vya
kodi. Sasa naomba kutoa uzoefu tuliouona hapa Zanzibar kutokana na
bidhaa kuongezewa kodi. Itakumbukwa yakua kulikuwa na kodi hapa
Zanzibar zilizowaruhusu wafanyabiashara kuuza kwa bei za chini kulingana
na kwengineko Africa Mashariki katika miaka ya 1990s na mapema ya
2000s. Matokeo ya bei hizo ni kuwa wafanya biashara wengi kutoka nje
kama vile Comoro, Malawi, Burundi, Rwanda, Zambia, Kenya n.k walikuja
kwa wingi kununua bidhaa, na kuzichukua makwao. Mbali na kukuza mfuko wa
kodi walikuwa wakiishi kwenye mahoteli na kutumia huduma za mikahawa,
taxi, mikokoteni nk. Yote hayo yalipotezwa kwa uamuzi wa TRA kuwatoza
kodi za ziada bandarini Dsm hata kama wikuwa wakipita tu njia Dar es
salaam. Katika hili Zanzibar imekosa kila kitu na wafanyabiashara pia
wamekosa kila kitu. Hakuna tena wafanyabiashara kutoka nchi za jirani
wanaokuja Zanzibar kununua bidhaa zao. Bila shaka kodi kwa Zanzibar nayo
imepotea.
19) Mheshimiwa Mgeni Rasmi, Ipo
haja ya kujiuliza kama matokeo ya aina hii yanasaidia kujenga moyo wa
ulipaji kodi katika wafanyabiashara wetu. Ni jambo la uhakika kwamba
kila mlipa kodi atalipa kodi kwa furaha bila kinyongo kwa kiwango
chochote pindipo tu akiona kwamba kodi anayoilipa inarudi kwake kwa
jinsi inavyotumika kweli kweli katika kuleta maendeleo na kutoa huduma
za jamii – afya ,elimu, miundombini n.k. Mifano hii inaonekana wazi
katika nchi za wenzetu zilizoendelea.
20) Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Naomba
kueleza kidogo kuhusu ukubwa wa kodi za Zanzibar kulingana na zile za
bara. Ingawa Corporate tax hapa ni 30% kwa Tanzania yote kodi halisi
yaani “effective tax rate”ni 40% hapa Zanzibar kulingana na uchambuzi
uliofanywa na “Doing Business in Zanzibar. Viwango vya walipa kodi
binafsi (Individual tax rates) pia vile vya Zanzibar ni vikubwa sana
kulinganisha na vya Tanzania bara ingawaje hali ya kipato cha
Wanzanzibari ni kidogo zaidi. Kodi ya Ujuzi wa Maendeleo – Skills
Development Levy (SDL) abayo ni asilimia tano (5%) ya mapato ya
mishahara ya wafanyakazi pia ni kubwa mno na tuna wasi wasi kwamba
haitumiki kwa malengo khasa yaliyokusudiwa. Kulingana na ukubwa wa
uchumi wa Zanzibar viwango hivi vya kodi ni vikubwa na vinadumaza juhudi
ya kujipatia kipato na vivyo hivyo juhudi za kuongeza makusanyo ya
kodi. Kwa upande wa sera naomba ieleweke kua kodi iliyo kubwa ina
punguza shauku ya wawekezaji kuweka mitaji yao katika uchumi husika.
Katika hali ya Zanzibar kodi kubwa na soko dogo ni mchanganyiko maalum
wa kuwatisha wawekezaji na hivyo kupunguza mapato ya kodi, ajira na
mengineyo. Kama washauri tunaomba viwango vya kodi viangaliwe ili
vyenyewe viwe ni vivutio kwa wawekezaji
21) Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Muundo
wa uongozi wa TRA Zanzibar (Organization Structure) bado hautoi mamlaka
ya maamuzi kwa mujibu wa taratibu za TRA, hivyo tunaishauri Serikali
iliangalie suala hili kwa undani zaidi ili maamuzi yanayotolewa na TRA
Zanzibar yaheshimike na yaonekane kuwa ni maamuzi sahihi kama yalivyo
kwa maamuzi ya TRA ya Tanzania Bara. Atawezaje kuisaidia Zanzibar
kupata kodi zaidi ikiwa maamuzi yake hayathaminiwi. Jambo hili nalo
linahitaji ufumbuzi.
22. Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Mwisho,
kwa vile leo ni siku yetu walipa kodi tunapenda kutoa kilio chetu juu
ya haki yetu ya msingi tunayonyimwa ndani ya sheria ya Rufaa za Kodi
(Zanzibar Tax Appeals Act (2006). Sheria hii ilianzishwa kwa misingi ya
kutoa haki kwa mlipa kodi pindi asiporidhika na maamuzi ya vyombo
vinavyokusanya kodi. Tuna hakika kwamba toka ilipoanzishwa bodi hiyo ya
rufaa mwaka 2006 hakuna kesi hata moja waliyoipokea na sisi kama walipa
kodi hatutegemei kupeleka kesi yoyote huko kutokana na ukandamizaji wa
sheria hiyo na jinsi isivyompa haki mlipa kodi. Sheria ina masharti
mawili makubwa kwanza- ni Lazima ikiwa mlipa kodi hakuridhika na kodi
aliyoamriwa kulipa na Kamishna, basi afanye Objection kwa Kamishna wa
chombo cha kodi kinachohusika (TRA/ZRB). Tatizo hapa ni kwamba kama
tokea mwanzo mlipa kodi na Kamishna wameshindwa kukubaliana vipi mlipa
kodi anatakiwa arudi tena kukata rufaa ya awali kwa huyo huyo kamishna
waliyekwisha kukosana na atendewe haki? Pili, sheria inamtaka mlipa
kodi alipe kwanza kodi aliyoamriwa na kamishna kiwango cha asilimia
hamsini (50%), ili kesi yake iweze kusikilizwa. Yupo mlipa kodi ambae
tayari amekisiwa na ameamriwa kulipa jumla ya kodi ya Tshs bilioni sita,
maana yake ni kwamba anatakiwa alipe kwanza bilioni tatu ili
asikilizwe, jambo ambalo milele haliwezekani. Mambo haya mawili
yanamnyima uhuru na haki mlipa kodi, na tunapendekeza yaondolewe mara
moja katika sheria ikiwa kweli tunataka ulipaji kodi wa hiari,
(Voluntary compliance) wenye uwajibikaji (accountability) na usafi
(transparency).
23) Umuhimu wa elimu ya kodi kwa
walipaji na wakusanyaji hauhitaji kusisitizwa zaidi. Lililo muhimu ni
uadilifu katika utendaji wa kazi zetu.
Ahsanteni sana kwa kunisikiliza.
ZNCCIA
Siku ya Mlipa Kodi
Zanzibar.
06/12/2011
Chanzo: Zanzinews
Hizi ndizo hoja za nguvu, hakuna Kiongoza hata mmoja wa Tanganyika anaeweza kujibu, then huu ndio muungano na faida zake , mmoja mkubwa kumnyonya mdogo, ni choyo tu,
ReplyDelete