Jaji wa Mahakama ya Rufaa nchini, January Msoffe amesema marekebisho
ya 10 ya katiba ya Zanzibar yemepora Mamlaka ya kikatiba ya Mahakama ya
Rufaa ya Tanzania ya kusikiliza kesi za haki za binadamu nchini.
Tamko hilo alilitoa jana alipokuwa akifungua maadhimisho ya siku ya
haki za binadamu Duniani katika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar
(SUZA).
Alisema kwa mujibu wa marekebisho hayo ya katiba wananchi wa Zanzibar
sasa hawana haki tena ya kikatiba ya kukata rufaa katika Mahakama ya
Rufaa Tanzania dhidi ya kesi za uvunjwaji wa haki za binadamu
zitakazokuwa zikifunguliwa katika Mahakama Kuu ya Zanzibar.
Jaji Msoffe, alisema katika mabadiliko hayo kuna tatizo kutokana na
kifungu cha 24(3) cha katiba ya Zanzibar kufuta mamlaka ya kikatiba ya
Mahakama ya rufaa Tanzania kupokea na kusikiliza rufaa za kesi za haki
za binadamu zilizofunguliwa Zanzibar na kutolewa uamuzi na Mahakama Kuu
ya Zanzibar.
“Mahakama ya Rufaa ya Tanzania imenyang’anywa uwezo wa kusikiliza
kesi za haki za binadamu kutoka Mahakama kuu ya Zanzibar,” Alisema Jaji
Msoffe.
Alisema kwamba kifungu hicho kinahitaji kuangaliwa upya kwa maslahi
ya wananchi na taifa kwa sababu kina wanyima haki ya kikatiba wananchi
ya kutumia Mahakama ya rufaa Tanzania iwapo watakuwa hawakuridhishwa na
maamuzi ya Mahakama Kuu ya Zanzibar.
Jaji Msoffe, alisema kwamba katiba ya Zanzibar na marekebisho yake
yamebadilisha yaliyomo ndani ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Mwaka
1977 ambayo ilikuwa ikitoa fursa kwa kila mwananchi wa Zanzibar
kufuatilia haki zake Mahakama ya rufaa kama ikitokea hakuridhishwa na
maamuzi ya Mahakama Kuu ya Zanzibar.
Alisema kwamba marekebisho hayo ya katiba yamempa uwezo Jaji Mkuu wa
Zanzibar kuteua majaji watatu wa kusikiliza rufaa na uamuzi wao utakuwa
wa mwisho kama mlalamikaji hatakuwa hakuridhika na uamuzi wa awali wa
Mahakama hiyo.
Kuhusu katiba mpya ya Tanzania, Jaji Msoffe alisema mambo ya haki za
binadamu lazima yaangaliwe upya katika katiba ya Muungano na ya Zanzibar
ili yaendane na wakati katika mabadiliko hayo.
Alisema kwamba mabadiliko hayo ya katiba juu ya haki za binadamu
vizuri kuangalia mifano ya Katiba za Kenya, Afrika Kusini na Uganda kwa
vile katiba za mataifa hayo zimezingatia kwa kiwango kikubwa juu ya
masuala ya haki za binadamu na utawala bora.
Jaji Msoffe alisema mabadiliko ya katiba ya Tanzania lazima
yazingatie haki za binadamu za kiraia, kisiasa haki za kiuchumi na
kiutamaduni katika pande zote mbili za muungano wa Tanganyika na
Zanzibar.
Alisema kwamba wakati umefika kwa wananchi na viongozi kufundishwa
juu ya haki za binadamu kwa sababu wapo ambao hawafahamu juu ya haki za
binadamu katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
“Siyo viongozi wengi wanaofahamu haki za binadamu. Huu ni mtihani
mkubwa kwa sababu wanatakiwa watende haki na haki zenyewe
hawazijui,”alisema Jaji Msoffe huku akipingwa makofi na washiriki wa
Kongamano hilo.
Alisema kutokana na tatizo hilo wananchi wengi Tanzania wamejigeuza
wao kuwa Polisi na Mahakama kwa kuwakamata watu na kuwaadhibu na wakati
mwingine kukatisha maisha yao jambo ambalo ni kinyume na misingi ya haki
za binadamu na utawala wa sheria. Alisema kwamba tatizo la wananchi
kuchukua sheria mkononi lilianzia huko Tanzania bara na sasa limeingia
kwa kishindo Zanzibar.
Alisema kwamba katika kuadhimisha miaka 63 ya tamko la umoja wa
mataifa juu ya haki za binadamu duniani ni vizuri kwa serikali kutoa
elimu ya uraia kwa wananchi wake ili wafahamu haki za binadamu katika
utekelezaji wa majukumu yao na kujiepusha kuchukua sheria mkononi.
Kongamano hilo limetayarishwa na Kituo cha huduma za sheria (ZLSC)
chini ya Mwenyekiti wake Profesa Chris Maina Peter, ambapo Mwanasheria
mwanadamizi kutoka Ofisi ya Mwendesha mashitaka Safia Masoud Khamis,
aliwasilisha katika kongamano hilo mada juu ya serikali katika kuheshimu
haki za Binadamu Zanzibar.
CHANZO: NIPASHE
No comments:
Post a Comment