Tuesday 6 December 2011

Tanzania yakataa ushirikiano ulinzi, siasa EAC

Keneth  Goliama
TANZANIA imekataa Shirikisho la  Ulinzi, Siasa  pamoja na Kinga za Viongozi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na   kutaka mambo hayo  kujadiliwa   kwa upana zaidi  kuhusu uundwaji wake ili wananchi waweze kushirikishwa kutoa maoni yao.

Hata hivyo Baraza la Mawaziri wa Afrika Mashariki, wamekubaliana kwa pamoja kuunda Sekretarieti maalum ya Watalaam  wa kufuatilia mchakato mzima wa maoni ya watu ili waweze kuyawasilisha katika mkutano ujao.

Katika mkutano huo pia kumependekezwa  kuanzishwa kwa Benki Kuu  Umoja wa Jumuiya ya  fedha, Bunge la Jumuiya lenye uwakilishi wa Kisiasa , Mamlaka ya Uangalizi, mahakama ya Jumuiya Afrika mashariki itakayosimamia na kuhakiki  mikataba .

Akizungumza na waandishi wa habari , Katibu Mkuu  Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki , Dk Stergomena Tax alisema Tanzania  haijakubaliana na Uundwaji wa Shirikisho la kisiasa , Ulinzi na Ardhi kwa madai kuwa masuala  hayo  yanahitaji muda zaidi wa kujadiliwa na wadau husika wa Jumuiya.

Aliyataja mambo mengine yaliyokubaliwa  katika  Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Baraza la Mawaziri  kuwa ni pamoja na  Sera ya mkakati wa uendelezaji wa viwanda, Kuimarisha Huduma ya Forodha, Itifaki ya kuzuia na kupambana  Rushwa  sambamba na Itifaki ya kinga na hadhi ya jumuiya zilizopo chini ya Jumuiya.

Dk .Tax Alisema  suala la Ulinzi Shirikishi na siasa katika mkutano huo liliibua mjadala mzito na kuonekana kuwa changamoto inayohitaji kufikiriwa kwa makini ili kuepusha nchi husika kuingia katika migogoro baina ya nchi na nchi pale zitakapo pingana .

 “Nikitolea mfano mambo ya vita katika kushirikiana na kusaidiana na nchi inayopigwa ndani ya Jumuia ya Afrika mashariki linatakiwa kujadiliwa kwa  kina na kufanyiwa marekebisho ili kujua mambo gani muhimu yatakayohusika katika Ulinzi ili kuweza kujulikana  na kukubaliana” alisema Dk Tax.
Katika Mkutano huo  Tanzania imeteuliwa  kuwa Mwenyeji wa Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika mashariki ambaye Makao Makuu yake yatakuwa Zanzibar huku Rwanda ikichaguliwa kuongoza Kamisheni ya Sayansi naTeknolojia  na Burundi ikiongoza Kamisheni ya Utafiti wa Afya.
Alisema upataji wa wenyeji huo unatokana na Tanzania kuwa mwombaji pekee sambamba na kuomba  nafasi zingine  za Afya na Sayansi na Teknolojia  ambazo haikufanikiwa badala  yake ilionekana kuwa na sifa katika Kamisheni ya  Kiswahili.

 Alisema kwa kupata nafasi hiyo  Tanzania itanufaika kwa kiasi kikubwa katika kuinua Uchumi wake kutokana na kuwepo kwa  soko huria  katika sekta za biashara ,viwanda na uwekezaji katika kupunguza vikwazo vya uchumi.

Katika kongamano la Jumuia ya Afrika mashariki kuhusu Maendeleo ya Bonde la ziwa Tanganyika, Katibu huyo alisema ,  walijadili nchi wanachama kuvutia biashara na kuongeza uwekezaji katika nchi wanachama ili kutumia maliasili nyingi zilizopo kwaajili ya  kuinua uchumi.

Dk Tax alisisitiza kuwa Tanzania haina budi kulipeleka  Suala la Ardhi, Ulinzi, Siasa kwa wananchi ili walijadili zaidi kwani matokeo ya awali yalionyesha kuwa  asilimia 75 ya Watanzania walikataa uharakishwaji wa uundwaji Shirikisho hilo .

Dk Tax alisema nchi wanachama zinatakiwa kupima Ardhi na kuanzisha vyombo vya msingi  vinavyotoa haki ya umiliki wa ardhi  kwa wananchi , Kusimamia  mgawo wa faida,  na gharama za mali asili kuwa sehemu ya majadiliano katika mkataba wa uundwaji wa shirikisho la kisiasa.
Kuhusu maombi ya uanachama wa Nchi za Sudan Kusini na Sudan Kaskazini , alisema majadiliano hayo yalifanyika na kwamba  Sudan Kaskazini ilikosa vigezo vya kujiunga  kutokana na umbali uliopo katika mipaka na nchi wanachama .

Alisema Sudan Kusini ilikidhi katika ibara ya tatu ya vigezo vya kujiunga lakini majadiliano zaidi yanaendelea ili kuhakikisha  wanapata mwafaka zaidi katika kuweza kujiunga
Chanzo: Mwananchi

1 comment:

  1. Jee Wazanzibari tunashirikishwa kwenye haya maamuzi ya East African community, kwani sisi ndio victim wakubwa hivi sasa hoteli zote zimejaa wafanyakazi wa kikenya na kiganda na watanganyika tunahitaji kuwa na sera maalum za uhamiaji kwanza kutokana kwamba visiwa vina ukomo, watanganyika wana ardhi mamilioni ya ekas lakini bado wanakuwa wagumu kuingia kwenye ushirika wa ardhi wazanzibari vipi?

    ReplyDelete