Monday 5 December 2011

Mapendekezo ya CUF kwa JK kuhusu Katiba haya

Mazungumzo kati ya Rais Jakaya Kikwete na ujumbe wa serikali yake pamoja na viongozi waandamizi wa Chama cha Wananchi (CUF), yamezaa makubaliano kadhaa, ikiwamo wanasheria pande zote mbili kukutana ili kujadili namna bora ya utekelezaji wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya Mwaka 2011 kama ilivyopendekezwa na CUF.

Pia pande mbili hizo zimekubaliana CUF iwasilishe mapendekezo rasmi serikalini ya namna ya kurekebisha sheria hiyo pamoja na mchakato wa mabadiliko ya katiba.

Makubaliano hayo yalifikiwa na pande mbili hizo katika kikao cha pamoja kilichofanyika Ikulu, jijini Dar es Salaam, Desemba 2, mwaka huu.

Naibu Katibu Mkuu wa CUF Tanzania Bara, Julius Mtatiro, alisema katika kikao hicho, walimkabidhi Rais Kikwete mapendekezo na maoni, kuhusu namna bora ya utekelezaji wa sheria hiyo.

Maeneo hayo ni pamoja na uteuzi wa Makamishna wa Tume ya Katiba pamoja na Sekretarieti yake; hadidu za rejea za Tume ya Katiba; uhuru mpana usio na vikwazo wa wananchi katika kutoa maoni na marekebisho ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na sekretarieti yake. Alisema maeneo, ambayo yanapaswa kuzingatiwa katika kuifanyia marekebisho sheria hiyo ili kuifanya kuwa bora zaidi, ni pamoja na kifungu cha 6 (4) cha sheria hiyo.

Mtatiro alisema kifungu hicho kimeweka sharti linalokataza kiongozi wa chama cha siasa wa ngazi ya taifa, mkoa au wilaya kuteuliwa kuwa mjumbe wa Tume ya Katiba.

Hivyo, alisema wamependekeza marekebisho ya kuondoa sharti hilo, kwa vile wanaamini kuwa katiba licha ya kuwa ni waraka wa kisheria, pia ni waraka wa kisiasa unaobeba malengo na matarajio ya taifa.

Pia wamependekeza watu watakaoteuliwa katika tume hiyo wawe waadilifu, wanaoheshimika na kuaminika mbele ya jamii, wawe na ujuzi na uzoefu wa kutosha katika masuala ya katiba wakiwa na uelewa mpana wa mambo ya sheria, siasa, uchumi na maendeleo.

Alisema kuteuliwa kwa watu wa aina hiyo kutajenga heshima na imani kubwa ya tume mbele ya jamii na hivyo kuondoa wasiwasi na hofu zinazojengwa za kutokuwapo kwa nia ya dhati na ya kweli ya kupata katiba ya kidemokrasia inayoyotokana na Watanzania wenyewe.

Mapendekezo mengine, ni Hadidu za Rejea za Tume ya Katiba kujulikana mapema na kufanywa sehemu ya sheria hiyo kama jedwali na pia ziwe zinatoa uhuru mpana na zisizobana kwa namna yoyote ili tume au wananchi watoe maoni yao kwa maeneo watakayoona yanapaswa kuzingatiwa na kuwamo katika katiba mpya.
Chanzo: Nipashe

No comments:

Post a Comment