Na Mwantanga Ame
WAKATI watanzania wakisubiri kuanza
kwa mjadala wa kuandikwa kwa katiba mpya, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar
Othman Makungu, amewetaka wananchi kuweka mbele mjadala wa uwazi kwa
kuzingatia hoja zenye kujenga uzalendo wataposhiriki kutoa maoni yao
wakijadili kupatikana katiba mpya.
Jaji Makungu, aliyasema hayo
jana wakati akitoa hotuba yake katika kumbukumbu ya Profesa Haroub
Othman Miraji iliyoandaliwa na kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar,
iliyofanyika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA),
Mkunazini Mjini Zanzibar.
Jaji Makungu alisema Profesa Haroub
Othman Miraji katika uhai wake alikuwa ni miongoni mwa alieanzisha wazo
la kupatikana kwa katiba mpya na ili kuweza kumuenzi vyema mawazo yake
hayo Wazanzibari watapaswa kuona wanaweka mbele mjadala wa uwazi kwa
kuzingatia kutoa hoja zenye kujenga uzalendo.
Alisema hivi sasa serikali
imeanzisha mchakato wa kupatikana kwa katiba mpya kwa dhamira njema na
lazima wananchi wataposhiriki kutoa maoni wahakikishe wanatumia vyema
fursa hiyo kwani ndio mustakbali wa taifa kwa kuchagua mambo yepi
wanayoyataka.
“Naomba tujadili kwa kina, uwazi
na kuweka uzalendo mbele kuliko chengine chochote kwani mjadala wa
katiba mpya ni fursa muhimu kwetu hasa Wazanzibari kwani ndio
itayotuletea mustakbali mzuri ule tunaoutaka” Alisema Jaji Makungu.
Alisema jambo la msingi kwa
wanajamii kuona wanajiandaa zaidi kuwa na hoja zitazokuwa na majibu
badala ya mtindo wa sasa wa baadhi ya watu kutoa hoja zinazokataa mambo
lakini wanashindwa kuelekeza namna vipi wanavyotaka liwe.
Akiendelea Jaji Makungu, alisema
wakati wakiwa na kumbukumbu ya Profesa haroub Serikali bado inathamini
mchango wake alioutoa katika uhai wake, kwani ameiwezesha taasisi ya
Mahakama kukabiliana na changamoto mbali mbali katika kusimamia haki na
sheria.
Alisema moja ya mchango huo ni
pale alipoiomba ofisi ya Katiba na Sheria kuanzisha siku ya sheria
Zanzibar, ambayo ikiwa na lengo la kuwakutanisha wadau wa sheria waweze
kutathmini kazi zao na kufahamu mabadiliko na changamoto zilizomo katika
sekta hiyo.
Alisema kutokana na wazo hilo
tayari Wizara ya sheria imeamua kuiweka Mwezi Febuari kuwa siku ya
sheria Zanzibar ambapo mwakani itaanza kuadhimishwa rasmi.
Alisema mawazo ya Profesa Haroub
yalikuwa ni mengi katika kuimarisha utawala wa sheria likiwemo suala la
haki za binadamu na ndio maana aliamua kuanzisha kituo kwa ajili
kuwasaidia watu wenye matatizo ya kisheria ambao hawakuwa na uwezo wa
kuajiri wakili kwa ajili ya kesi zao.
Alisema kuwepo kwa kituo hicho
kutaweza kutoa msaada mkubwa kwa Wazanzibari wasiokuwa na uwezo wa
kuajiri wanasheria katika kesi zao.
Hata hivyo alikiomba kituo hicho
kuendeleza kumbukumbu hiyo kwa kuhakikisha wanakiendeleza kituo hicho
ili jamii ya wazanzibari iweze kufaidika nacho jambo ambalo litaweza
kumuenzi kwa vitendo muasisi huyo.
Mapema mmoja wa wanafamilia ya
marehemu huyo Adalla Miraji, akitoa salamu za familia alisema
wamefarajika kuona serikali ya Tanzania kulikubali wazo la kiongozi huyo
wa familia yao kwani imethamini mchango wake katika kuliimarisha Taifa
la Tanzania.
Alisema kuwepo kwa mchakato wa
kupatikana kwa Katiba mpya ni wazo zuri lakini watanzania watapaswa
kutambua kuja kwa mchakato huo bado hakuondoi amani ya Tanzania kwa
kuanzisha mijadala itayokuwa inaanzisha jazba zitazochafua amani.
Alisema dhamira ya viongozi hao
kuomba katiba ya Tanzania kuandikwa upya haina nia mbaya kwa watanzania
na wataoendesha mijadala hiyo kwa dhamira ya kuchafua amani watakuwa
hawakuwatendea haki waasisi wa wazo hilo.
“Katiba ni kitu muhimu
inahitajika tutumie busara zaidi na sio jazba kwani inaweza kusababisha
lengo lisifikiwe tusijenge mazingira ya kuwagawa watu mshikamano uliopo
tuuendeleze na sio tunyosheane vidole wakati tutapokuwa tukiotoa maoni
kwa kumuona mtu hafai hili tutakuwa hatuwatendei haki walioanzisha wazo
hili” alisema Miraji.
Akiendelea alisema jambo la
msingi ambalo jamii watapaswa kuona wanajiandaa nalo ni kuona wanajenga
mshikamano kwa kuandaa hoja ambazo zitaiwezesha Zanzibar kukaa sehemu
nzuri katika mazingatio bora ya Katiba mpya.
Hata hivyo mwanafamilia huyo,
aliiomba taasisi hiyo kuona inajiandaa kwa kuweka mazingira bora ya
utoaji wa elimu ya uraia kuhusu Katiba iliyopo kutokana na hivi sasa
bado kuna watu ambao hawaifahamu.
Na Mwenyekiti wa Kituo hicho,
Profesa Chris Peter Maina, akitoa maelezo yake alisema ingawa ameteuliwa
kufanya kazi katika shirika la kimataifa, bado mchango wake utaendelea
kuwepo katika kukuza kituo hicho ikiwa ni hatua ya kumuenzi mwanzilishi
wa taasisi hiyo.
Alisema taasisi ya huduma za
Sheria imekuwa ni yenye mchango mkubwa kwa wazanzibari ambapo hivi sasa
wameanzisha utoaji wa huduma za sheria katika majimbo 50 ya Zanzibar
pamoja na vikosi Maalum vya SMZ ambapo watu 65 wanaifanya kazi hiyo.
Alisema hivi sasa wanajiandaa
kuutekeleza mradi mkubwa wa kituo hicho hapo mwakani utaokuwa unahusu
uandishi wa kitabu ambacho kitakuwa kikionesha kesi zote zitazokuwa
zimefikishwa mahakamani, zilizotolewa uamuzi na sheria zote zitazokuwa
zimepitisha na serikali.
Wakati wa mjadala wa katiba
wanahitaji kuzingatia kuwa na nia njema kwa kuhakikisha hawajadili suala
hilo kwa kuangaliana na mchango mtu anayoyatoa.
Jumla ya mada tatu zilijadiliwa
katika kumbukumbu hiyo ikiwemo inayohusu uhuru wa Mahakama na Katiba
mpya iliyotolewa na Mwanasheria Yahya Hamad, ambapo alisema inaonekana
bado haijatulia kutokana na baadhi ya wakati kuingiliwa maamuzi yake.
Mada nyengine ilihusu
ushirikishwaji wa wananchi katika mchakato wa kupatikana kwa Katiba mpya
ya Tanzania iliyowasilishwa na Marcus Albani, ambaye alisema kutambua
katiba ndio nyenzo ya kuendesha nchi na viongozi wazuri lazima waifuate
katiba.
Nae Rais wa Chama Cha Wanasheria
Zanzibar, Awadh Said, akitoa mada juu ya Katiba mpya ya Tanzania maeneo
ya migongano na makubaliano baina ya Zanzibar na Tanzania Bara, alisema
migogoro katika Muungano sio jambo jipya kwani imeanza tangu Muungano
ulipoanza lakini kinachotakiwa kufanyika ni kuona kunakuwa na
majadiliano kila pale wanapoona inafaa kufanywa hivyo
No comments:
Post a Comment