Ahmed Rajab
WATANZANIA ni watu wa ajabu kwelikweli. Angalia namna wanavyomtukuza
na wakati huohuo kumtweza Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Sina dhamiri ya kumpa Nyerere cheo cha uungu. Alikuwa binadamu na
kama tulivyo wana wa Adamu alikuwa na makosa yake; makubwa na
madogodogo. Mengine hayawezi kusameheka, mengine hayawezi kusahaulika.
Hata hivyo, hadi sasa Taifa hili halijapata kiongozi mithili ya
Kambarage. Mithili yake kwa namna alivyoweza kulidhibiti Taifa, kwa
kipaji chake cha kufikiri, kwa ulimi wake, kwa nadhari yake, kwa busara
zake, kwa haiba yake na hata kwa ujanja wake.
Simpambi bure. Miongoni mwa viongozi walioliendesha Taifa hili ni
Nyerere pekee aliyekuwa na nyingi ya sifa za uongozi zinazohitajika.
Waliomfuatia hawamfikii hata ukucha, seuze udole. Naweza kula amini
kuwa hakuna hata mmojawao anayethubutu kujigamba kwamba ana uwezo wa
kumpiku Kambarage. Si kwa hili si kwa lile.
Pamoja na kuwa kiongozi wa chama, wa watu na wa Taifa Nyerere
alikuwa hali kadhalika kiongozi wa viongozi. Hivyo, si ajabu kwamba
aliwaweza Watanzania.
Takriban kila siku utaisikia sauti ya Nyerere walau kwa muda wa
sekunde kadhaa kutoka Redio Taifa ya TBC. Tepu zake zinachezwa kwa
sababu moja tu: kwa sababu amekuwa kama moyo wa Taifa na matamshi yake
yanachukuliwa na Watanzania wengi kuwa ni mwongozo au dira ya Taifa.
Ndiyo maana miaka 13 baada ya mwili wake kulazwa kaburini bado
tunamsikia kila siku akiukaripia ukabila, udini na ulaji rushwa.
Kwa bahati mbaya, nadhani matamshi hayo yanawaingia Watanzania sikio
moja na kutoka sikio jingine bila ya kuwatwanga na kuwafanya
wayatafakari na kuyafuata.
Ndiyo maana mafisadi wanaendelea na ufisadi wao, walaji rushwa
wanaendelea kula rushwa, na wahongaji mirungura wanaendelea vivyo hivyo
na amali yao bukheri wa mustarehe. Wanaochochea ukabila na udini nao
hali kadhalika wanaendelea na chokochoko zao.
Labda wenye kusikitisha zaidi ni hawa Watanzania wa karne hii ya 21 —
hasa vijana — wenye mawazo ya ubaguzi wa kikabila. Wao wamekwishazoea
kuyatoa mawazo hayo bila ya kuona haya au aibu kana kwamba jambo la
kawaida.
Nilishtuka na kuhuzunishwa niliposoma maoni yaliyotolewa kwenye
mablogi mbalimbali ya Watanzania yaliyokuwa yakiuponda msimamo
aliouchukuwa wiki iliyopita Ismail Jussa Ladhu, mwakilishi wa Mji
Mkongwe, katika Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.
Jussa aliongoza upinzani wa wajumbe wa Baraza hilo kutoka vyama vya
CCM na CUF kupinga hatua iliyochukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya
Muungano ya kupeleka andiko lake makao makuu ya Umoja wa Mataifa huko
New York, kudai mipaka ya eneo la kiuchumi la bahari ya Tanzania
itanuliwe.
Ombi hilo liliwasilishwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya
Makazi, Profesa Anna Tibaijuka. Yeye alisema kwamba mpango wa Tanzania
wa kuomba iongozewe maili 150 (kilometa 241.5) kutoka mwambao wake
utaliwezesha Taifa kulifanyia utafiti zaidi eneo hilo kuhusu rasilmali
zilizoko chini ya bahari kwa lengo la kuinua uchumi wa nchi.
Wazanzibari wengi wanaamini kuwa lengo hasa la hatua hiyo ni
kuziingiza kwa ghiliba maliasili za Zanzibar, hasa mafuta na gesi,
katika orodha ya mambo ya Muungano. Ndipo mablogi ya Wabara yalipoanza
kumuandama Jussa.
Bila ya shaka, wanaompinga Jussa wana haki ya kumpinga. Ndivyo
demokrasia ilivyo. Lakini wampinge kwa hoja si kwa kuwa ana asili ya
Kihindi. Mmoja aliandika kwamba angekuwa yeye rais angemrudisha
‘kwao’.
Lakini jama, ninauliza tena, hivyo ni dhambi mtu kuwa na asili ya
Kihindi au ya Kiarabu? Uzalendo uko wapi? Haki na usawa wa uraia upo
wapi? Au ndo tuseme unafuatwa ule usemi wa ‘Baniani mbaya kiatu chake
dawa’? Yaani Baniani aonekane mbaya na abaguliwe ila pale anapokuwa wa
maslahi kwa haohao wenye kumbagua?
Tuna wajibu na dhamana ya kukumbushana kwamba ubaguzi kama huu na
chuki zake ndio uliopelekea mauaji ya kimbari ya Rwanda ya mwaka 1994.
Ajali ya ndege iliyomuua Rais Juvénal Habyarimana mwezi Aprili mwaka
huo ilikuwa kichocheo tu.
Wanamgambo wa Interahamwe na wa Impuzamugambi ndio
waliokuwa safu ya mbele kushika mapanga na kuwaua Watutsi lakini mbegu
za chuki zilikuwa tayari zishamea katika nyoyo za Wahutu.
Halaiki ya watu waliuliwa Kenya baada ya kutangazwa kuwa Mwai Kibaki
ndiye aliyeshinda uchaguzi wa urais wa mwaka 2007. Kwa vile Kibaki ni
Mkikuyu na wengi wa wafuasi wa Raila Odinga, mpinzani wake mkuu katika
uchaguzi huo, walikuwa Wajaluo na Wakalenjini watu wa makabila hayo
mawili wakaanza kuwaingilia Wakikuyu na kuwashambulia.
Wakikuyu nao wakalipiza kisasi kwa kuwashambulia Wajaluo na
Wakalenjini. Roho za watu wasiopungua 1,500 zilipotea bure, maelfu
wakajeruhiwa na maelfu wakawa hawana makazi ya kuishi. Ingawa siasa
zilikuwa kichocheo lakini mzizi wa fitina ulikuwa chuki za kikabila.
Lazima baadhi ya walioandika mitandaoni na magazetini kumshambulia
Jussa kwa kutumia uhuru wake tena ndani ya chombo cha kisheria —
Baraza la Wawakilishi — ama ni kizazi kipya au ni watu wasioijuwa
historia yao.
Lau wangeidurusu historia ya mapambano ya uhuru wangekutana na
michango ya wazalendo wasiokuwa na asili ya Kiafrika. Wangekumbana na
majina ya Watanzania kama akina Amir Jamal (Mhindi), Derek Bryecson
(Mzungu) na Alnoor Kassum (Mhindi) ambaye bado yu hai.
Hao ndio waliokuwa kwenye mstari wa mbele lakini walikuwepo wengi
wengine kama wao wasio na asili ya Kiafrika waliokuwa na hisia za
kizalendo zilizo sawa au pingine hata zaidi ya zile za Watanzania
wengine. Sema tu hawakuwa na umaarufu wa kujulikana kitaifa.
Bado tunaikumbuka aibu iliyolivaa Taifa pale baadhi ya vigogo ndani
ya chama cha CCM walivyoutumia ukabila kumuangusha waziri mkuu
(mstaafu) Dakta Salim Ahmed Salim wakati wa kumtafuta mgombea urais
kutoka chama hicho kwa uchaguzi wa mwaka 2005.
Waliompinga Salim walisema kwamba hafai kwa sababu ana asili ya
Kiarabu. Matamshi hayo yalikuwa ya fedheha na ya kashfa tupu. Tena
ni matamshi ya kinafiki.
Ni matamshi ya kinafiki kwa sababu mbili. Ya awali ni kuwa mtu
yuleyule waliyesema hafai kuwa Rais kwa sababu zao za kijinga
hawakumpinga alipolitumikia Taifa katika nyadhifa nyingine.
Pili, haohao waliokuwa wakimpinga Salim kwa ‘uarabu’ wake hii leo
ndio wenye kumuenzi na kumuengaenga. Hao mahasimu wake wa mwaka 2005
ndio wanaomtaja kama kiongozi mwenye kustahika si kwa kingine ila kwa
moyo wake wa kizalendo. Wakikutana naye wanathubutu kumpa shikamoo na
kutabasamu naye huku wakiutafuta ushauri wake kuhusu masuala ya uongozi
wa Taifa.
Mara tu baada ya kupatikana mgombea urais wa CCM kwa uchaguzi wa
2005 kwa ghafla mahasimu wa Salim wakamvua gamba la uarabu na
wakamvisha joho la uzalendo. Ndio wao ambao sasa wanamtukuza kuwa ni
mzalendo mwenye hekima na maarifa ya uongozi.
Baadhi ya wabaguzi wa Bara wana tabia ya kumhujumu kila Mzanzibari
mwenye kuukosoa Muungano kwa fimbo ya ukabila. Husingiziwa kuwa ama
anaupinga Muungano kwa sababu anataka usultani urudi au pawepo utawala
wa Waarabu au kwa sababu mtu huyo ni Mwarabu (hata ikiwa si Mwarabu) au
kama si Mwarabu basi ni mtumwa wa Waarabu.
Wabaguzi aina hiyo haiwaingii akilini kwamba kunaweza kuwepo
uzalendo Wakizanzibari uliokiuka tofauti za kikabila au hata imani za
kidini.
Katika Zanzibar ya leo wananchi wameshikamana kuzizika tofauti zao
za kisiasa na za kikabila. Lakini bado ziko chokochoko za kikabila
kwani vigogo vya Kizanzibari navyo si vidogo katika mambo haya. Wengi
wao wamo kwenye CCM na wanaupalilia ukabila kwa maslahi yao ya
kibinafsi.
Ithibati ya haya tuliishuhudia wakati wa mchakato wa kumtafuta
mgombea wa CCM katika uchaguzi mdogo wa kumchagua mwakilishi wa jimbo
la Uzini huko Unguja. Mara baada ya kujitokeza mfanyabiashara maarufu
Mohamed Raza Dharamsi akitaka awe mgombea wa CCM vikazuka vitimbakwiri
vilivyompinga kwa sababu babu zake walikuwa Wahindi.
Tuna habari kuwa kigogo mmoja wa CCM ndiye aliyeuandika ule uitwao
Waraka wa Wazee wa Uzini uliojaa chuki za kikabila na uliojaribu
kumuangusha Raza.
Jengine lililopo Zanzibar ni madharau na matusi dhidi ya wenzetu wa Bara. Hizo pia ni hisia za kibaguzi.
Labda umefika wakati wa Tanzania kufikiria kuweka sheria
itayoharamisha na kuwa ni kosa la jinai kutoa matamshi ya kikabila au
kuwabagua watu kwa sababu za kikabila, za kidini au hata za kijinsia.
Inafaa tulitie maanani onyo la Nyerere kuhusu dhambi ya ukabila.
Aliwahi kuonya kwamba Wabara wakishawamaliza Waunguja na Wapemba
wataanza kulana wenyewe kwa wenyewe. Wataanza kusema ‘hawa Wachaga,
hawa Wasukuma.’
Hatari kubwa iliyopo ni kuwa matamshi ya ubaguzi wa kikabila
aghalabu hupaliliwa na baadhi ya viongozi kwa ajenda zao maalumu.
Lakini viongozi hao wasisahau kwamba kiongozi anapopiga zumari la
ukabila na wafuasi wake wakacheza yeye ndiye chanzo cha midenguo ya
wachezaji.
No comments:
Post a Comment