Saturday 18 February 2012

Balozi Iddi: GNU imeunganisha wazanzibari

Na Mwanajuma Mmanga

MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi amesema mabadiliko yanahitajika katika nyanja mbali mbali zikiwemo za kiutendaji ili kuondokana na utaratibu wa kufanyakazi kwa mazoea ambao hauna tija.
Balozi Seif alieleza hayo jana ukumbi wa hoteli ya Bwawani kwenye ufungaji wa mkutano wa pili wa hali ya siasa visiwani Zanzibar, ulioandaliwa na Mpanago wa Utafiti na Elimu ya Demokrasia Tanzania (REDET) wa Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.


Alisema baada ya utulivu wa kisiasa ulioletwa na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliyo katika mfumo wa Umoja wa Kitaifa, jambo la msingi linalohimizwa ni mabadiliko katika utendaji na kuacha na tabia ya kufanyakazi kwa mazoea ‘business as usual’.
Alifahamisha kuwa tabia hiyo haitaleta maendeleo ya haraka kwa wananchi ambao wamekuwa na shauku kubwa ya kupiga hatua za maendeleo mbele baada ya kuwepo kwa utengamano wa kisiasa miongoni mwa Wazanzibari.
Balozi Seif alisema serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yenye mfumo wa Umoja wa Kitaifa, inafanyakazi kwa kuweka mbele maslahi ya wananchi kuliko maslahi binafsi. “Hakuna jambo linaloamuliwa na mtu mmoja peke yake bali serikali nzima chini ya uongozi wa Baraza la Mapinduzi. Tukisema huu ni uamuzi wa serikali uamuzi huo umefikiwa katika misingi hiyo”,alisema Balozi Seif.
Alifahamisha kuwa hakuna kitu kilichoundwa na mwanadamu ambacho hakiwezi kuboreshwa, hivyo changamoto zinazotolewa na wadau zinazoikabili serikali zitafanyiwa kazi. “Serikali itakuwa makini kuangalia mapendekezo hayo ili yaweze kuboresha si serikali tu bali hata taasisi nyengine zinazohusiana na utendaji wa kazi wa serikali yenyewe”, alisema Balozi Seif.
Aidha aliwaeleza wajumbe wa mkutano huo kuwa kuunda kwa serikali ya Umoja wa kitaifa imeamuliwa na wananchi wenyewe kwa kura ya maoni ambapo hivi sasa imekupo faida kubwa ya ushirikiano na kuaminiana miongoni mwa wananchi ikilinganishwa na hapo awali.
Alisisitiza kuwa pamoja na mabadiliko katika serikali kuhitajika, lakini hayapaswi kuwa ya haraka mno kwani huku akitolea mfano nchi ya Urusi ambayo ilitaka kufanya mabadiliko ya haraka.
Katika mkutano huo wa siku mbili wataalamu mbali wa sheria walipata nafasi ya kuwasilisha mada ambapo walionesha changamoto inayoikabili serikali ya Umoja wa Kitaifa katika kuwaletea maendeleo wananchi wake.
Katika mada yake Kaimu Katibu Baraza la Wawakilishi Yahya Khamis Hamad alisema serikali ya Umoja iliyopo Zanzibar inatofautiana na ile ya Kenya na Zimbabwe ambazo ziliundwa baada ya machafuko yaliyotokana na uchaguzi.
Alisema serikali hizo ni za muda wakati ile ya Zanzibar ni ya kudumu iliyobainishwa katika katiba baada ya wananchi kuridhia katika kura ya maoni.

No comments:

Post a Comment