Saturday 18 February 2012

Kiama cha kughushi vyeti chaja

18th February 2012
Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), imetangaza kwamba itaanza kuhakiki vyeti vyote vinavyotolewa na vyuo vikuu nchini na vya nje, pamoja na kuvisajili ili kutambua vyuo vinavyotoa elimu ya juu kiholela.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Katibu Mtendaji wa Tume hiyo, Profesa Sifuni Mchome, alisema imeamua kujaribu kujikita katika mfumo utakaoiwezesha kufanya mabadiliko mbalimbali ili kuboresha utoaji huduma zake.
Profe. Sifuni alisema kuwa katika utaratibu utakaoanza hivi karibuni, suala zima la ithibati litaangaliwa kwa umakini, kwani TCU inataka kuhakikisha programu zote zinatolewa kwenye vyuo vikuu vinavyotambulika na kwamba taarifa kuhusu utoaji elimu ya juu kiholela itatolewa hivi karibuni.
Aidha, alisema kuwa programu zote zitakazotolewa na vyuo vya juu ni lazima zithibitishwe na Tume hiyo na kama zinatolewa nje ya nchi zitambuliwe ikiwa ni pamoja na shahada na stashahada.
Alisema katika kutambua shahada ya kwanza, ya pili na ya uzamivu, Tume hiyo imewasiliana na wataalamu ili wasaidie kuweka kumbukumbu na mawasiliano kati ya TCU na wahitimu wa vyuo, ambapo baada ya mhitimu kujaza fomu ya kwenye mtandao ili kuomba cheti chake kitambulike, atatakiwa kupeleka cheti chake halisi ili kikaguliwe.
Aliongeza kuwa baada ya kukaguliwa, TCU itatoa cheti kitakachoonyesha kuwa cheti cha mhusika kimekaguliwa, na cheti hicho kinaweza kutumiwa na mhitimu sehemu yoyote na endapo watakitilia mashaka cheti chake ataweza kuwaonyesha cheti cha uthibitisho kutoka TCU.
Alifafanua kwamba lengo la utaratibu huo ni kuwasaidia wale wenye vyeti vya nje kuvisajili kwa muda mfupi, ambapo itachukua wiki mbili cheti kusajiliwa.
VYA WALIO KAZINI PIA KUKAGULIWA
Akijibu swali kuhusu wale ambao tayari wapo kazini na wana vyeti kutoka vyuo vya nje ambavyo havijatambuliwa na TCU, Profesa Mchome alisema wamekwisha kupokea maelekezo kutoka kwenye Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii kuwa pia vyeti vyao vinatakiwa kusajiliwa.
“Kwa wale wafanyakazi walio na vyeti vya nje, na ambao wapo kazini, lakini bado TCU haivitambui vyeti vyao, tutatangaza na kutoa muda ili wote wavilete tupate kuvitambua” alisema.
UDAHILI 2012/13
Profesa Mchome pia alitangaza kuanza kwa muda wa udahili wa wanafunzi kwa msimu wa masomo wa 2012/2013, ambapo watahiniwa wamegawanywa katika makundi matatu, ambayo ni waombaji wa moja kwa moja, waombaji wasio wa moja kwa moja, na waombaji wenye sifa zinazolingana.
Alisema kwa waombaji wa moja kwa moja, wanatakiwa kuanza kuomba udahili kuanzia Aprili 23 mwaka huu kutegemea na matokeo ya kidato cha sita kwa wale wote waliomaliza kidato cha sita mwaka 2010, 2011 na 2012, pamoja na wale walio na stashahada za ualimu mwaka 2010, 2011 na 2012.
Kundi la pili ni waombaji wasio wa moja kwa moja wanaotakiwa kuomba kuanzia Aprili 1, mpaka Aprili 30, 2012 waliomaliza kidato cha sita, wenye stashahada za ufundi na wenye stashahada za ualimu waliomaliza sio chini ya miaka miwili iliyopita.
Kundi la tatu ni wenye sifa zinazofanana na hizo, ambao wanaweza kuomba moja kwa moja.
Hao ni wenye stashahada zinazotambuliwa na Baraza la Mitihani la Taifa (NACTE), ambao hawapo kwenye kundi la kwanza wala la pili la waombaji.
Wengie ni wenye stashahada kutoka nje ya Tanzania ambazo zinatambuliwa na NACTE na wengine wenye shahada ambao wanataka kujiunga na programu nyingine za shahada kama uchumi na biashara
Wengine ni wahitimu wa kidato cha sita na wana vyeti vyenye sifa ya kuwaruhusu kujiunga na vyuo vikuu.
Profesa Mchome alisema TCU imeamua kuweka viwango vilivyo sawa katika ufundishaji hasa katika masomo ya biashara na mfumo wa kutambua tuzo za vyuo vikuu ili kuleta ulinganifu kwa vyuo.
Aidha, alisema TCU ina mpango wa kuviunganisha vyuo vyote vilivyopo chini ya NACTE na TCU ili viwe na mfumo mmoja utakaovitambulisha.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment