Na Joyce Mmasi
NI zaidi ya mwaka mmoja sasa tangu Wazanzibari
wafungue kurasa mpya za maisha ya kisiasa pale walipofanya mabadiliko ya
katiba na kuruhusu nchi hiyo kuwa na serikali ya Umoja wa Kitaifa
iliyoundwa na vyama viwili vya siasa ambavyo ni CCM na CUF.
Kuundwa
kwa serikali hiyo kumeleta matumaini kwa wananchi wa nchi hiyo ambapo
wengi wa Wazanzibar wamekuwa wakiiunga mkono serikali hiyo kwa kile
wanachosema imerejesha maelewano, upendo, amani na kutokubugudhiana kama
ilivyokuwa mwanzo.
Macho na masikio ya wapenda amani duniani
kote wamekuwa wakifuatilia maendeleo ya serikali hiyo kwa kuangalia
matokeo yake kufuatia kuundwa na hatimaye kuanza kuwatumikia wananchi
wake hadi sasa ambapo imetimiza mwaka na zaidi sasa.
REDET ni
Mpango wa Utafiti na Elimu ya Demokrasia Tanzania wa Idara ya Sayansi
ya Siasa na Utawala katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Ukiwa
miongoni mwa wafuatiliaji wa maendeleo ya serikali hiyo ya Umoja wa
kitaifa, Mpango huo umefanya semina ya siku mbili mjini Zanzibar kwa
ajili ya kuangalia hali ya kisiasa katika visiwa hivyo ambapo mada kuu
katika mjadala huo uliowahusisha viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa,
wasomi, wanasheria, watendaji wa serikali na watu wa kada mbalimbali
ilikuwa “Uimarishaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar”
Makamu
wa Rais wa serikali ya Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad ambaye ni
miongoni mwa wanasiasa aliyechangia kwa kiasi kikubwa kufanikiwa kwa
mpango wa kuundwa kwa serikali hiyo ya Umoja wa Kitaifa, ndiye alifungua
semina hiyo.
Mwaka mmoja wa SUK Zanzibar
Akifanya
tathmini ya mwaka mmoja wa serikali hiyo, Maalim Seif anaanza kwa
kutamka kuwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar ni imara na kuwa
uimara wake unaongeza mafanikio ya wazanzibar na maslahi ya Watanzania
wote.
“Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar imetokana na
matakwa ya wananchi wenyewe wa visiwa hivi, baada ya kuona mfumo
uliopita yaani mfumo tenganishi hauna faida kubwa katika kujenga umoja
na kukuza maendeleo ya Wazanzibari, ” anasema.
Licha ya uimara
wa serikali hiyo, Seif anaweka angalizo kwa kusema kama ilivyo katika
mataifa mengine, mfumo wowote mpya unapoanzishwa huja na changamoto
mbali mbali, hivyo kuhitajika marekebisho ya hapa na pale, ili kuufanya
uweze kufanikisha malengo yaliyokusudiwa tangu mwanzo.
“Uzuri
ni kwamba Zanzibar ina fursa nzuri ya kuweza kujifunza kupitia sehemu
nyingine za dunia, ambazo zina serikali zenye mfumo wa aina hii”
anasema.
Anaendelea kusema kuwa, jambo la kutia moyo kwa kila
aliyeuunga mkono uamuzi wa kuwa na serikali hiyo ni kuwa, katika kipindi
hiki cha mwaka mmoja wa serikali shirikishi wazanzibar wanashuhudia
faida nyingi.
“Faida moja kubwa ni maelewano makubwa miongoni
mwa wananchi wa Zanzibar. ..... kabla ya kuja kwa utaratibu huu tulikosa
maelewano, hali iliyokuwa imesababishwa kwa kiasi kikubwa na
kutofautiana kwetu katika itikadi za kisiasa na kukosa mashauri ya
pamoja katika kuendesha nchi yetu na kujiletea maendeleo” anasema.
Anasema,
Zanzibar iliyo chini ya mfumo wa serikali shirikishi wananchi wenye
itikadi tafauti pamoja na viongozi wao, wanakaa pamoja wakishirikiana
katika kila uwanja wa maisha na zaidi katika mambo ya kuwaletea
maendeleo yao.
“Sina budi kukiri kwamba changamoto za hapa na
pale zinatokea na hazitaacha kutokea, lakini kutokana na utaratibu
tuliojiwekea kuweka maslahi ya wananchi wetu mbele, changamoto
zinapojitokeza tunakaa pamoja kuzijadili na kuzipatia ufumbuzi kwa
haraka” anasema.
Maalim Seif anasema, Serikali ya Umoja wa
Kitaifa badala ya kupoteza muda mwingi kushughulikia kutatua migogoro,
muda karibu wote unatumiwa kufikiria, kubuni na kupanga mipango ya
maendeleo itakayowanufaisha wananchi ambapo anasema tayari wawekezaji wa
ndani na nje wamevutiwa na hali hiyo na wamo katika mazungumzo na
taasisi husika kuwekeza nchini humo.
Anaongeza kuwa, mafanikio ya
makubaliano ya muafaka yalianza kuonekana katika uchaguzi wa 2010 ambao
anasema ulionesha maendeleo makubwa katika uwanja wa kampeni, kwa vyama
vyote kutumia haki yao ya kufanya kampeni bila ya vizingiti.
“Kampeni
za 2010 zilikuwa za kiungwana. Pamoja na kuwa na hamasa, lakini kwa
kiasi kikubwa hapakuwepo na malumbano, matusi wala kushambuliana. Kila
mgombea alijikita katika kutetea sera na ilani ya uchaguzi ya chama
chake na kujenga hoja za kuwashawishi wananchi watoe kura zao kwa
mgombea na chama chake.... Haya ni maendeleo mazuri na ni wajibu wetu
sote kuyaendeleza na kuyafanya kuwa bora zaidi” anasema.
Hali ya kisiasa Zanzibar baada ya SUK
Maalim
Seif pia anaizungumzia hali ya kisiasa Zanzibar baada ya kuundwa kwa
serikali hiyo ambapo anasema ni shwari na kwamba ile tabia ya kupingana
kwa sababu za kisiasa inaelekea kwisha kabisa, jambo analosema
litawezesha serikali kufanya maamuzi kwa haraka na ambayo yatakubalika
kwa wananchi wa mirengo yote mikubwa na viongozi wao.
“Kwa ujumla
hali ya kisiasa ya Zanzibar hivi sasa ni shwari, na wananchi wanafanya
shughuli zao za kisiasa, kijamii na kimaendeleo bila ya bughudha yoyote.
ni maendeleo makubwa tukilinganisha na tulikotoka” anasema.
Anasema
kuwa na Serikali ya Umoja wa Kitaifa katika mfumo wa vyama vingi ni
hatua kubwa sana, ambayo inaonyesha upevu wa kisiasa ambao utaiwezesha
nchi hiyo kusonga mbele kimaendeleo kwa kasi zaidi.
Ile tabia ya
kupingana kwa sababu tu za kisiasa imepungua sana na kuelekea kwisha
kabisa, jambo ambalo litawezesha serikali kufanya maamuzi kwa haraka na
ambayo yatakubalika kwa wananchi wa mirengo yote mikubwa na viongozi
wao.
Anasema kutokana na matokeo hayo, sasa wawekezaji
wanavutiwa na hali ya amani na utulivu ya Zanzibar, ambayo hujenga
mazingira bora katika shughuli za uwekezaji na shughuli za kiuchumi kwa
jumla.
Changamoto wanazokabiliana nazo
Anasema licha ya
mafanikio hayo, zipo changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo na
kusema miongoni ni kuwa wapo baadhi ya viongozi na watu ambao
hawafurahishwi na Maridhiano ya Wazanzibari.
“Watu hao ni
wachache. Baadhi yao wamekuwa wakijaribu kutia fitna ili kuvuruga
maelewano, kwa bahati mbaya yako magazeti machache yanayotolewa Tanzania
Bara ambayo yamepania kuleta chochoko ili kuvuruga kuaminiana
kulikojengeka......Hata hivyo, kwa vile walio wengi wanaona umoja wetu
huu una faida kuliko hasara watu hao hawatafanikiwa” anasema.
Anaeleza
changamoto nyingine wanayokabiliana nayo ni katika kukidhi matarajio
makubwa ya wananchi juu ya serikali yao, pengine kuliko hali halisi
ilivyo ambapo anasema, wananchi wengi wanatarajia serikali yao itaweza
kutatua kwa muda mfupi kero kubwa zinazowakabili katika maisha, kama
vile mifumko ya bei za bidhaa muhimu na kuwepo hali ngumu ya maisha.
Hata
hivyo anasema tokea serikali hiyo ilipoanza kazi imekuwa ikichukua
hatua kubwa kuhakikisha ugumu wa maisha ya Wazanzibari unapungua, na
wananchi kote Unguja na Pemba wanapata nafuu katika maisha.
“Uhaba
wa fedha serikalini pamoja na hali isiyotarajiwa inayojitokeza
ulimwenguni, kama vile kupanda kwa bei ya mafuta mara kwa mara, kushuka
thamani ya shilingi dhidi ya dola, uharamia katika bahari yetu ya Afrika
Mashariki, pamoja na majanga ya ukame na mafuriko katika nchi
tunazozitegemea zaidi kununua bidhaa za vyakula, vitu hivi baadhi ya
wakati huchangia kutofikiwa malengo yetu’ anasema.
Anaongeza
kuwa serikali inachukua juhudi kubwa kupunguza ukali wa maisha kwa
wananchi ambapo wakati mwingine serikali hulazimika kupunguza kodi za
bidhaa zote muhimu, kwa kuzingatia hali za maisha ya wananchi wetu.
No comments:
Post a Comment