KATIKA wadhifa wa Waziri wa Maji, Ardhi, Nyumba na Nishati
anaoshikilia, Ali Juma Shamhuna amejisahau. Pengine sivyo. Yawezekana
amejaribu ujinga.Ameshiriki kutunga ombi la Serikali ya Jamhuri ya
Muungano bila ya kuihusisha serikali iliyompa madaraka kiutendaji –
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) inayoendeshwa kwa mfumo wa Serikali
ya Umoja wa Kitaifa (SUK).
Ombi hilo liliwasilishwa Umoja wa Mataifa 18 Desemba mwaka jana na
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wa Serikali ya Jamhuri ya
Muungano, Profesa Anna Tibaijuka.
Tanzania inataka kuongezewa eneo la bahari kuu tengefu la
kushughulikia harakati za kiuchumi juu ya eneo la awali la maili 200.
Eneo linaloombwa limo katika maji ya Bahari ya Hindi ambayo Zanzibar
inayatambua kuwa katika eneo lake la utawala.
Shamhuna mwenyewe alikiri kwenye Baraza la Wawakilishi alipotakiwa
kueleza kilichotokea kwa kadri ajuavyo. Kwa sauti ya kujiamini kama
ilivyo kawaida yake, alisema:
“Kama mimi waziri ndio serikali, basi nitasema serikali
tumeshirikishwa. Lakini kama tafsiri ya serikali ni kwa maana ya Baraza
la Mapinduzi, basi niseme hapa kuwa serikali yetu haikushirikishwa
katika suala hili.”
Kweli, namna mjadala ulivyokwenda na ulivyohitimishwa, ilithibitika
kuwa serikali haikushirikishwa maana BLM, nguzo yake kuu, halikujadili
suala hilo. Kiutendaji, BLM ni sawa na Baraza la Mawaziri
kwingineko.Laiti jambo lenyewe lingekuwa jepesi kisera na
lisilokirihisha wananchi wanapolichambua, nina hakika isingekuwa kitu.
Ni jambo zito. Sababu za uzito wake ni nyingi.
Kwa namna hiyo ya kutoishirikisha SMZ, Waziri Shamhuna ameridhia
kuandaliwa kwa ombi linalohusu maliasili ya Zanzibar – bahari kuu.
Waziri huyu mwakilishi wa jimbo la Donge, Mkoa wa Kaskazini Unguja,
anajua fika – sithubutu kusema alisahau yaliyotokea mwaka 2009 – kwamba
SMZ inafanyia kazi azimio la Baraza la Wawakilishi la kutaka suala la
bahari kuu litolewe katika orodha ya mambo ya muungano.
Anajua kuwa bahari kuu ni moja ya maeneo matatu ambayo baada ya
mjadala mrefu ndani ya Baraza yalitungiwa azimio rasmi.Azimio lilitaka
serikali ichukue hatua za kuhakikisha maeneo hayo yanatolewa kutoka
mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Zanzibar imetaka
isimamie matumizi ya maliasili hizo peke yake.
Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, ile iliyoundwa baada ya Zanzibar kupata
uhuru 10 Desemba 1963 na mapinduzi siku 33 baadaye – tarehe 12 Januari,
1964, iliungana na Jamhuri ya Tanganyika na kuundwa jamhuri moja ya
Muungano wa Tanzania.
Jamhuri hiyo ilisabiliwa mambo 11 mahsusi ya kuyashughulikia kiutendaji,
yaliyokuwa yakishughulikiwa na jamhuri mbili kila moja kivyake. Baadaye
orodha ya mambo haya iliongezeka. Maeneo haya matatu ni miongoni mwa
yaliyoongezwa.
Ni mtizamo wa Zanzibar kuwa hatua hiyo imezorotesha kasi ya matumizi
bora ya maliasili hiyo kwa umri wa muungano. Ndipo ilipokuja hoja
barazani ya kuielekeza SMZ kuyatwaa ya kuyasimamia mambo hayo.Yote hayo
yalitokea wakati SMZ ikiwa chini ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Lakini
mjadala wake uliozaa azimio ulifanyika katika hali iliyothibitisha
mshikamano imara wa wawakilishi wa chama hicho na wale wa Chama cha
Wananchi (CUF) kilichokuwa cha upinzani.
Kama suala hilo liliunganisha wawakilishi wakati huo 2009, itakuaje
kipindi hichi ambacho SMZ inaundwa na vyama hivyo kufuatia maridhiano
yaliyohalalishwa kikatiba na wananchi kupitia kura ya maoni ya Julai
2010.
Na hapa ndipo Waziri Shamhuna alipaswa kupazingatia baada ya kuletewa
wazo na waziri mwenzake Profesa Tibaijuka la kupeleka ombi la Tanzania
Umoja wa Mataifa la kutaka kuongezewa eneo la bahari kuu tengefu la
kiasi cha maili 245.
Sema alijisahau. Kwa bahati mbaya amejisahau kwa jambo alilopaswa
kulijua vizuri na mapema. Hilo lilikuwa suala lililohusu wajibu wake
kama waziri msimamizi wa maliasili za Zanzibar.Haitarajiwi kiongozi
mkubwa katika CCM na waziri mzoefu ndani ya Baraza la Mapinduzi kama
yeye ajisahau hivi.
Ingawa makosa ni kawaida kwa binadamu, na kila mtu hukosea, inakuwa
kituko mtu anapojisahau katika wajibu wake. Ukweli, hilo linakuwa ni
kosa la hatari. Na ukweli huo umedhihirika baraza lilipojadili hoja ya
Ismail Jussa Ladhu, mwakilishi wa Mji Mkongwe (CUF), kwa wawakilishi
wenzake wa CCM kumsulubu.
Sasa Shamhuna yupo katika shinikizo za kutakiwa ajiuzulu uwaziri kwa
kutuhumiwa kukiuka maadili ya uongozi na kukiuka mamlaka ya serikali.
Shamhuna amekiri kufahamu ombi tangu maandalizi yake, bali amekiri pia
kuwa kwa tafsiri ya serikali kuwa ni baraza la mapinduzi, basi serikali
haikushirikishwa. Anajua nini hasa maana ya serikali.
Sikiliza asemavyo Ali Mzee Ali, mwakilishi wa kuteuliwa na Rais
(CCM): “Mheshimiwa Shamhuna amejitia kitanzi mwenyewe katika kuelezea
ushiriki wake katika suala hili ambalo baraza tayari limelitolea msimamo
mwaka 2009.”
Hamza Hassan Juma, mwakilishi mwingine kutoka CCM (Kwamtipura),
anasema: “Inakuaje waziri anakuja hapa bila ya kuwa na msimamo juu ya
masuala nyeti kama haya… inabidi ajiuzulu au rais amuwajibishe.” Katika
majadiliano barazani, Hamza alitisha mamlaka aliposema, “Kama hatua (ya
kumtimua) haitochukuliwa, tunaweza kutumia kifungu cha 41 kupiga kura ya
kutokuwa na imani na serikali.”
Pamoja naye, wajumbe wengine waliochangia hoja ni Hija Hassan Hija
(Kiwani, CUF), Mbarouk Wadi Mussa (Mkwajuni, CCM), Asha Bakari Makame
(Viti Maalum, CCM), Omar Ali Shehe (Chake Chake, CUF) na Rashid Seif
Suleiman (Ziwani, CUF).
Asha Bakari, aliyewahi kuwa waziri katika SMZ na sasa Makamu
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa CCM, alisema Shamhuna anapaswa
kuwajibika mwenyewe kabla ya kuagizwa na rais. Yote hayo yalianzia kwa
Jussa, mwakilishi mpya na anayesifika kwa kuchokono mambo serikalini.
Aliwasilisha hoja yake baada ya kusoma taarifa za suala hilo kwenye
vyombo vya habari zikimnukuu Profesa Tibaijuka, alihoji uhalali wa
Serikali ya Muungano kuwasilisha ombi hilo bila ya kushirikisha Zanzibar
kikamilifu na katika hali ya kupingana na azimio la baraza.
Jussa alipendekeza ombi hilo lisitishwe na iwapo Serikali ya Muungano
itapuuza, SMZ iandike barua rasmi ya malalamiko na kuiwasilisha Umoja
wa Mataifa. Akitoa msimamo, kiongozi wa serikali barazani, Makamu wa
Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, alisema suala hilo
litajadiliwa kwenye BLM kwa kuangalia athari za hatua hiyo ya ombi la
kuongezwa kwa eneo la bahari kuu linaloihusisha Zanzibar, na kuja kutoa
kauli rasmi mbele ya Baraza.
Kama wawakilishi wametishia kupiga kura ya kutokuwa na imani na
serikali, ina maana hasa jambo hili ni zito na limewagusa wananchi. Ni
mtihani kwa serikali ya umoja wa kitaifa inayoongozwa na Dk. Ali Mohamed
Shein
Chanzo: Zanzibar Yetu
No comments:
Post a Comment