Thursday 16 February 2012

Ukosefu wa utawala bora ndio unaopalilia ufisadi

WIKI iliyopita waziri mkuu wa zamani wa Angola Marcolino Moco, akiwa ziarani Ureno, alimshambulia vikali Rais José Eduardo dos Santos kwa namna anavyoyatumia madaraka yake kuwatajirisha jamaa zake. Moco anamuelewa vilivyo dos Santos na anaujua nje ndani utawala wake.

Mbali ya kuwa waziri mkuu (1992 hadi 1996) aliwahi kwa muda wa mwaka, kuwa katibu mkuu wa MPLA, chama kinachotawala nchini humo. Nyadhifa hizo alizishika chini ya Dos Santos. Hali kadhalika, Moco ni katibu mtendaji wa kwanza wa Jumuiya ya Nchi Zizungumzazo Kireno (CPLP).

Moco, ambaye bado ni mwanachama wa MPLA, alisema kwamba ayafanyayo Dos Santos yanastahili kulaaniwa kwa sababu ni mambo ya fedheha na ni ya kashfa.

Dos Santos si kiongozi pekee barani Afrika mwenye kushtumiwa kwa kuyatumia vibaya madaraka yake kwa minajili ya kupora mali ya taifa au kwa kuvitumia vyombo vya dola kwa kujitajirisha yeye na wanawe na jamaa zake na wengine walio karibu naye.

Nchini Tanzania tumeshuhudia jinsi Ikulu ya Dar es Salaam ilivyogeuzwa na kuwa pahala pa kufanyia biashara wakati wa utawala wa Rais (Mstaafu) Benjamin Mkapa. Tunashuhudia pia jinsi ufisadi unavyozidi kushamiri nchini hadi leo.

Maovu hayo ya Angola na ya Tanzania yameweza kutendwa kwa sababu ya ukosefu wa ‘utawala bora’ na kutopevuka kwa demokrasia.

Inapofuatwa kikwelikweli, demokrasia huwa ni mfumo wa serikali ya watu, iliyoundwa na watu na kwa ajili ya watu. Tunapoutaja mfumo wa ‘serikali ya watu’ tunaikusudia serikali yenye kuwashirikisha wananchi kupitia wabunge waliowachagua.

Tunaposema kuwa serikali ya kidemokrasia ni ile iliyoundwa na watu tunakusudia serikali inayoendeshwa na waliochaguliwa na wale walio wengi. Huchaguliwa katika uchaguzi mkuu.

Na tunaposema kuwa serikali ya kidemokrasia ni ile iliyopo kwa ajili ya watu huwa tunaikusudia serikali yenye kuwatumikia wananchi.

Hadi sasa tumeizungumzia demokrasia kwa mkato.

Serikali ya kidemokrasia huhimiza na huruhusu haki za uraia kama vile uhuru wa kusema, uhuru wa kuabudu au kutoabudu, uhuru wa kutoa maoni na wa kushiriki katika harakati mbalimbali nchini.

Serikali aina hiyo, kadhalika, husisitiza na hulinda utawala wa sheria pamoja na kuheshimu haki za walio wachache katika jamii.

Kwa jumla, jamii inayoelezewa kuwa ni ya kidemokrasia ni ile jamii ambamo watu wake huonekana kuwa ni sawa mbele ya serikali na mbele ya sheria.

Yapo mengine pia katika mfumo wa kidemokrasia, kwani demokrasia si dhana au mfumo wa kisiasa tu, bali pia ni mfumo wenye kanuni ya kiuchumi na ya kijamii. Serikali inayofuata mfumo huo huwashughulikia wote katika jamii, hasa walio masikini na wengine wasio na hali nzuri za kimaisha.

Serikali hiyo huhakikisha kwamba inatoa huduma nzuri za kijamii ikiwa ni pamoja na huduma ya afya na elimu ya bure, kuwapatia wasiojiweza nyumba za kuishi kwa bei nafuu kama si bure. Huwa ni haki ya kila mwananchi kupata huduma zote hizo; wananchi wote huwa ni sawa na hawabaguliwi si kwa itikadi zao za kisiasa, za kidini, za kikabila, za kijinsia au kwa visingizio vyovyote vile.

Nchi ya kidemokrasia huwaona raia wake wote kuwa watu walio sawa mbele ya sheria. Na hii ina maana kwamba katika utumishi wa serikali watu huwa wanaajiriwa serikalini kwa mujibu wa vigezo maalumu, vikiwa pamoja na sifa za masomo na uzoefu wa kazi. Watu huwa hawaajiriwi serikalini au kupandishwa vyeo kwa sababu ya utiifu wao wa kisiasa au kwa sababu wamekifadhili chama kinachotawala.

Katika mfumo kama huo, ajira serikalini au katika taasisi nyingine za umma huwa hazirithiwi wala huwa hakuna kupendeleana kwa sababu watu wana udugu au ujamaa au usuhuba au kwa sababu muajiriwa ni mtoto wa fulani.

Kwa ufupi, huo ndio msingi wa mfumo wa kidemokrasia.

Jingine lililo muhimu ni kwamba katika mfumo aina hiyo kunakuwa na utenganisho wa madaraka au mamlaka kati ya Baraza la Kutunga Sheria (Bunge), Mahakama na Serikali (Rais). Hakuna mtu mmoja pekee anayekuwa na madaraka au mamlaka ya utendaji.

Badala yake kunakuwa na Katiba ya Kidemokrasia inayohakikisha kwamba vyombo vya dola vina taratibu za kudhibitiana ili kuepusha matumizi mabaya ya madaraka.

Hivyo, Bunge linakuwa na mamlaka ya juu dhidi ya tawi la Utendaji la serikali (yaani Rais) na Mahakama yanakuwa na uhuru kamili na huwa hayawezi kuingiliwa ama na Bunge au na Rais.

Sehemu muhimu ya mfumo aina hii ni kuheshimu haki za kimsingi za binadamu, kama zilivyotajwa na Umoja wa Mataifa katika Tangazo lake la Haki za Binadamu. Tangazo hilo linaharamisha kila aina ya ubaguzi na linasema kwamba wanadamu wote ni sawa na wana hadhi sawa ya utu.

Ili kuustawisha mfumo wa demokrasia ni muhimu kwamba wananchi wawe na uhuru wa kusema, uhuru wa kutoa maoni yao na uhuru wa kukusanyika na kuunda vyama wavitakavyo.

Watu wasioridhika na hali ya mambo ilivyo pia wawe na uhuru wa kueleza manung’uniko yao. Vyombo vya habari navyo lazima viwe huru pamoja na njia nyingine za mawasiliano na visiwe vinazuiwa au vinajizuia vyenyewe kueneza habari zisizopendwa na wakubwa.

Ikiwa hizi ndizo kanuni za kimsingi za demokrasia, basi tunaweza kuzipima nchi na kuangalia iwapo katiba zao zinazikumbatia kanuni hizi au la. Hili ni suala linalostahiki kutiwa maanani nchini kwa vile kuna mchakato utaopelekea kuandikwa kwa Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.

Tunaweza kujiuliza maswali kadhaa. Kwa mfano, kwa kiwango gani hii katiba ya sasa ya Tanzania inakidhi kanuni za kuifanya iwe ‘nchi ya kidemokrasi’, na hasa katika mfumo wa Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar. Kwa vile huu ni Muungano wa nchi mbili zilizo huru inavyotakiwa ni kwamba serikali yake iendeshwe kwa msingi wa usawa baina ya sehemu hizo mbili.

Swali jingine ni iwapo katiba ya sasa inaupa upande mmoja wa Muungano madaraka makubwa sana kushinda upande mwingine, labda kwa sababu ya ukubwa wake au wingi wa watu wake.

Tunaweza pia kujiuliza iwapo ni sawa katika jamii ya kidemokrasia kuwa na Rais Mtendaji aliye na madaraka yasiyo na kikomo? Katiba ya sasa ya Tanzania ina vifungu vyenye kumpa Rais nguvu kubwa mno bila ya kuwa na taratibu za vyombo vingine vya dola za kumdhibiti asiyatumie vibaya madaraka yake.

Ili kuweza kuipima nchi na kuingalia kama ni ya demokrasia changa au ya udikteta unaoendelea itatubidi tuyaangalie madaraka ya Rais, ya Bunge na uhuru wa Mahakama pamoja na ubora wa sheria za nchi na nguvu zisizoshindika za taasisi za serikali, urasimu ambao unapalilia hongo na ulaji rushwa.

Kuna kigezo kingine ambacho tunapaswa kukizingatia. Nacho ni jinsi Jumla ya Pato la Taifa (GNP) linavyogawiwa kwa wananchi.

Ni muhimu pia kuangazia jinsi fedha chafu, yaani zile zinazopatikana kwa njia mbalimbali za kifisadi, zinavyokuwa na dhima katika uchumi wa taifa na jinsi ‘zinavyofuliwa’ na kusafishwa kwa kuingizwa katika uchumi.

Kwa hiyo, tukiyaangalia yote hayo tutaona kwamba demokrasia ni mfumo wa kikatiba na wa kiserikali wenye kuhimiza pawepo maridhiano katika siasa pamoja na utaratibu wa kuihalalisha serikali.

Tunapoutaja ‘utawala bora’ tunakuwa tunauzungumzia uhalali wa serikali kutawala na mahusiano yaliyopo baina ya serikali na wanaotawaliwa. Utawala bora ni sehemu muhimu ya utawala wenye kujigamba kwamba ni wa kidemokrasia. Na ni lazima huo utawala bora uwe unakwenda sambamba na utawala wa sheria na uwaridhishe wananchi kwamba serikali ipo ili iwatumikie wananchi na si wananchi wapo kuitumikia serikali.

Katika jamii yenye utawala bora, serikali hupata uhalali wake kutoka kwa wapigaji kura. Kwa hakika, uchaguzi ni kijenzi muhimu cha ‘utawala bora’. Uchaguzi huwa unafanywa baada ya vipindi maalumu, unakuwa wa ushindani, unakuwa wazi, na unakuwa ‘huru na wa haki’ na washindani au wagombea wote wanapata fursa sawa. Chaguzi zinazofanywa namna hiyo aghalabu huwa na matokeo ambayo wagombea wote huyakubali wakitambua kwamba hakujapita mizungu yoyote wakati wa uchaguzi.

Nchi nyingi za Kiafrika zisemazo kwamba zina misingi ya demokrasia na utawala bora zimeunda wizara au idara za serikali zenye kushughulikia masuala haya pamoja na shughuli za kikatiba.

Wizara kama hiyo ipo Zanzibar. Huo ni mwanzo mwema; lakini si kuanzishwa kwa wizara aina hiyo kutakoifanya nchi iwe na utawala bora au muovu. Nchi itakuwa ni yenye utawala bora pale wananchi wake watapokuwa na uhuru wa kimsingi, maisha mazuri na watapokuwa wanalindwa na sheria bila ya ubaguzi au mapendeleo.

No comments:

Post a Comment