Saturday 25 February 2012

KWA NINI TUUJADILI MUUNGANO


Hoja 18 za Baraza la Katiba, juu ya Kwa Nini Tuujadili Muungano ni hizi zifuatazo: Tutakuwa tunawaletea hoja moja moja ili kuongeza ufahamu wa nini tufanye kama wazanzibari katika kuchangia katiba mpya ijayo
 1.  Kuundwa kwake
 Kuundwa kwa Muungano wa Tanzania kuna udhaifu wa kisheria kama ambavyo imeshawahi kuelezwa mara kadhaa na wanasheria na wanasiasa kadhaa wa kadhaa. Ni Muungano ambao ulianzishwa kwa utashi wa viongozi wawili wa kisiasa wakiwa ni Marais wa nchi mbili huru, lakini mambo ya msingi yakiwa hayajazingatiwa.

Ni utaratibu unaokubalika kimataifa na kisheria hata kufuatwa na nchi za Jumuia ya Madola, ambazo kwa kuwa Zanzibar na Tanganyika zote zilikuwa kwa njia moja au nyengine chini ya Himaya ya Uingereza, kwamba viongozi wakuu wa nchi wanaweza kuingia Mikataba ya Kimataifa kwa niaba ya nchi zao.Hivyo viongozi wakuu wawili marais Aman abeid Karume na Julius Nyerere wakaingia mkataba wa kuunganisha nchi zao

Utiaji huo wa saini ulishuhudiwa na viongozi kadhaa wa kila upande wakiwamo kwa upande wa Zanzibar Ali Mwinyigogo, Kassim Hanga, Abdulaziz Twala na kwa upande wa Tanganyika walikuwepo akina Ali Mwinyi Tambwe, Bhoke Munanka na Osca Kambona. Utiaji saini wa Mkataba wa Muungano haukuhalalisha kukubaliwa na kuridhiwa kwa Muungano na watu wa Zanzibar.

Na ndipo Rais Abeid Amani Karume wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar akaingia mkataba na Rais Julius Nyerere wa Serikali ya Tanganyika, lakini ilikuwa lazima hatua hiyo ifuatiwe na ile ya kuridhia Mkataba huo, na Mabunge ya nchi zao - hili ni sharti kwa mujibu wa mfumo wa kisheria, lakini pia lilifanywa ni sharti ndani ya Mkataba wa Muungano, (Kifungu cha 8) ambacho kilisema wazi kuwa baada ya kusainiwa na viongozi hao Mkataba huo ulilazimika upate ridhaa ya mabunge ya nchi zao.

Upande wa Tanganyika ulitimiza sharti hilo kwa kupitishwa Sheria Namba 22, 1964, ambapo nakala kivuli ya Mkataba wa Muungano iliambatanishwa, na huku sote tunajua kuwa hadi hivi leo nakala halisi ya Mkataba wa Muungano haijaonekana hadharani.

Nakala halisi ya Mkataba wa Muungano imeshindwa kutolewa na Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, ambaye alisema katika Hati ya Kiapo kwenye kesi Namba 20, 2005 iliyofunguliwa na Rashid Salim Adi na wenzake katika Mahkama kuu ya Zanzibar, kwamba Serikali ya Zanzibar haina hati halisi ya Muungano.

Bila ya shaka hili ni suala sio tu la kushangaza lakini ni la aibu kwa Serikali kukosa kuwa na Mkataba halisi wa kimataifa wa Muungano, na kwa hivyo si suala ambalo linafaa liendelee kufunikwa daima dawamu.

Kama ambavyo tumesema wakati Tanganyika iliridhia Mkataba huo Zanzibar haikufanya hivyo jambo ambalo Rais wa Pili wa Zanzibar Aboud Jumbe katika kitabu chake cha The Partnership amesema ni mgogoro kamili wa kisheria.

Zanzibar ikiwa ndio kwanza inatoka kwenye Mapinduzi na kusimamishwa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1963, ilitunga Sheria iliyoitwa Legislative Powers Decree, Namba 1, 1964 ambayo ilitoa mamlaka ya kutunga sheria kwa Baraza la Mapinduzi, na kwa hivyo Baraza hilo la Mapinduzi lingeweza kuwa Bunge la kuridhia Mkataba wa Kimataifa uliokuwa umetiwa saini baina ya Karume na Nyerere na sharti hilo likiwa limetajwa kwenye Mkataba wenyewe.

Lakini watu waliokuwa na dhamana ndani ya Serikali wakati huo pamoja na Jumbe wamesema Baraza la Mapinduzi halikuridhia Mkataba huo. Ikumbukwe wakati huo Baraza la Mapinduzi lilikuwa na mamlaka ya kikatiba ya kutunga sheria.

Wolfgang Dourado, aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar kwa wakati huo, kauli yake ni hiyo hiyo na zaidi ananukuliwa akisema hivyo katika Mkutano wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS) 1985,  na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Baraza la Mapinduzi kwa wakati huo, Salim Rashid amesema katika Hati ya Kiapo kwenye kesi ya Rashid Salim Adi na Wenzake kuwa Mkataba wa Muungano haukuridhiwa na Baraza la Mapinduzi.

Halafu pia msomi anaeheshimika katika uwanja wa Katiba, Professa Issa Shivji amethibitisha kupitia vitabu vyake viwili kile cha 1990 Legal Foundations of the Union of Tanganyika and Zanzibar na kile cha 2008 Pan-Africanism or Pragmatism. Lessons of the Tanganyika-Zanzibar Union kuwa hakuna pahala popote pale ambapo Mkataba wa Muungano inaonyesha umeridhiwa na mdau wa pili yaani Zanzibar.

Ila bila ya shaka hoja inakuja kuwa hakuna ambae amechukua hatua moja mbele ya kusaili uhalali wa Muungano ambao unakosa sifa muhimu na awali kabisa ya kuridhiwa au tuseme kwa usahihi zaidi kukosa kuridhiwa na upande mmoja na kwa hivyo ukaruhusiwa kusonga mbele hadi leo.

Na hio kwa wakati huu ndio sababu muhimu ya kujadili Muungano, maana kama sharti muhimu hilo halikutimizwa ina maana kila kilichofuatia kinakosa uhalali wa kisheria na wakati huu tukijadli kuja kwa Katiba Mpya hilo lazima liwe mbele kwenye ajenda

No comments:

Post a Comment