Ahmed Rajab
YAFUATAYO ni masimulizi mafupi ya kipindi kifupi cha Mapinduzi ya
Zanzibar ya Januari, 1964 yaliyoipindua serikali ya ubia ya chama cha
Zanzibar Nationalist (maarufu Hizbu) na kile cha Zanzibar and Pemba
People’s Party (ZPPP). Tunaangazia nini hasa kilitokea usiku wa Jumamosi
Januari 11, yaliyojiri siku ya pili yake na mwezi mzima wa Januari,
mwaka 1964 .
Tumeyakusanya masimulizi haya baada ya kuzungumza na walioshiriki
katika Mapinduzi hayo ambao baadaye walisaidia kudhibiti madaraka na
kuunda taasisi zilizoziba pengo la Serikali iliyopinduliwa ya Waziri
Mkuu, Muhammed Shamte Hamadi.
Usiku wa manane wa Januari 11, makada wapatao 200 wa Umoja wa Vijana
wa Afro-Shirazi (Afro-Shirazi Youth League) walielekea kwenye kambi ya
polisi ya Ziwani, nje kidogo ya mji huko Unguja.
Wakiongozwa na Yusuf Himid wapinduzi hao hawakukabiliwa na upinzani
walipofika Ziwani ila waliikuta ghala ya silaha iko wazi na
wakazinyakua silaha na kukimbia nazo hadi kwenye uwanja ulio nje ya
jengo la Raha Leo.
Hapo ndipo palipokuwa makao makuu ya Mapinduzi kwa siku chache na
ndipo wapinduzi walikokuwa wakipewa silaha. Studio za redio ya Serikali
pia zilikuwa hapo.
Moja ya sababu zilizoyafanya Mapinduzi yafanikiwe haraka ni uamuzi
wa viongozi wa Serikali iliyopinduliwa — Sheikh Muhammed Shamte na
Sheikh Ali Muhsin Barwani — kuwataka wafuasi wao wasitumie nguvu
kuyapinga.
Hivyo, mbali na mapigano yaliyozuka saa za asubuhi ya Jumapili
Januari 12, mbele ya Steshini ya Polisi Malindi, hapajazuka mapigano
Unguja kati ya waliopindua na waliopinduliwa. Pemba nako pia hakukuwa na
upinzani ijapokuwa kisiwa hicho kilikuwa ngome ya vyama vya ZNP na
ZPPP.
Wengi wa wapiganaji waliokuwa kwenye Stesheni ya Polisi ya Malindi
walikuwa wakuu wa polisi Wakiingereza. Wakipigana na makada wa Umma
Party ambao ndio pia waliouteka uwanja wa ndege, bandari pamoja na kituo
cha mawasiliano ya nje cha Cable & Wireless, kilichokuwa kwenye
jengo ambalo sasa ni Hoteli ya Serena Mji Mkongwe.
Kwa hakika, kinyume cha baadhi ya watu walivyoandika hapakutokea
mauaji ya kimbari. Aliyeanzisha uvumi huo alikuwa John Okello
aliyeandika kwenye kitabu chake kuhusu Mapinduzi ya Zanzibar kwamba
watu zaidi ya elfu kumi waliuliwa. Okello aliongeza kwamba aliamrishwa
na Yesu Kristo kuwakomboa ‘Waafrika’ wa Zanzibar kutoka kwa ‘wageni’.
Tutamrejelea Okello na wengine waliokuwa Raha Leo baadaye. Kwanza
tukumbushe kwamba mkesha wa Januari 12, mwaka 1964, Zanzibar haikuwa na
jeshi. Kulikuwa polisi waliokuwa wakiongozwa na Waingereza. Wengi wa
askari polisi walikuwa raia wa Tanganyika. Serikali iliyopinduliwa
ilikataa kuandikiana mkataba wa kijeshi na Uingereza kwa sababu ikihisi
mkataba kama huo utaonekana kuwa wa kikoloni.
Hatuwezi kusema ni nani hasa aliyepiga risasi ya mwanzo au ya mwisho
katika Mapinduzi. Naitoshe tusemapo kwamba kwa vile hakukuwa na
upinzani, Serikali iliyokuwa madarakani iliporomoka kama ‘nyumba ya
karata’.
Tuwarejelee sasa waliokuwa Raha Leo, makao makuu ya Mapinduzi kwa
siku chache. Kwanza tumuangalie Okello ambaye sauti yake ndiyo
iliyokuwa ikivuma kwenye Redio Zanzibar.
Hatuna uhakika nani alimpeleka Okello Raha Leo. Wengine wanasema ni
Yusuf Himidi. Wengine wanasema ni Seif Bakari aliyetoa rai atumiwe
kutoa matangazo kwenye redio kwa vile sauti yake ilikuwa na lafudhi
ngeni ya kutisha.
Uhakika tulio nao ni kwamba Okello alipotokea Raha Leo na mabastola
yake, Aboud Jumbe alishtuka na akauliza: “Nani huyu? Katokea wapi?”
Kijana huyo aliyekuwa na umri wa miaka 27 hakujulikana kabla ya
Mapinduzi. Alikuwa mtu asiyejua kuandika wala kusoma na akili zake
zikimtosha mwenyewe. Hakuwa na sifa za uongozi na wala hakushiriki
katika vuguvugu lolote la kisiasa.
Akijibandika cheo cha kijeshi cha Field Marshall ni yeye aliyetangaza kwamba serikali ya ZNP/ZPPP imepinduliwa.
Kwa hakika, kazi hiyo ya kutangaza kufanikiwa kwa Mapinduzi kwanza
alipewa Ramadhan Haji, mmoja wa wapinduzi. Lakini alikataa. Jina la
Okello lisingelisikika lau Ramadhan Haji angekubali kutangaza kwamba
Serikali imepinduliwa na kwamba wapinduzi waliidhibiti nchi.
Waliokuwa wakiongoza mambo Raha Leo tangu Mapinduzi yaanze, hadi
Jumatatu Januari 13, walikuwa Aboud Jumbe, mmoja wa viongozi wa chama
cha Afro-Shirazi (ASP), Thabit Kombo (Katibu Mkuu wa ASP) na Badawi
Qullatein wa Umma Party. Muda wote huo, Sheikh Abeid Amani Karume
(kiongozi wa ASP), Abdulrahman Babu (mwenyekiti wa Umma Party) na
Abdalla Kassim Hanga (ASP) walikuwa Dar es Salaam.
Mnamo siku hizo hizo liliundwa Baraza la Mapinduzi na Baraza la
Mawaziri lililokuwa na mamlaka kamili ya kuiendesha Zanzibar. Mabaraza
hayo mawili yalikuwa taasisi kuu za Serikali ya kimapinduzi ya Jamhuri
ya Watu wa Zanzibar. Na sio ile iitwayo ‘Kamati ya Watu Kumi na Nne’
ambayo baadhi ya watu wanasema kuwa ndiyo iliyoandaa Mapinduzi.
Okello akipenda kujigamba kwamba ndiye aliyeyapanga na kuyaongoza
Mapinduzi. Alikuwa akitoa matamshi ya kushtusha na ya ajabu-ajabu
kwenye Redio Zanzibar. Kwa mfano, siku moja alidai kwamba alipwe
mshahara mkubwa zaidi ya aliokuwa akilipwa Rais Karume. Siku nyingine
akasema kwamba kasri zote alizokuwa akitumia sultani kupumzikia apewe
yeye.
Kuna siku aliyotoa hukumu kwamba mzee mmoja wa zaidi ya miaka 60
afungwe kwa miaka 99. Alisema kama huyo bwana atakufa gerezani basi
mwanawe afungwe ili kuendeleza kifungo na mwanawe akifa basi mjukuu wake
afungwe mpaka itimie miaka 99.
Nyakati nyingine aliwaonya watu wazitie moto familia zao na wao
wenyewe mpaka wafe ‘kabla ya majeshi yangu kuja.’ Alikuwa akitoa vitisho
visivyowahi kamwe kusikika Zanzibar.
Kuna siku alitangaza kwamba wakazi wa eneo moja ambako alikuwa apite, wajipange foleni barabarani wakiwa wamevaa chupi tu.
Okello alikuwa ni adha, kitisho, kichekesho na fedheha kwa Zanzibar.
Viongozi wapya wa nchi walichoka naye na wakaamua kumchukulia hatua.
Salim Rashid, mmoja wa viongozi wa Umma Party aliyekuwa katibu wa
Baraza la Mapinduzi anasema kwamba, kwanza alilizungumza suala la
Okello na Sheikh Karume. Halafu akalizungumza na Brigadia Yusuf Himid
na mwisho yeye, Yusuf Himid na Kanali Ali Mahfoudh wakalitafutia dawa.
Ilisadifu kuwa siku moja Okello alisafiri kwenda Dar es Salaam
akifuatana na Jaha Ubwa, aliyekuwa katibu wake. Walipokuwa wanatarajiwa
kurudi Zanzibar, Karume, Yusuf Himid, Salim Rashid na Ali Mahfoudh
walikwenda uwanja wa ndege kumsubiri.
Siku hiyo anaikumbuka vizuri Luteni Hashil Seif aliyekuwa ofisa wa
zamu kwenye kambi ya jeshi huko Migombani karibu na uwanja wa ndege.
Alipigiwa simu akitakiwa aende kwa haraka uwanja wa ndege. Hakuambiwa
anaitiwa nini.
Alipofika ndipo alipoambiwa kwamba kuna ndege ya Shirika la Ndege la
Afrika ya Mashariki iliyokuwa inakuja kutoka Dar es Salaam ndani yake
wakiwemo pia Okello na Jaha Ubwa. Akaelezwa kwamba awaruhusu abiria wote
pamoja na Ubwa washuke, lakini amzuie Okello asishuke. Halafu amwambie
rubani ampeleke Okello Kenya.
Hashil naye akampigia simu komredi mwenzake Luteni Amour Dugheshina
kumwita aende uwanja wa ndege amsaidie. Maluteni wote wawili walikuwa
na bunduki za aina ya ‘machine gun’.
Ndege ilipotua walipanda ndani ya ndege, wakampokonya silaha Okello
na kutekeleza amri waliopewa. Rubani wa ndege alikasirika sana. ‘Uso
wake ulighadhibika, utafikiri mnyama aliyekosewa risasi,’ alieleza
Hashil.
Lakini rubani hakuwa na la kufanya ila kuiwasha ndege na kuelekea Kenya.
Huku nyuma Salim Rashid akampigia simu Oginga Odinga, Makamu wa Rais
wa Kenya, kumuarifu kwamba wamemfukuza Okello na ‘wanamrejesha’ Kenya.
Alifanya hivyo kwa makosa kwa sababu kutokana na jina lake akifikiri
kuwa Okello ni Mjaluo kutoka Kenya.
Kumbe alikuwa mtu wa kabila la Acholi aliyezaliwa Uganda na
alikwenda Unguja kabla ya kuhamia Pemba ambako alikuwa mwashi, mtiaji
rangi nyumba na mpasuaji mawe.
Swali la kujiuliza hapa ni; je, iwapo kweli Okello alikuwa ‘kiongozi
mpendwa wa Mapinduzi’ ilikuwaje wafuasi wake na wanamapinduzi wenzake
wasimtetee alipoadhiriwa uwanja wa ndege na kufukuzwa nchini? Ilikuwaje
akafukuzwa kwa urahisi hivyo?
Kuna uzushi mwingi kuhusu kipindi hiki kifupi cha historia ya
Zanzibar. Kwa mfano, kuna filamu ya kubuni ya Wataliana inayoonyesha
maiti chungu nzima za watu waliopigwa risasi. Filamu hiyo ilikuwa na
lengo moja tu; kuonyesha ‘ukatili na unyama wa Waafrika.’
Hakuna ithibati yoyote kwamba watu waliouawa katika siku za mwanzo
za Mapinduzi walifika elfu kumi. Ukweli ni kwamba jumla ya watu
waliouawa siku hizo haipindukii 200, katika sehemu za mjini hawazidi
25.
Uzushi mwingine ni kwamba walipelekwa Watanganyika, Zanzibar wakiwa
na silaha kwenda kupindua. Na si kweli kwamba Mapinduzi yalikuwa na
msisitizo wa kikabila. Katika kipindi cha mwanzo cha Mapinduzi
msisitizo ulikuwa wa kitabaka. Nyimbo zilizokuwa zikiimbwa kwenye
Redio Zanzibar zikiwazungumzia ‘wakwezi na wakulima’ na wafanyakazi kwa
jumla na si makabila.
Mapinduzi ya Zanzibar yalianzisha taasisi mpya za utawala zikiwa
pamoja na Baraza la Mapinduzi, Baraza la Mawaziri na ofisi ya Rais.
Taasisi hizo zilikuwa zifanye kazi kwa muda wa mwaka mmoja tu kwa vile
ilikwishaamuliwa kwamba Januari 1965 pafanywe uchaguzi wa kulichagua
Bunge la Katiba, lililokuwa litunge Katiba ya kudumu ya Zanzibar.
Baraza la Mapinduzi la Zanzibar pamoja na Serikali mpya zilianza kwa
ubia baina ya chama cha ASP na Umma Party. Ingawa wanachama wa ASP
ndio waliofanya Mapinduzi waliutambua mchango wa wafuasi wa Umma Party
na hasa mchango wa makada wao waliopata mafunzo ya kijeshi nchini Cuba.
Vijana hao wa Umma walizitia wasiwasi serikali za Marekani na
Uingereza na kuzifanya ziamini kuwa utawala mpya wa Zanzibar ulikuwa wa
‘kikomunisti’. Dhana hiyo ndiyo iliyosababisha kuchukuliwa hatua ya
kuyachimba na kuyagandamiza Mapinduzi ya Zanzibar yaliyodumu kutoka
Januari 12, hadi 26 Aprili, mwaka 1964.
Source: Raia Mwema
No comments:
Post a Comment