Sunday 20 January 2013

KIKWETE NA SHEIN IGOMBOENI Z ‘ BAR KATIKA MUUNGANO

WANANCHI wa kijiji cha Chwaka, Kusini Unguja wamewaomba Rais Jakaya Kikwete na Dk Ali Mohamed Shein, kushughulikia suala la Katiba ili kuweza kuirejeshea Zanzibar mamlaka yake kamili kama ilivyokuwa kabla ya kuungana na Tanganyika.
 Ombi hilo lilitolewa juzi kwenye mkutano wa wazi wa Baraza la Katiba Zanzibar (BAKAZA) wakati likitoa elimu ya Katiba kwa wananchi wa kijiji hicho. Huo ni mfululizo wa Baraza hilo katika kutoa elimu ya Katiba kwa wananchi wa Zanzibar.
 Akizungumza katika mkutano huo mmoja wa Wazee wa Chwaka, Fadhil Mussa Haji alisema suala la kuunganisha nchi lilifanywa na watu wawili, Mwalimu Nyerere na Mzee Karume na wote hawapo tena. Alisema ni jukumu la viongozi waliopo madarakani kulishughulikia suala hilo.
 “Mwalimu Nyerere na Mzee Karume waliunganisha nchi kwa kuamua wao wenyewe na kisha Mzee Karume akaja uwanjani kutuuliza mnakubali union watu wakaitikia…kwa kuwa alijua hakuna atakayeweza kupinga kwa wakati ule,” alisema na kuongeza:
 ”Lakini sisi hatujakubaliana na hayo tokea wakati huo…sasa kilichobaki tunamuomba Rais Kikwete na Rais Shein wao ndio wapo madakarakani waturejeshee mamlaka na hadhi ya Zanzibar,” alisema Mzee Fadhil, huku akishangiriwa na vijana waliohudhuria mkutano huo.
 Mzee Fadhil alisema yapo baadhi ya mambo ambayo yameingizwa katika orodha ya mambo muungano bila ya ridhaa ya Wazanzibari, lakini baadhi ya mambo Wazanzibari wenyewe walishiriki kuizamisha nchi yao kutokana na tamaa na kupenda madaraka, jambo ambalo alisema hivi sasa linawafanya wajute:
 “Ni sisi wenyewe tumefanya na tumetaka tutendewe hivi kwa sababu sisi tulikuwa tumeshapata uhuru wetu hapa mwaka 1963 lakini ni Wazanzibari wenyewe wakaleta mapinduzi na kuukataa ule uhuru halali,” alisema na kufafanua:
 ”Sasa tunasema hizi tamaa na kupenda madaraka sasa hivi ndivyo vitu vinavyotuadhibu sote katika nchi yetu kwa tamaa za hao wachache waliyokuwa wakituamulia,” alisema Mzee Fadhil.
 Alitoa mfano kwa viongozi wa Wazanzibari walivyojikaanga kwa mafuta yao wenyewe: “Ni tamaa ndizo zilizosababisha nchi kutokuwa na hadhi na mamlaka kamili ya kujiamulia mambo yake,” alisema Mzee Fadhil.
 Alisema ni tamaa ndiyo zilizofanya kuporwa mamlaka kamili ya Zanzibar na hivyo kubakisha nchi kukosa uwakilishi hata kwa yale mambo ya Zanzibar, ambayo sio ya muungano yanavyokosa uwakilishi wa Wazanzibari katika nchi za nje:
 ”Wakati umefika sasa kwa kila mmoja kufahamu kwamba mamlaka ya Zanzibar yanahitaji kuheshimiwa na kupiganiwa na kila raia ili hadhi ya Zanzibar irudi,” alisema Mzee Fadhil.
 Akitoa maoni yake alipendekeza Katiba mpya iweke bayana mamlaka ya Zanzibar na rais wake, kwani alisema hivi sasa rais wa Zanzibar, hana hadhi ya kweli kama itakiwavyo kwa rais wa nchi.
Chanzo: Mzalendo

No comments:

Post a Comment