Friday 23 March 2012

Wenye kutukosesha miujiza ya Singapore

Na Ahmed Rajab
MARA kadha wa kadha nimekuwa nikigusia katika safu hii jinsi viongozi wetu wanavyokosa mwelekeo au dira ya kuongoza. Badala ya kuikwamua nchi kutoka umasikini wanajikwamua wenyewe na wanaiachia nchi iselelee na hali yake ya ufukara.
Ukiwaangalia utawaona kila uchao wamo mbioni kujipendekeza kwa wanaowaita wafadhili japokuwa fadhila ya hao wafadhili ni kama fadhila ya punda kwa vile mara nyingi huwa ina harufu mbovu. Inawafanya viongozi wetu wasiweze kufikiria mbinu za kuiendeleza nchi bila ya kushikilia uzi uleule wa ‘omba omba’.
Viongozi wetu hawana kazi ila kila mara kuwabembeleza wafadhili wawasaidie kutuletea maendeleo kana kwamba wao na wananchi wenzao hawana uwezo wa kuiendeleza nchi.
Viongozi wetu wana tabia ya kusahau kama miujiza hutokea duniani hata katika upande wa maendeleo ya nchi. Hapa ningependa kukumbusha miujiza iliyotokea Singapore hasa kwa vile Zanzibar inalingana mengi na Singapore huko ilikotoka.
Nchi hiyo ilijitangazia uhuru mwaka 1963 na ikajiunga na Malaysia pamoja na Sabah na Sarawak kuunda Shirikisho la Malaysia. Sababu zilizowafanya viongozi wa Singapore wajiunge na Malaysia zinaeleweka.
Kwanza wakihisi kwamba Uingereza isingeliipa uhuru nchi yao kwa sababu ingeiona kuwa ni ndogo isiyoweza kujitegemea. 
Pia wao wenyewe viongozi wa Singapore wakiamini kwamba nchi yao isingeweza kujikimu kwa vile haikuwa na eneo kubwa la ardhi, haikuwa na maji ya kutosha, haikuwa na masoko wala maliasili. Tena wakitaka kuwa chini ya mwavuli wa Malaysia kujikinga na joto la Wakomunisti waliokuwa wakiyarandia madaraka.
Kwa muda wa miaka miwili Singapore ilikuwa sehemu ya Malaysia. Lakini kama ulivyo Muungano wetu muungano wao nao ulikuwa na kero zake na Singapore na Malaysia zilikuwa hazishi kusuguana roho. Hatimaye Malaysia ikaitoa Singapore kutoka Shirikisho. Ndipo Uingereza ilipoipa Singapore uhuru rasmi mwaka 1965.
Wakati huo taifa hilo dogo lilikuwa limetumbukizwa kwenye gunia la nchi za Ulimwengu wa Tatu.  Miujiza ya mambo ni kwamba leo limo kwenye kaumu ya nchi za Ulimwengu wa Kwanza.
Singapore imeweza kujipatia ufanisi wake licha ya kwamba haina idadi kubwa ya wakaazi, haina eneo kubwa la ardhi (ni taifa dogo lenye visiwa 63) na kama nilivyokwishagusia ina ukosefu wa maliasili. Ilipopata uhuru si wengi waliofikiri kwamba kijinchi hicho kitaweza kuwa na uhai. 
Wakati wa uhuru jumla ya Pato la Taifa kwa kila mtu huko Singapore lilikuwa sawa na dola 400; hii leo ni zaidi ya dola 22,000. Pato hilo ni la nne kwa ukubwa duniani na linalipita lile la Uingereza iliyokuwa ikiitawala Singapore.
Hii leo Singapore ina moja ya bandari zenye shughuli nyingi duniani, ni kituo cha tatu kwa ukubwa duniani cha kusafishia mafuta na nchi hiyo imegeuka kuwa kituo kikuu duniani cha kuzalisha bidhaa viwandani na katika makarkhana.  Singapore imeweza kuchupa kutoka kwenye umasikini na kusimama kwenye utajiri katika muda wa kizazi kimoja tu.
Nini kinachoizuia Zanzibar au Tanzania Bara isipate miujiza kama hiyo? Labda niligeuze swali naniulize ilikuwaje hata Singapore ikapata miujiza hiyo?
Jibu ni rahisi kulipata. Tangu ipate uhuru Singapore imekuwa na uongozi bora.  Anayepongezwa kwa ufanisi huo ni Lee Kuan Yew aliyekuwa waziri mkuu wa nchi hiyo kwa miongo mitatu tangu uhuru na aliyeendelea kuwa na ushawishi mkubwa katika uongozi wa serikali hadi hivi karibuni.
Ni yeye aliyekuwa akisisitiza kwamba maliasili pekee ya Singapore ni watu wake na jitihada yao ya kazi. Wengi nchini mwake wanamsema vyema kwa mvuto wa uongozi wake wakati wa uhuru na wa kujitenga na Malaysia.
Lazima nikumbushe kuwa Lee Kuan Yew si malaika. Alikuwa dikteta. Tena alikuwa jeuri; hakuwa akimsikiliza mtu; alitakalo ndilo. Utawala wake ukiingilia kila jambo.
Ingawa watu walikuwa na uhuru akisisitiza kuwa hawakuwa na uhuru wa kuwaudhi wengine. Kwa hivyo, si karaha tu bali ni kosa la jinai, kwa mfano, kutema mate njiani. Adhabu ya uhalifu huo ni faini ya dola 250 sawa na adhabu ya kuvuta sigara kwenye ofisi za serikali au kuvuka barabara hovyo hovyo bila ya kujali magari.
Wenye kutafuna ubani (chingamu) njiani nao pia hutozwa faini hiyo hiyo. Adhabu ya wanaopatikana na hatia ya kuingiza nchini mihadarati ni kifo.
Lee aliwalazimisha watu waweke akiba asilimia 25 ya pato lao ingawa kulikuwa na malalamiko kwamba serikali ilikuwa ikizitumia kwa ubadhirifu hizo fedha za akiba ya wananchi.
Hata hivyo, udikteta wake Lee ulikuwa na tofauti. Haukuwatia sana hofu wananchi. Lee alikuwa dikteta karimu.
Wakati wa zama za ‘vita baridi’ yaani zama za  michuano ya kisiasa baina ya nchi za kibepari na zile za kisoshalisti sisi tuliokuwa katika mrengo wa kushoto tukimponda Lee Kuan Yew kuwa alikuwa kibaraka wa nchi za Magharibi. Yeye mwenyewe akijinata kuwa alikuwa msoshalisti aliyeutumia ubepari kufikia lengo la kuunda jamii yenye haki na ustawi.
Ninaamini kwamba viongozi wetu wa Visiwani na wa Bara wana mengi wanayoweza kujifunza kutoka kwa kiongozi huyo wa Singapore. Nadhani kila mmojawao anapaswa asome kitabu alichokiandika kiitwacho ‘From Third World to First’ (Kutoka Ulimwengu wa Tatu hadi wa Kwanza).
Mengi aliyoyaandika yanataka utulivu na nafasi kubwa kuyajadili. Lakini naitoshe hapa tukiyapitia machache tu. Kati ya muhimu aliyoyataja ni kwamba utamaduni wa taifa, zaidi ya uchumi na siasa, ndio utaoamua mustakabali wa nchi.
Suala hili la nafasi ya utamaduni katika maendeleo ya nchi ni muhimu lakini mara nyingi hupuuzwa na viongozi wetu.  Nadhani ni kiongozi mmoja tu Wakiafrika, Amilcar Cabral wa Guinea-Bissau aliyelijadili kwa kina suala hilo ingawa kwa bahati mbaya hakupata kuongoza nchi kwani Wareno walimuua kabla ya nchi yake kuwa huru.
Kwa mujibu wa Lee walipoanza harakati za kisiasa katika miaka ya 1950 hawakujua namna ya kuendesha nchi au jinsi ya kuyatanzua matatizo mengi ya kiuchumi na kijamii. Lakini walikuwa na raghba kubwa ya kuibadili jamii isiyokuwa na usawa na haki na kuifanya iwe jamii ya haki na usawa.
Anasema alilazimika kuhakikisha kuwa ana watu wenye uwezo ambao aliwapachika katika nyadhifa kubwa kwa kuwateua wawe mawaziri na watumishi wakuu wa serikali. Lengo lilikuwa kuwafanya waendeshe utawala wenye mfumo aminifu, ulio mnyofu na wenye kuyakidhi mahitaji ya wananchi. 
Lee ameendelea kusema kwamba alikuwa na kazi ngumu ya kuwafanya wafanya kazi wawe upande wa serikali wakati ambapo serikali ilikuwa inayashughulikia mahitaji ya wawekezaji ambao wakiwategemea kwa rasilmali zao za fedha, maarifa, uweledi  wa menejimenti na wa kuendesha mambo kwa jumla na masoko yao ya nje.
Kitu cha awali alichohakikisha alipokuwa waziri mkuu (wakati huo akiwa na umri wa miaka 34)  ni kwamba pawepo mawaziri kadhaa wenye kupenda mno kusoma na wanaovutiwa na fikra mpya lakini wasiofadhaishwa au kupigwa na bumbuwazi na fikra hizo.  
Lee ameeleza jinsi yeye na mawaziri wake walivyokuwa wakiazimana vitabu na makala mbalimbali za kuvutia.  Walipoingia serikalini walikuwa madubu, wajinga hawakujuwa namna ya kutawala. Lakini walikuwa waangalifu na wakizizingatia sera kwa makini kabla ya kuzitekeleza. 
Muhimu yeye na mawaziri wake wakiaminiana. Wakijuwana nini uwezo wa kila mmojawao na nini udhaifu wao kwa hivyo wakichukuliana.
Alibahatika kuwa na mawaziri waliokuwa na azma moja na malengo sawa. Mawaziri waliokuwa karibu naye walifanya kazi pamoja kwa zaidi ya miongo miwili na walikuwa wakubwa zake kwa umri na hawakuchelea kumpasulia walivyokuwa wakifikiri, hasa alipokuwa akikosa.
Amesisitiza  kwamba jambo lililowapelekea wakafanikiwa ni kwamba kila mara wakitalii na kuangalia namna ya kutanzua matatizo au namna ya kuyafanya mambo yawe bora zaidi. Hakuwa mfungwa wa nadharia yoyote.  Mantiki na hali halisi ilivyo ndiyo mambo yaliokuwa yakimuongoza.
Jambo jengine ni kwamba akijaribu kujifunza kutokana na makosa waliyoyafanya viongozi wengine katika nchi zao.
Aligundua mapema alipoanza kutawala kwamba hakukuwa na matatizo yaliyoikabili serikali yake ambayo serikali nyingine hazijayakabili na kuyatanzua. 
Kwa hivyo, alikuwa na desturi ya kuchunguza nani mwengine alikabiliwa na matatizo kama ya Singapore, na kutaka kujuwa namna alivyoyashughulikia, yawematatizo hayo kuhusu ujenzi wa uwanja wa ndege mpya au mitindo ya kusomeshea maskuli. Alifanya hima ya kuwatuma maofisa wake wende kwenye nchi zilizofanya mambo yao vyema ili wajifunze. 
Lee anakumbusha kwamba akipuuza lawama na nasaha kutoka kwa mabingwa au mabingwa uchwara, hasa wasomi wa sayansi za kijamii na kisiasa.
Tukiyatafakari maandishi ya Lee tunaona kwamba miongoni mwa kanuni zilizoifanya Singapore iendelee ni pamoja na ile ya kuwa na umoja wa kijamii, kuufyeka ufisadi serikalini, kugawana kwa usawa matunda ya maendeleo, kuwapa wananchi wote fursa sawa na kuwa na mfumo wa serikali unaoongozwa na wataalamu na weledi.
Hizi ni kanuni za kimaadili na tunastahili kuziiga. Angalau huko Zanzibar tayari tuna umoja wa kijamii; yanayokosekana ni maendeleo na hayo mingine yanayofuata maendeleo

No comments:

Post a Comment