RAIS Ali Mohamed Shein ana dhamana kubwa kushinda kiongozi yeyote
mwengine wa Zanzibar, tangu nchi hiyo iungane na Tanganyika kuunda
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Dhamana yake ni kubwa hivyo kwa sababu
Wazanzibari wenzake wanasubiri kwa hamu matokeo ya mchakato wa
kuipatia Jamhuri ya Muungano Katiba mpya.
Imepangwa kwamba kazi hiyo imalizwe Aprili, mwaka 2014 wakati wa
maadhimisho ya miaka 50 ya Jamhuri ya Muungano. Miaka 50 ni muda mwingi,
uhai wa mtu wa kuzaa na kujukuu ingawa kwa kipimo cha kihistoria huo
ni muda mfupi sana kama wa kufumba na kufumbua macho.
Shein ana bahati. Bahati yake ni kwamba hakabiliwi na upinzani licha
ya shida za kiuchumi na za kijamii zilizozagaa huko Visiwani. Kama wapo
wenye kumpikia majungu chini kwa chini basi hawathubutu kujitokeza.
Hali iliyopo Visiwani haiwaruhusu. Shein anaiongoza nchi wakati ambapo
Wazanzibari wameungana baada ya kuziyayusha chuki zao za kisiasa na
kukubaliana, Novemba mwaka 2010 kuwa na suluhu ya kitaifa kwa
Maridhiano ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Wananchi (CUF).
Maridhiano hayo ndiyo yaliyosababisha kuundwa kwa Serikali ya Umoja
wa Kitaifa na kuibuka kwa ile iitwayo Ajenda ya Zanzibar. Na ni umoja
huo uliosababisha pasiwepo upinzani dhidi ya Shein, si wa dhahiri si wa
shahiri.
Hiyo ni bahati kubwa kwa Shein na inampa fursa adhimu ya kuongoza taifa
lilioungana. Lakini pia ni changamoto kwake yeye na serikali yake. Ni
changamoto kwa sababu Wazanzibari kwa pamoja wanataraji mengi kutoka
kwake. Awali ya yote wanamtaka awe na msimamo ulio imara wa
kumwezesha kuyatetea vilivyo maslahi ya Zanzibar.
Ni matumaini yao kwamba hatoteteleka wala kuyumba-yumba
atapohitajika kuwasilisha na kuyasimamia maoni yao kuhusu mustakbali wa
nchi yao na hususan suala la iwapo Muungano uendelee kama ulivyo au
la. Kwa ufupi, tegemeo lao ni kwamba hatowaendea kinyume kwa
kutoyapigania matilaba yao.
Wengi wa Wazanzibari wanataraji kwamba mfumo wa Muungano utaochomoza
baada ya kumalizika hiyo shughuli ya kutunga Katiba utakuwa tofauti
kabisa na ule wa sasa wa serikali mbili zisizo na mamlaka sawa wala
haki zilizo sawa.
Siku hizi Wazanzibari wana kiu cha kutamani ya kale wanapoukumbuka
ufanisi waliokuwa nao wakati wa kupigania uhuru kutoka kwa Waingereza.
Juu ya migawanyiko ya kisiasa ya zama hizo hali zao za maisha kwa jumla
zilikuwa za juu na uchumi wa nchi yao haukuathiriwa na mchafuko wa
kisiasa.
Hizo zilikuwa nyakati za maisha ya raha na furaha kinyume na sasa ambapo pameingia maisha ya dhiki.
Sisemi kwamba ufanisi huo ulikuwa timilifu au kwamba haukuwa na
kasoro, la. Nisemacho ni kwamba licha ya taksiri zake — na zilikuwa
nyingi —dosari hizo hazikuufanya uchumi wa Zanzibar uzorote. Nchi
ilikuwa na neema, watu wakipata ajira, sekta ya kilimo ilistawi na
pakipatikana vyakula vya kila aina tena kwa bei rahisi.
Siku hizo angalau kila Mzanzibari akimudu kula vyakula mbalimbali si
kama sasa ambapo waliobahatika siku nenda siku rudi wanakula ugali na
maharagwe mara tatu kwa siku. Huo ndio mlo wa wengi wa Wazanzibari siku
hizi na wapo baadhi yao wasiobahatika hata kuumudu mlo huo.
Ingawa utawala wa ukoloni Wakiingereza ulikuwa wa kimabavu, ulikuwa
hivyo dhidi ya wale waliokuwa wakiupinga na waliokuwa wakidai uhuru.
Wananchi kwa jumla walikuwa na uhuru wao wa kiraia ingawa hawakuwa na
uwakilishi wa kisiasa. Zanzibar ikitawaliwa moja kwa moja na
Uingereza.
Kinyume na wanavyofikiri wengi tangu mwaka 1890 masultani walikalia
kiti cha enzi huko Zanzibar lakini hawakuwa na nguvu za kutawala na
kuendesha nchi. Mabwana waliokuwa na amri walikuwa wakoloni
Wakiingereza na si masultani. Wao walikuwa wanyenyekevu kwa Waingereza.
Hii leo Wazanzibari wana mapato ya kujikimu tu, wengi wao hususan
vijana hawana ajira. Kuna mfumuko mkubwa wa bei na mapato, bei za
vyakula ni za kuruka, huduma za lazima ni duni kama vile za afya, maji,
umeme na kumekosekana mfumo wa kuchimba mitaro ya kuchukua maji
machafu.
Zama hizo zilizopita, mfumo wa elimu Visiwani ulikuwa wa kupigiwa
mfano. Mwaka 1961 Zanzibar ilikuwa na wahitimu wengi wa chuo kikuu
waliopata digrii au shahada kulinganishwa na wale wa Tanganyika.
Huo ndio ukweli uliokuwepo. Siku hizo Zanzibar ikitajwa kuwa na
nafasi ya pili baada ya Afrika ya Kusini katika mizani ya maendeleo
miongoni mwa nchi zilizo kusini mwa Jangwa la Sahara. Si leo.
Mfumo wa leo wa elimu hauwezi kamwe kufananishwa na ule wa kale. Kwa
sababu ya mfumo wa elimu uliopo sasa ni muhali kupata wataalamu
wataoiwezesha serikali ya Zanzibar iendeshwe kistadi na ipasavyo bila
ya ulaji rushwa au kupendeleana wakati wa kuajiri watu katika kazi za
serikalini.
Badala yake tunaona kwamba watu wasio na elimu ya kutosha au ujuzi
na uzoefu unaohitajika wanapewa madaraka makubwa serikalini ama kwa
sababu za kisiasa au za kupendeleana. Hawa ndio wenye kuhodhi nyadhifa
nyeti serikalini na kushika kwao nyadhifa hizo kunaleta madhara makubwa
kwa jamii kwani wanakuwa wanazitumia vibaya rasilmali za nchi na
wanapoteza fursa ya kuziinua hali za maisha Visiwani kwa kuwapatia
watoto elimu bora na kuwapatia wananchi kwa jumla huduma zote za
lazima.
Ingawa hii leo Zanzibar kuna umoja wa kitaifa pamoja na suluhu na hali
tulivu ya kisiasa uchumi wake si wa kuridhisha. Isitoshe huduma zake
za kijamii hazikidhi mahitaji ya kila Mzanzibari hasa wale walio
maskini na wasiojiweza ambao ndio walio wengi Visiwani.
Tumekumbushana kidogo hali ya mambo ilivyokuwa kabla ya Mapinduzi na
Muungano na Tanganyika na tukagusia hali ilivyo sasa. Na hatuna budi
kusema kwamba hali iliyopo sasa hairidhishi hata kidogo na ni lazima
ibadilishwe ili Zanzibar iweze tena kuwa nchi ya neema.
Kwa bahati nzuri, mchakato utaopelekea kupatikana kwa katiba mpya
unawapa Wazanzibari na viongozi wao fursa ya kuweza kujipatia ukombozi
na maendeleo kwa kuachana na hali ya sasa ilivyo.
Kwanza ili Zanzibar iweze kuendelea na kujipatia mamlaka yake ndani
ya Muungano na Tanganyika utaokuwa wa Mkataba na si wa Katiba, kuna
mambo mawili yanayohitaji kuzingatiwa na kutanzuliwa. La kwanza
linahusika na hali ya ndani Visiwani kwenyewe na la pili linahusika na
uhusiano wa baadaye kati ya Zanzibar na jirani wake wa kidugu
Tanganyika.
Hali ya ndani inatokana na kuzuka kwa utawala wa kisiasa wa kinasaba
(political dynasty). Hali hiyo nayo ni chanzo cha kuwako utawala mbovu.
Wanaonufaika katika mazingira hayo ni hao watawala wa kinasaba na
walio wao pamoja na wafanyabiashara wachache walio matajiri sana na
wakubwa wengine. Wao ndio wenye kustarehe ilhali wengi wa wananchi
wanahangaika kila uchao kutafuta chakula na uwezo wa kulipia huduma za
afya au wa kuwasomesha watoto wao.
Mustakbali wa Zanzibar, ndani au nje ya Muungano na jirani yake
Tanganyika, utaamuliwa katika kipindi cha miaka miwili ijayo.
Inavyoonyesha ni kuwa Wazanzibari hawatokubali zoezi la utungwaji wa
Katiba mpya lifanyiwe uzembe na kuachiwa lipindukie mwaka 2014 kwa
sababu wana hamu kubwa ya kuona kwamba serikali yao inarejeshewa
mamlaka yake yote ya kisiasa, kiuchumi na ya kijamii kutoka serikali ya
Muungano.
Wao wanaamini kwamba kurejeshewa mamlaka na madaraka hayo
kutawawezesha kuufyeka au angalau kuupunguza kwa kiwango kikubwa
umaskini uliopo sasa na kujipatia maendeleo na ufanisi.
Rais Shein na viongozi wenzake kwenye Serikali ya Umoja wa Kitaifa
wanayaelewa hayo kwa sababu kila siku Wazanzibari wa itikadi tofauti za
kisiasa, kuanzia wananchi wa kawaida hadi viongozi wao, wanashauriana
na kujadiliana kuhusu mustakbali wa nchi yao.
Suala kuu linalowashughulisha nilile la kuamua ni Zanzibar aina gani
waitakayo. Ni muhimu kwamba Shein ahakikishe ya kuwa Wazanzibari
wanaitumia kikamilifu haki yao ya kidemokrasi ya kushauriana na
kulijadili vilivyo suala la Katiba bila ya kuwekewa mipaka na hususan
haja ya kuujadili Muungano kwa ukamilifu bila ya woga.
Hilo ndilo jukumu kubwa alilonalo Shein na wenzake. Wazanzibari wenzao
wameshikamana na hadi sasa wako nyuma yao lakini wanachotaka hasa ni
kuwaona viongozi wao wakisema kwa kauli moja na kuitetea Ajenda ya
Zanzibar. Wanasema kuwa Shein na wenzake ndio ambao ama watainusuru au
wataitosa nchi yao. Hilo si jukumu dogo
No comments:
Post a Comment