Thursday 15 March 2012

Wakati umefika wa kuwa na ‘Mkataba wa Kijamii’ Zanzibar

Na Ahmed Rajab
MWANADAMU amezaliwa huru lakini kote duniani ametiwa minyonyoro,”  nimeyanukuu hayo kutoka katika maandishi ya Jean-Jacques Rousseau, mwanafalsafa na mwandishi mashuhuri aliyeishi nchini Ufaransa karne ya 18.
Rousseau aliwahi pia kuandika kwamba wenye mamlaka katika nchi ni umma na kwa vile umma hauna nguvu yoyote isipokuwa ya utungaji sheria, basi hutenda mambo kwa kutumia sheria.  Ameendelea kueleza kwamba sheria yoyote ile isiyoidhinishwa na umma huwa ni batili, kwa hakika huwa si sheria kamwe. Wenye nguvu ya kutunga sheria ni umma na ni umma tu wenye nguvu hiyo, kwa mujibu wa Rousseau.
Mwanafalsafa huyo ni maarufu kwa ile nadharia yake ya kutaka pawepo Mkataba wa Kijamii baina ya serikali na umma. Kitabu chake kuhusu ‘Mkataba wa Kijamii’ ni moja ya nguzo kuu za fikra za kisasa za kisiasa na za kijamii. Na ni moja ya misingi ya utawala wa kidemokrasi.
Maandishi ya Rousseau kuhusu siasa na elimu yalikuwa na athari kubwa kwa nadharia za kisiasa za karne mbili zilizopita. Maandishi hayo ndiyo yaliyowavutia na kuwaathiri wanamapinduzi waliokuwa wakiandaa Mapinduzi ya Ufaransa yaliyotokea baada ya kufariki kwake.
Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 1964 yaliwaahidi Wazanzibari mambo kadhaa ambayo hadi leo bado hayajatimizwa. Waliopindua waliiona jamii ya Visiwani kabla ya Mapinduzi kuwa ni jamii isiyokuwa na haki na iliyokuwa ya kibaguzi. Wanazungumzia hasa kuhusu haki za kimsingi za binadamu na fursa zilizokuwepo, fursa ambazo wanasema walikuwa wakipewa wachache na walio wengi wakinyimwa.
Hadi leo wenye kujiona kuwa ni warithi wa Mapinduzi hayo haweshi kuelezea kuhusu yale wanayoyaona kuwa ni maovu na madhambi ya utawala uliopinduliwa. 
Kama ilivyo kawaida ya wanaopindua wapinduzi wa Zanzibar muda wote huu wamekuwa wakidai kwamba wao ndio wenye utatuzi wa matatizo yote yanayoikabili nchi na hivyo wamekuwa wakiahidi kuwa watawapa wananchi wenziwao fursa sawa bila ya kujali hadhi zao katika jamii. Mtu hatoangaliwa ikiwa ni wa tabaka la wanaotawala au la matajiri wa juzi juzi au ikiwa ni mwana wa mkulima kutoka shamba. Wote watapewa fursa sawa.
Ahadi zilizotolewa na Mapinduzi zimevunjwa. Matokeo yake ni kwamba wengi wa watu wa mijini na wa mashambani wangali wanaishi katika mazingira magumu ya umasikini, magonjwa na uhaba wa chakula.
Hali hiyo haishangazi kwa sababu hii leo uchumi wa Zanzibar umeanguka. Mdororo huo wa uchumi unazidi huku wale wenye dhamana ya kuushughulikia, ingawa wanajaribu, bado hawakufanikiwa kuchukuwa hatua madhubuti za kuuzuia uchumi huo usizidi kuporomoka. 
Hali ya mambo inazidi kutatanika kwa vile sekta ya kilimo nayo imeanguka na wakati huo huo hakuna fedha nchini na hivyo kuna ukosefu mkubwa wa ajira (kama asilimia 70 ya watu wenye uwezo  wa kufanya kazi hawana ajira). Watu hawana fedha za kutumia na serikali haina mpango wa kutoa huduma za jamii bure.
Huo bila ya shaka sio urithi wa kujivunia wa wale walioyaasisi Mapinduzi. Na historia haiwaonei huruma inapowahukumu na kuangalia iwapo wameineemesha jamii au wameisakamiza kwa kuufisidi uchumi uliokuwa ukistawi kabla ya Mapinduzi.
Kuna swali ambalo Wazanzibari wana haki ya kuliuliza, nalo ni: nini matokeo ya miaka 50 ya serikali za awamu zote ya kuuimba na kuufatiliza ule wimbo wa ‘Mapinduzi Daima’? Hilo ni swali rahisi kulijibu kwani tukiiangalia hali ya mambo ilivyo hatuna budi ila kukubali kwamba sera zilizokuwa zikifuatwa na Serikali ya Mapinduzi kwa muda wa miaka 50 iliyopita ni sera zilizoshindwa kuleta tija na ufanisi. Na tunakuwa tunajidanganya tu tusemapo kwamba Wazanzibari wote au wengi wao wanaishi maisha stahifu yasiyo na unyonge.
Hii leo si uchumi tu bali hata sekta muhimu za elimu ya kijamii na afya zinahitaji kufanyiwa marekebisho makubwa. Jambo la kutia moyo ni kuona kwamba pamoja na jitihada za wachache serikalini za kujaribu kuibadili hali ya mambo pia kuna asasi za kiraia zinazotoa mchango wao.  Mojawapo ya asasi hizo na iliyo mbele katika haya ni taasisi ya ZIRPP ambayo hivi majuzi ilimkabidhi Rais Ali Mohamed Shein ripoti mbili, moja kuhusu upangaji wa miji na ya pili kuhusu uchumi.
Wanachopaswa serikali na wananchi kukumbuka ni kuwa Zanzibar ni ya Wazanzibari wote; ni kama shirika lao wote. Kila mmojawao ana hisa na pia dhamana katika shirika hilo. Kila mmojawao, si serikali pekee, ana wajibu wa kuibadili hali iliyopo.
Lazima hali iliyopo ibadilike. Na inaweza kubadilika. Duniani kuna mifano mingi ya nchi ambazo zamani zilikuwa nyuma kimaendeleo na ambazo sasa ziko katika safu za mbele miongoni mwa nchi zilizoweza kubadili mifumo yao ya kiuchumi na ya kijamii.
La awali kufanywa ni kwamba serikali itambue kwamba inapaswa iwe na mkataba na wananchi. Ili Zanzibar iweze kupiga hatua na kuendelea kuna mambo yanayohitaji kutekelezwa na serikali na hivyo kuutimiza ule mkataba wake wa kijamii na wananchi. Muhimu ni kuwa na sera zitazoweza kuvinyanyua viwango vya sekta mbalimbali zikiwa pamoja na za elimu, afya, kilimo, biashara na utalii.
Inatia moyo kuona kwamba Wizara ya Elimu ya Zanzibar imeanza kampeni ya kuvinyanyua viwango vya elimu nchini humo na kwamba wenye kuhusika katika wizara hiyo wana hisia ya kuikuza elimu. 
Changamoto kubwa inayoikabili serikali ni kufuata sera ya uchumi itayoigeuza Zanzibar iwe Visiwa visivyotoza ushuru na kodi za kibiashara.  Ikifanya hivyo itakuwa rahisi kuwavutia wawekezaji kutoka nje waingize rasilmali zao katika sekta zilizo muhimu za uchumi wa nchi hiyo. Rasilmali hizo zikiingia kuufufua uchumi pataweza kupatikana fursa nyingi za ajira.
Uwekezaji huo pia utaufanya uchumi ukue kila mwaka si kitakwimu tu bali kwa kuongezeka kwa mapato ya kila Mzanzibari na hivyo kuwapatia wananchi uwezo halisi wa kujikimu kimaishi. Kwa sasa wengi wao wanaishi kwa kasoro ya dola moja ya Marekani kwa siku.
Hatua nyingine zinazoweza kuchukuliwa na serikali ni kuwa na mkakati wa kuvigeuza visiwa vya Unguja na Pemba viwe ni kituo cha huduma za fedha na za shughuli za benki.
Sambamba na hatua hizo ni kuifanya tena Zanzibar iwe ni kitovu cha biashara na usafiri kwa eneo zima la Afrika ya Mashariki na ya Kati.  Hatua zote hizo zitachangia sana kutanzua matatizo ya kiuchumi ya Visiwa hivyo.
Linalotakiwa kufanywa ni kuchukuliwa hatua ambazo zitaweza kwa haraka kuirejeshea Zanzibar ile hadhi yake ya kale ya kuwa kituo madhubuti cha kiuchumi katika eneo la Afrika ya Mashariki na Kati. Kwa bahati mbaya kwa sasa Zanzibar haiwezi kujichukulia hatua zote hizo za kiuchumi kwa vile inahitaji ridhaa na ushirikiano wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.
Na hatua kama hizo zisipochukuliwa basi hali za kimaisha ya wengi wa Wazanzibari zitaendelea kuwa ngumu kwa muda mrefu ujao kwa sababu uchumi wa nchi yao haumudu kuwahudumia wananchi kwa kuyakidhi mahitaji yao ya kila siku.
Wazanzibari wana matumaini mema wakizingatia utajiri unaoweza kupatikana Zanzibarna zaidi wakiyafikiria mafuta yaliyo chini ya maji ya bahari ya Zanzibar.Wana matumaini na wana subira.
Wazanzibari wa ndani ya nchi na walio ughaibuni wote wana hamu ya kuendelezwa kwa hali iliyopo Visiwani ya amani, umoja na utulivu wa kisiasa. Na wote wanataka nchi yao ipate maendeleo ya kiuchumi na ya kijamii.
Kwa haya na kwa mahitaji ya baadaye ya uchumi, kuna haja muhimu ya kuukuza uwezo wa watendaji katika sekta za serikali na au za mashirika ya watu binafsi. Hii ina maana kwamba Zanzibar lazima iwe na uwezo wa kuzipokea fedha nyingi za rasilimali zitakazoingia nchini na pia iwe na uwezo wa kuhudumia uchumi utakaokuwa unatanuka kwa haraka.
Changamoto iliyopo hapo ni kwamba kwa sasa Zanzibar ina ukosefu wa watendaji wenye ujuzi au waliopata mafunzo yatayostahiki kwa uchumi wa aina hiyo.  Hivyo, serikali inawajibika kuchukuwa hatua za dharura ili kuiitayarisha Zanzibar kwa mustakabali huo.
Chanzo: Raia Mwema

No comments:

Post a Comment