WIZARA ya Kilimo na Maliasili ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
imesema tayari imetoa miche ya mikarafuu na mazao ya matunda ipatayo
200,000 kwa ajili ya msimu wa kilimo wa mvua za masika Unguja na Pemba
zinazotarajiwa kuanza.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo na Maliasili, Affan Othman Said alisema
utoaji wa miche ya mikarafuu pamoja na mazao ya matunda ni utekelezaji
wa agizo la Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein ambaye ameitaka
wizara hiyo kutoa miche hiyo kwa wakulima.
“Tumeanza kutekeleza agizo la Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed
Shein la kutoa miche ya mikarafuu pamoja na ya matunda kwa wakulima
katika matayarisho ya kilimo yanayotokana na mvua za masika,” alisema
Affan.
Alisema wananchi wameitikia vizuri agizo la Rais la kuchukua miche
ya mikarafuu kwa ajili ya kilimo hasa katika kisiwa cha Pemba ambako zao
la karafuu linastawi vizuri.
Katibu Mkuu huyo alisema mikakati inayochukuliwa na wizara hiyo kwa
sasa ni kuotesha miche ya mikarafuu na matunda mengine kwa wingi katika
vitalu vinavyomilikiwa nayo.
“Tumeanza kuimarisha vitalu vya miche ya mazao mbalimbali ikiwemo
mikarafuu pamoja na miti ya matunda....wakulima wameitikia vizuri na
wanakuja kwa wingi kuchukua miche hiyo na kuotesha katika mashamba yao,”
alisema Katibu Mkuu.
Affan alisema kazi kubwa inayofanywa na Wizara kwa sasa ni kutoa
elimu juu ya kuotesha miche ya mikarafuu kwa mafanikio ili miche hiyo
iendelee kukua vizuri.
Alisema wamechukua uamuzi huo kutokana na kuwepo kwa malalamiko kwa
wakulima kwamba miche ya mikarafuu imekuwa na matatizo mengi yakiwamo ya
ukuaji mgumu kwani ukipanda miche 50, inayokubali na kustawi vizuri ni
10 tu.
“Tumeanza kutoa elimu kwa mabwana shamba pamoja na mabibi shamba kwa
wakulima juu ya mbinu za kisasa za kuotesha miche ya mikarafuu kwa
mafanikio makubwa,” alisema Affan.
Wizara ya Kilimo na Maliasili imeweka lengo la kuotesha na kusambaza
miche ya mikarafuu pamoja na ya matunda kwa wakulima ipatayo 200,000
Unguja na Pemba.
Chanzo: habari leo
No comments:
Post a Comment