Thursday 1 March 2012

SMZ yakerwa wanafunzi kufutiwa matokeo

TATIZO la wanafunzi wengi wa kidato cha nne Zanzibar kufutiwa matokeo ya mitihani yao limeisikitisha Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, na sasa imeanza kufanya uchunguzi kutafuta kiini chake.
Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi alisema hayo jana wakati alipozungumza na waandishi wa habari nje kidogo ya mji wa Unguja.
“Serikali imesikitishwa sana na tatizo la kufutiwa kwa mitihani ya wanafunzi wengi wa Zanzibar...kwa sasa tunafanya uchunguzi zaidi kujua kiini cha tatizo hilo kwa ajili ya kulifanyia kazi,” alisema Balozi Seif.
Alisema tatizo hilo limezusha malalamiko na majonzi makubwa kwa wananchi na wazazi kwa kuwa kitendo cha kufutiwa mitihani kwa wanafunzi, kinatishia maendeleo na mustakabali wa elimu.
Awali Kamati ya Wazee iliyoundwa kuangalia suala hilo, walilitaka Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA) kutengua uamuzi wa kuwafutia wanafunzi mitihani ya kidato cha nne.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Ali Hassan alisema si kitendo cha kiungwana kuwafutia wanafunzi mitihani wakati hawahusiki na tatizo hilo na kupendekeza kiini cha tatizo hilo kitafutwe na kuchukuliwa hatua za kinidhamu wahusika.
“Sisi kamati ya wazee tunalitaka Baraza la Taifa la Mitihani kubadilisha uamuzi wake wa kuwafutia wanafunzi mtihani wa taifa kwa sababu makosa si ya wanafunzi waliovujisha mitihani hiyo,” alisema Hassan.
Kamati hiyo imepinga adhabu ya miaka mitatu ya wanafunzi kutofanya mitihani baada ya kubainika kufanya udanganyifu wa mitihani hiyo na kusema hayo si makosa yao.
Imedai kuwa wanafunzi 1,045 wameathirika baada ya kufutiwa mitihani hiyo kwa upande wa Unguja na Pemba ambapo shule 30 zilihusika na mpango huo

No comments:

Post a Comment