Monday 1 October 2012

Azam yaleta meli mpya Zanzibar

KAMPUNI ya Azam Marine inayomiliki boti ziendazo kasi hapa nchini, imeingiza meli mpya na ya kisasa itakayochukua zaiidi ya abiria 1,500 na magari 200.
Meneja Mkuu wa Kampuni ya Azam Marine, Hussein Mohammed Saidi, amesema hayo mjini Zanzibar jana kuwa meli hiyo ambayo itafanya safari zake kati ya Dar es Salaam, Zanzibar na Pemba itatoza nauli nafuu kwa abiria wake.
Alisema meli hiyo inatarajiwa kuanza safari zake mara baada ya kukamilisha taratibu za mamlaka mbalimbali.
Meli hiyo inayoitwa Azam SeaLinki ni ya kisasa katika ukanda huu wa mwambao wa nchi za Kusini na Pembe ya Afrika.
Hussein alisema, meli hiyo ambayo imetengenezwa nchini Ugiriki, inatayarishiwa eneo maalumu litakalotumika kwa kupakia na kushusha abiria na mizigo yakiwemo magari.
Alisema meli hiyo itasafiri kwa muda wa saa tatu kutoka Dar es Salaam hadi Zanzibar na saa nne kutoka Zanzibar hadi Pemba ama saa 7 kutoka Dar es Salaam hadi Pemba.
Meneja huyo aliongeza kuwa pamoja na kuwasili kwa meli hiyo, Kampuni ya Azam pia inatarajia kuleta meli nyingine ya abiiria inayojulikana kama Kilimanjaro namba 4.
Kwa upande wao, baadhi ya wananchi wa visiwa vya Zanzibar walipongeza ujio wa meli hiyo, lakini wakaitaka serikali kuendelea kudhibiti uingizwaji wa meli chakavu na kukuu ili kuepuka uwezekano wa kutokea ajali za mara kwa mara.
Rajabu Khamisi, mkazi wa Pemba na Rehema Omari wa mjini Zanzibar, walisema kuna haja ya serikali kusimamia ukomo wa nauli ili kila mwananchi aweze kusafiri kutoka sehemu moja hadi nyingine kwani vipato vyao havilingani.
Chanzo: Nipashe

No comments:

Post a Comment