Friday 5 October 2012

Jussa atangaza kujiondoa uongozi wa juu CUF

Salma Said, Zanzibar na Elias Msuya
NAIBU Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF) Zanzibar, Ismail Jussa Ladhu jana amemuandikia barua rasmi Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba kutaka kujiuzulu wadhifa wake huo chamani.
Kwa mujibu wa barua hiyo ya Oktoba 5 mwaka huu iliyosambazwa kwa vyombo vya habari nchini iliyotiwa saini na yeye mwenyewe, Jussa amesema amemuomba mwenyekiti wake kuwa utekelezaji wa maamuzi ya kujiuzulu uanze kutekelezwa rasmi Oktoba 10, 2012.
“Nimechukua uamuzi huu baada ya kuzungumza na kushauriana na viongozi wangu wa juu wa Chama ambao ni Mwenyekiti, Profesa Lipumba, Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Machano Khamis Ali na Katibu Mkuu Maalim Seif Sharif Hamad takriban miezi miwili iliyopita. Nawashukuru baada ya kunitaka niwape muda wa kulitafakari walinikubalia lakini wakaniomba nibakie hadi tutakapokamilisha baadhi ya shughuli muhimu za Chama katika kipindi hichi,” alieleza.
Akitaja sababu za kutaka kujiuzulu, Jussa alisema, “Sababu kubwa zilizonisukuma kukiomba Chama kiniruhusu niachie nafasi hii ni kwa kuwa muda mrefu sasa kuhisi kwamba majukumu niliyo nayo ya kuwa msimamizi mkuu wa utendaji wa Chama kwa upande wa Zanzibar na wakati huo huo kuwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi wa jimbo la Mji Mkongwe hakunipi fursa ya kujifaragua na kutumikia nafasi zote mbili kwa ufanisi unaotakiwa,” alisema Jussa.
Hata hivyo alkizungumzana Mwananchi kwa njia ya simu Jussa alisema kuwa lengo la kujiuzulu ni kupata nafasi zaidi ya kushiriki kwenye operesheni hizo kwani kuwa katika cheo hicho kunamnyima nafasi hiyo.
“Lengo langu ni kupatikana kwa mtu atakayekuwa ofisini wakati wote ili wengine washughulike na operesheni kama hizo. Kwa sababu katika chama chetu ukiwa naibu katibu mkuu unakuwa mtendaji wa chama kwa wakati wote. Lakini mimi kwa shughuli za majukwaani au kwenye operehseni nitakuwepo wakati wote.
Aidha Jussa alisema, “Nataka kuona kazi ya kuibana Serikali ndani na nje ya Baraza ili iwajibike zaidi kwa wananchi inaimarika zaidi.”
Sababu nyengine ya kutaka kujiuzulu Jussa alisema, “Nimekusudia kutumia muda mwingi zaidi kutoa mchango mkubwa zaidi katika harakati za wananchi wa Zanzibar zinazoendelea za kuhakikisha kuwa Zanzibar inarejesha mamlaka yake kamili kitaifa na kimataifa itakayofuatiwa na kuwepo kwa Muungano wa Mkataba kati yake na Tanganyika yenye mamlaka kamili kitaifa na kimataifa.”
Alisema harakati zinazoendelea hivi sasa Zanzibar kwa njia za amani na za kidemokrasia kwa kutumia mchakato wa Katiba Mpya zinahitaji kuungwa mkono na kupewa msukumo wa dhati na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi waliochaguliwa na wananchi wa Zanzibar.
Naibu Katibu Mkuu huyo alisema lengo lao kama wawakilishi ni kwenda kusimamia maslahi ya wananchi ndani ya vikao vya Baraza la Wawakilishi hivyo baada ya kutafakari kwa kina ameona ni vyema akiachia ngazi ili apate muda mzuri wa kufanya kazi hiyo ya kuwasaidia wananchi wa Zanzibar.
Jussa ambaye ni Mwakilishi wa Jimbo la Mji Mkongwe ambaye kwa kiasi fulani amekuwa akitoa changamoto kubwa kwa Serikali katika uwajibikaji tokea kuingia kwake katika chombo cha kutunga sheria, ametetea uamuzi wake huo kwa kusema, “Nikiwa sina majukumu mengine ya kiutendaji nitakuwa na muda kutosha wa kulifanya hili mimi na Wawakilishi wenzangu tunaotoka CUF na CCM, vyama viwili vya siasa vilivyomo Barazani”.
Wakati huo huo, leo kumeandaliwa kongamano kubwa la kitaifa ambalo pamoja na mambo mengine linatuzungumzia mchakato wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unaoendelea nchini na kutoa fursa ya wananchi mbalimbali kushiriki na kutoa mawazo yao katika kongamano hilo ambalo limetayarishwa na kamati ya maridhiano ambayo Jussa ni mjumbe.
Kwa mujibu wa taarifa iliyosambazwa kwa vyombo vya habari na kutiwa saini na Mwenyekiti wa Kamati ya Maridhiano Zanzibar, Mzee Hassan Nassor Moyo alisema kongamano hilo litakalofanyika katika ukumbi wa Salama Bwawani litatoa fursa ya wazanzibari kutoa maoni yao juu ya mustakabali wa nchi yao ndani ya Muungano.
Mwenyekiti wa kongamano hilo litakalowashirikisha watu mashuhuri, wasomi na wanasiasa wa vyama mbalimbali ni Professa Abdul Shareef huku wazungumzaji ni pamoja na aliyekuwa Katibu wa mwanzo wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Salum Rashid, Mzee Hassan Nassor Moyo, Mwanasheria Mkuu Othman Masoud Othman, Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) Ibrahim Mzee.
Wengine ambao wamepangiwa kuzungumza katika kongamano hilo ni Amiri Mkuu wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (Jumiki) Sheikh Msellem Ali Msellem, Waziri asiye na Wizara Maalum na Mwakilishi wa Kiembe Samaki Mansoor Yussuf Himid, Mwenyekiti wa ZAHILFE Ndugu Kassim Hamad Nassor, Mwenyekiti wa Vijana wa Umoja wa Kitaifa Ndugu Khaleed Said, Rais wa Zanzibar Law Society (ZLS) Salim Toufiq.
Jussa ni miongoni mwa wanasiasa na viongozi waliojitokeza hadharani ya kuonesha msimamo wa kutaka Zanzibar yenye mamlaka kamili ndani ya Muungano huku wakitaka suala la Muungano wa Mkataba badala ya Muungano wa katiba kama ulivyo sasa.
Jusa
Jussa ameongeza kuwa anataka kutumia muda mwingi zaidi kutoa mchango mkubwa katika harakati za wananchi wa Zanzibar zinazoendelea za kuhakikisha kuwa Zanzibar inarejesha mamlaka yake kamili kitaifa na kimataifa itakayofuatiwa na kuwepo kwa Muungano wa Mkataba kati yake na Tanganyika yenye mamlaka kamili kitaifa na kimataifa.
“Harakati zinazoendelea Zanzibar kwa njia za amani na za kidemokrasia kwa kutumia mchakato wa Katiba Mpya zinahitaji kuungwa mkono na kupewa msukumo wa dhati na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi waliochaguliwa na wananchi wa Zanzibar kwenda kusimamia maslahi yao na ya nchi yao. Nimetafakari na kuona kwamba nikiwa sina majukumu mengine ya kiutendaji nitakuwa na muda kutosha wa kulifanya hili mimi na Wawakilishi wenzangu tunaotoka CUF na CCM, vyama viwili vya siasa vilivyomo Barazani,” alisema.
Vuguvugu hilo la kudai Zanzibar huru linaungwa mkono baadhi ya viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar huku watu wachache wakiwakataa kuunga mkono maamuzi ya wazanzibari wengi ambapo limeanza zamani lakini katika siku za hivi karibuni tokea kuanza kwa mchakato wa katiba limeubuka upya ambapo kwa kiasi kikubwa wazanzibari wamekuwa wakitumia muda wao mwishi kujadili suala hilo.
Kufuatilia kujiuzulu wadhifa wake huo Jussa kutampa nafasi ya kushughulikia suala zima la kuitetea Zanzibar ndani ya muungano katika kipindi hiki cha mchakato ukusanyaji wa maoni ya katiba lakini bado Jussa atabaki kuwa Mjumbe wa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa na Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa katika chama.
Akiwatoa khofu wafuasi na viongozi wenzake wa chama katika uamuzi wake wa kujiuzulu Jussa alisema “Nawahakikishia viongozi na wanachama wenzangu wa CUF kwamba tutaendelea kushirikiana pamoja katika shughuli nyengine zote za kisiasa za Chama na kwa pamoja tutafanya kazi kuyatimiza malengo tuliyojiwekea. Naahidi kumpa ushirikiano kikamilifu mwanachama yeyote atakayeteuliwa kujaza nafasi ninayoiwacha” .
Jussa amekitumikia chama hicho kwa muda mrefu tokea kuanzishwa kwake wakati akiwa shule ya sekondari ambapo wakati wa ukusanyaji wa maoni ya kutaka kurejeshwa mfumo wa vyama vingi Jussa alikuwa ni kijana pekee katika Jimbo la Mji Mkongwe aliyesimama mwanzo na kutoa maoni yake akitaka kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi.
Baadae Jussa alijiunga na CUF na kuanza kupanda ngazi moja baada ya nyengine akiwa karibu sana na Katibu Mkuu wa Chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad ambapo alishika nafasi mbali mbali ikiwemo ile maarufu ya Mkurugenzi wa mambo ya nje na ushirikiano na kimataifa ambayo kwa kiasi kikubwa ndio iliyompa umaarufu ndani na nje ya nchi kwa kuwasiliana moja kwa moja na mabalozi mbali mbali nchini.
Nafasi ya Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Jussa amekabidhiwa tokea Disemba 2010 ambapo kabla ya hapo aliwahi kushika nafasi mbali mbali katika chama hicho.
Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment