Friday 5 October 2012

Dr Shein Apokea Waya Mpya wa Umeme

Dr Shein akikagua waya mpya wa umeme
 HATIMAE waya mpya wa umeme utakaolazwa baharini kutoka Ras Fumba Zanzibar hadi Ras Kiromoni Dar-es-Salaam umewasili Zanzibar na kupokewa rasmi pamoja na kukaguliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, huko katika bandari ya Malindi mjini Unguja. Waya huo utakaotumika katika mradi wa uwekaji wa waya wa pili wa umeme kutoka Ras-Fumba hadi Ras Kiromoni Dar-es-Salaam, shughuli zake za ulazaji zinatarajiwa kuanza siku ya Juamatatu majira ya asubuhi. Akitoa maelezo yake huku akionesha furaha kubwa Dk. Shein alitoa pongezi kwa Kampuni iliyotengeza waya huo pamoja na Wakandarasi waliotengeza waya huo alieleza kuwa licha ya kuwa kazi hiyo ni ngumu lakini imefanywa vizuri. Dk. Shein alisema kuwa kuja kwa waya huo kutapunguza usumbufu wanaoupata hivi sasa wananchi wa kupata umeme kwa mgao kwani waya huo utakuwa na umeme wenye megawati 100 ambazo zitatosheleza kwa kiasi kikubwa na nyengine kubakia.
Alisema kuwa matumizi ya umeme kwa kisiwa cha Unguja ni megawati 45 tu kwa hivi sasa lakini waya una megawati 100 ambazo zitasaidia kutoa huduma hiyo pamoja na kuweza kujipanga vizuri kwa shughuli nyengine za maendeleo hapo baadae. Aidha, Dk. Shein alisema kuwa waya huo ambao pia, utasaidia kutoa huduma nyengine za mawasiliano yakiwemo mtandao wa intaneti utawezesha kutoa huduma za e- Government pamoja na huduma za mkonga wa taifa kama ulivyo kwa waya uliolazwa kisiwani Pemba. Rais Dk. Shein anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa ulazaji wa waya huo katika hafla itakayofanyika siku ya Jumaatatu asubuhi. Akipata maelezo kutoka kwa jopo la wakandarasi wa waya huo Kampuni ya VISCAS, na mhandisi mdogo pamoja na Mhandisi Mshauri kutoka Kampuni ya ESB International pamoja na Msaidizi Mtendaji Mkuu wa MCA-T kwa upande wa Zanzibar Bwana Ahmed Rashid, walieleza kuwa shughuli hizo za ulazaji wa waya zitafanywa si zaidi ya siku 12 kwa kutumia meli na vifaa walivyonavyo kwa kushirikiana na meli nyengine. Walieleza kuwa waya huo wenye urefu wa kilomita 37 na uzito wa tani 2000, shughuli za ulazaji pamoja na zile za kuunganisha katika vituo maalum vilivyopo Mtoni na vile vya Dar-es-Salaam zinatarajiwa kumalizika na kutoa huduma ya umeme unatokana na waya huo mpya mnamo mwanzoni mwa mwezi wa Novemba. Aidha, uongozi wa MCA-T ulitoa shukurani kwa uongozi wa Mkoa wa Mjini Magharibi kwa mashirikiano makubwa ya mazungumzo na viongozi wa dini katika mchakato mzima wa kuvunjwa nyumba, madrasa na baadhi ya nyumba za ibada kwa lengo la kupitisha waya mpya wa umeme kutoka Fumba hadi Mtoni. Uongozi huo wa MCA-T pia ulieleza kuwa kuna hakiba ya waya upatao mita 450 ambao utawekwa katika kituo cha Mtoni kwa ajili ya dharura pale itakapohitajika na kusisitiza kuwa tayari nguzo maalum za ardhini zimeshawekwa katika baadhi ya sehemu. Walieleza kuwa waya huo mpya utalazwa sambamba na waya huu uliopo hivi sasa na kusisitiza kuwa shughuli hizo za ulazaji zinatarajiwa kuanza siku ya Jumatatu asubuhi. Nae Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Bwana Hassan Ali Mbarouk alisema kuwa waya huo unauwezo wa kuishi zaidi ya miaka 30. Mradi wa waya huo wa umeme umenza miaka mine iliyopita ambao umetengenezwa na Kampuni ya VISCAS kutoka Japan ambao mbali ya kutengeneza pia, watakuwa na jukumu la ulazaji wa waya huo ambao utasimamiwa na Wahandisi washauri wa Kampuni ya ESB International kutoka Ireland. Mradi huo unafadhiliwa na Shirika la Changamoto la Milenia (MCC) kutoka Marekani. Baadhi ya wananchi ambao walikuwepo katika hafla hiyo fupi huko katika bandari ya Malindi mjini Unguja wakizungumza na mwandishi wa habari hizi walieleza kufarajika kwao na juhudi zinazochukuliwa na Serikali yao inayoongozwa na Dk. Shein katika kuwatatulia kero zao. Walieleza kuwa kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza huduma za maendeleo kwa wananchi sambamba na kuimarisha sekta za maendeleo zikiwemo mawasiliano pamoja na sekta ya utalii ambayo ndio sekta inayoipatia fedha nyingi serikali.

No comments:

Post a Comment