Saturday 10 November 2012

Unyama huu ukomeshwe Zanzibar

Na Salim said Salim
KATIKA mwisho wa mwezi Aprili, mwaka 2005 nilieleza katika gazeti hili namna nilivyosikitishwa na kushitushwa na baadhi ya watu katika nchi mbali mbali walivyodhalilishwa, kuteswa na hata kuuliwa na vyombo vya dola kwa visingizio mbali mbali.
Vyombo vya dola ambavyo ndio dhamana vya usalama wa raia vilikataa kuhusika na kuishia kulaumu wahuni.
Lengo la makala ile lilikuwa kuieleza serikali ya aliyekuwa Rais wa Zanzibar, komandoo Salmin Amour, kwamba historia haitafumbia macho mwenendo wake wa utawala na kumtaka achukue haraka zitakazowapa nafasi watu wa Visiwani kuiona serikali kuwa ni yao na ipo kwa masilahi yao.
Hivi sasa komandoo anakumbukwa zaidi kwa vitendo vile kuliko mengine. Leo ninakusudia kurejea simulizi ile kwa vile yanayotokea Zanzibar hivi sasa yana muelekeo unaotaka kufanana na tuliyoyaona wakati wa utawala wa komandoo.
Katika makala yangu ile ya zaidi ya miaka saba iliyopita nilieleza kuwa nilipokuwa kijana mdogo ninasoma Czechoslovakia, sasa imegawika na kuwa nchi mbili za Czech na Slovak, katika mwaka 1964 nilitembelea kijiji kimoja cha Slovakia, nje kidogo ya mji wake mkuu wa Bratislava.
Nilielezwa namna ambavyo kijiji hiki kilichopo kando kando ya Mto Danube, kilivyoshuhudia halaiki ya aina yake wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia (1939-45).
Maelezo niliyoyapata kutoka kwa watu walioshuhudia halaiki ile na kupoteza ndugu, jamaa na marafiki ilinipelekea kukosa usingizi kwa karibu wiki nzima.
Maelezo yale yalikuwa juu ya namna askari wa kinazi wa Adolf Hitler, dikteta wa Kijerumani aliyesababisha vita walivyotesa watu na kutia moto nyumba huku watu wakiwamo ndani usiku na mamia kupoteza maisha.
Furaha yangu ya kutembelea Slovakia ilinitumbukia nyongo, lakini nilipata mafunzo ya namna mbavyo madikteta wanavyokuwa hawathamini maisha ya watu.
Hadithi za kusikitisha za watu wale sitazisahau daima. Sikujua kwamba ipo siku nitakaporudi nyumbani nitasikia hadithi zinazofanana kwa kiasi fulani na zile.
Nilieleza mara kadhaa nilipokuwa Addis Ababa, Ethiopia, wakati wa utawala wa Mengistu Haile- Mariam, ambaye sasa anaishi Zimbabwe kama mgeni wa rafiki yake Rais Robert Mugabe.
Niliwaona askari wa mgambo waliokuwa wakiitwa Kabele walivyokuwa wakipiga watu barabarani na majumbani. Walichokuwa wakifanya waliiga askari wa dikteta wa Haiti Papa Doc waliojulikana kama Tom Tom Makut.
Siku moja nilipokuwa Addis Ababa, katika eneo linaloitwa Markato, yaani markiti (sokoni) vijana hao waliwapiga watu wawili mpaka wakafa hapo hapo na siku ya pili yake vyombo vya habari vya serikali vilieleza kuwa vijana wale walikuwa wapinga mapinduzi na wachochezi.
Kosa lao ni kuwa vijana wale hawakuitikia na kukaa kimya pale mwanamgambo mmoja wa Kabele aliposema kwa sauti ‘Maisha marefu kwa Mengistu’.
Kila mtu alitarajiwa ajibu : ‘Aishi’. Baadaye nilikuja kupata habari kwamba mmoja alikuwa amelewa na mwingine alikuwa hasikii vizuri.
Nilikwenda Arusha ambapo nilifanya kazi kama mwandishi wa magazeti ya serikali ya Daily News na Sunday News kabla hayajataifishwa mwaka 1971.
Huu ni mji nilioufurahia sana kwani maisha yalikuwa mazuri kwa kipindi cha karibu miaka saba niliyokuwepo huko tangu mwaka 1967, mara tu baada ya kuundwa jumuiya ya kwanza ya Afrika Mashariki.
Lakini nilipotembelea Arusha mwaka 2000 kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari nilijikuta nakumbuka Czechoslovakia. Hii ilitokana na siku moja kwenda kusikiliza kesi za mauaji ya halaiki ya Rwanda ya 1994.
Sikustahamili na nilitoka nje mapema kutokana na maelezo yaliyotolewa kuonesha binadamu anavyoweza kupoteza utu wake na kuwa mnyama, katili kama nilivyowaona wanyama pindi nilipotembelea mbuga za Manyara, Ngorongoro, Serengeti na Momella nilipokuwa ninaishi Arusha.
Mashahidi walielezea mauaji na mateso yaliyofanywa na vijana wa Interahamwe yaliyoandamana na uchomaji nyumba moto huku watoto wadogo wakilia ndani walivyokuwa wakijiona wanapoteza maisha yao wakiwa hawana la kufanya.
Wakati nilipoandika makala ile kwa gazeti hili nikiwa Zanzibar nilishuhudia mambo ambayo sikutaka kuyaamini.
Siku moja baada ya kutoka Ofisi ya Tume ya Uchaguzi Kilimani, nilipigiwa simu kwenda Hospitali ya Al-Rahma iliyokuwepo masafa ya mita 300 toka mahali nilipokuwepo.
Nilipofika hapo niliona watu waliokatwa katwa mapanga kichwani, miguuni na wengine kupigwa nondo, huku wakimiminika damu. Wawili walikuwa wamepoteza fahamu. Ilinikumbusha mbali na kutoamini niliyoyaona. Picha na video za matukio yale zipo.
Jumla ya watu waliofikishwa pale wakiwa majeruhi walikuwa 10, wote taabani na nilielezwa kuwa walipigwa mapanga na nondo wakati wakingojea kujiandikisha kuwa wapiga kura katika kituo cha Kijiji cha Kinuni.
Wakati ule watu wengi walichomewa moto nyumba zao na kulazimika kwenda kuishi porini na kupoteza mali zao. Visima na maskuli yalitiwa kinyesi na kina fulani ili papatikane visingizio vya kukamata watu.
Baadaye komandoo aliamrisha kuvunjwa nyumba kadha hapo Mtoni Kidatu na wapo waliopoteza maisha yao kwa mshituko wa moyo na ufukara waliotiwa na komandoo kwa sababu za kisiasa. Kinara wa uvunjaji nyumba zile alidaiwa kuwa ni Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magahribi, Abdulla Rashid.
Watu wengi, hasa wenye asili ya Kisiwa cha Pemba, walifunguliwa kesi bandia za madai ya kuwa wazembe na wazururaji au kumtukana rais. Ilikuwa balaa ya aina yake.
Kwa hakika hali hii si tu kuwa ilikuwa inasikitisha, bali pia ilikuwa ya kutisha. Wakati ule nilisema: Hii ni hali ambayo haipaswi kunyamaziwa kimya na aliyekuwa Inspekta Jenerali wa Polisi, Omar Mahita.
Nilimueleza Mahita, kuwa baadhi ya hao waliopigwa vibaya sana ni maofisa wastaafu wa Jeshi la Polisi ambao wakati ule walikuwa mara kwa mara wakikamatwa na kupigwa panapotokea mtafaruku wa kisiasa Visiwani.
Nilieleza kuwa uzoefu wangu wa kufanya kazi kwa karibu na aliyekuwa Rais Benjamin Mkapa alipokuwa Mhariri Mtendaji wa Daily News ulinipa mashaka kama hali ile ya mateso waliokuwa wanapata Wazanzibari ilikuwa inamsumbua.
Wakati mmoja Mkapa alisema baadhi ya mambo ya Zanzibar yalikuwa yanamkosesha usingizi, lakini nikaeleza wasiwasi wangu kama alikuwa na nia hasa ya kumaliza balaa ile iliyokuwepo wakati ule. Sikushangaa alipomuachia urithi wa maovu yale Rais Jakaya Kikwete mwaka 2000.
Nimeeleza haya hii leo kuonesha wasiwasi wangu kwamba ile hali mbaya ya siku za nyuma huenda ikarudia Zanzibar kama hapatakuwepo ustahamilivu, kuondosha uonevu na kuachana na mtindo wa kubuni kesi bandia.
Panapotokea mzozo sheria iachiwe ichukue mkondo wake na siyo kudhalilisha watu kwa kuwapiga bakora, kuwanyoa ndevu, kuwanyima chakula na haki ya kukoga na kubadili nguo wakati wakiwa mahabusu kama tunavyoona hivi sasa. Jamani tukumbuke Mungu yupo!
Hivi sasa tayari watu wamekuwa na mashaka makubwa na hali iliyopo Zanzibar na baadhi ya nchi zimeshaanza kulalamika juu ya vitendo vya uvunjaji wa haki za binadamu Visiwani.
Sura iliyopo sasa Zanzibar ya serikali ya umoja wa kitaifa ni chafu na inanuka na inahitaji kusafishwa na kufukizwa ubani na udi. Kweli Polisi wanaosema hawahusiki wanashindwa kuwadhibiti hao tunaoambiwa ni vikundi vya Ubaya Ubaya na Mbwa Mwitu?
Au Zanzibar ya leo ina vikundi vya mafia kama tunavyoona katika baadhi ya nchi za Amerika ya Kusini?
Dunia inatuangalia na tayari taasisi za kutetea haki za binadamu kama Amnesty International zinasema hakuna utawala bora Zanzibar.
Mahakama zetu lazima zifanye kazi ya kuonekana kuwa huru na si zinavyoonekana hivi sasa. Hatutaki baadaye kuwasikia mahakimu na majaji wanajikosha kama ilivyofanyika katika miaka ya karibuni kwamba walikuwa wanapelekewa vikaratasi kuelezwa wazishughulikie vipi kesi mbali mbali.
Siasa ni mchezo wa mbinu nyingi za wazi na za siri, lakini huu mchezo mbaya wa kupiga watu majumbani, kuchezea miili yao kwa kuwanyoa ndevu na kuifanya dhamana kama siyo haki ya mshitakiwa ni wa hatari.
Viongozi wakuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Rais Ali Mohamed Shein na Makamu wake wawili, Maalim Seif Sharif Hamad na Balozi Seif Iddi, wajue wao ni dhamana na hawawezi kukwepa dhamana hiyo watakapotakiwa watoe maelezo kwa nini waliruhusu maovu yanayofanyika sasa.
Huu mchezo wa kunyamazia maovu, kama utaachiwa kuendelea, utatoa sura mbaya katika kumbukumbu za historia kama ilivyo kwa iliyokuwa Czechoslovakia, Ethiopia wakati wa utawala wa dikteta Mengistu, Chile wakati wa utawala wa Agostino Pinochet na mauaji ya halaiki yaliotokea Rwanda.
Zanzibar haiwezi kukaribia huko lakini kila jambo lina mwanzo wake . Wakati wa utawala wa komandoo Salmin Amour hali mbaya ilianza kama hivi na baadaye tukashuhudia watu wengi wakipoteza maisha yao na kuwa vilema.
Orodha ya majina ya watu waliouawa, kujeruhiwa na kufungwa jela kwa maonevu inajaza ukurasa huu. Huo ndio ukweli na waliofanya kama hawataki yaelezwe wasingethubutu kutenda maovu yale.
Ni vizuri hatua zikachukuliwa haraka kuzuia hali tete iliyojaa hasama na maonevu yaliopo sasa kudhibitiwa. Moto huanza na cheche na tayari cheche tunaziona na zikiachiliwa watatokea watu kuzimwagia petroli.
Tusingojee moto kupanda juu ya paa na ndipo tukaanza kufanya juhudi za kuuzima. Tukumbuke ule wimbo wa Malindi usemao: Moto ukija kuwaka mzimaji nani?
Wale wenye kupanga njama hizi za maovu na kutaka kuirejesha Zanzibar ilipotoka wasipewe mwanya wa kupumua. Mchezo wao utatuponza sote na kuja kujutia.
Tukumbuke ni rahisi kubomoa kuliko kujenga na wazee walituasa kwa kutuambia….majuto ni mjukuu na tukifanya masihara majuto yetu yanaweza kuwa ya vilembwe na vitukuu.
Tushirikiane kuirejesha Zanzibar katika hali ya utulivu na kama mtu anataka kupiga watu anunue ngoma na apige mpaka ipasuke, si kupiga migongo ya watu na anayetaka kunyoa ndevu anunue beberu na ajifunze kunyoa ndevu na si za watu wengine.

No comments:

Post a Comment