Sunday 3 February 2013

Uwanja wa ndege Z`bar kuwa wa Kimataifa mwakani

Chapa
Uwanja wa ndege wa Abeid Amani Karume Zanzibar utafikia vigezo vya Kimataifa baada ya kukamilika mradi wa miezi 18 wa kuzungusha ukuta na kutanua sehemu ya maegesho ya ndege mwakani.
Tamko hilo limetolewa na Mkurugenzi wa Viwanja vya ndege Zanzibar , Kapteni Said Ndumbugani, katika ziara ya Naibu Waziri wa Miundo mbinu na Mawasiliano Zanzibar, Issa Haji Gavu ya kukagua mradi huo.
Ndumbugani, alisema mradi huo unatarajia kutumia dola za Marekani Milioni 50 ikiwa ni mkopo kutoka Benki ya dunia na ujenzi wake unafanywa na Kampuni ya Sogea Satom ya Ufaransa.
Alisema kuanzia Febuari 4 mwaka huu kilomita 2.2 za eneo la kuegesha ndege katika uwanja huo litafungwa kupisha ujenzi wa mradi huo.
Hata hivyo alisema huduma za ndege zitaendelea kama kawaida katika uwanja huo wakati wote wa ujenzi.
Alisema eneo la ukuta unaojengwa utakuwa na mzunguko wa kilomita 12 hadi baada ya kukamilika na tayari kilomita saba zimekamilika tangu kuanza kwa ujenzi wa mradi huo Novemaba mwaka jana.
Aidha alisema kiasia cha Shilingi Bilioni 3 kimetumika kulipa fidia wananchi pamoja na kufanikisha kazi ya kujenga ukuta unaozunguka uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Zanzibar.
Mkurugenzi huyo alisema baada ya kukamilika mategenezo yote uwanja huo utakuwa na uwezo wa kutoa huduma kwa ndege nane kwa wakati zikiwemo aina ya Boeing badala ya ndege tatu.
Alisema uwanja wa ndege Zanzibar baada ya njia ya kutua na kuondokea kukamilika ujenzi wake sasa umekuwa na urefu wa kilomita 3.22 na hupana mita 45.
Naibu Waziri Gavu alisema ameridhishwa na utekelezaji wa mradi huo na kutaka uongozi kuhakikisha ujenzi unakamilika muda muafaka.
Gavu, alisema kukamilika kwa mradi wa kuzungusha ukuta kutaondoa tatizo la mifugo kukatisha uwanjani pamoja na maeneo ya makaazi ya wananchi kuvamiwa.
“Lengo kubwa la serikali kuona uwanja wa ndege Pemba unatoa huduma kwa muda wa saa 24 tayari tumepanga kutumia dola za Marekani milioni 1.5 kwa ajili ya kufanyiwa matengenezo makubwa mwaka huu,”alisema Gavu.
Alisema kwamba kuimarishwa kwa viwanja vya ndege kutaongeza pato la Taifa kutokana na idadi ya watu wanaotumia huduma za ndege kufikia milioni moja kwa mwaka Zanzibar.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments:

Post a Comment