Matukio ya kusikitisha, kufedhehesha na yakushangza yamekuwa yakitokea
Zanzibar tangu mwaka jana baada ya wazinzabar kuanzisha harakati za kurudisha
Zanzibar yenye mamlaka kamili (Zanzibar huru), harakati zilizoanzia kwenye
baraza la wawakilishi mwaka 2010, kwa kubadili katiba ya Zanzibar na kuitaja
Zanzibar kuwa ni nchi kamili! Vugu vugu lililochagizwa zaidi na jumuia ya
mihadhara na ya kiislam ( al maarufu kama UAMSHO)!
Vugu vugu hilo lilipelekea mvutano kati ya jeshi la polisi na wafuasi wa
masheikh wanaoongoza jumuia ya UAMSHO. Chakushangaza mvutano au mapambano
yalikuwa ni kati ya polisi na wafuasi wa UAMSHO, lakini tukaamka asubuhi
nakusikia MAKANISA kadhaa yamechomwa moto! Eti waZanzibar hao (UAMSHO) ambao
wamekuwa wakiishi kwa amani na upendo na wakristo kwa karne tele zilizopita, leo
hii wameacha nyumba zote za askari wanaopigana nao, wanaCCM, viongozi wa SMZ, na
masheha badala yake wameenda kuchoma moto makanisa! Hapa tukaambiwa uchunguzi
utafanyika na wahusika watafikishwa kwenye vyombo vya sheria….watu wakakamatwa
kwa nzo, wakatafutwa kila mwenye ndevu akanyolewa, wakahilikishwa, na kwa
kutumia technologia (kama alivyosema Kamishna Mussa), wakaangalia kanda za video
kubaini walokuwepo kwenye vurugu zile na kuwakamata! Tukasubri majibu , tuambiwe
ni nani hasa alochoma makanisa? Ikabaki kuwa “watu wasiojulikana” Jibu mpaka leo
hakuna!
Tutakaa tena kidogo, tukasikia Sheikh Farid katekwa, jeshi la polisi likasema
hajui alipo, itakuwa kajiteka! Vurugu zikazuka tena, makanisa yakachomwa tena,
lakini mara hii wakaongeza na kuchoma maskani za CCM, na polisi mmoja akauliwa
kwa kukatwa katwa kwa mapanga! Mkuu wa jeshi la polisi nchini Said Mwema,
akasema ametuma makachero wenye ujuzi wa hali ya juu (walobobea) kutoka makao
makuu Dar es salaam, kuja Zanzibar kuwatafuta wahusika wote walouwa na kuchoma
makanisa ili wafikishwe kwenye vyombo vya sheria…tukasubiri na tunaendelea
kusubiri, bila kupata majibu mpaka leo!
Hatujakaa vizuri, tukasikia Sheikh Soraga, kamwagiwa tindi kali usoni, na
“mtu asiejulikana”! Kama kawaida tukaambiwa tena, jeshi la polisi linafanya
uchunguzi kuwatia nguvuni wahusika….mpaka naandika habari hii hakuna jibu la
nani alommwagia Sheikh Soraga tindi kali! Jeshi la polisi bado lafanya uchunguzi
tu!
Tukiwa bado tunatafakari hayo, tunasikia tena Padri Ambrose kashambuliwa kwa
risasi, na “watu wasiojulikana”! Lengo ilikuwa ni kumuuwa, lakini bahati nzuri
yupo hai! Hili likaendelea kutushangaza wengi, eti mara hii wazanzibar wamekuwa
wanamiliki silaha za moto, na ni wajuzi wakuzitumia?!! Hapa sasa tukasikia
kauli kali zaidi, tena kutoka kwa viongozi wajuu zaidi kisiasa katika nchi yetu,
akiwemo Rais wa Tanzania, Kanali, Dr. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa serkali ya
Zanzibar Biochemist, Dr. Ali Shein, wakilaani nakuvitaka vyombo vyote vya jeshi
la polisi, wakiwemo usalama wa taifa kufanya uchunguzi kwa weledi wajuu kabisa
ili kubaini na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria wahusika! Tukasubiri na
tunaendelea kusubiri kuwajuwa wahusika, lakini mpaka sasa hakuna jibu!
Eeeh juzi tena tunasikia Pandri Mushi, ameuliwa kwa risasi na “watu
wasojulikana”! Mauaji hayo yanatokea tena ndani ya Zanzibar hiyo hiyo! Mara hii
Tanzania zima ikatikisika, kauli nzito nzito, kutoka kila kiongozi wanchi hii,
kuanzia rais wa Tanzania, rais wa SMZ, waziri wa mambo ya ndani, n.k…karibu kila
mwenye mdomo (access ya vyombo vya habari) alisema na kulaani. Tukaambiwa FBI,
CIA, Mossad wote hao wakishirikiana na TISS watakuja kuchunguza na kuwatia
nguvuni walomuuwa na walo ratibu mauwaji hayo….tukasubiri nab ado twasubiri!
Tukiwa bado tumehamanika na matukio hayo, tukiwa bado tunanyoosheana vidole,
na kutupiana lawama, tukiwa tunazidi kuandamwa na wingo zito…leo tunasikia imamu
sheikh Ali Khamis huko kitope (kaskazini Unguja), ameuliwa kwa kukatwa katwa
mapanga na “ watu wasiojulikana”! Nategemea kauli zitakuwa hizo hizo “Uchunguzi
utafanyika…” Na sisi ni kama vifaranga vya kuku…tutanyonya kesho, nabado
twasubiri kunyonya!
Kwa kweli ukiangalia ukubwa wa visiwa vyetu (Zanzibar) na population yake na
ukilinganisha na matukio haya, utaona kwamba ni matukio mengi sana na yametokea
katika kipindi kifupi sana, matukio yakusikitisha na kulaaniwa na kila
muungwana! Matukio yasiyopaswa kutokea katika jamii ya watu walostaarabika kama
Zanzibar.
Chakusikitisha na kutisha ambacho ndicho kilichonisukuma kuandika haya, ni
kuwa matukio yote haya, yamekuwa yakiishia kuhukumiwa na jamii kwa hisia tu,
huku serkali ikiishia na jibu la “watu wasojulikana upelelezi unaendelea”,
lakini jamii, na hata viongozi wa serkali na dini wamekuwa wakitumia hisia zao,
utashi na mihemko yao kushutumu na hata kuhukumu baadhi ya kikundi au kundi
katika jamii.
Mwanzaoni wapo walojaribu kuhusisha matukio hayo na CUF, lakini walipoona
wazanzibar wa hivi sasa hawatopigana wala kuuwana kwa sababu ya vyama vya siasa,
wakakosa nguvu! Lakini mara zote kundi la UAMSHO, likawa ndio kitambaa chao
(leso) cha kufutia mafua, jasho, mate, n.k., kila tukio likitokea, basi utaskia
UAMSHO hao, kauliwa padre “UAMSHO” , Kamwagiwa tindi kali sheikh -“UAMSHO”,
limechomwa kanisa-“UAMSHO”! Khaa, mengine enhe, lakini mengine nkinehe!
Serkali imeacha kufanya kazi yake (Jeshi la polisi) kama walivyoafanya kule
mwanza alipouliwa RCO , badala yake imeachia jamii ihukumu kwa hisia, ni hatari!
Maana sasa viongozi wa UAMSHO wako ndani, UAMSHO hajulikani ni nani, lakini
mauwaji yanaendelea! Sasa akiuliwa padri au kuchomwa kanisa utaskia ni waislam
hao, naam hisia hisia, waislam hao wa Zanzibar sasa washakuwa magaidi! Si ndo
alivyosema Nchimbi! Na sasa akiuliwa sheikh au ikichomwa misikiti, kwa hisia tu
watasema “ WAKRISTO hao” na wakristo nao washakuwa magaidi! Tunako kwenda
siko!
Siamini na kamwe sitoamini kwamba eti matukio haya yanafanywa na mzanzibar
wakawaida, awe mkiristo au muislam, kamwe siamini kama mzanzibar wakawaida
anamiliki silaha ya moto, na amekuwa mjuzi wakuitumia kiasi kwamba anaweza
kulenga shabaha kwa ustadi mkubwa huku akiwa kwenye vespa na kumuuwa padri!
Siamini kabisa, kama kweli mzanzibar anaweza kumvamia sheikh na kumkata kata
mapanga! Nani basi anae fanya haya? Na anafanya haya kwa nini? Na Kwanini
mapaka leo Kamishna Mussa hajatoa majibu ya walofanya matukio haya?
Inasikitisha na kushangaza sana, waziri mwenye dhamana na ulinzi wa taifa
hili, anaibuka akiwa na maruwe ruwe (hangover) ya mapombe yake alokunywa “Rose
garden” anasema eti wanaofanya matukio hayo ni MAGAIDI, huyu ni msomi wa PhD,
eti daktari wa falsafa! Kwa falsafa ya aliepata Div 0 matokeo ya mwaka huu ya
form 4, basi inatosha kumwambia waziri wakati unatanganza hayo, hukupaswa
kuendelea kuwa waziri wa wazara hiyo tena! Ikiwa umeshindwa kudhibiti magaidi
mpaka wameweza kuingia ndani ya nchi yako, lakini kama haitoshi, wakaweza
kumiliki silaha, wakaweza kupanga na kutekeleza mauwaji na uharibifu wa nyumba
za ibada wakati wewe ndie mwenye dhamana ya kulinda hayo yasitokee, sijui
alikuwa au bado anangoja nini kwenye ofisi yake? Lakini pia angetwambia hawa
magaidi wana demand (madai) nini?
Maana ya neno gaidi (terrorist), ni mtu anaeletea madhara katika jamii au
anaefanya mashambulizi au utekaji kwa lengo la kugofya mamlaka au mtu husika ili
atekelezewe madai yake! Kwa misingi hiyo gaidi huwa akishatenda huwa hutokeza
wazi wazi na kusmema, mimi ndio niliofanya jambo kadhaa, ili unipe, au utekeleze
masharti kadhaa, usipotekeleza ntafanya tena jambo kadhaaa…! Sasa matukio yote
haya hakuna kikundi, wala mtu alojitokeza kukiri kufanya na kusema amefanya ili
apewe nini au anadai nini. Sasa Dr. Nchimbi atwambie magaidi wake hawa wana mdai
nini? Atwambie, wanauwa mapadri ili wapewe nini na kanisa katoliki? Wanauwa
masheikh ili wapewe nini na waislam?
Nakumbuka, nilipokuwa na miaka 12, ilikuwa tukifunga skuli (nilikuwa skuli ya
Jadida, Wete), nikienda kwa bibi yangu Pandani kwa mwewe, kuna mengi niliyapenda
huko pandani ikiwemo kuchota maji kwenye kisima cha ndoo kwa kutumia “roda”,
lakini jambo jengine ilikuwa lilonifanya niamke mapema sana ni “mchezo wa
kupiganisha kuku” ! Niliupenda sana mchezo huu! Walipiganishwa majongoo wakila
aina kuanzia makuchi, majogoo upanga n.k. Lakini ugomvi wa makuchi ulikuwa
mtamu sana, hawachoki haraka, wajuzi wakupigana, hawakubali kushindwa, si woga
na wepesi wakupiganishwa!
Walipiganishwa makuchi wale bila wenyewe kuwa na sababu ya msingi yakupigana!
Walipiganishwa bila kujuwa kwanini wanapigana? Walipigana sababu tu wametumwa
kupigana! Kupigana kwao makuchi hawa ndo furaha ya wapiganishaji, pengine
wapiganaishaji hucheza kamari, na mwenye kuchi alieshinda akapata malipo!
Historia ni mwalimu nzuri, tunasoma kwamba kule India wakati wa harakati za
kudai Uhuru zilizokuwa zikiongozwa na Mahtma Gandhi, wakati huo India ikiwa
koloni la British, wakoloni hawa walikuwa wakiwapiganisha waislam na wahindu,
ili kujenga hoja ya kutowapa uhuru! Walikuwa wakichinja nguruwe kasha wakiwatupa
kwenye misikiti ya waislam…kwa hisia waislam wakiwashutumu wahindu kwa kuwatupia
nyama haramu, najisi kenye nyumba zao tukufu za ibada, kisha wakoloni hawa
wakichnja ng’ombe na kuwatupa kwenye mahekalu ya wahindu, wahindu nao kwa hisia
tu, wakawashutumu waislam, kwamba ndio wanaowauwa miungu yao (wahindu wanaabudu
ng’ombe kama mungu wao), kisha wanawatupa kwenye nyumba zao za ibada! Kwa hisia
wakaishia kupigana na kuuwana….mkoloni akazidi kutawala!
Hali hii ndio nnayo iona Zanzibar, matukio ya kumwagia mavi visima vya maji,
kuchomwa moto nyumba za masheha, kulipuliwa mabomu ofisi za CCM, tuliyaona
mageni yalipoanza miaka 90 kule kisiwani Pemba, tukawa twaambiwa ni wapinzani,
wafukuwa hadi barabara na kuvunja mabomba ya maji! Lakini kisha tukayazoea, na
jamiii ikamjuwa hasa anaefanya hayo ni nani! Sasa kuna kumezuka jipya, lakini
safari hii si Pemba, ni kwa dada yake, Unguja, kumezuka fasheni ya sampuli yake
ya kuwauwa viongozi wa dini, wanauliwa mapadri leo, na kesho wanauliwa
masheikh, kwa zamu!
Ni lazima tutumie akili zetu vizuri katika kutafakari mambo haya! Tuweke
hisia zetu na misukumo ya kiimani pembeni! Tumuombe Mungu wetu atupe hekima ya
kuangalia matukio haya kwa jicho la 3, atupe hekma ya kuwa waadilifu katika
kuchambuwa matukio haya! La sivyo, basi, leo atauliwa Padri John, kwa hisia
upande mmoja utasema –“WAISLAM hao”, kesho atauliwa Sheikh Abdalllah, kwa hisia
upande mwengine utasema – “WAKRISTO hao”, kitakachofuata sihitaji kukieleza
hapa, maana wote tunajuwa! Mungu atunusuru!
Wapiganishaji watakuwa wamekaa pembeni wakitutazama tunavyouwana kwa ujinga
wetu! Watakuwa wanasubiri kuleta misaada ya kibinaadam” (kama wanavyoita
wenyewe), watasubiri kuleta majeshi yao kusimamia amani, watapa habari za
kutanganza kwenye vyombo vyao vya habari kama vile CNN, BBC, Al jazeera n.k
Zanzibar itakuwa maarufu kama ilivyo afghanstan, Iraq, Syria, n.k! Watapata
sababu za kutosha za kuifanya Zanzibar kuwa mkoa wa Tanzania! Utamaduni na asili
ya Zanzibar sasa ndo itapotea kabisa!
Tusikubali kufanywa makuchi tukapiganishwa sie kwa sie….!
Chanzo: Mzalendo
No comments:
Post a Comment