Monday 21 May 2012

Jengo la Wizara Pemba labomoka

Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Fedha na Uchumi Zanzibar, imekubwa na kashfa ya kutoa zabuni ya mradi wa Ujenzi kwa Kampuni isiyokua na sifa na kusababisha jengo la ghorofa kubomoka kabla ya kukamilika huko kisiwani Pemba.
Kwa mujibu wa ripoti ya kuchunguza ubadhirifu wa mali za Serikali ya Baraza la Wawakilishi (BLW), imesema wizara hiyo ilifunga mkataba na Kampuni ya Ujenzi Jonsons Costruction Limited kutoka nchini Kenya Mei 13, 2009.
Ripoti hiyo imesema kwamba wizara hiyo ilitoa zabuni ya ujenzi wa makao makuu ya wizara hiyo Pemba mradi ambao ulikuwa na thamani ya Sh 1,460,000,000, kinyume na sheria namba 6 ya usajili wa wakadarasi ya mwaka 2008.
Akihojiwa na kamati hiyo mhandisi kutoka Idara ya Ujenzi ya SMZ, Sabra Ameir Issa, alisema kwamba serikali iliwataka kufanya uchunguzi baada ya jengo kuanza kutitia kabla ya kukamilika.
Akifafanua mbele ya kamati hiyo, mhandisi Sabra, alisema tatizo kubwa waligundua mjenzi wa mradi huo, hakuwa na utaalamu unaohitajika katika kazi kama hiyo.
Mhandisi huyo alisema kwamba kampuni hiyo haina sifa ya kufanyakzi Zanzibar hata kupewa kwake zabuni na Wizara hiyo ilikuwa ni kwenda kinyume na sheria kwa sababu haikusajiliwa katika bodi ya wakandarasi Tanzania bara wala Zanzibar.
Alitaja sababu nyingine za jengo hilo kutitia kuwa ni ubunifu mbaya ya jengo, usimamizi mbovu, ujenzi uliokosa utaalamu, na uwezo mdogo wa mjenzi huyo.
Mhandisi Sabra, alisema katika uchunguzi wao walibaini hakuna Mhandisi hata mmoja wa ujenzi katika kampuni hiyo aliyesajiliwa na Bodi ya Wakandarasi Tanzania bara au Zanzibar.
Hata hivyo, mshauri mwelekezi wa mradi huo mhandisi Arch Yared Dondo, kutoka kampuni ya K&M Archplans Tanzania LTD, alieleza Kamati ya uchunguzi kwamba katika mchakato kumtafuta mkandarasi wa ujenzi huo Kampuni yake hakushirikishwa na Wizara huyo.
Alisema kwamba kwa upande wake hakuona kama ni tatizo kwa kuwa katika mkataba wao haikuonyeshwa kuwa anatakiwa kushiriki katika mchakato wa kumpata Mkandarasi wa ujenzi wa jengo hilo.
Aidha Dondo, alisema kwamba mmiliki wa kampuni hiyo bahati mbaya sio mtaalamu wa ujenzi (Civil Enginer) bali ni fundi Bomba na kampuni yake haikuajili Muhandisi wa ujenzi hata mmoja kabla ya kuanza kwa utekelezaji wa mradi huo.
Mshauri mwelekezi pia alisema ujenzi wa jengo hilo ulianza kufanyika bila ya kuwepo ‘Local Engineer’ hadi jengo linafikia hatua ya uwekaji msingi.
Hata hivyo alisema kabla ya kuanza kwa ujenzi huo walielekeza kila kitako cha nguzo kiwe na ukubwa wa Milimita 250 badala yake waliweka ukubwa wa Milimita 200 na kuna baadhi ya nguzo hazikuwekewa vitako na kutitia ardhini. “Msingi ulipokuja kubeba mzigo nguzo zikatitia kwenye matope.” Mshauri mwelekezi alisema katika mahojiano na kamati hiyo.
Ripoti ya kamati hiyo ambayo imeibua mjadala mkubwa Zanzibar, imesema Wizara hiyo pia haikuwa makini katika matumizi ya fedha za umma kwa vile mshauri mwelekezi alitakiwa kulipwa kwa kazi ya uchoraji na ushauri mil. 81,552,200/- lakini hadi kazi inafikia hatua ya awali tayali amelipwa Mil 65,344,470/- kabla ya maendeleo ya mradi kuonekana.
Upande wake Mkandarasi wa Ujenzi huo ambaye ni mmiliki wa Kampuni ya Jansons Construction LTD,LTDrvinder Singu Jandu, amekiri kuwa Kampuni yake imesajiliwa na Msajili wa Makampuni na sio Bodi ya Wakandarasi Tanzania Bara au Zanzibar.
Akihojiwa na Kamati ya Uchunguzi alisema mradi huo umeathiriwa na tatizo la maji ya bahari baada ya vitako vya nguzo vya zege kuathirika na kusababisha jengo kutitia chini ya ardhi.

No comments:

Post a Comment