Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Fedha na Uchumi Zanzibar, imekubwa na kashfa ya
kutoa zabuni ya mradi wa Ujenzi kwa Kampuni isiyokua na sifa na kusababisha
jengo la ghorofa kubomoka kabla ya kukamilika huko kisiwani Pemba.
Kwa mujibu wa ripoti ya kuchunguza ubadhirifu wa mali za Serikali ya Baraza
la Wawakilishi (BLW), imesema wizara hiyo ilifunga mkataba na Kampuni ya Ujenzi
Jonsons Costruction Limited kutoka nchini Kenya Mei 13, 2009.
Ripoti hiyo imesema kwamba wizara hiyo ilitoa zabuni ya ujenzi wa makao makuu
ya wizara hiyo Pemba mradi ambao ulikuwa na thamani ya Sh 1,460,000,000, kinyume
na sheria namba 6 ya usajili wa wakadarasi ya mwaka 2008.
Akihojiwa na kamati hiyo mhandisi kutoka Idara ya Ujenzi ya SMZ, Sabra Ameir
Issa, alisema kwamba serikali iliwataka kufanya uchunguzi baada ya jengo kuanza
kutitia kabla ya kukamilika.
Akifafanua mbele ya kamati hiyo, mhandisi Sabra, alisema tatizo kubwa
waligundua mjenzi wa mradi huo, hakuwa na utaalamu unaohitajika katika kazi kama
hiyo.
Mhandisi huyo alisema kwamba kampuni hiyo haina sifa ya kufanyakzi Zanzibar
hata kupewa kwake zabuni na Wizara hiyo ilikuwa ni kwenda kinyume na sheria kwa
sababu haikusajiliwa katika bodi ya wakandarasi Tanzania bara wala Zanzibar.
Alitaja sababu nyingine za jengo hilo kutitia kuwa ni ubunifu mbaya ya jengo,
usimamizi mbovu, ujenzi uliokosa utaalamu, na uwezo mdogo wa mjenzi huyo.
Mhandisi Sabra, alisema katika uchunguzi wao walibaini hakuna Mhandisi hata
mmoja wa ujenzi katika kampuni hiyo aliyesajiliwa na Bodi ya Wakandarasi
Tanzania bara au Zanzibar.
Hata hivyo, mshauri mwelekezi wa mradi huo mhandisi Arch Yared Dondo, kutoka
kampuni ya K&M Archplans Tanzania LTD, alieleza Kamati ya uchunguzi kwamba
katika mchakato kumtafuta mkandarasi wa ujenzi huo Kampuni yake hakushirikishwa
na Wizara huyo.
Alisema kwamba kwa upande wake hakuona kama ni tatizo kwa kuwa katika mkataba
wao haikuonyeshwa kuwa anatakiwa kushiriki katika mchakato wa kumpata Mkandarasi
wa ujenzi wa jengo hilo.
Aidha Dondo, alisema kwamba mmiliki wa kampuni hiyo bahati mbaya sio mtaalamu
wa ujenzi (Civil Enginer) bali ni fundi Bomba na kampuni yake haikuajili
Muhandisi wa ujenzi hata mmoja kabla ya kuanza kwa utekelezaji wa mradi huo.
Mshauri mwelekezi pia alisema ujenzi wa jengo hilo ulianza kufanyika bila ya
kuwepo ‘Local Engineer’ hadi jengo linafikia hatua ya uwekaji msingi.
Hata hivyo alisema kabla ya kuanza kwa ujenzi huo walielekeza kila kitako cha
nguzo kiwe na ukubwa wa Milimita 250 badala yake waliweka ukubwa wa Milimita 200
na kuna baadhi ya nguzo hazikuwekewa vitako na kutitia ardhini. “Msingi
ulipokuja kubeba mzigo nguzo zikatitia kwenye matope.” Mshauri mwelekezi alisema
katika mahojiano na kamati hiyo.
Ripoti ya kamati hiyo ambayo imeibua mjadala mkubwa Zanzibar, imesema Wizara
hiyo pia haikuwa makini katika matumizi ya fedha za umma kwa vile mshauri
mwelekezi alitakiwa kulipwa kwa kazi ya uchoraji na ushauri mil. 81,552,200/-
lakini hadi kazi inafikia hatua ya awali tayali amelipwa Mil 65,344,470/- kabla
ya maendeleo ya mradi kuonekana.
Upande wake Mkandarasi wa Ujenzi huo ambaye ni mmiliki wa Kampuni ya Jansons
Construction LTD,LTDrvinder Singu Jandu, amekiri kuwa Kampuni yake imesajiliwa na
Msajili wa Makampuni na sio Bodi ya Wakandarasi Tanzania Bara au Zanzibar.
Akihojiwa na Kamati ya Uchunguzi alisema mradi huo umeathiriwa na tatizo la
maji ya bahari baada ya vitako vya nguzo vya zege kuathirika na kusababisha
jengo kutitia chini ya ardhi.
No comments:
Post a Comment