Thursday 31 January 2013

SMZ yashtuka idadi ya watu kuongezeka kwa kasi

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar imewasisitiza Wazanzibari kutumia uzazi wa mpango ili kupunguza idadi ya watu ambayo imekuwa ikiongezeka siku hadi siku katika visiwa vya Zanzibar.
Kauli hiyo ilitolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi wakati akiufunga Mkutano wa 10 wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar katika Ukumbi wa Baraza hilo uliopo Mbweni nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.
Kwa mujibu wa Sensa ya 2002, Zanzibar ilikuwa na watu wapatao 980,000 na katika Sensa iliyofanywa mwaka jana 2012, ambapo ni miaka kumi baadaye, Zanzibar imekuwa na idadi ya watu 1,303,560 jambo ambalo Baloazi Seif alisema Serikali inapaswa kutoa elimu ya uzazi wa mpango kwa wananchi wake.
“Mheshimiwa Spika ongezeko ni watu 323,560. Hili ni ongezeko kubwa sana. Hatuna budi sasa tufanye maarifa ya kupunguza kasi ya kuzaliana ili watoto wetu tuwalee vizuri zaidi,” alisema Balozi Seif mbele ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi.
Balozi Seif alisema idadi hiyo ya watu iliyoongezeka Zanzibar, Serikali haina budi kuwa na mipango madhubuti ya kudhibiti ongezeko la kasi la idadi hiyo ya watu na hivyo kushauri kuongeza bidii katika kufanya kazi na kuzalisha kwa wingi bidhaa zitakazokidhi mahitaji ya watu wake ndani na kupata ziada ya kuuza nje ya nchi.
Alisema wakati wa maadhimisho ya miaka 49 ya Mapinduzi ya Zanzibar jumla ya miradi 53 ya maendeleo iliwekewa mawe ya msingi na kuzinduliwa yenye thamani ya wastani wa Sh97 bilioni katika sekta ya elimu, maji safi na salama, afya, kilimo, uvuvi na miundombinu ya habari, mawasiliano na barabara.
“Hii ni hatua kubwa ya maendeleo ambayo nchi yetu imepiga katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita. Nachukua nafasi hii kuwashukuru kwa dhati viongozi katika ngazi zote na wananchi wote kwa kushirikiana katika kufanikisha sherehe zetu hizi adimu ambazo zilifana sana,” alisema.
Akizungumzia suala la sheria zinazotungwa na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa nia ya kuwatumikia wananchi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwasihi watekelezaji wa sheria hizo wazisimamie na kuhakikisha kuwa zinatekelezwa ipasavyo bila ya kumuonea haya au aibu mtu yeyote atakayezikiuka sheria hizo

Tanesco yaidai Zanzibar mabilioni

Shirika la Umeme Zanzibar, (Zeco) linadaiwa Sh. bilioni 22.6 na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).
Hayo yalielezwa jana na Mwenyekiti wa Kamati ya kuchunguza Hesabu za serikali na Mashirika ya Umma (PAC) Ali Omar Shehe, alipokuwa akiwasirisha ripoti maalum ya kuchunguza utendaji wa Zeco.

Alisema kabla ya kufanyika mazungumzo baina ya Wizara ya Ardhi Makazi, Maji na Nishati Zanzibar na Wizara ya Nishati na Madini ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, jumla ya deni lilikuwa la Sh. Bilioni 62.3 hadi mwaka 2010.

Mwenyekiti huyo alisema baada ya mazungumzo ya Viongozi wa pande mbili za Muungano waliafikiana kuwa Serikali ya Muungano itasadia kulipa Sh. bilioni 39.7 kupunguza mzigo wa deni hilo.

Shehe ambaye Mwakilishi wa Jimbo la Chake Chake, alisema baada ya deni kupunguzwa, Zeco inatakiwa kulipa Sh. bilioni 3 kwa mwezi kupunguza deni la matumizi ya umeme.

Shehe alisema kwamba viwango vya umeme vimeathiri Zeco kwa kiwango kikubwa na kushindwa kumudu kulipa gharama deni kwa muda mwafaka.
Chanzo: Nipashe

Wednesday 30 January 2013

Ufisadi Watikisa Zanzibar


KWA mara nyingine watu wa Zanzibar wameshitushwa na habari za ubadhirifu mkubwa wa fedha uliogunduliwa na Kamati ya Baraza la Wawakilishi katika uchunguzi wake wa Shirika la Umeme la Zanzibar (ZECO).
Kwangu mimi hili ni jambo la kawaida, ila ninashangaa kuwa kimepita kipindi kirefu kidogo tokea mara ya mwisho kusikika habari za aina hii, za baadhi ya watu kuchezea wanavyotaka fedha na mali za serikali na taasisi zake.
Nasema hivi kwa sababu bado haijaonekana kwa vitendo watu wanaofanya ufisadi na kuitia serikali hasara ya mabilioni ya shilingi kuwajibishwa kisheria.
Panapotokea vishindo vya kuwabana wanaodaiwa kuhusika na ufisadi basi wanaokabwa ni dagaa na wale mapapa kubaki wakielea habarini.
Watu hawana wasiwasi kama vile fedha walizochezea ni zao au za familia zao. Huku ndiko kutesa kwa zamu.
Machi mwaka jana, Kamati ya Kuchunguza Mahesabu ya Serikali na Mashirika ya Umma (PAC) ya Zanzibar ilionya kuwa ingeliwapelekea mahakamani baadhi ya watendaji wakuu wa serikali na wahasibu ifikapo Mei wale waliokiuka sheria za matumizi ya fedha za serikali.
Sasa ni karibu mwaka mmoja na hakuna aliyefikishwa mahakamani kwa wizi au ubadhirifu wa fedha za umma uliogunduliwa wakati ule.
Hii ilitokana na PAC kuona kwamba ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Fedha za Serikali iligundua kuwa miradi mingi iliyokamilika ilikuwa hailingani na fedha zilizotumika.
Ripoti ile ilieleza kuwa yapo magari ya serikali yaliodaiwa kuwa mabovu, lakini ukweli ni kwamba huo ulikuwa mradi wa kuiba vipuri.
Katika mambo yaliyogunduliwa wakati ule ni kwamba katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2008-09 fedha za masurufu zilizopotea zilikuwa sh mibilioni 5.1.
Mambo mengine yalikuwa na sura ya ufisadi uliokithiri na unaonuka yaliyoelezwa katika ripoti ile ni pamoja na :
Malipo ya dola 94,000 za Marekani yalifanywa bila ya kuwepo stakabadhi.
Fedha zilizopotea katika mikataba ni sh milioni 413.6, vifaa vingi vilinunuliwa na baadhi ya ofisi za serikali bila kutumia zabuni.
Tulielezwa na baadhi ya watu kuamini (si mimi) kwamba PAC haitakuwa tena na muhali au kumuonea huruma mtu yeyote aliyeiba au kutumia vibaya fedha za serikali.
Hivi sasa tunapewa hadithi mpya ya ubadhirifu unaosemekana kufanyika ZECO, lakini ukweli ni kwamba kilichofanyika ni kuendeleza utamaduni wa kuiba na kuvuruga fedha za umma. Wapo wanaosema fedha za umma hazina mwenyewe na ukizipata ni sawa na zile za kuokota! Hivyo ni haki kuzichota.
Tunaambiwa kuwa miongoni mwa madudu yaliyogunduliwa katika Shirika la Umeme ni haya yafuatayo:
Kuwapo tofauti ya malipo kati ya kazi zinazofanana na baadhi ya malipo yaliyopo kwenye risiti yanatofautiana na malipo halisi.
Wapo wateja wanaotumia umeme bure na hawamo kwenye orodha ya shirika. Ipo tofauti kubwa ya ada za malipo zinazotozwa kwa wanaounganishiwa umeme na majina ya watu wanaodaiwa kufaidika kutajwa.
Yupo mteja (ametajwa jina) anayedaiwa kuungiwa umeme wa njia tatu na kuonesha kuwa amelipa sh milioni nane wakati mtu huyo anadai amelipa sh milioni 37, lakini kwenye akaunti ya mtu binafsi.
Benki moja inasemekana kuwa ilitozwa sh 3,718,000 kuungiwa umeme, lakini vifaa hasa vilivyotumika kwa kazi hiyo vina thamani ya sh milioni 14.
Baadhi ya wateja, zikiwamo hoteli za kitalii, hawamo kwenye orodha ya malipo ya shirika, nguzo feki zimetumika kuunga umeme, mafaili ya wateja wakubwa 147 yamekosekana.
Ipo kampuni iliyokodishwa mnara na haijawahi kulipa tangu ilipokodishwa. Hakuna maelezo yanayoeleweka juu ya ununuzi wa jenereta 32 ya akiba ya shirika yaliyopo hapo Mtoni. Hapakuwepo na zabuni za ununuzi wa majenereta haya.
Kwa kweli yapo madudu mengi katika ripoti hii na tuhuma zilizoambatanishwa na madai haya ya ufisadi ni nzito na zinaunguza kuliko huo umeme wenyewe.
Ni mahakama tu, kama ipo huru na inaachiwa kufanya kazi yake inayotarajiwa kufanya, ndiyo inayoweza kutoa uamuzi wa haki na ukweli kujulikana. Inawezekana pia tuhuma hizo ni majungu, lakini mahakama ndiyo itakayosema kama ni jungu au sufuria.
Lakini kwa Zanzibar ninayoijua, labda ibadilike kama ilivyo kwa usiku na mchana, hili suala litamalizikia hewani kama lile la kugunduliwa zaidi ya wafanyakazi hewa 3,500 katika serikali miaka mitatu iliyopita.
Kikwazo kikubwa kilichopo ni utamaduni wa kulindanana na kuwaonea muhali watu wanaosemekana wamewiba fedha za umma na kuharibu mali za serikali.
Mafisadi huonewa huruma kama vile wameiba kwa bahati mbaya na rungu la dola siku zote huwaaangukia wanaoiba embe, ndizi, chapati na mandazi au kutoa kauli za kisiasa, kama juu ya Muungano, zisiowafurahisha wakubwa.
Tuliwahi kuambiwa katika miezi ya mwisho ya utawala wa Rais Amani Abeid Karume kuwa Zanzibar haina mafisadi na kwamba viongozi wake ni wasafi na sasa tunaendelea kuuona usafi huo wa viongozi!
Ukweli ni kuwa ufisadi unanuka Visiwani na kama maelezo yaliyotolewa na Kamati ya Baraza la Wawakilishi yana ukweli basi ufisadi uliopo unatisha.
Tusijidanganye na kutaka kuwafanya malaika viongozi wetu na watumishi wa ngazi za juu wa serikali. Wapo miongoni mwao ambao ni wezi wakubwa na wabadhirifu na haifai kuwafumbia macho wala kuwazibia masikio.
Tuache kulindana kwa mambo maovu kwani watu wazuri ni wale wanaolindana kwa mema na si uchafu. Mwenendo huu wa kuwalinda mafisadi utaiponza Zanzibar.
Ukiangalia matokeo kama ya wakubwa kudaiwa kupora mali, ardhi na mashamba ya watu na hata kuua, japokuwa si kwa makusudi, utaona wanakingiwa kifua na kulindwa.
Kwa bahati mbaya waandishi wa habari wanaofichua haya kwa kuwapa nafasi ya kusikika wale wanaodai kudhulumiwa huandamwa kama wao ni wahalifu na hata kuhatarishiwa maisha yao.
Sasa waandishi wa habari wamekaa pembeni na kupumua huku wakiiangalia kwa masikitiko Zanzibar inakwenda mrama na badala yake wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wapo mbele kufichua ufisadi.
Sijui kwa uoza huu ulioanikwa katika Baraza la Wawakilishi serikali itasemaje au itachukua hatua gani kwa wanaotuhumiwa au vyama vyao vitaambiwa wawashughulikie wawakilishi wao walioweka mambo hadharani.
Tunasubiri kitakachotokea na wakati ndio utatupa jawabu. Maskini Zanzibar. Au sasa ndiyo tuseme Zanzibar ni njema, atakaye aibe?
Chanzo: Tanzania Daima

Tuesday 29 January 2013

Misri yarejesha mabilioni ya dola ya mafisadi yaliyofichwa nje ya nchi

CAIRO WAKATI Serikali ya Tanzania ikiendelea kupiga kimya katika kuwashughulikia mafisadi papa ambao wamebainika kuficha mabilioni ya dola za kimarekani katika mabenki ya Uswisi, Serikali ya Misri tayari imeshaanza kutaifisha na kurejesha mabilioni ya dola yaliyokuwa yamefichwa na viongozi wa enzi za utawala wa Hosni Mubarak. Mwendesha Mashtaka Mkuu wa serikali ya Misri amesema kuwa, nchi yake imefanikiwa kurejesha dola bilioni moja na milioni mia nane za serikali ya nchi hiyo zilizokuwa zimeporwa na viongozi wa utawala uliong’olewa madarakani nchini humo.

Adel al Saeed, alibainisha kuwa vyombo vya sheria vya Misri bado vinaendelea na uchunguzi wake dhidi ya mafisadi na wale wote waliopora mali za Baitul Maal, wakati wa utawala wa Hosni Mubarak. Aliongeza kuwa uchunguzi uliofanywa kuanza Februari 2011 hadi 31 Oktoba mwaka huu, umeweza kubaini na kukusanya dola bilioni moja na milioni mia nane zilizoporwa na Hosni Mubarak, familia yake, na idadi kadhaa ya mawaziri na wafanyabiashara wakubwa nchini humo.
Amesema kuwa serikali ya Cairo inaendelea kuwasiliana na nchi nyingine kwa njia za kidiplomasia lengo likiwa ni kuzuia na hatimaye kurejeshwa mamilioni ya dola ambayo yalitoroshwa na viongozi wa zamani wa nchi hiyo. Utawala wa kiimla, ufisadi uliokithiri na ukandamizaji dhidi ya wananchi wa Misri ni miongoni mwa mambo yaliyosababisha wananchi wa Misri kuanzisha harakati za kuiondoa mamlaka ya Hosni Mubarak
Chanzo: Annur

Monday 28 January 2013

Athari ya Vyombo vya dola Kujiingiza kwenye Siasa

Katuni na -- malikiblog
Na mwandishi wetu
muonekano wa jeshi la polisi kwa raia umekuwa ukidorora siku hadi siku. Hii ni kutokana na athari za chombo hicho cha dola kutofanya kazi zake kwa uadilifu. Police ni chombo kinachotegemewa kusimamia uslama wa raia wote ambao raia wa tanzania wamegawanyika dini tofauti, makabila tofauti, na vyama tofauti, akiwa mpinzani au chama tawala, akiwa mkristo au muislamu akiwa mmakonde au mchaga wote hao ni watanzania. kutokana na uhalisia wa jamii ilivyo uadilifu kwa makundi yote ni kitu kuhimu sana ila iwapo jeshi letu la police litaegemea upande fulani ndio hayo yanayojitokeza sasa hivi imeonekana raia adui zao nambari moja ni jeshi la polisi, ila haya ni matokeo ya kilichopandwa na jeshi hilo, na inahitajika kazi ya ziada kuweza kurejesha imani ya raia kwa jeshi hilo. Kama ni kuzuia maandamano au mikutano basi ni kwa vyama vyote, dini zote na makabila yote.
Wakatabahu

Thursday 24 January 2013

Wednesday 23 January 2013

Mishahara hewa yaitesa Zanzibar

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar(SMZ) katika kukabiliana na wimbi la wafanyakazi hewa imekusudia kufanya uhakiki kwa baadhi ya taasisi zake za ulinzi ili kujua idadi kamili ya watumishi wake.
Hali hiyo imekuja kufuatia matukio ya ubadhirifu wa fedha na kukabiliana na tatizo la kulipa mishahara kwa watumishi hewa.
Hayo yalisemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Haji Omar Kheri wakati akijibu swali la Mwakilishi wa Jimbo la Muyuni (CCM), Jaku Hashim Ayoub aliyetaka kujua Serikali imekabiliana vipi na tatizo la mishahara hewa kwa kikosi cha KMKM.
Katika swali lake, Jaku alisema kwamba katika kikosi cha KMKM Serikali inalipa watumishi hewa waliostaafu zaidi ya Sh18 milioni kwa mwezi jambo ambalo linaipa Serikali wakati mgumu wa kutoa mishahara isivyo stahiki.
Akijibu swali hilo Waziri Kheri alikiri kuwapo kwa ubadhirifu huo ambao umegunduliwa kutokana na ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti
Mkuu wa Hesabu za Serikali na ambapo kwa sasa tukio hilo linafanyiwa kazi na wahusika. ”Waheshimiwa tumepokea taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhusu upotevu mkubwa wa fedha za umma katika Kikosi cha KMKM ambao hulipwa wastaafu hewa...Hatuna wasiwasi na taarifa ya mkaguzi, lakini ripoti hiyo hivi saa inafanyiwa kazi,” alisema waziri huyo.
Alisema ni marufuku kwa watumishi wa umma kulipwa fedha wakati wanapostaafu utumishi wa umma serikalini na kitendo hicho ni kinyume na sheria za utumishi wa Serikali na kuwataka watu ambao wanawatambua wenye kufanya hayo waripoti.
katika vyombo vya sheria.
Akijibu swali la nyongeza la mwakilishi wa Jimbo la Chake Chake (CUF), Omar Ali Shehe aliyesema kwamba zipo taarifa katika Kikosi cha Mafunzo tatizo kama hilo lipo, Kheri alisema Serikali itafanya ukaguzi wa taasisi zake vikiwamo vikosi maalumu vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
Chanzo: Mwananchi

Umoja wa Ulaya na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar

Leo tunaendelea na mjadala wetu kuhusu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa muktadha wa kutazama muundo wa Umoja wa Ulaya (EU).
Kama tunavyofahamu kuwa Umoja wa Ulaya si Muungano wa Kikatiba, ni wa mkataba ambao haujavunja zile dola za nchi wanachama.
Umoja huo umekubaliana kuwa na baadhi ya mambo katika ushirikiano wao ambapo wameunda vyombo vya Umoja ikiwemo Halmashauri ya Ulaya.
Halmashauri hii ni mkutano wa Wakuu wa nchi na viongozi wa Serikali za nchi wanachama. Wanakutana mara mbili kwa mwaka na kutoa maazimio muhimu.
Nafasi ya Urais wa EU hubadilika kila baada ya miezi 6, ifahamike kuwa Urais uliokusudiwa hapa si ule wa dola kwa maana ya ukuu wa nchi.
EU pia ina Baraza la Mawaziri ambapo ni katika yale mambo tu waliyokubaliana kushirikiana kwa pamoja ndiyo hukutana kupanga mipango ya utekelezaji katika Mataifa yao.
Tofauti kubwa ni kwamba katika Muungano wa Kikatiba kwa mfano wa Tanganyika na Zanzibar kuna Baraza la Mawaziri la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambalo linajumuisha mawaziri wote wa SMT wanaosimamia mambo ya Muungano na yasiyokuwa ya Muungano.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ni mjumbe katika baraza hili. Hapa napo kuna msongo wa kazi kwa mfano ni wakati gani Baraza la Mawaziri inajadili mambo ya Muungano na yasiyokuwa ya Muungano kwa kutumia baraza hilohilo?
Wenzetu wa EU wana Kamati ya Ulaya ambayo majukumu yake ni kusimamia utekelezaji wa maazimio ya Halmashauri na Bunge ambayo ina makamishna 24 na mwenyekiti. Ingawaje inaonekana kama ni Serikali, lakini haimo hasa katika mfumo wa Serikali kwa maana haina madaraka.
Chombo kingine cha Umoja wa Ulaya ni Bunge la Ulaya ambalo lina wabunge 732 wanaochaguliwa na wananchi. Ikiwa muundo wa Muungano wetu utakuwa katika mfumo wa aina hii malalamiko mengi ya upande mmoja kuona unaonewa hayatakuwepo.
Hii haina maana kwamba ndiyo matatizo hayatakuwepo, lakini kwa sehemu kubwa utakuwa si kama muundo wa sasa wa Serikali mbili ambao tume zote zilizoundwa na Serikali zimeukosoa kwa kushauri kutafutwa kwa muundo muafaka wenye kufaa.
Tazama tatizo la msingi la mfumo wa muundo katika utekelezaji wa mambo ya Serikali, kwa mfano, Katiba ya Tanganyika imelindwa kwenye mkataba wa Muungano na pia ilipaswa kuwepo na Serikali yake, pamoja na viongozi wake kuwepo na kusimamia mambo yasiyo ya Muungano.
Tunaona pia Katiba na sheria za Tanganyika ndizo zilizotakiwa zitumike katika eneo la Tanganyika kwa mambo yasiyokuwa ya Muungano kwa upande wa Tanganyika kama ambavyo Katiba na sheria za Zanzibar zinavyotumika katika eneo la Zanzibar kwa yale mambo ambayo si ya Muungano.
Watanganyika wanaodai Tanganyika yao wana hoja katika hili maana licha ya kufutwa kwa Serikali hiyo, lakini kuendelea kutambua kuwepo kwa sheria zisizo za muungano ni kutambua kuwepo kwa mamlaka ya Tanganyika ambako sheria hizo kwa mambo yote yasiyo ya Muungano ziliendelea na zinaendelea kutumika hadi leo kwa Tanzania Bara.
Kwa mfano kifungu cha 3 (1) cha Provisional Transitional Decree kinatajwa kuwa ni miongoni mwa kero pale kilipohalalisha wafanyakazi wa iliyokuwa Serikali ya Tanganyika kugeuzwa kuwa watumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Utaona hali hiyo katika kifungu cha 6 (i) cha Decree kinasema mara tu baada kuanza Muungano, Mahakama ya Tanganyika na Majaji wake wote nao watakuwa ndiyo Mahakama na Majaji wa Jamhuri ya Muungano kinyume na Makubaliano ya Muungano. Mpaka leo Katiba zote mbili hazitambui Mahakama kama ni suala la Muungano. Nembo ya Tanganyika inatumika kama nembo ya Serikali ya Muungano na Idara ya Mwanasheria Mkuu wa Tanganyika inachukuliwa kama Idara ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Muungano.
Kwa mifano hiyo michache utaweza kubaini udhaifu wa msingi wa mfumo wa muundo wa Muungano ambao bila shaka kama utafanyia marekebisho kwa kutafuta mfumo mujarab utaondoa zile zinazoitwa kero za Muungano.
Hoja ya waumini wa muundo wa Muungano wa mkataba inaonekana kuwa na nguvu zaidi hasa wakiitazama Umoja wa Ulaya ambao umepata mafanikio na kufanya Mataifa mengine ya Ulaya ambayo hapo awali hayakuwa wanachama kuweza kujiunga.
Leo Umoja huo una nguvu kubwa kiuchumi, tumeona wakati wa msukosuko wa kifedha kama Taifa la Ugiriki lilivyokuwa katika hali mbaya na linavyosaidiwa na wanachama wenzake wa EU hasa Ujerumani.
Ingawa ziko Tume zilipendekeza muundo wa Serikali tatu, lakini yafaa kukumbuka kuwa tatizo si idadi ya Serikali, tatizo ni muundo au maumbile yake Muungano huu ambao kiasi kidogo unafanana na ule wa Marekani na Uingereza.
Imeelezwa mara nyingi juu ya ripoti ya Tume ya Jaji Nyalali iliyosema muundo muafaka wa Muungano ni Serikali tatu.
Jaji Mstaafu Francis Nyalali, alieleza wazi katika ripoti yake kuwa muundo wa Serikali mbili una matatizo mengi, muundo muafaka ni wa serikali tatu.
Wakubwa ndani ya CCM walipokutana Mjini Dodoma wakasema haiwezekani kutekeleza maoni ya Tume, lakini kwa ushauri uleule, Tume ya Jaji Robert Kisanga nayo ikaeleza udhaifu wa muundo wa Muungano, lakini kama ilivyo kwa mtangulizi wake, Tume ya Kisanga ikaambiwa hapana sera ya Chama Cha Mapinduzi hazibadiliki.
Ni muhimu kuelewa kuwa msingi wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar haukujengeka kwa sababu ya hisani ya kisiasa, kiuchumi kiutamaduni au jiografia pengine utashi wa utawala, lahasha. Huu ni mkataba wa Kimataifa kama ilivyo mikataba mengine ambayo Washiriki wote wana haki sawa.
Mapenzi ya haki hufanya maisha kuwa matamu hasa ikiwa haki yenyewe mtu huweza kuifahamu na kusadiki. Ni vigumu sana kuijua haki pasipo kuitenda na watu wengine hawawezi kufaulu kwa sababu ya kupuuza haki na ukweli.
Haki na kweli ni sawa na watoto pacha, mtu na awe na wingi wa akili wa kushinda mchwa, lakini iwapo ana mazoea ya kupuuza mambo mawili haya, basi anafanya ujinga ulio mkubwa wa fikra na fahamu.
Kuelekea kwenye mchakato wa kutoa maoni katika Tume ya Katiba ni lazima kila mtu kuheshimu haki na uhuru wa mwingine si vyema kubeza maoni ya wengine, kama unatofautiana kimtazamo salia na wako waache wengine waeleza mitazamo yao.
Chanzo: Rai

Monday 21 January 2013

KUVUNJIKA KWA MUUNGANO SI JAMBO GENI

Na Salma Said
TUME ya mabadiliko Katiba mpya nchini Tanzania, imeelezwa kuwa Baraza la Mapinduzi halikushauriwa wala kushirikishwa katika Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, uliyoundwa Aprili 26, 1964.
Wanasiasa wakongwe waliyokuwa katika Serikali ya Mapinduzi, wakati wa kuundwa kwa Muungano huo, Bw Salum Rashid na Bw Hassan Nassor Moyo waliiyambia Tume hiyo, walipokuwa wakitoa maoni yao Maisara, mjini Zanzibar.
Katika maoni yao walisema: Tangu awali ya kuundwa Muungano huo, kulikosekana uhaliali wake, licha ya kuwa umedumu kwa miaka hamsini huku kukiwa na malalamiko kadhaa ya wananchi.
Wakizungumza kwa pamoja, Wanasiasa hao waliunga mkono kuwepo kwa Muungano, lakini walishauri mfumo mpya wa Muungano wa Mkataba, ili kila nchi kuwa na mamlaka yake kamili:
“Kwa hali ilivyo miaka 50 ya Muungano kushindwa kutatua mambo mbali mbali, mfumo pekee unaofaa kwa sasa na kwa kizazi hiki ni Muungano wa Mkataba. Utaratibu wake utajulikana baadae,” walisema Wanasiasa hao.
Bw Moyo alisema Serikali ya Muungano, isiogope maoni ya wananchi kwani kwa takriban miaka 50 matatizo ya Muungano yameshindwa kutatuliwa na njia pekee kwa sasa ni kukubali kubadilisha mfumo wa Muungano huo:
“Tukiwa na mfumo mpya wa Muungano, utakwenda sambamba na wakati huu ambao idadi kubwa ya wananchi wameamka na kuona kuna matatizo katika Muungano wetu,” alisema Bw Moyo.
Bw Moyo ni Waziri wa kwanza wa Sheria wa Serikali ya Muungano, na Bw Salum Rashid alikuwa Katibu Mkuu wa kwanza wa Baraza la Mapinduzi.
Kwa pamoja walishauri kuwepo kwa Muungano lakini walisisitiza, ili kuimarisha Muungano kwa nchi zote mbili, ni kusikilizwa kwa maoni ya wananchi ambao wanataka aina mpya ya Muungano wa Mkataba:
“Sisi ndiyo tulikuwa na dhamana wakati ule na tulitakiwa tuunganishe Serikali kwa kuimarisha udugu na kuimarisha uchumi wetu, bahati mbaya sasa kuna kero, mimi siziiti kero naita ni matatizo, ni wakati wake kuondoshwa” alisema na kubainisha:
“Msimamo wangu ni Serikali ya Mkataba na ndiyo ninavyoamini na naamini kwamba huu muungano tuliyonao ni Muungano wa Mkataba, hili siyo jambo jipya, Mwalimu Nyerere na Mzee Karume walitia saini ya Mkataba,” hili sio jambo jipya,” alisisitiza Mzee Moyo.
Bw Moyo alitaka kurudishwa kwa utaratibu wa zamani, ili Rais wa Zanzibar aendelee kuwa Makamo wa Kwanza wa Rais wa Tanzania, akimaanisha Muungano huo ni wa Tanganyika na Zanzibar.
Naye, Katibu Mkuu wa Kwanza wa Baraza la Mapinduzi, Bw Salum Rashid ambaye alikuwa Dar es Saalm na Mzee Karume siku ya kusainiwa Mkataba wa Muungano, alisisitiza kuwepo kwa Muungano wenye maslahi kwa wananchi wa nchi zote mbili:
“Serikali ya Muungano isiwe na woga wa kuvunjika kwa Muungano. Hilo sio jambo kubwa na wala siyo jambo geni, baadhi ya nchi za Afrika ziliwahi kuungana, na Muungano ukavunjika,” alisema na kufafanua zaidi:
“Sioni jambo zito kuvunjika kwa Muungano, mbona Muungano wa Senegal na Gambia ulivunjika na wote walikuwa ni wanachama wa Umoja wa Afrika na hakuna jambo lolote lililotokea,” alisema Bw Salum Rashid.
Alisema wananchi wanaotaka Muungano wa Mkataba, hawamaanishi kuvunja Muungano, bali wanataka mfumo mpya wa Muungano ili kuirudishia Zanzibar, mamlaka na madaraka yake kamili.
Alisema ifahamike kwamba, kuwa nje ya Serikali siyo sababu ya kuwa ni fursa ya kuzungumza hayo, lakini wakati ule likizungumzwa suala la Muungano, ilikuwa inaonekana ni uhaini:
Alisema kwa sasa haiwezekani tena kuburuzwa na hasa vijana. Hivyo matumaini yake kwa tume hiyo ni makubwa: “Naamini watafanya kazi zao kwa uadilifu mkubwa na maoni ya wananchi ambayo wameyatoa kwa Tume, yatatekelezwa,” alisema Bw Salum Rashid.
Alisema Muungano wa Mkataba ndiyo sahihi kwa sasa na hakuna sababa ya viongozi kuogopa hilo, Wazanzibari na hasa vijana wanataka nchi yao kuwa na mamlaka kamili.
Bw Moyo na Bw Rashid wote wawili kwa pamoja wamewatoa hofu Wazanzibari kuhusu utendaji wa Tume hiyo, na walisema wanaiamini kwamba itafanyakazi yake kwa uadilifu, bila upotoshaji.
Tume hiyo inayongozwa na Mwenyekiti wake Jaji Joseph Warioba na Katibu wa Tume, Assa Rashid tayari imeshachukuwa maoni ya baadhi ya viongozi wakuu, pamoja na Marais wastaafu wa Seriakli ya Zanzibar.
Viongozi waliyokwisha toa maoni yao ni pamoja na Makamo wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, Rais Mstaafu Dk Salmin Amour, Dk Amani Abeid Karume na baadhi viongozi wengine wa Serikali ya Zanzibar.

Sunday 20 January 2013

KIKWETE NA SHEIN IGOMBOENI Z ‘ BAR KATIKA MUUNGANO

WANANCHI wa kijiji cha Chwaka, Kusini Unguja wamewaomba Rais Jakaya Kikwete na Dk Ali Mohamed Shein, kushughulikia suala la Katiba ili kuweza kuirejeshea Zanzibar mamlaka yake kamili kama ilivyokuwa kabla ya kuungana na Tanganyika.
 Ombi hilo lilitolewa juzi kwenye mkutano wa wazi wa Baraza la Katiba Zanzibar (BAKAZA) wakati likitoa elimu ya Katiba kwa wananchi wa kijiji hicho. Huo ni mfululizo wa Baraza hilo katika kutoa elimu ya Katiba kwa wananchi wa Zanzibar.
 Akizungumza katika mkutano huo mmoja wa Wazee wa Chwaka, Fadhil Mussa Haji alisema suala la kuunganisha nchi lilifanywa na watu wawili, Mwalimu Nyerere na Mzee Karume na wote hawapo tena. Alisema ni jukumu la viongozi waliopo madarakani kulishughulikia suala hilo.
 “Mwalimu Nyerere na Mzee Karume waliunganisha nchi kwa kuamua wao wenyewe na kisha Mzee Karume akaja uwanjani kutuuliza mnakubali union watu wakaitikia…kwa kuwa alijua hakuna atakayeweza kupinga kwa wakati ule,” alisema na kuongeza:
 ”Lakini sisi hatujakubaliana na hayo tokea wakati huo…sasa kilichobaki tunamuomba Rais Kikwete na Rais Shein wao ndio wapo madakarakani waturejeshee mamlaka na hadhi ya Zanzibar,” alisema Mzee Fadhil, huku akishangiriwa na vijana waliohudhuria mkutano huo.
 Mzee Fadhil alisema yapo baadhi ya mambo ambayo yameingizwa katika orodha ya mambo muungano bila ya ridhaa ya Wazanzibari, lakini baadhi ya mambo Wazanzibari wenyewe walishiriki kuizamisha nchi yao kutokana na tamaa na kupenda madaraka, jambo ambalo alisema hivi sasa linawafanya wajute:
 “Ni sisi wenyewe tumefanya na tumetaka tutendewe hivi kwa sababu sisi tulikuwa tumeshapata uhuru wetu hapa mwaka 1963 lakini ni Wazanzibari wenyewe wakaleta mapinduzi na kuukataa ule uhuru halali,” alisema na kufafanua:
 ”Sasa tunasema hizi tamaa na kupenda madaraka sasa hivi ndivyo vitu vinavyotuadhibu sote katika nchi yetu kwa tamaa za hao wachache waliyokuwa wakituamulia,” alisema Mzee Fadhil.
 Alitoa mfano kwa viongozi wa Wazanzibari walivyojikaanga kwa mafuta yao wenyewe: “Ni tamaa ndizo zilizosababisha nchi kutokuwa na hadhi na mamlaka kamili ya kujiamulia mambo yake,” alisema Mzee Fadhil.
 Alisema ni tamaa ndiyo zilizofanya kuporwa mamlaka kamili ya Zanzibar na hivyo kubakisha nchi kukosa uwakilishi hata kwa yale mambo ya Zanzibar, ambayo sio ya muungano yanavyokosa uwakilishi wa Wazanzibari katika nchi za nje:
 ”Wakati umefika sasa kwa kila mmoja kufahamu kwamba mamlaka ya Zanzibar yanahitaji kuheshimiwa na kupiganiwa na kila raia ili hadhi ya Zanzibar irudi,” alisema Mzee Fadhil.
 Akitoa maoni yake alipendekeza Katiba mpya iweke bayana mamlaka ya Zanzibar na rais wake, kwani alisema hivi sasa rais wa Zanzibar, hana hadhi ya kweli kama itakiwavyo kwa rais wa nchi.
Chanzo: Mzalendo

NANUSA HARUFU YA ‘GEORGE ORWELL’ MCHAKATO WA KATIBA

Riwaya ya Shamba la wanyama (1945), ni moja kati ya kazi nzuri kabisa za kibunifu katika Tasnia ya fasihi andishi hapa duniani. Riwaya hii ambayo iliandikwa na Muingereza ambaye ni maarufu kwa jina la George Orwell, ni mtiririko wa sitiari (allegory) unaoakisi dhana nzima ya ujamaa wa kidemoskrasia katika tawala mbali mbali za kidunia.
Kazi hii yenye ubora, ladha na mvuto usiochosha, inahusu kisa cha dola la wanyama. Wanyama ambao kwa pamoja walikubaliana kuungana na kuishi kwa misingi ya usawa na haki. Moja kati ya kanuni hizo za usawa, ilikubaliwa kwamba hakuna mnyama mmoja atakemdhuru mnyama mwengine ama kwa kumla, kumpiga, kumdhulumu na hata kumuuwa. Kanuni hii ilipita na ikaandikiwa kauli mbiu (slogan) isemayo ‘Wanyama wote ni sawa’!
Kwa muda baada ya kanuni hii kupitishwa na kukubaliwa na wanyama wote, wanyama wadogo wadogo na wale waliokuwa waathirika wa vitimbi, viteweji na mateso ya wanyama wakubwa, walihisi kupata faraja kubwa kwa kuhakikishiwa usalama wao. Imani yao hii ilichangiwa na kuona kauli ile mbiu ikiimbwa na kuandikwa kila kona ya dola lao lile kiasi ya kumfanya kila mnyama aamini kile anachokiona katika kauli mbiu ile.
Waswahili husema ‘Taa haachi mwiba wake’. Haikutimia wiki, kuna baadhi ya wanyama hasa ndege, walianza kuona dalili mbaya katika jamii yao. Moja ya dalili hio ni kupotea kwa baadhi ya wanyama katika mazingira ya kutatanisha. Kwa lugha nyepesi, kuna baadhi ya wanyama walianza kuwala wengine kimya kimya kila siku.
Wanyama wadogo walipogundua usaliti huu walirudi kwa mkubwa wao kushitaki na kusimulia masikitiko yao juu ya kitendo hiki cha uvunjifu wa amani, na usalama wa wanyama katika dola yao. Kwa bahati mbaya walipofika mahala pa mashtaka na kueleza makosa yao, waliona ile kauli mbiu imebadilishwa kidogo kutoka ilivyokuwa mwanzo.
Awali kauli ilisomeka ‘Wanyama wote ni sawa’, lakini sasa inasomeka ‘Wanyama wote ni sawa, lakini baaadhi ya wanyama, ni sawa zaidi kuliko wengine’! Kisa hichi kikaishia hapo. Kumalizika kwa kisa hiki ndipo tunapopata nadharia hiyo niliyoitumia katika kichwa cha makala hii hapo juu, ambayo ni moja ya nadharia maarufu duniani kwa sasa. Yaani nadharia ya ‘Ki-Orwelli’.
Nimewajibikiwa na kuandika kwa kusema kuwa kwa namna mchakato mzima wa maoni ya katiba unavyokwenda, nanusa harufu ile ile waliyoinusa wanyama wadogo kama mimi katika ‘Shamba la wanyama’. Harufu ya kwamba kuna baadhi ya wanyama ni sawa kuliko wengine. Na hii si tuhuma kutoka katika ombwe la uwazi, bali ina kila aina ya ithibati na visherehesho vya kuutilia shaka mapema mchakato huu wa katiba nchini.
Nilitegemea iwapo maoni ya katiba yalilenga kukusanya maoni ya wananchi, kwa haki na usawa, na ili yanipe imani kuwa haki itatendeka, basi yalikuwa yafanywe kwa wanachi wote bila kuweka tabaka (strata/ social classes). Hii ni kutokana na ukweli kwamba katika mchakato wa katiba, wananchi wote, wake kwa waume, wakubwa kwa wadogo, viongozi na waongozwa, mashehe na mapadiri, wanasiasa na majeshi, wote kwa pamoja ni wananchi walio sawa. Na mchakato wa katiba ulikuwa uanze na kauli mbiu hiyo ya ‘ Wananchi wote ni sawa mbele ya haki na sheria’!
Kuwe na usawa kwamba, maoni ya katiba yafanyike kama vile tunavyofanya uchaguzi. Yapitie kimajimbo au maeneo ya ukazi wa wananchi. Sasa maoni yakifika jimbo ambalo kiongozi mkuu wa nchi au mstaafu anapoishi, basi hio ndio iwe zamu yake ya kwenda kutoa maoni hapo kwao. Kwa mfano, ikiwa Rais wa Zanzibar anaishi Mbweni, basi maoni yakifika jimbo la eneo hilo, iwe ndio zamu yake ya kutoa maoni na wananchi sawia, ijapokuwa atapewa nafasi ya kwanza kufanya hivyo, lakini utaratibu uwe hivyo.
Na nilitegemea iwe hivi kwa watu wote nchi nzima. Wa Bagamoyo akatowe maoni kwao, alie Dar es Salaam atatoa maoni hapo jimboni kwake, alie kambini kwa jeshi bila shaka kambi hio haiko angani, aende jimbo ilipo kambi hio akatoe maoni. Na kwa mpangilio kama huu angalau tungeweza kuamini kwamba mchakato wa katiba una sura ya usawa na hivyo haki haichezi mbali.
Lakini ni jambo la kushangaza sana kuona tume ya Katiba inapitia majumbani mwa viongozi na wastaafu, wizara, idara, na mashirika ya Serikali, na halafu pengine hata taasisi za kidini, ili kukusanya maoni. Utaratibu huu unaleta matabaka kwa wananchi. Na asili na maumbile ya mfumo wa kitabaka duniani dumu daima hautendi haki. Huu ndio uhalisia wa nadharia na mifumo yote ya kitabaka duniani.
Kwa mujibu wa mwenendo wa mchakato huu wa katiba unavyoendeshwa, wa kuanza kijumba hodi, unaonesha wazi kuwagawa wananchi na kuwafanya wasiwe sawa mbele ya haki. Binadamu ni mtu aliemumbwa na fikra, akili, na maarifa. Unapomleta mtu kama Mkapa jimboni kutoa maoni na wanachi wengine, hata akizomewa, watu watahisi kuwepo kwa usawa. Na unapompa siku yake pekee tena nyumbani kwake, unaanza kuuumba dudu moja baya mno la ubaguzi na ngazi refu ya utabaka baina ya wananchi na wakubwa wao.
Taswira inayojengeka machoni mwa wananchi hivi sasa, kwa tume kuanza kupitia watu binafsi majumbani kukusanya maoni yao, eti tu kwa sababu ni wakubwa, haina mustakabali mzuri. Haina kwa sababu tafsiri iko wazi ya utaratibu kama huu. Iko wazi hata kwa kujiuliza swali dogo tu. Hivi kweli maoni waliyotoa wananchi wote wa Zanzibar, yanawezajae kuyapindua maoni aliyoyatoa Mkapa na Mwinyi? Sipati picha!
Yaani, hivi kweli maoni ya wananchi wa kawaida yatasikilizwa bora kwa kulinganisha wingi wao kuliko ukubwa na maoni ya wenye cheo, kauli, na nguvu katika nchi hii? Hili si kweli, maana tumeona katika chaguzi nyingi hapa nchini, ambapo sauti ya wananchi walio wengi ikipinduliwa na kauli ya mtu mmoja. Hili liko wazi kama sabuni ya mche!
Na ndio hapa ninapoona kuwa ile kauli mbiu isemayo ‘Watu wote ni sawa mbele ya haki na Sheria’ ikibadilika na kusomeka ‘Watu wote ni sawa mbele ya haki na sheria, lakini baadhi ya watu, ni sawa zaidi kuliko wengine’. Kwa hali hii naanza kukosa imani na kutawaliwa na ruwaza za nadharia ya ‘Ki-Orwell’ ninapautazama mchakato mzima wa katiba hapa nchini unavyokwenda.
Chanzo: Mzalendo.net

Wednesday 16 January 2013

‘Kidau nipeleka Pemba, nina haja nako’

HUKU kwetu Uswahilini kabla ya kuja kwa vyombo vya kisasa vya mawasiliano na yale yaitwayo siku hizi ‘majukwaa ya kijamii’ watunzi wa mashairi au nyimbo walikuwa na dhima kubwa katika jamii. Wao ndio waliojitwika kazi ambayo leo hufanywa na waandishi.
Washairi walikuwa wakitangaza mambo au kupinga mambo yawe mema au mawi. Ilikuwa ni kazi yao kuhadharisha palipohitajika kutolewa indhari, kunasihi palipopasa kutolewa nasaha, kuwakosoa watawala na hata kuwatukana au kuwaapiza maapizo yalipolazimika.
Si mara zote wakinusurika. Nao pia yakiwasibu yanayowasibu waandishi wa leo. Wakipingwa na kuzomewa; mara nyingine wakipigwa na hata kufungwa gerezani.
Mombasa tu kuna mfano wa Suudi bin Said Al-Maamiriy (1810-1878) aliyewahi kufungwa kwa kuandika mashairi yaliyomuunga mkono mpiganiaji uhuru Mbaruku bin Rashid Mazrui. Kifungo cha gerezani hakikumrudisha nyuma Suudi kwani alipofunguliwa aliendelea na harakati zake.
Kwa mfano huo tunaona jinsi washairi wa kale wa Uswahilini walivyokuwa na sifa ambayo kila mwandishi wa leo anahitajika kuwa nayo — sifa ya ushujaa wa kutowaogopa watawala. Sifa ya kuisema kweli japokuwa hiyo kweli yawauma watawala.
Bila ya shaka, kama ilivyo kwa baadhi ya waandishi wetu wa leo kuna baadhi ya washairi wa zama za kale waliokuwa wakinunuliwa na watawala. Ufisadi haukuzaliwa jana.
Hao waliokuwa wakinunuliwa walikuwa ni wachache na hawakumbukwi kama wanavyokumbukwa waliokuwa na ujasiri wa kuisema kweli na waliokuwa wakifuatwa kama wanavyofuatwa waimbaji wa kileo wa muziki wa ‘pop’.
Kuna mfano mwingine. Huu ni wa ushujaa wa mshairi wa Pate, Ali Koti, ambaye alipojitosa katika siasa za Pate hakuchelea kumkosoa mfalme mpya na viongozi wenzake waliompindua Sultani wao.
Mifano hiyo imetajwa na Abdurrahman Saggaf Alawy (Maallim Saggaf) na Ali Abdalla El-Maawy kwenye Dibaji ya kitabu kiitwacho Kale ya Washairi wa Pemba: Kamange na Sarahani. Kitabu hiki kimechapishwa na shirika la uchapishaji la Mkuki Na Nyota la Dar es Salaam. Kimehaririwa na Abdilatif Abdalla, gwiji wa mashairi kutoka Mombasa na mshairi wa Sauti ya Dhiki. Mhariri ametupatia lulu kwa Utangulizi wake wenye kutufunza mengi.
Kale ya Washairi wa Pemba ni mkusanyiko wa mashairi ya Kamange na Sarahani, washairi wa Kipemba waliokuwa wakivuma hadi Unguja na pwani za Tanganyika na Kenya.
‘Kamange’ alikuwa Ali bin Said bin Rashid Jahadhmiy (1830-1910) aliyezaliwa Bogowa, Pemba, na aliyekuwa na lakabu nyingine ya ‘Basha-Ali.’ Lakabu hii ilitokana na cheo cha ‘Basha’ (Pasha) kilichokuwa kikitumika katika majeshi ya Misri na Uturuki.
Sarahani alikuwa Sarahani bin Matwar bin Sarahan al-Hudhry, Hinawy (1841-1926) aliyezaliwa Pondeyani, Chake Chake, Pemba. Sarahani alimpiku Kamange kwa usomi kwa vile pamoja na kubobea katika masomo ya kidini, historia ya Kiislamu na fasihi pamoja na historia ya fasihi ya Kiarabu alijifunza Urudhi (kaida za Ushairi) na Qawafi. Kadhalika alijifunza elimu ya Unajimu.
Sarahani pia alikuwa shekhe aliyekuwa akipigapiga mbizi katika falsafa kama mshairi mwengine wa Pemba, Nassor Muhammad Jahadhmy (Kichumba) ambaye kwa utaalamu wake wa historia akipenda kutoa mifano yake kutoka historia ya Ukristo, ya Yemen na ya Misri.
Asili za koo za washairi Kamange na Sarahani ni Omani lakini ziliingia Uswahilini miaka mingi sana iliyopita, zikaoana na Waswahili na vizalia vyao vikawa ni Waswahili.
Kamange na Sarahani wakipenda kutaniana na kujibizana hata watu wakifikiria kwamba wanagombana. Ukweli ulidhihirika alipokufa Kamange pale Sarahani kwenye ubeti mmoja wa kuomboleza kifo cha mwenzake alipoandika:
“Twali tukitukanana, watu wasitudhaniye
Kama hawa wapatana, ya ndani tusiwambiye
Kufurahisha fitina, kusudi watuzomeye
Naliya leo sinaye, ya mawadda na swafawa.”
Hawa ni washairi ambao zama zao Washairi wa Pemba waligawika mapande mawili: pande la Kamange na la Sarahani. Kamange ndiye aliyekuwa malenga na shaha; mshindani wake alikuwa mmoja tu, Sarahani.
Baadhi ya mashairi ya Kamange yanamuibuwa kuwa ni mtu aliyekuwa tayari ilipohitajika kuwakaripia na kuwapinga wakuu wa serikali. Alikuwa heshi kusuguana roho na wakuu wa Pemba. Aliwapinga kwa mwendo wao mbaya wa ubadhirifu wa mali ya umma na kwa kula rushwa.
Katika shairi lake ‘Doriya Kapatikana!’ lililokuwa likimsema na kumlaani Doriya, askari wa gereza Kamange alisema:
“Naende mbele afike, Pemba asirudi tena
Jamii wanusurike, yawaondoke mahana
Khuduma waitumike, pasiwe kusukumana
Doriya kapatikana, naende mbele afike…
Hajuwi Pemba peremba, haufai ujagina?
Mashumu yakikukumba, haukutoki mdhana
Nenda kamwulize Simba, dola ilivyombana
Doriya kapatikana, naende mbele afike…”
Kamange alikuwa pia stadi wa mashairi ya mapenzi. Katika shairi ‘Muwacheni Anighuri’ anakisifu hivi kichwa cha mwanamke:
“Kichwa chake mviringe, ndiyo mwanzo wa khabari
Hakuumbwa vungevunge, kama hawa khantwiri
Hana pazi hana tenge, sawasawa mdawari
Muwacheni anighuri, ndiye Badii Jamali.”
Serikali ya kikoloni ilipopiga marufuku uwindaji na ikatoa hukumu ya viboko 50 kwa apatikanaye anawinda, Sarahani akijua kwamba Kamange akipenda kuwinda, alimpelekea ubeti ufuatao:
“Mwenye kuondowa miko, ilani tumeletewa
Ni khamsini viboko, na mnyoo akatiwa
Basha uwinja hauko, natule vya kununuwa
Ndege wamerufukuwa, wawinja tahadharini!”
Kale ya Washairi wa Pemba kinawazungumza pia washairi wengine wa kale ya Pemba miongoni mwao wakiwa akina Bahemedi wa Sinawi (Hemed bin Seif Al-Ismaily), Ruweihy (Bwana Muhammad bin Juma Al-Kharusy) na Hemedi bin Khatoro.
Kitabu hiki kinawazindua wenye kuidhania Pemba kuwa ni debe tupu kifasihi, kwamba haina urathi wa ushairi wa kupigiwa mfano. Chaonyesha jinsi ushairi wa Pemba, kwa lahaja ya Kipemba, ulivyo na ladha ya aina yake ingawa washairi wa Pemba walikuwa na tabia pia ya kuchanganya Kipemba na lahaja nyingine kama za Kimvita, Kiamu, Kimrima, Kivumba na kutumia maneno yenye asili ya Kiarabu.
Kiswahili chetu kimeporwa. Walokipora sasa watamba kwamba wao ndio wenye kuitamalaki lugha hii. Wanajipurukusha na kujitia kusahau kwamba Kiswahili kina wenyewe na kina mila na utamaduni wake.
Maallim Saggaf na El-Maawy wanatukumbusha kwenye Dibaji yao kwamba: “Ushahidi wa kihistoria waonyesha wazi kuwa pwani ya Afrika ya Mashariki kulikuwa na Waswahili kabla ya kuzaliwa Nabii Isa...”
Swali wanaloliuliza na wanalohoji kuwa lahitaji utafiti zaidi ni: nani aliyewaita watu hao ‘Waswahili’, na lugha yao ‘Kiswahili’ na utamaduni wao ‘Uswahili’? Inavyoonyesha hawaridhiki kwamba asili ya ‘Swahili’ ni neno la Kiarabu saahil, yaani pwani
Raia Mwema

Friday 11 January 2013

Ufisadi: Ugonjwa uliowavaa watawala wetu

Barazani kwa Ahmed Rajab
TEODORO Nguema, mtoto wa Rais wa Equatorial Guinea, ana jumba mjini California, Marekani, lenye thamani ya zaidi ya dola za Marekani milioni 30. Pia ana ndege yake binafsi ya aina ya Gulfstream jet na anamiliki aina kwa aina ya magari ya kifahari.
Kadhalika Teodoro ametumia kiasi cha dola milioni moja na laki nane kununua baadhi ya vitu vilivyokuwa vikimilikiwa na mwimbaji Michael Jackson. Unakaa na kujiuliza: amepata wapi fedha za kujinunulia vitu vyote hivyo? Tunajuwa kwamba yeye ni waziri lakini mshahara wake ni dola za Marekani 81,600 kwa mwaka.
Mtoto wa Rais mwingine wa Kiafrika mwenye kuogolea kwenye bahari ya fedha ni Isabel dos Santos, bintiye Rais wa Angola. Isabel (40) ananukia uturi na wakati huohuo ananuka tuhuma za ufisadi. Inakisiwa kuwa ana utajiri wa thamani ya dola za Marekani milioni 500.
Ingawa Isabel ana shahada ya uhandisi kutoka Chuo cha King’s College, London, na alianza kujihusisha na biashara tangu awe na umri wa miaka 24 ni wazi kwamba asingaliweza kuupata utajiri wote alionao sasa lau asingelikuwa binti wa Rais Eduardo dos Santos.
Kama ilivyo Tanzania na baadhi ya vigogo vya CCM, ufisadi nchini Angola umekuwa zaidi ukihusishwa na baadhi ya viongozi wa chama kinachotawala cha MPLA.
Ufisadi ulianza kufurutu ada Angola kama miaka 10 au 15 hivi iliyopita. Umezidi kutia mizizi kwa sababu utawala wa chama cha MPLA unategemea vitendo vya ufisadi ili uweze kuendelea.
Nchini Angola ufisadi umekuwa ukihusishwa sana na biashara ya mafuta yanayochimbwa nchini humo na kuuzwa na serikali. Kwa hakika, kampuni ya taifa ya mafuta, Sonangol, ndiyo moja ya mihimili mikuu ya serikali.
Mara kwa mara, Manuel Vicente, Mkuu wa Sonangol, ambayo ndiyo kampuni kubwa ya umma nchini humo, amekuwa akitajwa kuwa ni mmoja wa mafisadi wakubwa wa Angola. Wengine wanaotajwa naye ni Jenerali Helder Manuel ‘Kopelipa’ Vieira Dias ambaye ni mshauri wa kijeshi wa Rais pamoja na kuwa waziri na Jenerali Leopoldino Fragoso do Nascimento, mkuu wa idara ya mawasiliano ya Rais.
Watatu hao wanatuhumiwa kujipatia utajiri wenye thamani ya mabilioni ya dola za Marekani kwa njia za kifisadi. Moja ya njia walizotumia ni kuyabinafsisha mashirika ya umma kwa faida yao. Si kwamba mashirika hayo yalikuwa yakila hasara. La.
Katikati ya walaji rushwa na mafisadi wa wanaotuhumiwa Angola ni mwenyewe Rais wa nchi. Kuna wasemao kwamba hana budi kuwako katikati ya duru ya ufisadi kwa vile yeye na chama chake kama nilivyokwishagusia, wanautegemea ufisadi ili kuweza kuendelea kutawala. Wengine wanasema kwa kejeli kwamba nchini Angola ufisadi ni ‘taasisi’ ya aina yake na kwamba hiyo ndiyo taasisi kuu yenye kuiendesha nchi.
Kwa jumla bara letu la Afrika limepata sifa mbaya kwa sababu ya ufisadi uliokithiri na unaowahusisha au kuwagusa baadhi ya viongozi wa nchi zetu. Kelele kubwa zimekuwa zikipigwa ndani na nje ya Afrika dhidi ya ufisadi na hatimaye kuna dalili nzuri kwamba asasi za kiraia, makampuni, taasisi za umma na hata baadhi ya serikali za Kiafrika, zimekuwa zikichukua hatua madhubuti za kupiga vita ufisadi.
Sote tunazijuwa athari za ufisadi kwa maendeleo ya nchi zetu. Tunaelewa jinsi ufisadi unavyochangia kuzifanya nchi zetu ziwe masikini, zikose maendeleo, zikose barabara, zikose maji safi, umeme na hata madeski skulini.
Kuna maswali mengi tunayopasa kujiuliza tunapoutafakari ufisadi. Kwa mfano, nini hasa ufisadi? Nini historia yake, akina nani wanaoathirika nao, nini kinachoupa nguvu na nini kinachouzuia?
Hayo ni baadhi tu ya maswali yanayojadiliwa katika kitabu kipya kuhusu ufisadi duniani. Kitabu hicho (‘Global Corruption: Money, Power and Ethics in the Modern World’) kimeandikwa na Laurence Cockroft, mtu ambaye kwa muda mrefu amekuwa katika safu ya mbele ya wale wenye kupiga vita ufisadi. Kimechapishwa na shirika la uchapishaji la Uingereza la I.B.Tauris.
Cockroft ni mmoja wa waasisi wa ile asasi ya kimataifa ya kupiga vita ufisadi, Transparency International, na kwa muda mwingi alikuwa mwenyekiti wa tawi lake la Uingereza.
Cockroft anaijua vyema Tanzania ambako aliwahi kufanya kazi katika miaka ya 1960 na baadaye amekuwa akishughulika na miradi kadha wa kadha ya maendeleo nchini humo.
Uzuri wa kitabu cha Cockroft ni kwamba kina mada mbalimbali za kuzichambua katika kuangalia nini kinachoupa nguvu ufisadi. Kwa mfano kinauchambua ‘uchumi uliofichika’ — huu ni uchumi usio rasmi ambao takwimu zake hazijulikani na unaorahisisha malipo ya hongo kulipwa bila ya kujulikana.
Kinaangalia pia jinsi fedha ambazo aghalabu hupatikana kwa njia za kifisadi zinavyotumiwa kisiasa. Kwa hili amekitaja chama cha CCM na jinsi baadhi ya viongozi wake walivyojitajirisha kutokana na shughuli za kukipatia fedha chama hicho.
Cockroft amejaribu kuonyesha kwamba ufisadi si ugonjwa wa Afrika pekee, bali ni wa dunia nzima; umeambukiza kwingi na ufisadi wa Afrika uko chanda na pete na ufisadi katika madola makubwa ya Marekani na barani Ulaya.
Ametoa mifano mingi ya ufisadi katika nchi kadha wa kadha zisizo za Kiafrika na za Kiafrika. Tanzania imejaa tele. Mingi ya mifano hiyo tunaijuwa. Lakini kitabu chake kinachemsha bongo si kwa mifano aliyoitoa bali kwa simulizi zake kuhusu jinsi ufisadi unavyofanya kazi katika sehemu mbalimbali duniani na hatua zinazoweza kuchukuliwa kuuzuia.
Hiki ni kitabu muhimu kwa yeyote yule anayetaka kuelewa jinsi ufisadi unavyokuwa na mitandao yake na jinsi mitandao hivyo inavyowahusisha wengi walio madarakani katika nchi zenye chumi zilizoendelea na pia katika nchi kama zetu ambazo bado zinasotasota zikitafuta maendeleo.
Barani Afrika wako wababe kadhaa wanaoshika panga kupambana na ufisadi. Cockroft amewataja watatu tu walio maarufu sana: Nuhu Ribadu wa Nigeria, John Githong’o wa Kenya na Zitto Kabwe wa Tanzania. Amemsahau mwandishi na mwanaharakati wa Angola Rafael Marques ambaye maisha yake yamo hatarini kwa kazi anayoifanya ya kuufichua ufisadi wa Angola.
Chanzo: Raia Mwema