SHEREHE ZA UHURU ‘FEKI’ WA TANZANIA…!
• Msimu wa Tanganyika kuizuga dunia wawadia!
• Hufanya sherehe za
mamilioni ya walipa kodi dunia nzima!
Tarehe 09 Disemba mwaka huu, yatajwa kitaifa na kimataifa kuwa ndio siku ya
Uhuru wa Tanzania ambao hadi siku hio, Taifa hilo la ‘kufikirika’ la Riwaya za
Shaaban Robert litatimiza miaka 51, tangu lipate uhuru kutoka kwa Wakoloni wa
nchi jirani ya ‘Kusadikika’ pia ya Shaaban Robert.
Kwa wasiokuwa wasomaji wa Riwaya za Mwandishi mahiri, na baba wa fasihi ya
Kiswahili hayati Shaabani Bin Ufukwe (Shaaban Robert), nataka niwakumbushe tu
kuwa katika Riwaya zake mbili za Kusadikika na Kufikirika, alijaribu kusawili
mazingira ya nchi zisizokuwepo kiuhalisia bali kivitendo na muonekano wa
kitaswira nchi hizo hufanywa zionekane zipo au huwepo kimawazo. Lakini kiuhakiki
nchi hizo zaweza kuwa sawa na nchi yoyote ile yenye sifa zilizotajwa na
mwandishi huyo.
Nalazimika kujenga hoja kuwa uhuru wa Tanzania ni wa nchi za Kusadikika na
kufikirika kwa sababu dhana nzima ya uhuru na nchi yenyewe haipo kiuhalisia na
kimantiki. Kwanza hakuna nchi ambayo inaitwa Tanzania kiukweli hasa na kama ni
jina tu, ‘Tanzania’ ni sawa na jina lilibuniwa na watu la Dar es Salaam kuiita
‘Bongo’ na si vyenginevyo. Pili, hata kama nchi hiyo tunalazimishwa kuamini kuwa
ipo, basi haihusiani kabisa na dhana ya uhuru na Ukombozi wan chi za Afrika na
ndio hata ukifuatilia harakati za uhuru na ukombozi wa bara la Afrika utakutia
nchi iitwayo Tanzania haimo kabisa.
Dhana ya uhuru wa nchi haihitaji mtu aliesoma sana kuijua fasili yake. Kwani
kimsingi Uhuru ni hatua ya nchi kujipatia nafasi ya kujitawala yenyewe na uwezo
wa kujifanyia maamuzi ambapo kabla ilikuwa mamlaka hayo hayakuwa mikononi mwa
Wazalendo au wananchi wenyewe, bali yalikuwa chini ya mikono ya wageni waitwao
Wakoloni.
Kwa mantiki hii tunarudia kusema kuwa, Tanzania haikuwepo kabla na hata muda
mfupi baada ya Uhuru wa bara na Visiwani, itakuwaje iwe nchi huru? Unaposema
Uhuru wa Tanzania, kwa wenye akili za kidadisi watakuuliza nchi hio ilitawaliwa
na nani? Labda tujikumbushe historia kidogo ya Afrika Mashariki. Zanzibar
ilitawaliwa na Muarabu, Kenya Muingereza, Uganda Muingereza, na Tanganyika au
German East Africa, ilitawaliwa na Mjerumani.
Hili ni somo la Hitoria ya darasa la sita na la saba hapa kwetu.
Pia tujikumbushe tarehe muhimu za Uhuru wa nchi hizo. Kenya ilipata Uhuru
tarehe 10 Disemba 1963, Uganda tarehe 09 Oktoba 1962, Zanzibar 12 Disemba, 1963,
na Tanganyika Tarehe 09 Disemba, 1961. Kwa hivyo, hapa hapana cha kuwazuga watu,
kwani kwa hakika katika nchi hizi kuu nne za Afrika Mashariki utaona kuwa
Tanzania haimo.
Juu ya hayo, hivi sasa kuna mabango kila pahala duniani na katika mitandao ya
jamii inayosema na kunadi Sherehe za kufa mtu za Uhuru wa Tanzania kutimiza
miaka 51. Wenzetu wa bara wamezoea kuwazuga Wazanzibari kwa sababu ndio ‘mazuzu’
labda au ‘mayakhe’ au ‘mdebwedo’ kama walivyozoea kutuita, na wanafikiria kuwa
Wazanzibari waliokuwa ‘mazuzu’ wakati huo watakuwa mazuzu na vizazi vyao vijavyo
kiasi ya kutoweza kujua hata hesabu ya kutoa na kujumlisha.
Kwa vile wanaaamini waliweza kuitawala Zanzibar kwa hadaa, ujanja, na
kuwazuga wazanzibari kwa kuwapa vyeo na kuwatisha wengine kwa adhabu na mambo
mbali mbali, wenzetu hawa bado wanaamini kuwa dunia nzima ina mazuzu kama hivi
wanvyowaona Wazanzibari walioshindwa kujuwa hesabu ya Mwalimu ya 1+ 1 = 2 (
Wazanzibari walisema 1+1=3).
Baada ya kuona kuwa hatujui hesabu ndio hapo ukaona kuwa Uhuru wa Tanganyika
unatimiza miaka 51 yaani ni sawa na 2012-1961, wao wakidhani na hesabu hii
itaushinda pia.Cha kushangaza, hesabu ya darasa la kwanza hadi la tatu tu hii na
bado dunia nzima inazugwa ik iamini kuwa Tanzania leo inatimiza miaka 51 ya
uhuru wakati nchi yenyewe hata haipo, imeundwa tu kutokana na Riwaya za Shaaban
Robert za kusadikika na kufikirika.
Mpaka hapa naamini umeweza kuona kuwa wenzetu wa bara wanatumia hila na mbinu
kuudanganya Ulimwengu na huku wakitumia pesa zisikuwa kidogo za walipa kodi
ndani na nje ya nchi kwa kusherehekea Uhuru wa nchi isiyokuwepo katika nchi
zilizotawaliwa. Huu ni upotoshaji mkubwa wa dunia na kusema kweli unaiondolea
hadhi nchi yetu kwa kusema Uongo ulio dhahiri mbele ya kadamnasi ya
kimataifa.
Leo hii kuna Sherehe kila pahali: London, Canada, Italia, China, Ufaransa,
Ujerumani, Marekani na nchi zote; eti ‘Miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania’. Hii
haileti maana wala haina mvuto wowote zaidi ya kuuonesha Umma ufinyu wetu wa
mawazo na fikira za kutojua maana ya neno Uhuru na baya zaidi hata kutojua
historia yetu na hesabu ya kujumlisha na kutoa tu ambayo kila mtoto wetu wa
darasa la kwanza na la pili anaijua.
Nionavyo, Ipo haja tubadilike. Hakuna ubaya kusema ukweli hata kama unauma.
Wala haitaibabua sura haiba ya bara kwa kuandika na kujitangazia ‘Miaka 51 ya
Uhuru wa Tanganyika’. Si vibaya kwani huu ndio ukweli. Ni afadhali tuseme ukweli
tuepuke kuchekwa na kuadhirishwa.
Nakumbuka mwaka jana pale London, kuna Mzanzibari mmoja alifanikiwa kupenya
na kuingia katika Sherehe za Miaka 50 ya uhuru wa ‘Tanzania’. Alipofika
alimuuliza balozi ‘Hivi Tanzania ilipata uhuru kutoka kwa nani?’. Balozi hakuwa
na Jibu. Baada ya hili, tulifikiri watajirekebisha, lakini ndio kwanza wanazidi
kujitangaza hivyo ilhali dunia inajuwa kuwa huu wanaoufanya ni Uongo wa mchana,
kuzimu hakuna nyota.
Kwa muungwana ni wajibu ukweli usemwe, hakuna uhuru wa Tanzania.
Tusidanganyane na kudanganya watu kwani mwisho tutashindwa kwani ukisema uongo,
Ukweli haujifichi,na ukiibuka ukweli kinachofata ni kuona aibu tu. Kwani wazungu
husema ‘Unaweza kuwadanganya baadhi ya watu, baadhi wa wakati, lakini huwezi
kuwadanganya watu wote, siku zote’.